My Blog List

Wednesday, December 12, 2007

MAWAZIRI NAO HAWALIPI BILI YA MAJI MPAKA WAKATIWE?

Kama unataka kuamini kuwa ni vigumu kwa nchi ya Tanzania kuendelea basi amini kwa haya ya vigogo wa serikali tena mawaziri eti hawalipii kodi ya maji mpaka wakatiwe.
Ni wazi hatuwezi kuendelea kama hata mawaziri hawako makini kiasi hiki. Sasa kama waziri halipi bili ya maji je wananchi wa kawaida watalipa? Nakwambia bado tuko kwenye lepe la ujamaa ambapo kila kitu kilifanywa na serikali.
Hebu soma habari hii alafu ushangae ni vigogo gani hao?

Mawaziri wasiolipia maji watajwa

::Yumo Waziri wa Maji, Msola, Hawa Ghasia
::jumbe wa vitisho watumwa DAWASCO


na yasmine protace

MAJINA ya mawaziri sita, ambao ni miongoni mwa wateja wa Kampuni ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASCO), waliokatiwa maji baada kushindwa kulipia ankara, yametajwa.

Mawaziri hao wanaoishi eneo la Masaki, jijini Dar es Salaam, pamoja na wakazi wengine wa eneo hilo, walikatiwa maji wiki iliyopita.

Kabla ya kuwakatia maji, DAWASCO kupitia Ofisa Mtendaji Mkuu wake, Alex Kaaya, iliwaomba wateja wanaodaiwa kulipia ankara wanazodai.

Katika maombi hayo kwa wateja, DAWASCO ilitoa siku tatu wateja hao kulipia ankara hizo, hata hivyo ni wachache tu waliotii.

MTANZANIA imefanikiwa kupata baadhi ya majina ya mawaziri wanaodaiwa ankara, ambao ni pamoja na Waziri wa Maji, Dk. Shukuru Kawambwa.

Wengine wanaodaiwa ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mizengo Pinda na Waziri wa Maendeleo ya Mifugo, Anthony Diallo.

Katika orodha hiyo, Waziri wa Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Peter Msolla, naye ametajwa, pamoja na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Hawa Ghasia, naye ni mmoja wa mawaziri hao.

Akizungumzia kilichomsibu hadi kushindwa kulipia ankara zake kwa kipindi kirefu, Waziri Ghasia alidai kuwa tangu aanze kuishi katika nyumba hiyo amekuwa hapati huduma ya maji.

Alisema amekuwa akinunua maji kutoka kwa wafanyabiashara binafsi na si kampuni ya DAWASCO.

“Kwa hili jambo ni la binafsi mno. Lakini hata hivyo, lakini sikuwahi kupata huduma ya maji ya DAWASCO na zaidi sikuwahi kupata hizo bili. Sikuwahi kuletewa bili hadi leo,” alidai Waziri Ghasia.

MTANZANIA pia iliwasiliana na Waziri Msolla kwa simu, ambaye alikiri kudaiwa, lakini akadai kuwa hakuwa akifahamu taratibu za kupata ankara na malipo.

“Ni kweli kwamba hilo suala (la kudaiwa) lilikuwapo, nami sikuwapo nchini… lakini last week (wiki iliyopita) tulipata bili na tumekwishalipia,” alisema Prof. Msolla, ambaye hakuwa tayari kuzungumza zaidi kutokana na kile alichodai yupo katika mkutano.

Waziri Simba hakuweza kupatikana, baada ya kuwasiliana naye kupitia simu yake ya mkononi. Majibu kutoka kwa aliyepokea simu hiyo yalieleza kuwa waziri huyo yuko safarini Marekani.

Waziri wa Maji, Dk. Shukuru Kawambwa, Waziri wa Maendeleo ya Mifugo, Anthony Diallo, Waziri wa TAMISEMI, Mizengo Pinda, hawakupatikana, baada ya simu zao za mkononi kuita kwa muda mrefu bila kujibiwa.

Hata hivyo, katika hali ya kushangaza, DAWASCO imesita kuzungumzia majaliwa ya viongozi hao kurejeshewa huduma ya maji.

Meneja Uhusiano wa kampuni hiyo, Badra Masoud, alisisitiza kwamba, walichokifanya ni kukata maji kwa wadaiwa.

“Tunadai fedha nyingi sana Masaki, hivyo tunataka tuendelee kutoa huduma bora kwa wateja wetu ambao wanalipa na wasiolipa tumewakatia mpaka hapo watakapolipa,’’ alisema.

Eneo jingine lililokatiwa maji mbali na Masaki ni Mbezi Beach. Hata hivyo, tofauti na Masaki, wateja wa Mbezi Beach wamekuwa wakijitokeza kulipia ankara zao.

Katika hatua nyingine, DAWASCO imedai kupokea vitisho baada ya kuwapo kwa operesheni hiyo ya ukataji maji.

“Watu wananipigia simu na kunitaka niwarudishie maji eti sijafanya vizuri, lakini mimi nimesema kwamba maji yatarudishwa kama watumiaji watalipia ankara zao,’’ alisema.

Aliongeza kwamba pamoja na kupigiwa simu, pia amekuwa akitumiwa ujumbe wa maneno ya kashfa kutoka kwa watu asiowafahamu.

Takwimu za DAWASCO zinabainisha kuwa, eneo la Masaki lenye wateja 1,270 linadaiwa Sh milioni 574, wakati Mbezi Beach kuna wateja 1,271 wanaodaiwa Sh milioni 578.

Eneo la Ada Estate lenye wateja 475 wanadaiwa Sh milioni 527, Mwenge wateja 733 wakiwa wanadaiwa Sh milioni 463 na Regent kwenye wateja 222 wanadaiwa Sh milioni 200,’’ alisema.

Ni kwa misingi hii jamani tutaendelea kama tunakuwa na viongozi makupe?Yaani kwao kila kitu bure tuu? Ni wazi hata kodi nyingine nadhani hawalipi?Pafanyike uchunguzi hapa.

No comments: