My Blog List

Tuesday, April 25, 2006

TFF NA SOKA LA TANZANIA USINGIZINI.

Wakati bado TFF haijampata kocha wa kuinoa timu ya Taifa-Taifa Stars-hapa Uganda viongozi wapya wa shirikisho la soka hapa Uganda-FUFA- tayari wamemleta mwalimu mpya wa timu hiyo kutoka Serbia. Kocha huyo ni Tomislav Sicic kutoka Serbia.
Viongozi wapya wa FUFA wameingia madarakani mapema mwaka huu tu na tayari wanafikiria juu ya safari ya timu hiyo ya Kombe la dunia na lile la Mataifa ya Africa.
Kama tunavyojua TFF walishaadiwa ushirikiano na Rais JK. Nataka tuwaulize hawa mabwana mbona wamelala? September si mbali wajameni. Nataka niangalie hii mikakati Tenga anayodai ipo je itafanikiwa?
Si soka tu ila Tanzania chini ya JK ni lazima ichukue hatua madhubuti ili kuendeleza michezo. Mimi ninaamini kama tutaendeleza michezo basi tutawainua vijana wengi ambao hawana ajira na hawatakaa waipate kutokana na fursa chache. Ninaunga mkono juhudi za serikali kufanikisha ziara ya timu ya ndondi wiki hii kwenda nchini Uhispania.
Hii ifanyike pia kwenye soka kwani ikiwa kombe la dunia litafanyika hapa Afrika hatuna budi tuanze leo kama wenzetu wa Uganda. Hainifurahishi kwa viongozi wa TFF kutuambia eti timu inakwenda Ushelisheli kwa mechi za kirafiki baada ya kualikwa huko. Pia eti Malawi imetualika kwa michezo ya kirafiki. Nasema hivi kwani inaonesha kwamba labda TFF hawana mipango madhubuti ila wanasubiri mialiko na kama isipokuja itakuwaje? Pia nataka nitoe rai ya makocha wazalendo hawakidhi haja ni muhimu tukawa na makocha kutoka Ulaya kwani tunahitaji mambo ambayo watanzania wenzangu hawana katika suala zima la kuiandaa timu ya Taifa. Kwa mfano, nina hakika kwa aina ya makocha tulionao nchini Tanzania si makini sana kwenye masuala ya kudhibiti wachezaji kinidhamu. Nidhamu ni msingi wa wachezaji kutekeleza wajibu wao na kama wachezaji wetu hawakai kambini na kufuata taratibu za kambi tusitarajie kufuzu kwenda Ghana au Afrika kusini 2010. Tayari hata katibu mkuu wa TFF, Tenga kakiri wachezaji wa Stars ni kama "chokaraa". Sijafurahishwa kabisa na hali ya sasa ambapo inabidi Tenga awakumbushe makocha akina Msola juu ya kutoa ruhusa. Hivi kweli tuna makocha wenye taaluma ya kutosha kuongoza timu ya Taifa? Jibu ni hatuna, hebu tujaribu kufuatilia timu kadhaa zitakapoanza kupiga kambi kwa ajili ya kombe la dunia kama utakuwa unasikia mchezaji kaomba ruhusa eti akachukue begi lake nyumbani kama wachezaji wetu wanavyofanya.
Alafu ni lazima tucheze na wapinzani wenye kutumia staili ya uchezaji kama ya wale tunaotarajia kukutana nao.Nionavyo mimi hii TFF bado ni kama FAT ya akina Rage na Ndolanga kwani bado sioni mabadiliko yenye kasi na ari mpya.

No comments: