My Blog List

Thursday, March 16, 2006

MKAPAISIM--LEGASI YA AWAMU YA TATU

Mimi ni mmoja wa watanzania wachache sana ambao wakati JK anaingia madarakani sikuwa namwamini kabisa. Unajua nimezaliwa nikakuwa nikiona wanasiasa wa CCM wakituongoza kwa migengwe ya kila aina. Ndio maana niliwahi kuandika JK Anatania tu. SOMA
Kama nilivyosema katika makala ile, kuwa JK anawafahamu walarushwa waliojikia mizizi ndani ya dola. Na nikahisi ataendeleza sera ya kulindana ya aliyemtanglia, mheshimiwa Mkapa. Nafurahi kusema kwa ninayoyaona sasa, JK kadhihirisha kuwa nilikosea. Kwa kiasi fulani ninaanza kuona Kasi Mpya. Na hii ni wazi kwangu ni juu ya suala la “Ujambazi”.
Ninasoma habari jinsi ambavyo serikali imewavalia njuga baadhi ya matajiri ambao wanalea majambazi nikafurahi sana. Imani yangu imeanza kumea kwani nataka niseme baadhi ya matajiri waliokamatwa ni watu ambao wamekuwa wakitawala tetesi kuwa ni majambazi tangu nikiwa mtoto nasoma shule ya msingi. Kwa hiyo mimi nimefurahishwa na hatua ya serikali.
Labda nimkumbushe kamanda Saidi Mwema kuwa tafadhali hakikisha dola inajua shughuli za wenye fedha wote. Kuna umuhimu wa serikali kujua baadhi ya wafanyabishara wanapata wapi mitaji mikubwa ya kuendeshea miradi yao feki. Utandawazi isiwe ndio mwanzo wa watu kuachiwa huru kujifanyia chochote watakacho. Nikumbushe pia hawa wafanyabiashara wanajihusisha na vigogo wa serikali; hivyo ni muhimu na vigogo kadhaa waanze kuhoiwa kama kweli tunataka kupambana na ujambazi kwa ari mpya na kasi mpya. Hii mambo ya kuhamisha baadhi ya maofisa polisi na kuwapeleka jijini makao makuu nataka niseme ni doa katika hii vita ya ujambazi. Yaani mtu anahamishwa eti kutoka mkoa unaosemekana ni kitovu cha ujambazi alafu anakwenda makao makuu? Kwa nini tusiwastaafishe watu kama hawa kwa manufaa ya umma? Hapa nimechanganyikiwa kabisa.
Katika gazeti la Nipashe toleo la tarehe 10/3 nilisoma eti kuna afisa wa polisi eti akaunti zake zimesimamishwa. Hakutajwa kwa jina na mimi naona nisimtaje ila walipoandika eti anatoka mikoa ya kaskazini hisia zangu zilinicheza. Unajua Tanzania watu wa kawaida wanaishi na kuzungumza tetesi nyingi sana. Ila tatizo ni kwamba hasa kipindi cha Mkapa alikuwa akipiga tetesi kabisa. Alikuwa anasisitiza eti wananchi walete ushahidi. Dhihirisho la jinsi ambavyo alivyokuwa anapenda kulea watendaji wake, wengi wao wakiwa wala rushwa na mafisadi wakubwa. Hii madhila ya jeshi la polisi ni dhihirisho la sera mbovu za uongozi mbovu wa awamu iliyopita.
Madhila ya ujambazi tunayoyaona leo ni matokeo ya sera: MKAPAISM—kuficha maovu, wala rushwa, mafisadi na kutochukua hatua dhidi ya maafisa wakubwa wa serikali pale walipokwenda mrama. Hii ilipelekea kwa mfano jeshi la polisi likafika mahali haliheshimu hata raia. Jeshi linaendeshwa kama mali ya mtu binafsi bwana. Nakumbuka kila mara ninapokuwa kule Moshi huwa nashangaa sana. Sina hakika kama ni watu wote wanashangaa kama mimi pale unapoona askari polisi wa usalama barabarani wanasimamisha vipanya navyo havisimami na unasikia kondakta akitumwa akawaone hawa mabwana. Huko nasikia huwa anapeleka noti ya shilingi 1500 au 2000. Huwa nabaki kujiuliza je hawa ni wafanyakazi wa umma au wakusanya ushuru? Kama unataka kuyaona haya nenda karibu na kituo cha mabasi Moshi Mjini sehemu inaitwa BORA, kuna nguzo ya umeme na utakuta askari kasimama pale mida ya asubuhi.
Hapa kamanda Saidi Mwema atajiju kwani jeshi letu la polisi lilikuwa likiendeshwa bila maadili, kizamani na kila aina ya michezo michafu. Mwisho, niulize: polisi imewatia kizuizini matajiri kadhaa lakini nikumbushe kitu kimoja: wataalam wa sosholojia wanasema wanawake pia wanajihusisha sana na uhalifu. Mbona hamjawatia lupango Wabejing? Wanalea majambazi sana pia.
Pamoja na kumkandia Mkapa na "Mkapaism yake" nafikiri ni bora pia tujue anaendeleaje na mapumziko yake. Hebu bonyeza hapa uone.

1 comment:

boniphace said...

Bora na wewe umesema maana wengine tulishaonekana wapinzani tukijisemea kuwa huyu jamaa alilostisha nchi. Sina mengi ya kumzungumzia huyu maana makala zangu nyingi nimemuandika na kutoa vithibitisho vingi. sIJUI TUOMBE mUNGU AWEZE KUBARIKI JITIHADA HIZI ZA JK zisiishie njiani kama zama za Mfalme Mkapa. Lakini Inno si jamaa kajenga sana kwenu huko mbona nawe haumpi tano? Hapa natania mshkaji, salamu zao kwa fashisti Museveni