Monday, October 26, 2009

KIMBEMBE CHA UCHAGUZI WA SERIKALI ZA MITAA

Ilikuwa ni kivumbi na jasho katika Uchaguzi wa serikali za mitaa jana.Uchaguzi wa serikali za Mitaa niliushuhudia mwenyewe katika Kata moja iitwayo Kaloleni katika Manispaa ya Moshi. Katika uchaguzi huo, ningependa niulezee kwa kadri nilivyouona tanga hatua za awali, yaani uandikishaji wa wapiga kura hadi siku ya kupiga kura.

Mosi, kwa mujibu wa kanuni za uchaguzi ambazo zilitangazwa na wizara ya Tamisemi, kulikuwa na siku saba (7) za kujiandikisha kwa wapiga kura. Kwa Kata ya Kaloleni, kulikuwa na Mitaa miwili: Kaloleni na Kalimani. Katika mitaa yote hii walijiandikisha watu wachache sana hasa ikizingatiwa kuwa hata theluthi ya wakazi wa Mitaa hii miwili wanaostahili kupiga kura hawakujiandikisha. Hii inamaanisha kuwa, katika Mitaa yote ya Kata hii, viongozi ambao wamepatikana, si wanaotokana na kukubalika na asilimia kubwa ya wakazi. Ila kwa misingi ya kidemokrasia, mtu halazimishwi kujiandikisha, hivyo viongozi hawa ni halali kwa mujibu wa demokrasia.

Pili, kwa muono wangu naamini kuwa zoezi la uandikishaji wapiga kura lilikwenda vizuri sana kwani katika kila kituo cha kujiandikisha, kulikuwepo mawakala wa kila chama cha siasa ambacho kilikuwa kinashiriki katika uchaguzi huo. Kila wakala alionekana akiwa bize na kalamu wakati wote katika eneo la kujiandikishia kitu ambacho kilinifanya niamini kuwa baada ya zoezi hilo la uandikishaji basi ningelipata malalamiko ya pingamizi dhidi ya walioandikishwa.

Kabla sijaendelea, labda niseme tu kuwa katika uchaguzi huu, mimi nilikuwa ni msimamizi msaidizi msaidizi wa uchaguzi katika Kata husika. Kwa nafasi yangu nilipaswa kuratibu zoezi zima jambo ambalo nililifanya kwa weledi wangu wote. Baada ya kueleza ushiriki wangu katika zoezi hili, nigusie juu ya jambo la tatu, nalo ni yale mapingamizi ambayo niliyategemea sana kutoka vyama vyote baada ya uandikishaji. Kanuni zilitoa kipindi cha siku kadhaa kwa kila chama kuwasilisha mapingamizi dhidi ya wale wote waliokuwa hawakutimiza masharti ya kujiandikisha. Katika kipindi chote kilichotolewa, hakuna hata pingamizi moja liliwasilishwa na hivyo nikaamini basi zoezi la uandikishaji lilikwenda vizuri ajabu.

Ikumbukwe pia, wakati zoezi la uandikishaji likiendelea, wagombea wa nafasi za mwenyekiti wa Mtaa, wajumbe wa serikali ya Mtaa pamoja na wale wa Viti Maalum walichukua fomu za kugombea na kwenda kuzijaza kwa mujibu wa utaratibu na kuzirejesha. Baada ya urejeshaji wa fomu, wasimamizi wasaidizi wa kila Mtaa walizipitia na kuhakikisha zinatimiza masharti ya kugombea. Baadaye, wale wagombea wote walithibitika kuwa wamekidhi matakwa ya sheria na hivyo wote waliteuliwa wawe wagombea. Fomu zao zilibandikwa katika mbao za Matangazo ya Ofisi ya Kata na wasimamizi wasaidizi wa uchaguzi wa Mitaa yote husika. Pia wagombea wote walipewa nakala ya fomu hizo na siku tatu zilitolewa kwa mapingamizi dhidi yao kuwasilishwa.

Katika siku hizo tatu, wagombea wote wa chama cha Chadema waliwekewa mapingamizi hasa wakilalamikiwa kuwa hawakuthibitishwa na Ofisi ya ngazi ya chini kabisa ya chama chao yaani Tawi. Katika fomu zao, wote walikuwa wamethibitishwa na ngazi ya Kata ambayo viongozi wa chama hicho tayari walikuwa wamewajulisha wasimamizi wasaidizi kuwa hiyo ndiyo ngazi ya chini ya chama chao kupitia barua maalum ya kuwasilisha majina ya wagombea. Maadam kila chama cha siasa kina utaratibu wake wa kiutawala, ilionekana dhahiri hili si tatizo la msingi kwani kuthibitishwa na Ofisi ya Kata, ama wilaya ama Taifa na hata Tawi hakumuongezei au kumpunguzia mgombea sifa za kugombea kama raia mwema. Hivyo pingamizi hili lilitupwa mara moja lakini pia lilipelekwa hadi ngazi ya juu zaidi na likatupwa pia.

Baada ya mapingamizi haya kutupwa, uchaguzi ulikuwa umewadia na hivyo vyama vyote vilisahau kuhusu pingamizi na vikabakia vikijiimarisha na kushiriki katika uchaguzi siku ya tarehe 25/10/2009.

SIKU YA UCHAGUZI
Siku moja kabla ya uchaguzi nililala mapema ili niweze kuamka mapema kutekeleza jukumu la kitaifa. Na kweli niliweza kuamka mapema muda wa saa 12:00 asubuhi, kulikuwa kumenyesha mvua hivyo ili niweze kuwahi, ilinibidi nichukue teksi na nikafika katika Ofisi ya Kata asubuhi ya saa 12:50 nikamkuta Msimamizi Msaidizi Mkuu kutoka Halmashauri akiwa na vyombo vya uchaguzi tayari amefika. Mara moja kazi ya kusambaza vyombo ilianza kwa kutumia gari la Halmashauri katika eneo langu la kazi ili ifikapo saa 2:00 asubuhi upigaji kura uweze kuanza.

Mungu alisaidia, ilipofika saa 2:00 asubuhi upigaji kura ulianza na mara moja kulikuwa na vitimbi. Kwanza katika kituo kimoja, Ofisi ya Kata, alifika mpiga kura mmoja akapiga kura kimakosa na kugundua kuwa alitumia karatasi za aina moja tu kupiga kura zote tatu: mwenyekiti Mtaa, mjumbe wa Mtaa na Viti Maalum. Wakati tayari ameshatumbukiza karatasi ya kupigia kura kwenye visanduku husika, mara akawa mbogo na kuniita kama Msimamizi Mkuu akiwa na mawakala wa chama chake wakisisitiza tufungue sanduku la kura ili arekebishe. Hili nilimwambia kuwa haliwezekani na kama kweli amekosea basi kura hizo zitakuwa zimeharibika.

Baada ya jaribio hili kushindikana, huyu bwana akiwa na mawakala wake walisisitiza kuwa basi wakati wa kuhesabu kura tuzitambue kura hizo. Hapa pia niliwajibu hatutaweza kujua kama kweli ndizo zitakuwa kura zilizopigwa na bwana huyu. Baada ya mimi kuonesha ugumu wa kuwasikiliza, busara iliwaingia mawakala pamoja na mpiga kura wao, na alikubali yaishe na akaaga kwa amani. Zoezi likaendelea; ila pia katika Kituo kingine katika Mtaa wa pili wa Kalimani, kitimbi cha kwanza kabisa ilikuwa ni pale kabla hata ya upigaji kura kuanza, mawakala wa chama Fulani na wapenzi wao, walinijia kwa jazba sana wakidai kuwa kabla ya zoezi kuanza ni lazima mawakala wote na wasimamizi wote wakaguliwe.

Hali hii ilijitokeza kuwa Msimamizi Mkuu wa Kituo hiki, ambaye alikuwa ni mwanamama, alikuwa amebeba begi la mkononi, yale mabegi ya fasheni za kisasa kwa akina mama, lakini kelele zilipigwa zikidai kuwa mama huyu amebeba kura ndani ya begi lake. Kuona hivyo mama huyu kwa weledi wa hali ya juu alikabidhi begi lake kwa askari wa mgambo aliyekuwepo alikague na akaguliwa mbele ya wananchi. Hakukuwa na kitu ingawa binafsi nilisikitika wananchi wanalazimisha mwanamama akaguliwe na askari wa kiume kwani kulikuwa hakuna askari wa kike. Pia sikupendezwa sana kwa begi kukaguliwa hadharani, kwani kikawaida, mabegi haya yanakuwa na vitu vya faragha. Lakini maadam ndiyo tafsiri ya demokrasia wananchi wetu wanayoijua isiyojali sana haki za kibinafsi basi sikuwa na njia kwani kulikuwa na kila dalili ya dhahama kutokea.

Mungu aliepusha mbali ukaguzi ulifanywa, wananchi wakaridhika na hamasa ikabakia katika kuhesabu kura na kupata mshindi.

KUHESABU KURA NA KUPATA WASHINDI

Kwa mujibu wa taratibu, ilipotimu saa 10:00 kamili zoezi la upigaji kura lilifungwa rasmi na shughuli za kuhesabu kura zilianza mara moja. Hapa napo hapakukosekana vitimbi kama si vimbembe. Katika kituo cha Kaloleni, mawakala wa vyama vilivyogombea: CCM na Chadema waliruhusiwa kuwepo wakati wa kuhesabu kura ndani ya chumba maalum pamoja pia na wagombea waliruhusiwa kushuhudia. Katika hali isiyo ya kawaida ama isiyoeleweka, mgombea wa CCM hakuwepo ilisemekana kuwa amekwenda kuswali huku wengine wakidai alikwenda kupumzika nyumbani. Mgombea wa Chadema aliruhusiwa kuingia katika chumba cha kuhesabia kura kitu ambacho kiliibua kelele nyingi dhidi ya Msimamizi Msaidizi kuwa anapendelea chama cha Chadema.

Hata pale wapenzi na viongozi wa CCM walipoelezwa kuwa mgombea wao hajakatazwa ana haki ya kuingia katika chumba cha kuhesabia kura, bado walilazimisha zoezi lisimamishwe na asubiriwe mgombea wa CCM arejee ndipo zoezi liendelee. Nikiwa kama Msimamizi Msaidizi, niliamua kuwa ili kutimiza haki ya msingi bila kuminya nyingine, na kwa kuzingatia kuwa haikujulikana ni saa ngapi mgombea wa CCM angelirejea basi ni vyema nimwombe mgombea wa Chadema atoke nje ili mawakala wasalie ndani na zoezi la kuhesabu liendelee ili kuokoa muda. Nilipomuomba aliridhia maelezo yangu na akatoka nje na zoezi likaendelea.

Kiroja kingine juu ya hili kilijitokeza muda mfupi baadaye wakati niliposikia kelele za wapenzi wa CCM wakisogelea eneo kuhesabia kura huku wakiwa wamemzingira mgombea wao ambaye walikuwa wamekwenda kumleta ili aje ashiriki zoezi la kuhesabu kura. Kama msimamizi msaidizi nilitoka kuona kunani? Wapenzi wenye jazba walikuwa wanapiga kelele kuwa mgombea wao aruhusiwe kuingia ndani ya chumba cha kuhesabia kura. Mara moja nilipomueleza mgombea huyo juu ya kilichotokea aliniambia kuwa yeye kamwe hawezi kuingia ndani ya chumba cha kuhesabia kura. Alianza kunilaumu kuwa mbona sikumjulisha kuwa ni haki yake kuwepo katika zoezi hilo? Mimi nilishangazwa kidogo kwani haikuniingia akilini eti mtu anagombea nafasi wakati hajui taratibu za uchaguzi. Hii ilinikumbusha kuwa kuna tatizo katika vyama vyetu katika kuwaandaa wagombea wetu.

Alipokataa kuingia ndani kwa kisingizio kuwa mawakala wake wafanye hilo, huku nyuma mgombea wa Chadema alikuwa yuko tayari aingie ndani. Kutokana na hali kuwa tete, ilibidi nimsihi mgombea wa Chadema asiingie ndani ingawa ni haki yake, kwani niling’amua kuwa maadam tayari kuna dalili za kuonesha kuwa ninampendelea mgombea wa Chadema nilidhani ni vyema nikawanyima wote wakae tu nje na wawaachie mawakala wao kuhesabu kura. Nilimnyima mgombea wa Chadema haki ya kushuhudia zoezi la kuhesabu kura kwani niliamini kuwa pindi matokeo yatakapotangazwa inawezekana kabisa uwepo wake mwenyewe ndani ya chumba cha kuhesabia kura ikawa ni chanzo cha kuibua sintofahamu juu ya ushawishi wake katika matokeo. Sikutaka kamwe matokeo ya uchaguzi ule yawe na mashaka. Mungu alisaidia na uchaguzi ulikwenda shwari na mwishoni baada ya kuhesabu kura, wagombea wote wawili waliitwa ndani ya chumba na wakaoneshwa matokeo yao wakiwa na mawakala wao na kupewa fomu maalum kusaini kukubali ama kukataa matokeo.

Wagombea wote walikubali matokeo na kusaini fomu kabla ya Msimamizi Msaidizi kuyatangaza hadharani kwani ilibidi ifanyike hivyo ili kuweza kuwadhibiti wapenzi wao ambao walikuwa nje na shauku kubwa. Hali hii ilikuwa inatishia amani hivyo, ilibidi tuwaombe kuwa wagombea watusaidie kuwadhibiti wapenzi wao ili mshindi atakapowekwa wazi basi kuwe na utulivu huku wakiwa wamekwishawaonesha hali ya kukubali matokeo hayo. Hili lilifanyika na mwisho matokeo yaliwekwa hadharani na zoezi lilifungwa kwa amani baada ya mgombea wa CCM kushinda.

KUHESABU KURA MTAA WA KALIMANI

Ikumbukwe kuwa katika Mtaa wa Kalimani, zoezi la upigaji kura lilianza kwa kimbembe cha wasimamizi na mawakala kukaguliwa pochi zao na hata maungoni (mifukoni) pale watu walipoamini kulikuwa na uwezekano wa kura kufichwa. Imani hapa ilikuwa ni ndogo sana dhidi ya watumishi wa serikali. Wafuasi wa chama cha Chadema walikuwa na hamasa na hali ya kutowaamini kabisa watendaji wa serikali.

Kabla ya kura kuhesabiwa, tayari wananchi kadhaa akiwemo Diwani wa Kata ya Kaloleni walinifikishia malalamiko yao kwa mdomo na kwa njia ya simu kuhusu kuwepo kwa wapiga kura wasio kuwa na sifa, yaani watoto. Binafsi niliwajibu kuwa kuleta pingamizi siku hiyo si sahihi kwani kulikuwa na muda wake ambao hawakuutumia. Lakini pia niliwasihi kuwa mawakala wao si wapo eneo la kupigia kura, basi kwanini wasiwazuie na zifanyike juhudi za kuwatambua kiumri? Ni wazi majibu yangu haya dhahiri hayakuwaridhisha walalamikaji hawa wa chama cha CCM lakini sikuwa na njia nyingine ya kuwasaidia zaidi ya kutembelea vituo vyote vilivyolalamikiwa na kukuta zoezi la kupiga kura likiendelea huku wasimamizi pamoja na mawakala wa vyama vyote wakiwa wametulia wakiniambia hakuna taabu wala shida yeyote. Nilifanya upitiaji huu mara tatu kabla ya zoezi la kupiga kura kufungwa na sikukuta jambo hili likisemwa na wakala yeyote kama ni tatizo.

Kwa hali hiyo niliridhika kuwa labda hili ni hali ya homa ya uchaguzi miongoni mwa wapenzi wa CCM. Uchaguzi uliendelea vyema hadi kufungwa na zoezi la kuhesabu kura lilianza ambapo lilikwenda hadi mnamo saa sita za usiku. Hapa palitokea vimbembe kadhaa: Kwa mfano, wakati kura za nafasi ya uenyekiti zikihesabiwa mara baada ya zile za wajumbe na viti maalum kukamilika, ilikuwa tayari imeonesha kuwa wagombea wa Chadema walikuwa na mwelekeo wa kushinda karibu viti vyote. Hesabu ya kura ya nafasi ya mwenyekiti ilijaa hamasa, jazba na hofu miongoni mwa mawakala na wagombea wote. Ikiwa ni karibu zoezi la kuhesabu kura limalizike, nje ya chumba cha kuhesabu kura wananchi walijawa na bashasha na hamasa kubwa zikiambatana na jazba ya kupata matokeo. Kelele ziliongezeka sana na walinzi (mgambo na polisi) walipata taabu sana kuwadhibiti vijana hao.

Mara taa za chumba hicho cha kuhesabia kura zilizimwa na mawe yalianza kurushwa juu ya paa kwa wingi na makelele ya kila aina. Hali ya mkanganyiko ilijitokeza wengi tukidhani ni umeme umekatika. Kumbe la, kuna mmoja miongoni mwa mawakala ama wagombea waliokuwa ndani ya chumba cha kuhesabia kura alikuwa amezima taa. Mimi pamoja na Msimamizi Msaidizi wa Halmashauri tulikuwa nje tukijaribu kuwatuliza wananchi ambao walikuwa wakivurumisha mawe na kupiga makelele.

Baada ya muda mfupi, taa iliwashwa na mara mawakala wawili ambao pia ni mke na mume walionekana wakihimiza wenzao kuwa haitawezekana tena zoezi la kuhesabu kura liendelee kwani kuna mtu (mmoja wa msimamizi aliyekuwa akiendesha zoezi la kuhesabu kura ambaye pia ni mwalimu kitaaluma amechukua kura za mgombea wao na kuzihamisha). Kutokana na hali ile, wasimamizi wote watatu tuliokuwemo ndani ya chumba kile tulijaribu kuwatuliza watu wote na tukaamuru kuwa zoezi la kuhesabu kura za nafasi ya mwenyekiti wa Mtaa lianze upya.

Nilisisitiza kuwa ni lazima zoezi lianze upya kwani wakati taa zilipozimika, alikuwepo mgombea mmoja ambaye alikuwa na tochi na alikuwa ameiwasha kuelekea katika eneo la kuhesabia na ilionekana dhahiri kuwa kila mtu eneo lile alikuwa ametulia na hakuna aliyekuwa akifanya lolote hadi pale taa zilipowaka. Nilijiridhisha na hili na ndio maana niliamua kuamuru kuhesabu kura kurejewe kwani nilikuwa nina uhakika kuwa hakuna aina yeyote ya ukiukwaji wa utaratibu ulifanyika wakati taa zimezimika kwani kwa mwanga wa tochi na mimi nikiwa dirishani niliweza kuona kila kitu katika eneo la kuhesabia. Niliamini kuwa mawakala hawa wawili walikuwa ni chanzo cha uvurugaji wa zoezi zima la uchaguzi na hivyo sikutaka kuwapa mwanya. Kama Afisa Mtendaji wa Kata tayari nilikwishasikia tetesi kuwa wafuasi wa chama Fulani walikuwa wamekutana kwenye nyumba Fulani siku mbili kabla ya siku ya kupiga kura na kupanga nini cha kufanya pale itakapodhihirika wanashindwa. Hivyo, niliamini kuwa huenda kuzimwa taa ndiko kulikokuwa chanzo cha utekelezaji wa tetesi nilizokuwa nimezisikia.

Kwa kutumia ushawishi wa kimamlaka, zoezi zima la kuhesabu kura za nafasi ya mwenyekiti wa Mtaa lilirejewa na hadi mwisho mgombea wa Chadema pamoja na wajumbe wanne waliibuka washindi huku CCM ikipata mgombea mmoja. Mara baada ya matokeo kuwa dhahiri, wagombea wote wa CCM walikataa kusaini fomu za matokeo kwa ushawishi mkubwa wa wale wavurugaji wawili ambao nimewaelezea hapo awali. Pamoja na kukataa huko, ilibidi tuombe ulinzi wa FFU ili kuwakaribia wapenzi wa Chama cha Chadema waliokuwa na shauku ya matokeo wakiwa na jazba ya ajabu. Mgombea aliyeshinda wa Chadema aliombwa awatulize wapenzi wake na matokeo yakatangazwa na watu wakaondoka zao. Muda wa saa saba usiku tuliyafikisha matokeo ya uchaguzi pamoja na vyombo vya uchaguzi Halmashauri na siku ikawa imekwisha.

CHANGAMOTO ZA UCHAGUZI HUU:

Uchaguzi huu ambao kwa kiasi Fulani uliboreshwa umeonesha kuwa bado watanzania wengi hawajiandikishi kupiga kura kwani wengi hawaoni umuhimu wa serikali za mitaa. Na wengi wa wananchi wala hawajui nini ni wajibu wa serikali ya mitaa.
Pili, wengi hamtaamini lakini ukweli ni kuwa wananchi wengi wa Tanzania hawajui kusoma wala kuandika. Wananchi wengi wamepigiwa kura, huku hili likiwa ni mwanya wa baadhi ya kura kupigwa kwa mgombea ambaye si chaguo halisi la mpigaji aliyepaswa; kwani vyama viliwaandaa vijana kuwadanganya wasiojua kusoma wala kuandika kwa kupigia kura wagombea wa vyama vyao.

Tatu, pamoja na serikali kutoa miongozo mingi ya uchaguzi huu, lakini uchunguzi binafsi unaonesha kuwa vyama vya siasa havikushirikishwa kwa dhati. Kwa mfano utakuta Msimamizi Msaidizi unalumbana na wagombea na wapenzi wao kutokana na hali ya wao kutokujua taratibu za uchaguzi. Kuna haja ya makabrasha yote ya uchaguzi kugawanywa kwenye vyama vyote ili viweze kuyatumia kwa kuyasoma na kuwafunza wafuasi wao na hata wagombea wao. Hili likifanyika, tutapunguza sana mizozo inayoibuka ama hisia mbaya na potofu za kupendelea zinatojitokeza kwa wasimamizi.

Nne, ni wazi kuwa kutokujitokeza kwa wapiga kura wengi kunatokana na Serikali za Mitaa kutokuwa hai vya kutosha. Sehemu nyingi serikali za Mitaa imebaki jina zaidi na si vitendo ndio maana watu wengi hawajui umuhimu wake.

Tano, kutokana na kukuwa kwa demokrasia nchini mwetu, umefika wakati watu kufundishwa kuaminiana hata kama mtu mmoja yuko chama pinzani. Uchaguzi wa Kaloleni ulikuwa umejaa kutokuaminiana miongoni mwa vyama viwili; na pia ni vyema misingi ya kidemokrasia ya kushindwa na kushinda ikafundishwa zaidi kwani bado kuna watu wanaoamini kuwa katika kila kinyang’anyiro lazima washinde tu.

Sita, hatua ya chama cha CCM kuweka pingamizi dhidi ya wagombea wa Chadema katika eneo nililokuwa nalisimamia ilileta picha kuwa CCM ilitaka wagombea wake watangazwe washindi bila uchaguzi kufanyika. Sidhani na wala siamini ni sahihi kutegemea zaidi ushindi wa mezani kwani mara nyingine tunaweza kuwa na viongozi waliopendekezwa tu na wanachama Fulani na wala si wakazi kwa maslahi yao. Pia ningedhani kuwa ni vyema kama mgombea aliyebakia ni mmoja basi iwepo ile sheria ya “proportional representation” yaani uwiiano,kura zipigwe na mgombea ashinde kwa kufikia kiwango fulani cha kura ndipo atangazwe halali ni mshindi. Naamini tabia ya kupenda kupata kiongozi aliyepita bila kupingwa si demokrasia makini bali ni “primitive politics” au siasa za porini. Ni lazima kila kiongozi katika jamii ya kidemokrasia achujwe kwa wapiga kura wake na wala si tu kupitia chama chake.

Jambo la saba, kuna haja ya wanasiasa kutenganisha nafasi ya wanasiasa na watendaji wa serikali katika chaguzi zetu. Kwa mfano, wasimamizi wa uchaguzi wanapata shida sana kutokana na mibinyo ya wanasiasa na hata wapenzi wa vyama vya siasa. Wanasiasa wa CCM katika ngazi za chini wanaamini kabisa kuwa Afisa Mtendaji wa Kata au Mtaa ni Kada wa chama kitu ambacho si sahihi. Wanaamini kabisa uwepo wa Afisa huyu ana wajibu wa kuweka mazingira mazuri ili washinde. Haya ni mawazo ya watu wasiosoma, wenye mawazo ya kale “primitive thinking”.

Kutokana na hali hii, pia upande wa vyama vya upinzani, wao wanaamini kuwa maafisa wa serikali wanaosimamia uchaguzi ni sehemu ya Chama Tawala na hivyo si rahisi watende haki. Hali hii inasababisha mikwaruzano mingi isiyo ya lazima. Kuna haja ya serikali na hata asasi mbalimbali kuliweka hili vizuri. La sivyo bado tutabaki tukifikiri katika mitizamo ya Chama kushika hatamu kitu ambacho kilishapitwa na wakati.

Jambo la nane, ni vyema wakati wa kuandaa karatazi za kupigia kura, basi kwa upande wa wajumbe, kuwe na karatasi za kupigia kura kwa idadi ya wajumbe badala ya kuweka majina yote ya wajumbe katika karatasi moja. Hii itarahisisha zoezi la kuhesabu kwani muda mwingi ulitumika sana katika kupata idadi ya kila kura za mgombea kutoka katika karatasi moja. Ni vyema hapa pakawa na karatasi tano zilizo tupu anapewa mpiga kura na yeye mwenyewe anazijaza kwa kuweka majina ya wagombea anaowataka kwa Wajumbe na kwa Viti maalum. Kupigia wajumbe kwenye karatasi moja kumefanya zoezi la kuhesabu kuwa gumu na la muda mrefu.

Jambo la mwisho, ningewashauri wale wote wanaofanya mafunzo ya utafiti wajaribu kuandika tafiti zao juu ya Serikali za Mitaa kwani panahitajika marekebisho mengi sana kiutendaji ili Serikali za Mitaa ziweze kuwa kweli kioo cha jamii katika maendeleo yao. Sehemu nyingi nchini bado Serikali za Mitaa ziko chini sana kiutendaji. Hili ndilo linalochangia kwa wananchi wengi hadi leo hasa wasomi hawajui ni nini umuhimu wa serikali za Mitaa.

MWISHO
Kwa nilivyoeleza hapo juu, hiyo ndiyo picha halisi ya kimbembe cha uchaguzi katika Kata ya Kaloleni. Kama matokeo yanavyoonekana, ni wazi kuwa sasa vyama viwili: CCM na Chadema vitaongoza mtaa mmoja kwa mmoja. Kama Mtendaji nasubiri nione ni changamoto zipi za kiuongozi na kiutawala zitajitokeza katika kufanya kazi na serikali ya Mtaa ulio chini ya Chama cha Upinzani.

Kama mfanyakazi wa serikali ambaye nina uelewa wa taratibu za kiserikali za utawala bora naamini shughuli zitatekelezeka kama tutafuata misingi ya kidemokrasia. Ni imani yangu kwa watu wengi hawaamini itakuwaje ila naamini kwa kuzingatia sheria na kwa kuzisimamia sheria bila kuzipindisha, mambo yatakwenda shwari.

Thursday, October 22, 2009

Vyama tawala Africa ni wizi mtupu.

Wednesday, October 21, 2009

UCHAGUZI WA SERIKALI ZA MITAA -2009 UMEDODA

Jumapili, tarehe 25th October 2009, ni siku ya uchaguzi wa serikali za Mitaa hapa nchini Tanzania. Nataka nitoe tathimini fupi tu juu ya zoezi zima hili kabla ya siku ya uchaguzi. Niseme tu, tathmini yangu inaanzia tangu siku ya kujiandikisha miongoni mwa wapiga kura. Nitaonesha ni nini hasa chanzo cha tatizo la wananchi wengi kutojiandikisha na pia ni jinsi gani vyama vya siasa vimeandaa wagombea wao pamoja na kasoro kadhaa ambazo zitachangia tuchague viongozi bomu miongoni mwa wagombea tunaopaswa kuwachagua mwaka huu.

Mosi, kwa uchunguzi wangu, wananchi wengi hawakujiandikisha kabisa katika zoezi la kuchagua viongozi wa serikali ya mitaa. Hali hii haijashangaza kabisa kwani ni wazi watanzania wengi sana hasa wasomi hawaelewi kabisa ni nini maana na wala umuhimu wa serikali za Mitaa. Wala hawajui wajibu wa serikali za mitaa na ndio maana wengi wa wananchi hawakwenda kujiandikisha na wala hawana mpango wa kupiga kura.

Pili, kuna sababu nyingine ambayo ni ya msingi sana inayochangia wananchi wengi kutozingatia wala kutokupenda kutegemea ofisi ya serikali ya mtaa. Ukiangalia, kwa kupitia mazoea ya utendaji kazi katika Halmashauri mbalimbali hapa nchini, ni wazi serikali za Mitaa ni hafifu sana hapa nchini Tanzania; na kwa uhalisia Ofisi hizi zinaendeshwa kienyeji sana kwa kutozingatia taratibu za “Utawala bora” huku rushwa ndogondogo zikibakia kama ndio tegemeo kuu la watendaji wakuu wa Ofisi hizi.

Tatu, labda nitoe mifano michache hapa: nenda Ofisi za Vijiji au Kata pamoja na Mitaa, hapa utawakuta maafisa mbalimbali ambao wameajiriwa na serikali za Mitaa kupitia halmashauri mbalimbali hapa nchini. Kwa mfano, kuna Maafisa Watendaji wa Kata na Mitaa ambao ndio waratibu wakuu wa shughuli za serikali katika Mitaa na Kata. Wapo maafisa waratibu wa elimu, maafisa afya, maafisa kilimo, na maafisa maendeleo ya jamii. Lakini katika Ofisi hizi nyingi hapa nchini ukijiuliza kama kweli maafisa hawa wanafanya kazi zao kwa kuwajibika au la, unapata jibu kuwa hamna kitu. Ni wizi mtupu nchi hii. Mara nyingi maafisa hawa wako pale kwa ajili ya kuibia serikali fedha kupitia mishahara bila kufanya kazi.

Ninasema hivi kwani kiutaratibu ili wananchi waweze kuona thamani “value”, ya serikali za Mitaa ni kupitia shughuli ambazo maafisa hawa wanapaswa kushirikiana na wananchi katika utekelezaji. Uzoefu na uchunguzi wangu umenionesha kuwa wananchi wengi hawajui kabisa ni nini wajibu wa maafisa hawa katika Kata au mitaa yao. Kuna pia utaratibu wa kuitisha mikutano ya hadhara kwa kila Mtaa ama Kijiji, lakini utashangaa, hakuna juhudi zozote zinazofanyika kuhakikisha taratibu hii inafanyika.

Changamoto kubwa hapa inakuwa ni kuwa hata wananchi huwa hawapatikani katika kuhudhuria mikutano hii. Lakini pia hata pale wananchi wanapopatikana, maafisa hawa hawako tayari kuhudhuria kwani huwa hawalipwi marupurupu ambayo wangestahili kwani hii huwa ni kazi nje ya muda wa kazi na hasa siku za wikendi. Kwa hili ni dhahiri kuwa Halmashauri nyingi hapa nchini pamoja na kuwa zinasifiwa kwa kufanya mikutano ya hadhara, mara nyingi mikutano hii haifanyiki na inaandikwa mihutasari ya gagari na kuonekana kama vile inafanyika. Na ndio maana hadi tunapofanya uchaguzi huu unakuta kuwa wananchi wengi wala hawana habari na Serikali za Mitaa.

Kwa ufupi ni kuwa kuna haja kubwa kwa serikali za mitaa kuamka hasa kwa upande wa watendaji wa sekta hii kwani kama hali itaachwa hivyo, basi tusishangae hali hii ya kutojitokeza katika kupiga kura itaendelea.

Jambo la nne ambalo lazima niliweke wazi: nimejionea kasumba fulani ya chama fulani kujitokeza katika kuwawekea pingamizi wagombea wa vyama vingine na kujaribu kung’ang’aniza uchaguzi huu uendeshwe ukiwa na mgombea mmoja tu wakiamini kuwa angelitangazwa kuwa hana mpinzani na hivyo kuwa ni mshindi. Kasumba hii kama itaachwa tu iendelee basi ni wazi bado nchi yetu ina watu ambao bado wana mawazo ya chama kimoja na kwao demokrasia ya ushindani hawaitaki kabisa. Pia hata waliotunga kanuni za uchaguzi huu ni lazima waipitie tena kanuni ya wagombea kwani imedhihirika wazi kuwa hawakuzungumzia nini kifanyike pale ambapo mgombea anapobakia ni mmoja kama wengine wakijitoa. Hili nimeliona kwani nadhani kidemokrasia si sahihi kwa mgombea kutangazwa mshindi wakati hajapigiwa kura.

Kwa mantiki hiyo, naamini uchaguzi huu tutapata wagombea ambao hakuna ushahidi wa dhati unaoonesha kukubalika kwao miongoni mwa wananchi watakaowaongoza. Nasema hivyo kwani naamini kulihitajika iwapo mgombea ni mmoja, basi apigiwe kura na kuwe na kiwango ambacho atastahili akifikie ili aonekane anakubalika kuwa mshindi. Hii habari ya kusema eti huyo amepitwa bila kupingwa kwa kiasi fulani ni dhihirisho kuwa nchi yetu bado tuna tatizo la kufikiri sahihi na kwa mantiki. Kwa maelezo yangu kwa hili, uchaguzi wa serikali za mitaa wa mwaka huu utazalisha viongozi haramu kwa kiasi Fulani kwani inawezekana kabisa mtu akatumia ama nguvu za fedha au vitisho vya ushirikina ili achaguliwe kilaini bila kupigiwa kura kwani wale ambao wangeweza kujaribu kupingana naye wataogopa. Na hii si demokrasia.

Pia nimeshuhudia kuwa vyama vya upinzani pamoja na kujua kuwa uchaguzi huu ulikuwepo, vimekurupuka sana katika kuweka wagombea wanaofaa. Sehemu kadhaa nimeona wagombea waliowekwa ni wa kuokoteza tu, si watu makini ambao wana uwezo wa kuongoza. Ni dhahiri, vyama vya upinzani vikiendelea na hali hii basi vitakuwa kama chanzo cha demokrasia ambayo haina tija. Haiwezekani watu wanaokotezwa tu, watu ambao jana tu walikuwa hawana itikadi yeyote leo wanakuwa na itikadi fulani na wanapewa uongozi. Huwezi kwenda kumuokota mpiga debe katika vituo vya mabasi au jitu lisilokuwa na shughuli yeyote ya maana zaidi ya kuendesha shughuli zinazojulikana kama “mission town” kuwa mgombea katika zama hizi licha ya kuwa kila mwananchi ana haki ya kugombea na kuchaguliwa. Tunavyolifanya hili ni dhihirisho kuwa vyamba vyetu vya siasa bado vina tatizo. Hili nimeliona sana katika vyama vyote vya upinzani na nadhani kama kweli tutakwenda hivi basi tusishangae uchaguzi huu hautakuwa na tija tarajiwa.

Si vyama vya upinzani tu, Chama tawala nacho kimeonesha mapungufu sana katika zoezi la kuweka wagombea. Chama hiki bado hakijafika mahali kikaona kuwa uchaguzi ni wakati muafaka kuleta mabadiliko. Kwa chama hiki, hata kama aliyekuwa kiongozi wao alikuwa mzembe na asiye mtendaji bora, wao hawakuchuja. Ule mfumo ambao ulisifiwa kuwa ni wa uwazi kupata wagombea umechezewa. Kura za maoni katika chama hiki ziliendeshwa kienyeji. Kadi za chama hiki ziligawanywa kama njugu huku kila mgombea akizinunua na kuzigawa kwa wapiga kura ambao aliamini wangemchagua. Ni kwa mtizamo huu bado unaona hata chama tawala bado hakijakuwa na mfumo bora na wa kisayansi kupata wagombea.

Kwa ujumla, vyama vyote, vile vya upinzani na mtindo wa kuokoteza wagombea pamoja na CCM kuendesha zoezi la kura za maoni lisilo la kisayansi wameboronga katika kupata wagombea bora. Hapa simaanishi kuwa wagombea wote si bora ila kuna mwanya mkubwa wa kuwa na wagombea bomu katika uchaguzi wa serikali za Mitaa mwaka huu. Uchaguzi wa mwaka huu basi uwaamshe viongozi wetu kutizama upya uendeshaji wa serikali za Mitaa hapa nchini, na kuzingatia umuhimu wa kuwa na viongozi waadilifu na wenye weledi na akili timamu zinazoendana na alama za nyakati tulizonazo. La sivyo, nchi hii haitabadilika kamwe.

Umefika wakati akina Mizengo Pinda wajue kuwa Serikali za Mitaa zikiendeshwa kwa kujali maafisa wakuu katika ngazi za juu tu katika Halmashauri zetu basi kamwe hata siku moja, wananchi hawatakaa waelewe umuhimu wa serikali za Mitaa. Kwa hali ilivyo sasa, juhudi kubwa za kiuwezeshaji zinalengwa kwa maafisa katika makao makuu ya Halmashauri ambao wao ni kukaa ofisini zaidi na kuhudhuria vikao visivyokwisha na baadaye kutoa amri za utekelezaji kwa simu kwa maafisa wa chini huko kwenye Kata, Mitaa na Vijiji. Maafisa hawa wadogo kutokana na kutokupewa mtizamo chanya kiuwezeshaji ili watekeleze kazi zao mara nyingi wamedoda na hawatekelezi lile wanalopaswa na ndipo hapa wananchi wengi wala hawana habari kama kuna serikali za Mitaa.

Ni wazi kwa mtizamo wangu ambao nimeufanyia uchunguzi na kujiuliza sana kwanini wananchi wengi hawazijali Serikali za Mitaa, ni wazi kuna tatizo la kiutendaji bado katika kuziendesha Halmashauri zetu pamoja na kudhani kuwa tayari tuna mafanikio. Ni lazima tukubali mafanikio tulionayo lakini tukubali pia kuwa kuna changamoto kedekede ambazo ni lazima tuzifanyie kazi na uchaguzi utakaokuja basi watu wawe na ushiriki zaidi ya sasa. Kwangu mimi, kutokujiandikisha miongoni mwa wananchi wengi ni dhihirisho la wazi la utendaji dhaifu, usiokuwa na tija wa miongoni mwa Halmashauri zetu.

Monday, October 19, 2009

MWALIMU NYERERE NA MAFANIKIO

Mwalimu Nyerere kama wanadamu wengine alipata sapoti kubwa sana kwa waliomzunguka hadi kufikia mafanikio. Pia ni vyema kujua je, Nyerere alikuwa mwana wa Africa nzima ama tu ile Afrika kusini mwa jangwa la sahara?
Kama baba wa Taifa alikuwa na mtizamo juu ya hali ya Elimu ya Juu. Alitaka Elimu ya Juu iwe ya kiwango cha juu pia si ya bora liende tu. Si elimu tu, ila alipigania hasa, Uhuru wa Mwafrika.

MWALIMU AWA MTAKATIFU: Kanisa katoliki limeanza mchakato wa kumfanya mwalimu kuwa ni mtakatifu.
Mwisho, yuko bwana mmoja anampenda sana mwalimu, hebu soma barua yake.

Saturday, October 17, 2009

SIKU YA CHAKULA DUNIANI NA VIMBWANGA VYAKE

Ugh! kwa wasomaji wangu, nimekuwa kimya sasa narejea kwa kuwapa machache niyasoayo. Huko Uganda Mambo ya MDGs juu ya Ukimwi, je inawezekana?
Wanasema pia tusishangazwe na Uganda kuendelea kuwa chini ya kutokuwa na amani kwa miaka mingi, ni kuwa chuki ilipandwa tangu wakati wa uhuru.
Pia kwa kuwa jana ilikuwa siku ya chakula duniani, ni wazi kuna watu wanapata taabu sana kwani wanahitaji kula vizuri lakini hakuna chakula hasa wale wanaotumia dawa za kuwaongezea maisha.

Kwa wale wanaopenda kuwa na akina dada karibu, ni wakati mtu kujiuliza, unajua makundi ya akina dada hasa katika maeneo ya shule? Huko huko mashuleni, je tunajua maprofesa wanafanya nini?

Sunday, September 13, 2009

TUNAHITAJI "NEW CCM" au "CCM DEMOCRATIC CHANGE".

Tunaishi katika nchi ya Tanzania; nchi inayosifika kwa utulivu, amani na utengamano. Ni nchi yenye historia ya kupitia mfumo wa chama kimoja ambao uliweza kuiunganisha nchi katika nyanja zote za kijamii kwa uzuri ambao nchi nyingi za Afrika hazijaweza na zinatamani. Chini ya sera za siasa ya Ujamaa, watanzania walifundwa juu ya Utaifa unaoegemea mtizamo na matakwa ya Chama tawala. Hii inaweza kuthibitishwa kabisa kupitia kauli mbiu zilizokuwa maarufu enzi za Chama kimoja: “ Kidumu Chama cha ………….., Zidumu fikra za Mwenyekiti wa Chama cha ………….. na mambo mengine mengi ambayo baada ya kurejeshwa kwa siasa za vyama vingi yaliondolewa katika maandishi ingawa katika hisia, imani na itikadi zimebakia mioyoni mwa wengi wa Watanzania hasa walioko katika taasisi zote za serikali.

Kwa msingi huu wa kubakia katika nyoyo zao zile kauli mbiu ambazo nimezitaja hapo awali, ni wazi Tanzania itabakia chini ya mizozo ya kimtizamo kati ya watendaji wengi wa serikali, wabunge na hata wanasiasa kadhaa dhidi ya wazalendo wa nchi hii ambao wana mtizamo wa kisasa katika masuala ya kisiasa na ni jinsi gani nchi inapaswa kuendeshwa hasa kupitia taasisi zake hasa mihimili mitatu: serikali, bunge na mahakama. Labda nipende kuonesha nia yangu kutoa mchango wangu juu ya yaliyojitokeza hivi majuzi hapa nchini Tanzania hususan juu ya Waraka wa Wakatoliki na Kutingishwa kwa Spika wa Bunge la Tanzania juu ya uendeshaji wa taasisi hiyo nyeti ya nchi.

Kilichompata Mheshimiwa Spika naamini ni Ukomunisti uliojikita katika Chama tawala ambapo ingawa mfumo tuliopo ni wa vyama vingi, bado katika akili na mioyo ya viongozi wa chama tawala kuanzia juu hadi ngazi ya chini wanaamini kuwa “Chama kushika hatamu” ndio utaratibu wa kuendesha siasa na utawala wa nchi. Nimekaa na kuwasikiliza baadhi ya viongozi wa chama hiki katika ngazi za matawi wanazungumza kama vile bado Taifa hili liko katika enzi za chama kimoja. Ni kauli kama hizi unazikuta zinatolewa na mtu wa hadhi ya Katibu Mkuu wa Chama hicho Taifa basi unajua wazi kuwa Ukomunisti ndio tatizo.

Ukomunisti ni mfumo wa kidikteta ambao hauruhusu uwazi wala uhuru wa kutoa mawazo. Ni mfumo ambao hautaki mawazo mbadala na unategemea kutoa adhabu kali kwa wale wote wanaokwenda kinyume na maagizo ya chama bila kukaa chini na kutafakari kimantiki. Ni mfumo wa kikundi cha watu ambao kwa kutozingatia kufikiri kwa mantiki hawajali hisia wala imani za kundi lenye mtizamo pinzani. Ni mfumo unaoogopa kuguswa hasa nyakati zinazohitaji mawazo mbadala. Kwa yaliyotokea kwa Spika Sitta, ni kwamba kwa staili yake ya uendeshaji bunge “Spidi na viwango”, haukubaliki katika nchi ambayo watawala wake wote ni wakomunisti na hawajawahi kujaribu kuruhusu demokrasia pana katika chama ama bunge.

Katika mfumo wetu, sishangai kuna watanzania lukuki ambao wana ndoto za kugombea ubunge hapo mwakani. Lakini asilimia kubwa wanataka kugombea kupitia chama tawala na kwasababu tu wanajua na kuamini kuwa ili ufanikiwe kisiasa lazima uwe ndani ya chama hicho. Wanajua kuwa kwa uwezo wao wa kuhoji wakiwa ndani ya upinzani hawatapata suluhisho ya hoja watakazoibua na sana sana wakijaribu kupambana watabakia kupewa adhabu za kusimamishwa kuhudhuria vikao kadhaa. Wameamua wabaki huko tu kwani hawana ujasiri wa kuleta mabadiliko kwa kuyatetea hadi mwishoni. Wengi wao hawawajui watu kama Lech Walesa.

KWA NINI TUNAHITAJI CCM MPYA?
Najaribu kuchambua mtizamo wa Chama tawala juu ya mwenendo wa Spika wa Bunge eti anashabikia na anakigawa na kukiharibia chama tawala kwa kugawa serikali na bunge utadhani serikali na bunge ni chombo kimoja hivyo hafai. Eti Spika ameshindwa kuwa refa ila anaungana na wachezaji wa timu Fulani kugawa chama. Pia Spika anaonekana kuwa anatumia mfumo usiokuwepo popote pale duniani wakati Bunge letu linapaswa kuegemea mfumo wa Westminster kutoka Uingereza. Spika Sitta anatishwa na anafyata. Kama ni kweli hili lilitokea na akaomba msamaha kwa kuogopa kuvuliwa uanachama ni wazi Spika Sitta anataka kuturudisha kule tulikokwishatoka; yaani kuturejesha kwa bunge mamluki wa chama tawala.

Hivi kama Spika Sitta anaogopa kunyang’anywa uanachama wa CCM, kwani hiyo itaathiri vipi juhudi zake za kuendesha bunge la “Kasi na Viwango”? Kwani ni lazima awe mwanachama wa CCM ndio awe Spika? Ni kweli ni lazima awe mwanachama kwani kwa kuegemea mfumo wa Westminster, chama chenye viti vingi kinatawala kila mwelekeo wa bunge hilo. Na ni kawaida kuwa kama mbunge wa chama chenye viti vingi akienda kinyume na maagizo ya chama chake basi lazima aadhibiwe. Hii ndio kanuni ambayo NEC imeitumia kumtwanga rungu Spika Sitta pamoja na kuwatisha wabunge ambao wamekuwa mwiba kwa chama chao.

Katika mfumo wa Westminster, wabunge ambao wanakiuka maagizo ya Chama basi watakumbwa na kufukuzwa uanachama am mara nyingine wataadhibiwa kwa kunyimwa uteuzi katika chaguzi zitakazofuatia kama wagombea kwa tiketi ya chama chao. Ndio maana ni wazi kuwa katika uchaguzi ujao, lazima tushuhudie baadhi ya wabunge machachari wa chama tawala wakiwajibishwa kwa ama kufukuzwa uanachama au kunyimwa uteuzi kugombea tena majimboni mwao.

Kwa kutizama utendaji wa Samwel Sitta, ni wazi ameruhusu uhuru ambao unaendana na katiba ya Jamhuri ya Muungano ibara ya 100 inayoruhusu Mbunge kuchangia bila kuhojiwa kwa alichosema. Waliotunga katiba hii walijua kuwa pamoja na kwamba tunafuata mfumo wa Westminster lakini uhuru wa kusema ni jambo la msingi zaidi. Kwani kama tutaegemea zaidi kama mfumo huo wa kifalme wa Uingereza unavyotaka basi tusishangae chama Fulani kinaweza kutekwa na kikundi cha maharamia na kutumika kama rungu dhidi ya wale wanaotetea maslahi ya umma. Hapa sina maana kuwa CCM inatumiwa na watu Fulani lakini mtanzania yeyote anaweza kuona kuwa wabunge kuruhusiwa kuzungumza kuhusu Rais mstaafu, kashfa ya Richmond kwa uwazi ndio chanzo kikuu cha spika Sitta kuonekana kama anakidhalilisha chama. Na ndio hapa nalazimika kuhoji je maslahi ya umma ndio lengo la CCM ama ni maslahi ya wale ambao ni vigogo wa chama lakini wanahusishwa na kashfa hizi?

Ni wazi kwa hatua tuliyofikia kwa sasa kisiasa hapa nchini tunahitaji mabadiliko makubwa ndani ya Chama tawala. Nina wasiwasi CCM imejaza viongozi na makada waliopitwa na wakati. Panahitajika “CCM MPYA” – NEW CCM, au CCM DEMOCRATIC CHANGE; chama ambacho kitakuwa na viongozi wenye utashi wa kusimamia maslahi ya umma na si ya kibinafsi. Chama ambacho kitakuwa tayari kuwabana viongozi wake ama makada wake watakapojihusisha na ufisadi wa aina yeyote. Chama ambacho kitaruhusu uhuru wa mawazo “divergent views” kwa kuzingatia hoja za kimantiki bila ubabe ama zinazokosa mashiko kwa mtanzania wa kileo ambaye ameelimika na anaelewa pale anapodanganywa au anapopewa jibu la kisiasa lisilojali kuwa kila mwanadamu ana uwezo wa kufikiri.

Viongozi wa CCM MPYA au CCM DEMOCRATIC CHANGE wapo ila wanakosa ujasiri wa kujitoa mhanga. Kwa mfano, Spika Samwel Sitta kuonywa na kutishiwa na Chama chake ni wazi mienendo yake na hata jinsi anavyofikiri si kama vile chama chake kinavyotaka Kada wa hadhi yake atende na kufikiri. Hilo analijua wazi; wapo wengine kama Harrison Mwakyembe, Selelii, Mpendazoe na hata Injinia Stella Manyanya si watu ambao wanaendana kimtizamo na CCM ya Kikwete. Ni watu wanaostahili katika kile ninachokiamini kuwa ni CCM MPYA au CCM DEMOCRATIC CHANGE. Ni watu ambao wangetegemewa kuleta itikadi mpya za kisiasa ndani ya chama, itikadi zinazoenda na wakati tulionao; yaani zinazozingatia misingi ya kidemokrasia, haki za binadamu na utawala bora. Ni wanasiasa wanaojali na kujua kwa dhati kuwa hizi ni enzi za uwazi, na uwajibikaji wa dhati kwa kila kiongozi bila kujali cheo cha mtu pale anapokosea. Ni wanasiasa wanaojua na wana dhamira kwa kiasi fulani kubadili mtizamo wa watanzania juu ya suala zima la demokrasia.

Ninaposema CCM MPYA au CCM DEMOCRATIC CHANGE, naamini kuwa tatizo linaloizuia kutokea ni ile hali ya makada wale makini kukosa dhamira ya dhati katika kuleta mabadiliko ingawa wanatamani yaje labda kimiujiza. Matokeo yake wanaendeleza hali iliyopo “status quo” kwa woga wa maisha yao na hata mali zao au mipango yao kuvurugwa na rungu la dola. Ukosefu huu wa dhamira ya dhati uko wazi kwani kama mtu unafuatilia baadhi ya wale wanaojitahidi kupiga kelele juu ya ufisadi, utashangaa mtu analalamika sana dhidi ya maswahiba wa kiongozi fulani mkubwa kuwa ni mafisadi na hapo hapo wanamaliza kwa kusema wanamwamini huyo kiongozi mkubwa kama kinara wa vita dhidi ya ufisadi. Kama wataacha unafiki ndani yao, basi naamini CCM MPYA itatokea.

Ninaona hitaji la CCM MPYA au CCM DEMOCRATIC CHANGE lakini niulize kuwa ni nani anayekiongoza Chama hiki kwa sasa? Mimi nina mashaka kwani inaonekana wazee wastaafu na wenyeviti wa Mikoa ndio madereva. Wengi wao ni wazee wa zidumu fikra za……….. Ndio maana tumeona wakiongoza juhudi za kumkaripia Samwel Sitta bila kuzingatia kuwa kikatiba Sitta amekuwa akizingatia haki ya kila mbunge kusema kwa uhuru. Wenyeviti hawa na wazee wengine wa enzi ambao ndio watoa ushauri wakuu kwa viongozi wa sasa wa chama ni watu wanaotumia sera za kikomunisti kama alivyotukumbusha Muadhama Kadinali Pengo; sera zenye kujali maslahi ya kimakundi na si yale ya jumla “ common interests”. Ni wazee ambao hawana tofauti na Robert Mugabe kwani wao hawajui kuwa kwenye siasa kuna wakati chama kinaweza kushindwa uchaguzi. Kwa stahili ya Mugabe ni wanasiasa ambao wanaweza hata kutumia mabavu na ushawishi hasi kuhakikisha wanatibua juhudi zozote za kuleta mabadiliko katika Taifa.

Labda niseme zaidi kuwa sasa tusubiri kuona Bunge la viwango na kasi likibadili gia na litarudi kwa staili ya enzi za akina Adam Sapi na Pius Msekwa. Kipindi ambacho Bunge lilijali zaidi matakwa ya Chama tawala hata pale inapokuwa maslahi ya umma yanachezewa kwa kufunika kombe mwanaharamu apite.

JE SPIKA ANAWAJIBIKAJE KWA KUFUATA SERA ZA CHAMA CHAKE?

Ni wazi kwa mkwara aliopigwa hivi majuzi, NEC ya CCM kwa kiasi Fulani iliegemea zaidi kwenye utashi wa Chama na kusahau kabisa ni nini wajibu wa Spika wakati anapokuwa bungeni. Kwa maamuzi na matamshi ya viongozi kadhaa wa Chama, imani iliyojengeka ni kuwa Spika maadam anatoka chama tawala basi ni lazima kwa gharama zozote zile atetee chama tawala hata kama ni kwa kukiuka na kuminya haki za kimsingi za wabunge anaowaongoza.

Spika Sitta ameonekana kuwa ni mshabiki wakati wa majadiliano; mimi sidhani ni sahihi kusema hivyo. Kwa mujibu wa jukumu la spika, ni lazima aunge mkono yale yote ambayo yana tija kwa maslahi ya jamii kwa ujumla. Hili nadhani ndilo amekuwa akilivalia njuga kwa kuegemea zaidi misimamo na mitizamo ya kikundi Fulani cha wabunge ndani ya mjengo. Ningetarajia malalamiko ya NEC yawe kuwa Spika Sitta alivunja taratibu za kuongoza bunge basi labda waziainishe. Kwa mfano, Spika anawajibu kadhaa kama:

Mosi, ni mwenyekiti wa mijadala kwa kuhakiksha taratibu za kibunge zinazingatiwa. Hapa inajumuisha kuchagua ama kuwaita wabunge watakaochangia mijadala. Katika hili ni lazima Spika azingatie anawajibika kutunza maslahi ya wachache (minorities) ndani ya Bunge. Pili, kama mwenyekiti, atazingatia maslahi ya makundi mbalimbali ya kijamii kama vile mambo ya majimbo, ni mada gani inayojadiliwa na maslahi ya jumla kwa usawa kadiri wabunge wanavyojitokeza kuchangia. Katika kutekeleza haya, wabunge nao wana wajibu kumtaarifu Spika juu ya nia yao ya kuzungumza katika mjadala Fulani ingawa uamuzi wa mwisho unabaki kwa Spika huku akizingatia hajavunja sheria ama kanuni za bunge. (Speaker’s discretion). Hapa namaanisha si kazi ya NEC kuamua Spika awaruhusu au awazuie akina nani kuchangia.

Tatu, Spika anawajibika kuzingatia busara kwa uangalifu wa hali ya juu (discretion) katika matukio mbalimbali wakati wa mijadala. Kwa mfano, wakati wa mbunge kuwasilisha ombi la kuwasilisha muswada binafsi, kuruhusu maswali ya lazima, kuelimisha au kukumbushia wabunge juu ya angalizo la kuzingatia kanuni na hata wakati inapotakiwa kwa mtu kufuta kauli.

Nne, Spika anawajibika kuzilinda haki za wachache juu ya mawazo yao (opinions) hata kama maoni hayo ni ya kuumiza ama kugusa hisia dhidi ya serikali (executive) ama kikundi cha watu fulani. Hapa kama kuna haja ya kushurutisha mjadala ufungwe pia ni wajibu wa Spika kujua ni wapi azuie kuendelea kwa mjadala. Haya ni baadhi ya machache tu kuonesha ni jinsi gani Spika ana mamlaka ya kiutendaji wakati wa mijadala kule bungeni. Inawezekana kabisa, kwa kuzingatia madai ya NEC kuwa Spika Sitta ni mshabiki wa baadhi ya mijadala inayoletwa na kikundi Fulani cha wabunge basi moja kwa moja anazingatia uhuru ambao anao katika kusimamia mambo kule bungeni hasa katika kulinda haki za kila mbunge bila kuathiri uhuru wa mbunge yeyote.

JE NEC INAJUA SPIKA WA BUNGE NI NANI?

Kwa mujibu wa tamaduni za mabunge ya Jumuiya ya Madola, mara baada ya mwanachama yeyote wa chama Fulani cha siasa katika nchi za jumuiya ya Madola anapochaguliwa kuwa Spika, basi anapaswa na kuwajibika kubakia mtu huru kisiasa asiyeegemea mitizamo ama imani yeyote ya kisiasa (IMPARTIALITY)
kwa kipindi chote cha uspika licha ya kwamba anatoka chama fulani.
Spika ni lazima awe nje ya misuguano yeyote ya kisiasa (political controversy) na asiwe na upande wowote katika masuala yeyote ya umma. Kanuni hii inazingatia uhalisia kuwa wabunge wote katika bunge wanategemea kuheshimiwa na spika katika hali ya usawa bila kujali chama wanachotoka. Bunge lolote lile la staili ya Westminster kama lilivyo la kwetu hapa Tanzania linategemewa kuwa na spika wa aina hii. Inasemekana kuwa dhahiri katika mazingira haya Spika anapochaguliwa kuwa Spika, moja kwa moja anastaafu au anajiuzulu kutoka Chama chake cha Siasa ingawa anabakia na majukumu yake ya Ubunge. Hii kwa nchi ya Chama tawala kama tulichonacho, bado hatujafikia hatua Spika anajiuzulu Ubunge wake kama wenzetu wanavyofanya nchini Kenya. Tungekuwa tumefika hapo, basi moja kwa moja bunge lisingedhibitiwa na chama tawala kama ilivyo sasa kwa vitisho kwa Spika.

Kwa wenzetu ambao ndio vinara wa mfumo huu wa kibunge “Westminster”, kuonesha umuhimu wa utakatifu wa kiti cha Uspika, pale inapotokea Spika amestaafu baada ya kulitumikia Bunge basi haruhusiwi tena kushiriki katika masuala ya siasa. Kwao, kitendo cha mtu kuwa Spika ina maanisha kuachana na hisia na upenzi wa kimtizamo na kiufuasi ndani ya bunge. Huko nchini Uingereza, katika kuonesha uadilifu wa Spika, ni lazima ajitenge na maswahiba wake wa zamani wa Chama anachotoka, au kikundi chochote au maslahi yoyote. Hapaswi hata kujichanganya na wabunge mara kwa mara kwenye mabwalo ya kulia au baa wakati akiwa spika. Hii ni tofauti na hapa kwetu ambapo mtu atakuwa Spika, wakati huo huo ni mjumbe wa NEC, mwenyekiti wa Bodi ya Shirika fulani na kadhalika. Hapa hakuna utawala bora kabisa kwani natilia shaka sana kama Spika anamaliza muda wake alafu anarejea kuwa Kiongozi wa Juu wa chama tawala kama ni sahihi au la.

Ukiyatizama niliyoyazungumzia hapo juu, ni wazi kuwa wanaomtisha Spika Sitta wamepotoka kwa kiasi Fulani. Wao kwao Spika ni kijakazi wa chama na ni wajibu wake kutetea maslahi ya chama. Ni mazoea ya kipindi cha kale wakati wa udikteta wa chama kimoja. Ndio maana kwa kuonesha kuwa bado tumelala katika lindi la usingizi wa pono kidemokrasia, nimeeleza hapo juu kuwa hushangai kumuona mtu leo ni Spika wa Bunge alafu kesho ni kiongozi mkubwa kwenye chama Fulani cha kisiasa au ni mjumbe wa Bodi ya Shirika Fulani ambalo lina uwezekano wa kufikishwa katika Bunge na yeye asimamie majadiliano bila kuingilia mgogoro wa kimaslahi.

Ni wazi nchi yetu imefikia mahali ambapo tunahitaji kama Taifa tukae chini na tuiunde Katiba yetu upya na taratibu za kuongoza nchi hii ziangaliwe upya. Hili ni tatizo la Ukuu wa Bunge kupokwa na chama cha siasa. Linalokatisha tamaa katika Tanzania ni kuwa tangu kazi ya Uspika ianzishwe chini ya Sir Thomas Hungerford, na hata enzi za “ Mad Parliament” bunge la vichaa enzi za 1258 chini ya Peter de Montfort. Bunge la Tanzania nalo bado halijaweza kupita enzi zote hadi kufikia kuwa Bunge la “Viwango na Kasi”.
Hii inakumbushia enzi za Spika Lenthall karne ya 17 ambapo Spika alikuwa ni kijakazi wa Mfalme Charles I ambapo Mfalme aliweza kuwakamata wabunge watano kutoka bungeni bila Spika kuwa na kauli ya kuwatetea kwa kukiri kuwa yeye ni kijakazi wake. Kuanzia kipindi hicho, “Ukuu wa Bunge ulikufa” hadi nyakati za karne ya Arthur Onslow ambaye anajulikana kama mwanzilishi wa uspika wa kisasa wa aina ya kina Samweli Sitta au Kenneth Marende ambao haujali nafasi ya Chama cha Spika anakotokea na unazingatia zaidi Uhuru wa taasisi ya Bunge mbele ya Serikali na hata Chama cha siasa. Hapa ni wazi wale wote waliomshambulia Samweli Sitta walikuwa hawajui wanafanya nini, na nadhani walikuwa hawajui kuwa Spika wa Bunge ni kiongozi aliyetukuka ambaye sidhani ni sahihi akemewe na mtu wa hadhi ya mwenyekiti wa Chama wa Mkoa.

JE MFUMO WETU NDIO TATIZO?

Pamoja na kuwa nimejadili kuwa “Ukuu wa Bunge Umekufa”, lazima nikiri kuwa mfumo wetu wa kuongoza siasa zetu unaegemea mfumo wa kiuraisi ( Presidential system). Ni mfumo ambao mhimili wa watendaji (executive) wanatawala, na mara nyingi hawalazimiki kuwajibika kwa mhimili wa bunge ingawa hawapaswi kulidharau bunge. Katika mfumo huu, mhimili wa Bunge unakuwa unadhibitiwa na Chama cha Raisi wa Taifa husika. Na kama kuna mbunge atakayejaribu kwa dhati kupingana na hili basi atakuwa anahatarisha kupoteza uanachama wake kama alivyofanyiwa Samweli Sitta hivi karibuni. Pia anaweza kufukuzwa kutoka kwenye chama chake ama pia kutimuliwa kwa aibu.

Kwa kawaida wachunguzi wa kisiasa wanasema kuwa katika mfumo wa kiuraisi “Presidentialism” ni mfumo wa kibabe “ authoritarianism” na kamwe hauheshimu sana katiba katika nchi nyingi unakotumika. Katika za mfumo huu, Taasisi ya Uraisi (Presidency) na ile ya Bunge ( Legislature) zinafanya kazi kwa sambasamba (parallel). Kwa kawaida, mfumo huu unapunguza sana uwezekano wa kiuwajibikaji (accountability). Hapa linalotokea zaidi ni kulaumiana na kutuhumiana kati ya mihimili hii kila kukicha kama tunavyoona wanavyotunishiana misuli katika masuala ya Richmond na Kiwira.

Kwa ujumla, tunavyoona migongano ya mihimili hii miwili ni wazi kuwa serikali haifanyi kazi vyema na kinachohitajika kwa sasa ni mizengwe ya kikatiba ya aina yake ili kuweza kuinusuru serikali dhidi ya makucha ya mhimili wa Bunge. Kwa hili tusishangae baada ya muda mizengwe itafanywa na mambo yatatulia na watanzania tutasahau. Kwa kiasi Fulani jinsi Samweli Sitta anavyoongoza bunge letu, anajaribu kurudisha Ukuu wa Bunge kama mhimili mwenza wa ile mingine ya watawala na mahakama ambayo inapaswa isiingiliane katika utendaji wake.

Kazi ya Bunge ni kuihoji serikali juu ya sheria ambazo Bunge huwa imezitunga. Serikali nayo ni kutekeleza kazi zake kwa mujibu wa sheria zilizotungwa na Bunge. Pale ambapo Serikali inapovunja sheria, basi Mahakama ndiyo huchukua hatua katika kutafsiri sheria. Kwa mantiki hii, NEC ya CCM inadhani wabunge Fulani kupewa uhuru wa kukemea juu ya uvunjwaji wa taratibu na sheria mbalimbali basi wanakiharibia chama. Inawezekana hawajui ni wajibu wa Bunge kuhoji serikali bila kujali maslahi ya chama pale ambapo dhahiri sheria ambazo wabunge wamezitunga hazifuatwi. Na kama wabunge hawa wapinga ufisadi watazibwa mdomo, basi ningedhani ni vyema sasa waende mahakamani wakaiombe mahakama ifafanue sheria zimevunjwaje katika matukio kadhaa kama Richmond, Kiwira, Meremeta, Kagoda na mambo mengi ambayo yameigharimu fedha nyingi nchi yetu bila sababu.

Nimalizie kwa kusema tu kuwa umefika wakati kwa Watanzania kuondokana na mawazo ya kizamani katika masuala ya uongozi na hasa kisiasa kama kweli tunataka utawala bora.








Wednesday, September 09, 2009

KIKWETE - CHARISMATIC LEADER

Jana Raisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliongea na wananchi kwa njia ya mawasiliano ya moja kwa moja. Ni jambo ambalo sikulitarajia hasa ukizingatia tabia na kasumba ya viongozi wa Tanzania wasivyopenda kuwasiliana moja kwa moja na watu na hata waandishi wa habari. Sijui kama kweli ule ulikuwa ni ubunifu wa rais Kikwete au ni ushauri wa akina Tido Mhando lakini tukio la jana linabakia kama kufanikiwa sana kwa Kikwete kujiweka karibu na wananchi.
Rais alikuwa muwazi na mwenye taarifa za wazi kuhusu karibu kila kitu alichoulizwa ingawa kuhusu vita ya mafisadi alionekana kuvitupia vyombo vya uchunguzi na mashtaka mzigo wote wa kuwachukulia hatua mafisadi.
Kwa ufupi mimi nadhani rais alinikuna kwa hatua aliyochukua; amedhihirisha kuwa yeye ni "Charismatic leader".