My Blog List

Friday, January 25, 2008

TANZANIA IMETEKWA NYARA NA CCM

Miezi kadhaa imepita sasa baada ya mwanasaikolojia na mshindi wa nishani ya Nobel kuja na wazo lake kuwa “Waafrika ni dhaifu katika kufikiri ukiwalinganisha na wazungu ama watu wasio weusi”. Si mwingine bali ni daktari James Watson, mtaalam maarufu wa Saikolojia na mgunduzi wa sayansi ya chembe hai ( DNA) nchini Marekani na duniani kwa ujumla. Mawazo yake yalipokewa kwa machungu sana na watu weusi wengi kila kona ya dunia; lakini kwangu nilijaribu kuona hili kama changamoto hasa nikizingati mambo kadha wa kadha yanayotukia hapa nchini mwetu Tanzania na Afrika kwa ujumla.

Naye David Landes kaja na kitabu chake “The Wealth and Poverty of Nations: Why Some are so Rich and Some are So Poor”, akijaribu kutuonesha kwanini waafrika wako nyuma ya wazungu kiuchumi. Tatizo ni utamaduni anadai kwani anasema wazi utamaduni wa mwafrika ni dhaifu ama ni wa kiwango cha chini sana ukiulinganisha na ule wa wazungu. Kwa mfano anadai utamaduni wa mwafrika unakosa vikolezo kama kufanya kazi kwa bidii (hard working), uaminifu (honest), uwazi (open mindedness), na utashi wa dhati katika demokrasia (commitment to democracy)

Landes anasisitiza pia maendeleo ya kiuchumi yanategemea sana hisia (attitudes) za wananchi wake hasa uwezo wao katika kutumia au kutokutumia sayansi na teknolojia na hata fursa za kiuchumi pindi zinapojitokeza. Ni wazi utamaduni una nafasi kubwa sana katika kuendelea ama kutoendelea kwa jamii Fulani. Kwa mfano, Wajapan wanaamini kuwa utamaduni wao ndio chanzo cha mafanikio yao tunayoyaona leo hii. Yoshihara Kunio, kwa mfano ameandika kuwa: “Sababu moja kuendelea kwa Japan ni kuwa ina utamaduni wa maendeleo”. Wajapan wameweka msisitizo katika utafutaji mali (material pursuit), kufanya kazi kwa bidii, kuweka akiba ya siku zijazo( serving for future), kuwekeza katika elimu na kujali jamii (community value).

Tukirejea kwa Landes, anatuonya kuwa kuna tamaduni fulani ambazo ni sumu na mtu akiziamini na kuziishi basi ni umasikini. Kwa mfano, utamaduni wa wazungu/ magharibi ni wa ubinafsi (individualistic) zaidi wakati ule wa kiafrika ni wa kijamii zaidi ama tunaweza kusema kiasili ni utamaduni wa kijamaa unaojali wengi katika migawanyiko ya aina mbalimbali hasa kikabila. Ni katika msingi huu naweza kusema kuwa nadhani ni wazi utamaduni wetu hasa watanzania ni wa kijamii ambao leo hii umehama kutoka ukabila hadi kufikia kikundi cha watu ama jamii kisiasa: namaanisha vyama vya siasa vinavyowakutanisha makabila mbalimbali yenye maslahi yao ikiwa ni pamoja na kuing’ata nchi yetu bila huruma.

Kwa mfano, watanzania na waafrika kwa ujumla wao wamekuwa wakiamini ni lazima watumikie maslahi ya makabila yao. Hali si Kenya tu ila hata hapa kwetu mambo ni hayo tu. Katika kutumikia maslahi ya kikabila ndipo kwa mfano watanzania tunajikuta tukijirudisha nyuma sana kimaendeleo. Utamaduni huu mara nyingi hauruhusu kukosoana hasa pale viongozi ama wakuu wa kaya ama makabila mbalimbali wanapokiuka taratibu za kijamii. Kwa kawaida, wakuu wa familia ama jamii za kiafrika mara nyingi hawaadhibiwi; hakuna mfumo wa udhibiti kwao. Hawa ni sawa na miungu watu wanaotenda visivyo bila kuadhibiwa (impunity).

Maadam waafrika na watanzania tuna kasumba ya kutumikia jamii ama makabila yetu zaidi, basi leo hii tabia hii imejipenyeza hadi katika sehemu za kazi. Angalia hata siasa zetu sasa zimegeuka kuwa ni watu ndani ya vyama mbalimbali kama kikundi kwa maslahi yao na wala si maslahi ya pamoja (common interests) kama ilivyo Japan. Ni katika hili ambapo suala “uzalendo” limekufa na sasa ni maslahi ya kivikundi. Kwa mfano, unaposikia Taifa linakumbwa na upotevu wa fedha nyingi alafu serikali kuanzia Raisi hadi mawaziri wanashindwa kuweka mambo wazi juu ya wapi Gavana Ballali anakotibiwa, basi mtu unapata picha ni jinsi gani serikali ya CCM haiko tayari kuwa wazi kwa suala hili.

Hii yote ni kuonesha jinsi gani utamaduni wa kutoadhibu ama kutowajibisha wakuu wa kaya ama makabila ya kiafrika unavyoitafuna nchi yetu. Ni utamaduni wa karne kadhaa zilizopita ambao CCM inahakikisha utadumishwa ili watu fulani waitafune nchi yetu kwa maslahi yao na chama chao. Ukienda Bungeni na jinsi ambavyo hadi leo hii tangu kashfa ya BOT iibuliwe hakuna mbunge wa CCM aliyethubutu kusema jambo kuonesha kukerwa na hili. Nasubiri nione jinsi watakavyojiuma huko bungeni kuanzia wiki ijayo watakapokuwa wanachambua uchunguzi wa ripoti ya uchunguzi wa kashfa ya Richmond.

Tuna tatizo kubwa kitaifa: yaani mentalite (fikra) za viongozi wengi wa Tanzania ni mzigo mkubwa kwa Taifa. Kizazi cha uongozi cha sasa ni balaa kubwa sana kwa taifa hili kwani hawana tofauti sana na mababu zetu zamani enzi za ukoloni ambao hawakujua kufikiri kwa dhati. Naamini kama Rais Kikwete atatawala kwa miaka kumi basi utakuwa ndio mwisho wa mawazo mgando. Siku za kizazi cha mawazo mgando zinahesabika; kizazi kipya cha sasa chenye mawazo ya kisasa ya kuivusha nchi kutoka umasikini kinakuja taratibu. Ni kizazi ambacho kinawaza zaidi “utaifa” na si maslahi binafsi kama akina Balali na wenzake ambao wanajifanya wametengua uteuzi wake ilihali wengi wao ndio chanzo cha madudu aliyoyafanya.

Ninasema haya kwani hata yaliyotukia Kenya situ ni ukabila bali ni utamaduni huu wa watu katika vikundi vyao vya kikabila na kisiasa wanang’ang’ania madaraka ili kulinda maslahi yao. Chunguza kashfa kubwa kama Goldernberg alafu kama unalijua kundi la “ Mount Kenyan Mafians” ujiulize kwanini Kibaki anang’ang’ania madaraka? Ni hii tabia ya makundi fulani ya viongozi wetu ambao wataiibia nchi huku wakilindwa na wabunge wa chama chao dhidi ya ufisadi wao; kwani kwao bunge ni muhuri (rubber stump) wa kupitisha uchafu wao kwa maslahi yao. Ni tabia kama hii naiona ndani ya CCM ambapo ‘kupitia wingi wa wabunge wao ni wazi Tanzania imetekwa nyara na CCM’.

Kama kweli CCM kingekuwa ni chama cha kuiendeleza nchi yetu basi leo hii hizi kashfa za BOT, Richmond, Buzwagi zisingechukua muda na kutumia muda mrefu bila wahusika kuchukuliwa hatua za kuwajibishwa namna tuonavyo leo. Chama chochote kinapokubali kutumika kama muhuri wa kupitisha wizi na utapeli wa baadhi ya watawala basi ujue ni kwa ajili ya utamaduni mbovu wa kiafrika umekimeza.

Na kwa maana nyingine ni kuwa uwezo wa kufikiri wa wengi walioshikilia hatamu za chama hicho ni mdogo kama alivyosema daktari Watson anavyomwona mwafrika. Jamii kama hii haishangazi hata kidogo sera za kishikaji zinawekwa mbele sana; na jamii hii kufikia maendeleo ya kweli ni vigumu sana ukiacha maendeleo ya wachache wenye mashiko ya kikabila, dini, rangi na kisiasa hasa ukada wa chama. Ni kwa msingi huu naiona Tanzania, nchi yangu kama Taifa lililotekwa nyara na kikundi cha watu Fulani wachache lakini wanaoungwa mkono na watu wenye wajibu wa kuwawajibisha lakini hawataki. Hawa ni wabunge fulani ambao ama kwa makusudi kabisa ama kwa ufinyu wa kufikiri kama ule aliouelezea Dr. Watson basi wanaamua kuhakikisha Mafioso wa Tanzania wanashamiri.

Ni wazi CCM ndio pekee kwa uwingi wa wabunge wao wakiamua wataisafisha nchi yetu na kupambana na mafisadi wa Taifa hili. Mafisadi wengi wa nchi hii ni wanachama wa chama hicho; na ndio hapa pagumu kutegua kitendawili. Mungu wangu: mara nyingine mtu unajuta kuzaliwa katika Taifa lisilopenda kufikirisha bongo ilihali likijiita eti ni Bongo land.

No comments: