My Blog List

Monday, January 07, 2008

Tunamwonea Kibaki, tatizo ni Kivuitu

SAMUEL Kivuitu, Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Kenya (ECK) ndiye chanzo cha machafuko yaliyojitokeza nchini Kenya baada ya kumtangaza Mwai Emilio Kibaki kuwa mshindi katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika mwishoni mwa mwaka jana, huku hana uhakika iwapo Kibaki alikuwa ameshinda kweli au la.

Baada ya kumtangaza kuwa mshindi, Kibaki aliapishwa chapuchapu kuwa Rais wa Kenya katika kipindi kingine cha miaka mitano ijayo.

Nilifuatilia matangazo ya moja kwa moja ya radio na televisheni, tangu uchaguzi hadi siku ya kutangazwa mshindi; mwenendo mzima wa uchaguzi huo ulithibitisha kuwepo dalili za matokeo ya kura za urais kuchezewa yalipofika katika ofisi ya Kivuitu kutoka vituoni.

Kabla hajatangaza matokeo hayo, Kivuitu alionekana kuwalaumu maofisa wasimamizi wa baadhi ya vituo vya uchaguzi kwa kuchelewesha kuleta matokeo.

Hii ilikuwa dalili ya kwanza ya kuwepo kwa mchezo mchafu, na hata alipofika mbele ya waandishi wa habari kutangaza mshindi, siku ya Jumapili iliyopita, alianza kutaja matokeo ya vituo vilivyochelewa na alipofikia kituo cha Molo, alisoma kura za Kibaki akitaja namba ya juu zaidi ya kura alizopata.

Kwa ushujaa kabisa, William Ruto, mmoja wa viongozi wa ODM, alisimama akihoji hesabu ya kura hizo, alimtaka ofisa aliyesimamia na kusaini fomu ya matokeo (form 16A) aliyekuwepo eneo hilo, athibitishe kama kilichokuwa kikisemwa na Kivuitu mbele ya hadhara ni kweli.

Lakini kwa bahati mbaya, katika kile kinachoweza kutafsiriwa kuwa kunyongwa kwa demokrasia, maofisa usalama walimdaka Ruto haraka haraka, wakamwondoa na kumpeleka ndani huku wakiacha zogo ndani ya ukumbi, matokeo yalipokuwa yakitangazwa.

Wakati nashuhudia zogo hilo likiendelea, mara Kivuitu alionekana katika kituo cha taifa cha televisheni akitangaza matokeo ya jumla ya kura za urais na kubatiza ushindi wa Kibaki na baadaye kidogo, redio na televisheni zikawa zikitangaza tukio la kuapishwa kwake Ikulu. Ilikuwa ni kama sinema vile, na nilijikuta nikiifurahia kwa kicheko maana yake muandaaji wake alifanikiwa sana.

Mara moja mawazo yalinijia na nikamkumbuka dikteta wa zamani wa Urusi: Joseph Stalin. Alijulikana kama bingwa wa mizengwe ya kisiasa. Aliwahi kusema kuwa: “Not the voters decide the winner in an election, but those who counts votes will decide everything.” Alikuwa akimaanisha kuwa katika uchaguzi, mshindi apangwi na wapiga kura, bali wale wanaohesabu kura.

Binafsi huwa sipigi kura katika chaguzi zetu kwa sababu naamini ni sawa na kupoteza muda na kuchafua kidole changu wakati mtu huwa tayari keshachaguliwa.

Mambo yanayotokea Kenya hayakuanzia hapo na wala si mageni barani Afrika. Mambo kama hayo yameshawahi kutokea katika nchi nyingi, tuna mfano mzuri kwetu sisi, ni yale yaliyowahi kutokea Zanzibar katika chaguzi kuanzia mwaka 1995.

Kwani tatizo hapa ni mgombea mmojawapo kutotakiwa na wanaoamini wao ni wazalendo zaidi ya wengine.

Hawa wamejipa kazi ya kuwachagulia wenzao viongozi. Kwao si kila mtu anayechagulika ni kiongozi, hivyo huamua kulifanya zoezi la uchaguzi kama kupoteza muda na fedha.

Kwa uchaguzi wa Kenya, Kivuitu ndiye tatizo baada ya kutangaza matokeo yenye hila na shaka. Alitangaza matokeo yaliyopikwa katika ofisi za makao makuu ya ECK. Baadhi ya makamishna wenzake walianza kuthibitisha hilo na hata yeye mwenyewe, alipoona maji yamefika shingoni aliibuka na kuthibitisha.

Kivuitu kama alivyokiri mwenyewe, ana dhambi dhidi ya wananchi wa Kenya: Mosi, wiki hii amenukuliwa na gazeti la The Standard, akidai hana hakika ni mgombea yupi alishinda urais. Inashangaza! Ilikuwaje akatangaza ni Kibaki?

Pili, ameamsha hasira ya wananchi kwa kudhani kwamba uelewa wake ni mkubwa kuliko wa Wakenya wote juu ya haki yao kikatiba ya kuchagua na kuchaguliwa.

Hasira za Wakenya zilizosababishwa na Kivuitu ambaye naamini kabisa kuwa aliyafanya hayo aliyoyafanya akijua madhara yake na matokeo yake, ndiyo mauaji kama yanavyoripotiwa katika vyombo vya habari kwa wiki yote iliyopita.

Dhambi ya tatu ya Kivuitu ni kushindwa kutenda kazi inavyopaswa; kwa uaminifu na kwa wakati muafaka. Dhambi hii inamfanya achorwe kama mhusika mbaya (sad character) katika sinema hii ya uchaguzi wa Kenya.

Wiki hii kawaeleza waandishi wa habari kuwa, eti alitaka kujiuzulu lakini akaona si muafaka kwa vile angeonekana mwoga (coward).

Kivuitu ameyatamka haya bila kujua yanadhihirisha jinsi asivyokuwa mzalendo wa kweli kwa kukubali taasisi anayoiongoza kuruhusu mapinduzi yasiyo halali nchini Kenya.

Huo ndio ukweli kwa sababu baada ya kuapishwa Kibaki, ilitolewa amri kuwa redio na televisheni ziache kurusha matangazo ya moja kwa moja. Udhibiti wa vyombo vya habari, hasa vya elektroniki, ni moja ya sifa za wapinduaji wa serikali. Mara wanapokamata madaraka, au wakiwa katika hatua za mwisho mwisho kufanikisha kukamata madaraka, wanakimbilia kudhibiti vyombo vya habari.

Amri ya kupiga marufuku vyombo vya habari Kenya ilitolewa na Waziri wa Usalama wa Taifa, John Michuki, akidhihirisha kwa nmna nyingine kuwa naye ni mshiriki katika mapinduzi hayo.

Hili liliwanyima wananchi haki ya kuhabarishwa juu ya kilichokuwa kinatokea na ni wazi hata matumizi makubwa ya nguvu za dola kudhibiti wananchi waliokuwa wanadai haki yao, ni sifa nyingine ya mapinduzi.

Haina ubishi kuwa wanausalama hawakuheshimu matokeo ya uchaguzi, ila waliamua kumuweka mtu wamtakaye atawale. Na kama nionavyo ni sahihi, basi Kibaki atakuwa rais asiye na maamuzi sana kwa vile amewekwa pale na kikundi cha watu wakishirikiana na baadhi ya maofisa wa usalama.

Kivuitu pia kama mwanasheria ambaye anafanya kazi baada ya kuapa, aliamua kwa makusudi kabisa au kwa kulazimishwa kutoheshimu majukumu yake ya kutenda kwa haki.

Hata hivyo, kwa kuangalia rekodi yake ya kusimamia chaguzi mbili: mwaka 2002 na kura ya maoni 2005 kwa ufanisi kabisa, inawezekana kabisa Kivuitu alishinikizwa chini ya mtutu wa bunduki kumtangaza mshindi.

Angalia jinsi alivyotaka kuporwa cheti cha ushindi na watu ambao nia yao ilikuwa ni kuona kuwa Kibaki anaapishwa. Hata alipofika Ikulu kupeleka cheti hicho, alikuta maandalizi ya rais kuapishwa yameshakamilika!

Mwenyewe ametamka kuwa alishinikizwa atangaze mshindi, vinginevyo jukumu hilo lingechukuliwa na mtu mwingine. Kama mazingira haya yalikuwepo ni wazi kuwa maisha yake yalikuwa hatarini na tunaweza kumuelewa, lakini kama hivyo ndivyo kwanini hasemi wazi? Hii nayo ni dhambi, dhambi ya kutokuwa mkweli!

Dhambi nyingine mbaya kabisa inayomuangukia Kivuitu ni chanzo cha machafuko haya kubadilika kutoka kwenye upingaji wa matokeo hadi kwenye mtazamo wa kikabila.

Hisia za watu wengi hivi sasa juu ya sinema hii ya uchaguzi wa Kenya ni kwamba, Raila ni mkabila na hafai kuwa rais. Haya ni madai ya kushangaza kwa sababu ukiiangalia ODM, haijakaa katika mtazamo wa kikabila hata chembe.

Hata ilivyosukwa hasa viongozi wake wakuu (pentagon) ni wa uwakilishi mpana wa jamii mbalimbali za Kenya. Wengine nimeongea nao wanaenda mbali zaidi na kuegemea katika ngano (myth) kuwa ‘Mjaluo hawezi kutawala Kenya hata siku moja.’

Nakubaliana na ngano hizi kwa sababu nimezisikia muda mrefu sasa kwamba Wakikuyu wanawadharau Wajaluo kama watoto wadogo ambao hawajakua kwa sababu tu hawaendi jando!

Hapa unadhihirika ushahidi mwingine kuwa Kibaki na watu wake wanaomzunguka wanaogopa kivuli chao na wana wasiwasi na utawala wa Raila kwamba unaweza kulipa kisasi kwa Wakikuyu ambao wamekuwa wakifanya hila ili wasitawale Kenya.

Katika mazingira kama haya, yapaswa kutafuta jibu zuri kwa swali la nani ni mkabila kati ya Kibaki na kundi lake na Raila?

Jambo la muhimu kuzingatiwa katika utata huu uliosababishwa na Kivuitu ni kwamba, matatizo ya uhesabuji kura sasa yamekuwa mazoea Afrika Mashariki.

Mwaka 1995 kule Zanzibar yalitokea, 2001 na 2006 kule Uganda pia yalitokea. Ni wazi bado tu wachanga sana kwenye suala la utawala bora.

Yaani, taasisi zetu hazifanyi kazi kwa uhuru bali zinamtumikia mtawala (rais). Ni katika msingi huu tatizo la Kenya haliwezi kutatuliwa kwa majadiliano wala kwa kwenda mahakamani.

Haliwezi kutatuliwa mahakamani kwa sababu ni mahakama hiyo hiyo iliyomuapisha Kibaki kupitia kwa Jaji Mkuu, haraka haraka baada tu ya Kivuitu kumtangaza kuwa mshindi.

Hapa napo Jaji Mkuu wa Kenya, Moses Gicheru, naye keshapoteza mamlaka ya kimaadili katika kusimamia kesi yeyote dhidi ya uovu wa Kivuitu.

Itashangaza sana iwapo Raila akiamua kwenda mahakamani kulalamikia ushindi wa Kibaki, halafu mahakama hiyo hiyo, ambayo ndiyo iliyomuapisha Kibaki, iamue kuwa ushindi wa Kibaki ni batili. Lakini hawa wote wameingizwa dhambini na Kivuitu ambaye kama asingekubali kupindua matokeo, hali ya Kenya isingekuwa kama ilivyo sasa. Kama Kivuitu asingekubali kutangaza matokeo kwa shinikizo, angesubiri mpaka uhakiki ukafanyika na kila mmoja akawa na imani na matokeo, wala haya yasingetokea.

Waafrika tunapaswa kuwa makini zaidi sasa na watu wa aina ya Kivuitu ambaye historia yake inaonyesha kuwa hata wakati akisoma Chuo Kikuu cha Dar es Salaam aliwahi kumkorofisha Mwalimu Nyerere hadi akaitwa ikulu.

Utukutu wake wa utotoni ndiyo matokeo ya machafuko yanayoendelea nchini Kenya.

Kwa sababu hizo, kuna kila sababu ya kuchagua watendaji na wasimamizi wa shughuli mbalimbali za kitaifa kwa kuangalia historia zao.

MJUE UNDANI WA JOSEPH KONY

Leo nataka watu wamjue Joseph Kony ni mtu wa aina gani kutoka kwa mtu aliyesoma naye. Pia tujue ili Afrika iendelee, kuna mengi zaidi ya viwanda ya kufanya.

Wednesday, January 02, 2008

ETI KIVUITU ALISHINIKIZWA?

Imedhihirika kuwa mwenyekiti wa tume ya Taifa ya uchaguzi alishinikizwa kutangaza matokeo ya uchaguzi. Je hii si ndio chanzo cha uoza wa dhahama na mauaji?

KIU YA UONGOZI TATIZO LA WAZEE KAMA KIBAKI

Uchaguzi Kenya umekwisha kwa mizengwe lakini mambo ni mabaya kabisa. Ni wakati wa viongozi wa Kenya kufikiri sana. Mwanazuoni mmoja anatoa ni kwa vipi wanasiasa walikuwa wamejisahau.
Pia vurugu za Kenya ni chanzo cha madhara eneo zima la Afrika Mashariki. Kwa waganda wanajiuliza je ni Uganda ina demokrasia zaidi ya Kenya?

Wednesday, December 19, 2007

ZUMA AANZA HARAKATI ZA KUWA RAISI WA BONDENI

The image “http://www.mg.co.za/ContentImages/328066/zuma.jpg” cannot be displayed, because it contains errors.

Bado nina hisia mchanganyiko manake kuchaguliwa kwa Zuma kuiongoza ANC ni matokeo ya demokrasia. Ila mara nyingine demokrasia ina matatizo yake; hili ni tatizo kwa Afrika ya kusini kabisa.

Vijana wa ANC nao wana mashaka sana na uchaguzi wa Zuma kwani hana haiba nzuri ya kiongozi.

Wednesday, December 12, 2007

SIASA ZA BONDENI ZINACHEKESHA

Yaani mara nyingine inafikia wakati mtu anaamini kuwa siasa zetu zimebakwa na wanasiasa. Pia huko somalia, amechaguliwa waziri mkuu mpya je, ataweza kazi yake?

UHURU NA AKILI MGANDO ZA BAADHI YA WATAWALA

Taifa letu lilitimiza miaka arobaini na sita (46) tangu lizaliwe; jumapili iliyopita ilikuwa ni kumbukumbu ya siku ya uhuru kwa maana nyingine. Kama mtanzania, na mzalendo sina budi kuchukua kalamu na kutafakari kwa kina miongo kadhaa kama Taifa ni changamoto gani tumezikabili na zipi inatubidi tupandishe soksi (pull up socks) ili kuendeleza nchi yetu. Binafsi, naamini kama tutafanyia kazi changamoto ya “Utawala Bora” basi uhuru wetu utakuwa na maana sana. Mada yangu itaegemea sana hapa tu.

Kabla ya kujadili, nitoe pongezi kwa watanzania wote tangu raisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete na kwa ujumla watu wa kada zote hapa nchini kwa kuadhimisha siku hii.

Bila ubishi kabisa, nchi yetu imefanikiwa sana katika nyanja mbalimbali tangu uhuru hasa ukilinganisha na nchi nyingine za dunia ya tatu. Hapa ieleweke hata kama tungekuwa tumefanikiwa kiuchumi kama vile Wachina ama Wajapan bado kungekuwa tu na matatizo. Hivyo si vyema kubeza kuwa labda kila kitu ni mrama; yapo mafanikio kama vile umoja wa kitaifa ambao ni mfano dunia nzima. Binafsi nimekutana wa watu kadhaa kutoka pande mbalimbali za dunia wanaposikia umetoka Tanzania watasifia Umoja wetu. Hii yote ni heshima za mwasisi wa Taifa, hayati Mwalimu Nyerere.

Kuendana na mfumo wa kiutawala duniani, yapo mapungufu mengi ambayo nadhani ni vigumu kujikwamua nayo hasa ukizingatia mfumo mzima wa biashara ulimwenguni ni wa upendeleo na ukandamizaji kwa sera za mashirika makubwa ya kiuchumi na kibiashara ulimwenguni. Hapa nazungumzia sera za Mfuko wa Kimataifa wa Fedha (IMF), Benki ya Dunia (WB) na Shirika la Biashara Ulimwenguni (WTO) mwanzoni likijulikana kama GATT.

Ndio maana kama mtu anafuatilia hata yale majadiliano kibiashara ya kule DOHA yamekwama kabisa na ni wazi watawala wa dunia hawataki kabisa kukubali baadhi ya hoja ambazo zitalikwamua bara la Afrika kutoka umasikini usiokwisha. Hata hivi majuzi, Taifa letu limesaini makubaliano mapya ya mashirikiano ya kiuchumi na Jumuiya ya Ulaya (EU) yajulikanayo kama (EPA) kwa kutumia mgongo wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ambayo ni wazi yameshinikizwa na hayatailetea nchi yetu tija sana kinyume na inavyodhaniwa na wale waliosaini. Inajulikana wazi tumelazimishwa kwa kuharakisha kusaini kabla ya ule mkataba wa Cotonou kumalizika hapo December 31 mwaka huu. Nisijadili hili zaidi labda siku nyingine.

Ni katika mchakato huu wa changamoto hizi za mabepari basi hata kama watawala wetu wanao utashi inakuwa vigumu kuweza kusimamia maslahi yenye tija kwa nchi zetu. Kwani mara nyingine watawala wetu wanapokuwa na utashi wa dhati basi mambo kama yanayomkuta Robert Mugabe hayazuiliki kwani wanaishia kufanya maamuzi kwa pupa, bila kufikiri kwa mpangilio na kwa logiki ambayo yanagharimu maisha na uchumi wa nchi zao. Ndio changamoto za “Uhuru” ambazo kwangu ni jinamizi tu; kwani, tunaposherehekea siku hii lazima tuelewe inawezekana kabisa siku ile ilikuwa ni mwanzo wa kipindi cha giza. Ningependa nielezwe hivi Mwalimu Nyerere alipokwenda kule Lancaster alikwenda kusaini mambo gani? Manake inatia shaka huenda ndio ulikuwa wakati wa kujitia kitanzi badala ya kuwa huru. Kwani nina mashaka sana kama kweli tuko huru.

Na ndio maana bado tuna changamoto nyingi sana za kutafakari na kujiuliza tufanye nini? Kwa mtizamo wa serikali ya awamu ya nne, ni wazi changamoto kuu ambayo lazima ifanyiwe kazi ni hii ya “utawala bora”. Hii imebaki kuwa ngonjera na kama hatubadiliki kwa hili basi kamwe hatutapiga hatua yeyote. Nasema hivi kwani naamini pamoja na changamoto za jinamizi la uhuru linaloongozwa na sera dhalimu za kimataifa bado tuna mengi ya kufanya kwa hapa nyumbani ambayo yatatuwezesha tuwe bora tu mbali na mashinikizo dhalimu ya mabepari.

JE TUFANYE NINI?

Tunahitaji kufikiri zaidi ya kuongea sana; hii itatuwezesha kuwekeza katika kuwajibika kwa bidii (hardworking) badala ya kupiga siasa kwa muda mrefu zaidi. Ni wazi hadi leo hii, bado utendaji wetu umetawaliwa na mashiko ya kisiasa zaidi kuliko nidhamu ya kazi katika nyanja mbalimbali. Hasa katika chombo kama Bunge, ni lazima tubadilike; miaka arobaini na sita itufanye tuamue sasa ni mwisho wa siasa za upande mmoja usiozingatia maslahi ya umma. Njozi za chama kushika hatamu zisipoachwa basi hatufiki popote kama Taifa la miongo hii minne na ushehe.

Kwa watawala wetu, lazima kung’amua kuwa kama mhimili wa utawala (executive) unakuwa na nguvu kubwa dhidi ya mihimili mingine basi hatufiki. Pamoja na nguvu ya kikatiba ya taasisi ya uraisi, Uhuru unakuwa na maana kama kiongozi mkuu wa nchi atang’amua hili na kuruhusu utendaji unaoruhusu majadiliano ya vyama vyote vya mitizamo tofauti ndani ya bunge badala ya kuzingatia tu upitishaji wa maamuzi yenye kuegemea uchama na si umma.

Ingawa demokrasia inasema ‘wengi wape’, lakini nadhani pia tuangalie mfumo wetu wa upigaji kura na maamuzi ya upitishaji sheria ama maamuzi bungeni ukoje? Je unaruhusu upigaji kura wa wabunge wa chama tawala unaozingatia uhuru wa mawazo ya mbunge au ni kushurutisha kwa kuegemea maslahi ya chama yaliyofichwa ili kulinda maslahi ya vigogo wa chama tawala bila kutoa sababu za msingi kuhusu jambo fulani ili kulinda maslahi ya nchi.Uhuru unaweza usiwe na maana sana kama mfumo wa maamuzi ndani ya chombo kama Bunge unambana mbunge mwenye mawazo tofauti.

Hata ndani ya vyama vya siasa, ni changamoto pia kujiuliza hivi kuna uhuru wa mawazo wa mbunge katika kujadili mambo na hata kuhoji ndani ya chama? Yaani kwa miaka yote hii arobaini na sita, bado ni kosa la jinai ndani ya chama tawala kwa mtu kujadili hisia zake kwa uwazi inavyoonekana na hata kupinga ama kupiga kura ni udikteta tu (intra-party disagreement, debate and even voting is still a crime). Hapa lazima watawala wakumbuke hili ndilo linalokwamisha maendeleo yetu na hapana budi tuweke mizani ya usawa (strike a balance) katika utendaji wa serikali dhidi ya mihimili mingine miwili hasa ule wa Bunge tukianzia ndani ya vyama vya siasa.

Kwa mfano, kama tutazingatia utawala bora, basi lazima tubadili mitizamo yetu (mentality): yaani serikali iwe kwa ajili ya umma na si kama jamvi la kuficha mafisadi kama ilivyokwishajidhihirisha kwa watuhumiwa wa ufisadi kutajwa hadharani na wao kuamua kukaa kimya bila kujisafisha. Hata mamlaka yenye uwezo wa kuwawajibisha nayo haikuchukua hatua zozote. Ndio hapa bado inaonesha tunawaza zaidi katika kulinda maslahi ya kisiasa kuliko ya umma. Yote hii inashawishi mtu mwenye akili timamu kuwaza na kuamini labda ni kwa sababu ya utawala mbovu. Mfumo wa “Check and Balance” uko likizo ili tu kulinda maslahi ya kisiasa ya chama kinachotawala. Huu ni ugonjwa mkubwa barani Afrika na kama hatubadili mtizamo “Uhuru” unakuwa hauna maana.

Ninaamini kama watanzania, tuna bahati ya kuwa na raisi wa nchi ambaye ana karama ya kuongoza kwa kujali demokrasia; kwani anajitahidi kujumuisha pande na hisia mbalimbali za kisiasa katika utendaji wake. Mashaka yangu bado nadhani waliomzunguka raisi wetu mitizamo yao imepitwa na wakati na si endelevu. Ni mitizamo ya kusisitiza zaidi ‘umilele-chama’ (party-omnipresence) kuwa na woga labda chama kitaangushwa madarakani kwa kile wasichokijua. Na hii ndio chanzo cha madhila kadhaa zinazoisumbua serikali ya awamu hii.

Ni changamoto nzuri za kumfanya raisi na wasaidizi wake kuliona hili na kuamua kubadilika. La sivyo tuna hatari ya kubakiwa na “Kiongozi mwenye karama asiye na mwelekeo” (a charismatic leader without a cause). Mwelekeo wa sasa kwa nchi huru unatia shaka kwani uwezo wa kufikiri wa vigogo wengi ni mdogo sana na ni wazi unasababishwa na tamaa ya fedha na ulafi wa kila aina. Kitu woga kwa viongozi wetu ndio chanzo cha udhaifu wa viongozi wetu kuanzia juu.

Siku ya leo tujiulize ni kwa jinsi gani utawala wa shaghala baghala ulivyogharimu taifa letu kwa kipindi chote cha uhuru. Tunaweza tukalaumu sana na kusingizia mfumo wa kidunia (world order) ambao nimeuelezea awali, lakini kama tuna akili timamu ni wazi kwa nafasi yetu kwa mambo ya hapa nyumbani tuna mapungufu pia ambayo lazima tuamue kwa dhati kuyafanyia kazi. Ndio maana hata Raisi wetu majuzi alisikika akisema na kukiri hata hii mikataba ya madini ni sisi wenyewe wa kujilaumu mbele ya Waziri Mkuu wa Canada mheshimiwa Stephen Harper.

Kama Taifa, miaka arobaini na sita ya Uhuru haina maana sana kwani tumeshindwa kukabili changamoto za ndani kabisa. Inakuwa vigumu kukabili zile za nje manake watawala wa dunia wanatumia udhaifu wetu huu kutulaghai kwa kila hali. Kama hatubadiliki kwa kuruhusu kukosoana ndani ya vyama vyetu, bunge letu na kila mahali ili kulinda maslahi ya umma basi kamwe sioni maana sana ya uhuru. Ninachokiona ni sana sana ni juhudi kubwa tena hasi (highest retrogressive endeavour) za watawala na wanasiasa katika kuirudisha nyuma nchi yetu kwa kasi.

Uhuru bila ‘utawala bora’ ni kwa wachache na si kwa umma wa watanzania. Kama siku ya Jumapili, leo nitamwomba Mungu aizindue akili ya watawala na wanasiasa kwa ujumla wao kubadili mitizamo. Tuachane na akili mgando ndio uhuru utakuwa na maana. Miaka arobaini na sita ya Uhuru ije na mtimzamo (mentality) mpya kuhusu utawala wa Taifa hili. Hii ndio tafakuri yangu ya siku hii ya uhuru kwa leo.

MAWAZIRI NAO HAWALIPI BILI YA MAJI MPAKA WAKATIWE?

Kama unataka kuamini kuwa ni vigumu kwa nchi ya Tanzania kuendelea basi amini kwa haya ya vigogo wa serikali tena mawaziri eti hawalipii kodi ya maji mpaka wakatiwe.
Ni wazi hatuwezi kuendelea kama hata mawaziri hawako makini kiasi hiki. Sasa kama waziri halipi bili ya maji je wananchi wa kawaida watalipa? Nakwambia bado tuko kwenye lepe la ujamaa ambapo kila kitu kilifanywa na serikali.
Hebu soma habari hii alafu ushangae ni vigogo gani hao?

Mawaziri wasiolipia maji watajwa

::Yumo Waziri wa Maji, Msola, Hawa Ghasia
::jumbe wa vitisho watumwa DAWASCO


na yasmine protace

MAJINA ya mawaziri sita, ambao ni miongoni mwa wateja wa Kampuni ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASCO), waliokatiwa maji baada kushindwa kulipia ankara, yametajwa.

Mawaziri hao wanaoishi eneo la Masaki, jijini Dar es Salaam, pamoja na wakazi wengine wa eneo hilo, walikatiwa maji wiki iliyopita.

Kabla ya kuwakatia maji, DAWASCO kupitia Ofisa Mtendaji Mkuu wake, Alex Kaaya, iliwaomba wateja wanaodaiwa kulipia ankara wanazodai.

Katika maombi hayo kwa wateja, DAWASCO ilitoa siku tatu wateja hao kulipia ankara hizo, hata hivyo ni wachache tu waliotii.

MTANZANIA imefanikiwa kupata baadhi ya majina ya mawaziri wanaodaiwa ankara, ambao ni pamoja na Waziri wa Maji, Dk. Shukuru Kawambwa.

Wengine wanaodaiwa ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mizengo Pinda na Waziri wa Maendeleo ya Mifugo, Anthony Diallo.

Katika orodha hiyo, Waziri wa Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Peter Msolla, naye ametajwa, pamoja na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Hawa Ghasia, naye ni mmoja wa mawaziri hao.

Akizungumzia kilichomsibu hadi kushindwa kulipia ankara zake kwa kipindi kirefu, Waziri Ghasia alidai kuwa tangu aanze kuishi katika nyumba hiyo amekuwa hapati huduma ya maji.

Alisema amekuwa akinunua maji kutoka kwa wafanyabiashara binafsi na si kampuni ya DAWASCO.

“Kwa hili jambo ni la binafsi mno. Lakini hata hivyo, lakini sikuwahi kupata huduma ya maji ya DAWASCO na zaidi sikuwahi kupata hizo bili. Sikuwahi kuletewa bili hadi leo,” alidai Waziri Ghasia.

MTANZANIA pia iliwasiliana na Waziri Msolla kwa simu, ambaye alikiri kudaiwa, lakini akadai kuwa hakuwa akifahamu taratibu za kupata ankara na malipo.

“Ni kweli kwamba hilo suala (la kudaiwa) lilikuwapo, nami sikuwapo nchini… lakini last week (wiki iliyopita) tulipata bili na tumekwishalipia,” alisema Prof. Msolla, ambaye hakuwa tayari kuzungumza zaidi kutokana na kile alichodai yupo katika mkutano.

Waziri Simba hakuweza kupatikana, baada ya kuwasiliana naye kupitia simu yake ya mkononi. Majibu kutoka kwa aliyepokea simu hiyo yalieleza kuwa waziri huyo yuko safarini Marekani.

Waziri wa Maji, Dk. Shukuru Kawambwa, Waziri wa Maendeleo ya Mifugo, Anthony Diallo, Waziri wa TAMISEMI, Mizengo Pinda, hawakupatikana, baada ya simu zao za mkononi kuita kwa muda mrefu bila kujibiwa.

Hata hivyo, katika hali ya kushangaza, DAWASCO imesita kuzungumzia majaliwa ya viongozi hao kurejeshewa huduma ya maji.

Meneja Uhusiano wa kampuni hiyo, Badra Masoud, alisisitiza kwamba, walichokifanya ni kukata maji kwa wadaiwa.

“Tunadai fedha nyingi sana Masaki, hivyo tunataka tuendelee kutoa huduma bora kwa wateja wetu ambao wanalipa na wasiolipa tumewakatia mpaka hapo watakapolipa,’’ alisema.

Eneo jingine lililokatiwa maji mbali na Masaki ni Mbezi Beach. Hata hivyo, tofauti na Masaki, wateja wa Mbezi Beach wamekuwa wakijitokeza kulipia ankara zao.

Katika hatua nyingine, DAWASCO imedai kupokea vitisho baada ya kuwapo kwa operesheni hiyo ya ukataji maji.

“Watu wananipigia simu na kunitaka niwarudishie maji eti sijafanya vizuri, lakini mimi nimesema kwamba maji yatarudishwa kama watumiaji watalipia ankara zao,’’ alisema.

Aliongeza kwamba pamoja na kupigiwa simu, pia amekuwa akitumiwa ujumbe wa maneno ya kashfa kutoka kwa watu asiowafahamu.

Takwimu za DAWASCO zinabainisha kuwa, eneo la Masaki lenye wateja 1,270 linadaiwa Sh milioni 574, wakati Mbezi Beach kuna wateja 1,271 wanaodaiwa Sh milioni 578.

Eneo la Ada Estate lenye wateja 475 wanadaiwa Sh milioni 527, Mwenge wateja 733 wakiwa wanadaiwa Sh milioni 463 na Regent kwenye wateja 222 wanadaiwa Sh milioni 200,’’ alisema.

Ni kwa misingi hii jamani tutaendelea kama tunakuwa na viongozi makupe?Yaani kwao kila kitu bure tuu? Ni wazi hata kodi nyingine nadhani hawalipi?Pafanyike uchunguzi hapa.

Saturday, December 01, 2007

TANZANIA BILA UKIMWI INAWEZEKANA?

Siku ya Ukimwi duniani; ni wakati wa kila mtu hasa mwafrika kutafakari juu ya balaa hili ambalo limeshachukua roho za watu lukuki. Wakati naandika makala hii mara nasikia redioni kuwa huko Mbagala Kizuiani kuna jamaa mmoja kaamua kujiua baada ya kuthibitishiwa kuwa ana virusi mwilini mwakeMwingine kaamua kumuua mkewe huko Mbeya baada ya kusikia mkewe kapima bila ruhusa yake

.Ni habari za kusikitisha lakini ni lazima tujiulize hivi kweli hizi kampeni za upimaji ndio jibu la dhahama hili? Na pia tujiulize kwanini tunahofu juu ya kuambiwa tumeathirika?Je hatupo tayari kuwajibika na matokeo ya tabia zetu za ngono zembe?

Napenda niseme kuwa hizi kampeni za upimaji ukimwi zinanitia wasiwasi kama kweli ndio muarobaini wa gonjwa hili. Nasema hivi kwani ni zaidi ya miaka ishirini sasa tangu nimeanza kusikia habari za ugonjwa huu. Na kwa muda wote huo kampeni mbalimbali za kuhamasisha na kuelimisha kuhusu ugonjwa huu zimekuwepo. Ndio maana leo hii katika kampeni hizi za rais Jakaya Kikwete, hakuna jipya linalosemwa. Nimesikiliza, kutizama na hata kuhudhuria semina juu ya gonjwa hili kwa kweli sijaona kipya chochote juu ya elimu ya gonjwa hili.

Nikirejea kwenye mafunzo yatolewayo shuleni: msingi, sekondari na hata katika vyuo kupitia mitaala mbalimbali, nadhani watanzania kama jamii tuna tatizo. Ni jamii isiyojishughulisha kabisa kusoma na kujielimisha binafsi. Habari juu ya gonjwa hili zimesambaa kila kona kwa miaka ishirini iliyopita: vitabuni, majarida, vibwagizo, kwenye mitandao ya intaneti na magazetini, lakini watanzania hatujishughulishi kupata mafunzo lakini tunataka semina, makongamano na hata vipindi vya redio na televisheni visivyo na jipya juu ya gonjwa hili kila kukicha. Kuna haja ya watanzania kuamka katika kujali umuhimu wa kujua mambo yanayohusu maisha yao. Bila hivyo sidhani kama tutafika popote katika vita ya gonjwa hili.

Hivi kweli inaingia akilini kuwa hadi leo hii watanzania watu wazima kwa vijana hatuna uelewa wa gonjwa hili?Miaka yote tumeishi na gonjwa hili yaani hatulifahamu? Nisingetegemea tuwe na kampeni kubwa kama ya sasa na ambayo hatima yake bado ni kutokupungua kwa maambukizi kwani kuna kila dalili watu wengi wameziba masikio.

Nashangazwa na upimaji kwa siri: mosi, hivi kama napima kama nina virusi alafu nasema ni siri yangu, na sitaki watu wajue kama nimeathirika, si kuwa ninataka kuendelea kujichanganya visivyo na watu wengine ili niwaambukize? Kwanini tusiwe na utaratibu wa kistaarabu wa waathirika kuhimizwa kwa ushauri nasaha ili wajiweka wazi na hata kujiunga kwa uwazi na taasisi za waathirika kwani kwa sasa wengi wao ni kwa siri sana. Hapa siongelei unyanyapaa, ila ni vyema watu wawe huru kutambuliwa kwani kama usiri utaendelea kutiliwa maanani zaidi, basi hii kampeni haitatusaidia sana kwani kuna kila shaka ya kuendeleza uambukizi zaidi.

Uwazi huu pia ungeoneshwa hata kwa wanajamii vinara: wabunge, mawaziri, na viongozi mbalimbali wa jamii. Kwa mfano, kama tungejulishwa angalau taarifa za upimaji kule bungeni, je wangapi walipima, wangapi walionekana kuathirika ama kutoathirika. Lakini kupambana na ukimwi kwa usiri hakutakomesha ukimwi kamwe.

Pia nashangazwa na hizi juhudi za upimaji hazijaonekana sana katika taasisi za elimu hasa elimu ya juu. Huku kuna vijana lukuki na ingekuwa vyema hapa watu wapimwe manake ndio viongozi wa kesho tunaowatarajia na tukiwaacha ngono mbele kwa mbele basi tujue kuna mahali ambapo paangaliwe manake kwa muono wa karibu ni sehemu ambapo maambukizi yanawezekana kuwa kwa kasi sana.

Linalonishangaza sana ni kuwa Ukimwi umekuwa ni mradi mkubwa kwa baadhi ya watu flani na vitaasisi vyao vyenye utegemezi wa wafadhili. Ni wazi kuna watu wanafurahi sana ongezeko la wagonjwa wa ukimwi na hata yatima. Bila gonjwa hili watu wengi hawataajiriwa na wengine wangekuwa masikini kabisa. Najua siku hizi imani za kidini ni kiini macho kwa wengi kutokana na matendo yao. Ni kwa misingi hii vita ya gonjwa la Ukimwi inaonesha kama vile hakuna Mungu.

Ukimwi bado ni kiini macho kupambana nao kwani hadi leo bado watu wanaugua gonjwa hili lakini utasikia eti wamekufa kwa vigonjwa vingine ama wamelogwa na mambo mengine ambayo mtu mwenye akili inashangaza sana. Kuna haja mtu anaugua gonjwa hili awe tayari kusema nilikuwa naugua gonjwa hili bila aibu. Tunazika watu wengi hata wasomi kabisa ambao wakati wa kuugua anaonekana anaugua Ukimwi ila siku ya kufa utasikia eti anaumwa sijui kansa, presha na kadhalika. Ni usiri wa kijinga tunauendekeza na ambao hatima yake ni kiini macho cha vita ya ukimwi. Umefika wakati tuache usiri bila hivyo ni vifo bila mabadiliko.

Mwisho, nadhani kwa mwenendo wa sasa, “Tanzania bila Ukimwi” haitawezekana kama raisi wetu anavyotusihi. Usiri huu kwa kisingizio cha kuzuia unyanyapaa ni chanzo cha janga hili kuendelea. Siamini nchi yetu inaweza kuendelea, ni wazi gonjwa hili litaendelea kudumaza na kuwamaliza wasomi wa nchi yetu. Ni mwaka wa ishirini na saba tangu gonjwa hili livamie nchi yetu na bado watanzania wengi hawajaamua kuacha ngono zembe, ni mwanzo wa kiama Tanzania.

Thursday, November 29, 2007

MALKIA ALIVYOFURAHIA UGANDA

Leo nataka tuone ni wapi Malkia Elizabeth alilala na ni jinsi gani aliandaliwa na kufurahi maisha ya kiafrika alipokuwa nchini Uganda.

KAMATI YA MADINI--NI SARAKASI ZA KISIASA ZISIZO NA TIJA SANA

Katika makala yangu ya mwezi September, tarehe 9, mwaka huu,katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili: “Bunge letu ni jumba la Sanaa”, ukurasa wa 12—13 , nilieleza kuwa demokrasia ya Tanzania ni ya kipekee duniani na kusema hivi: “kwa misingi kwamba tuna serikali isiyozingatia mihimili mitatu: Watawala, Bunge na Mahakama. Tanzania ya leo, serikali inaendeshwa kwa mihimili miwili: watawala na mahakama.” Hapa nilionesha wasiwasi wangu jinsi gani Bunge linafanya kazi ya kubariki na kuisemea serikali (rubber stamping) mijadala ya serikali badala ya kuihoji.

Hii niliona kama chanzo cha Bunge, kupitia wabunge wengi (majority) wa CCM walivyohakikisha wanaizima hoja ya Zito Kabwe na kumfungia kama adhabu kwa kile walichodai ni uzushi na utafutaji wa umaarufu kirahisi (cheap popularity).

Leo nataka niendelee nilipokomea kwani kutokana na mada ile ile ya Zitto Kabwe, rais Kikwete kaja na mpya. Kuunda kamati ya raisi kuchunguza ama kuipitia mikataba ya madini ni jambo zuri japo ninapata wasiwasi na utashi wa kweli wa hatua yake. Yaani raisi kama mkuu wa mhimili wa utawala na pia sehemu ya Bunge, ni wazi maamuzi ya awali ya kumuadhibu Zitto hayakuanzia tu kwa wabunge bali yalipangwa na raisi pia kupitia baraza la mawaziri, alafu waziri mkuu akawafunda wabunge wa CCM na maamuzi yakawa jinsi ilivyokuwa.

Mpango mzima wa kuzima madai yale ulishindwa na ukaleta matokeo isivyotarajiwa (backfire) na ikadhihirisha aibu kubwa ya kifikra kwa wabunge wa CCM na serikali kwa ujumla. Raisi anapong’amua hili alafu anawageuka wabunge baada ya kuwaaibisha kwa kuwashurutisha wafikiri visivyo. Ni kichekesho kikubwa; hebu fikiri Bunge letu limejaa wasomi, maprofesa, madaktari wa falsafa lukuki wa fani mbalimbali. Ni hatari kwa nchi kubwa kama yetu yaani mafanikio yote haya ya kitaaluma hawawezi kufikiri sahihi wala kusoma alama za nyakati.

Ukiacha hilo, raisi anajaribu kukiuka ahadi yake ya Ari Mpya, Nguvu Mpya na Kasi Mpya. Raisi anaturudisha kulekule kufanya mambo kwa mazoea kitu ambacho amekuwa akikipinga. Uundwaji wa tume ya raisi wala si ya Bunge unanifanya nianze kukosa imani na raisi kwa hili. Swali: Inakuwaje Bunge, linaamua kufanya kazi ya mhimili wa watawala na kuacha wajibu wake wa kuhoji au kuchunguza madai halali ya Zitto kwa kisingizio cha Spika eti tungepoteza pesa bure baada ya kupoteza zile za tume ya madai ya Mengi awali. Pili, hivi hii tume ya raisi ya leo hii haitumii pesa?

Wajuzi wa masuala ya kiuchunguzi wanasema tume ya raisi haina meno kisheria kama ile ya kibunge. Ni wazi raisi anajaribu kutuchezea mchezo wa kisiasa katika kujaribu kuifuta ile kashfa ya Buzwagi. Hoja ya Kabwe ilikuwa juu ya uvunjaji wa taratibu kusaini mkataba wa Buzwagi kule hotelini Churchil. Raisi kaiteka nyara ile hoja na akageuza kuunda kamati kuchunguza mapitio ya mikataba yote ya madini. Hapa nashangazwa na utashi wa kupambana na ufisadi kama ni kiini macho tu. Najiuliza: hivi zile juhudi zote sa Spika na Wabunge wa CCM kutumia kanuni halali za Bunge na kuzima kwa msisitizo mkubwa hoja ya Buzwagi zilikuwa za kuwalinda akina nani?

Kuna harufu ya rushwa hapa, kwani kama tunapitia sheria zote za madini basi labda tunataka kuondoa akili ya watanzania wote kutoka Buzwagi na kuzika madai ambayo Spika ama kwa utashi wake ama kwa maagizo hakutaka kabisa iundwe kamati ya Bunge.

Hata hii kamati ya Bunge ya kuchunguza mkataba wa Richmond inatia wasiwasi sana juu ya utashi wa kweli kama upo. Ukifikiri sana unajiuliza: kwanini imeundwa leo hii na si wakati ule ambapo ilipingwa kwa nguvu zote? Hata taasisi nyeti ya uchunguzi wa rushwa (Takukuru) ilishaisafisha Richmond lakini mara tunaona mabadiliko ya bunge letu (U-turn) na sasa bunge linakubali kamati ya Bunge iundwe. Hapa nina wasiwasi sasa wahusika wameshaandaa nakala-vielelezo mpya za kufuta ushahidi wa rushwa na maadam wameshajihami basi wana hakika Kamati ya bunge itawakuta ni wasafi.

Jambo lingine kwenye hii kamati ya raisi kupitia sheria za madini: vipi miongoni mwa wajumbe wa tume ya raisi ni wabunge wawili wa CCM ambao kwa nguvu kubwa walipiga makelele kwa kupiga meza katika kuzima kabisa hoja ya Buzwagi? Kama hawakuona kabisa utata katika mkataba ule hivi kweli ni watu wenye utashi wa kuchunguza mikataba ya madini? Hapa ndio pananitoa imani na uamuzi huu wa kuunda kamati ya raisi.

Wasiwasi wangu mwingine, nakumbuka wakati anaongea na Sauti ya Amerika (VOA) akihojiwa na Shaka Sally kupitia kipindi cha Straight Talk Afrika kutoka Chamwino Dodoma, raisi alisema mikataba yote ya madini imeshapitiwa na sasa inaendana na viwango vinavyokubalika kimataifa. Nakumbuka alizungumzia mambo kama ya mirabaha inayolipwa na kampuni za madini na hata lile suala nyeti la mgawanyo wa kodi wa asilimia 3% kwa 97% na akasema sasa ni 30% kwa 60% kama sijakosea kukunukuu. Sasa kuunda kamati kupitia tena sheria za mikataba kunamaanisha alikuwa anadanganya? Nilitegemea raisi aunde kamati kuchunguza Buzwagi—kiini cha madai ya Zitto. Sasa hii upitiaji wa mikataba ambayo raisi amewahi kusema imepitiwa na wataalamu ni nini tena?

Hapa raisi mimi binafsi nadhani tumwamini kwa maamuzi yake japo utashi unatutia wasiwasi. Nampa imani ya kidhahania tu (benefit of doubt) na tusubiri tuone kweli kama tume yake itapendekeza nini na kama atafanyia kazi mapendekezo hayo. Mambo haya ya kufunikafunika ni mbinu za kisiasa zilizopitwa na wakati. Nina wasiwasi raisi hajui kuwa nchi yetu ipo katika kipindi cha kiongozi mkuu kufanya maamuzi magumu la sivyo umaarufu wa chama na serikali yako utagharimika sana. Ni wakati wa “Utawala Bora” kuachiwa ufanye kazi. Mihimili mitatu ya dola isipoachiwa ifanye kazi kwa kujitegemea bila kuingiliwa na watawala basi ndio tunashuhudia usanii kila kukicha hasa tangu awamu ya nne ianze.

Ule wakati wa kuwachukulia watanzania kama watu wa mawazo finyu (gullible) umekwisha. Ni wazi kama rais na chama chake hawakutaka kamati ya bunge kuchunguza Buzwagi ila anaamua kuunda kamati chini ya mamlaka yake. Lengo linaweza kuwa ni kuweza kudhibiti uchafu wote utakaoibuliwa usishughulikiwe kwa mujibu wa sheria. Tume aliyoiunda inawajibika kwake na wala haina nguvu za kisheria kuwezesha mapendekezo yake yafuate mkondo wa kisheria iwapo itathibitika kuna haja ya kuwawajibisha vigogo fulani.

Ndio maana ikiwa tume itawakilisha ripoti kinyume na matarajio ya Raisi, tusishangae yale yaliwahi kumkumba Jaji Robert Kisanga wakati wa enzi za uwazi na ukweli yakamkumba pia Jaji Mark Bomani. Binafsi nimeitafakari hatua ya kuunda kamati ya raisi na si ya Bunge kama sarakasi za raisi katika kufunika kashfa ya Buzwagi. Ni dhihirisho jinsi Bunge lilivyotekwa na mhimili wa watawala (executive’s hijack of the legislature). Raisi anafanya kila juhudi kuendeleza hali tata iliyopo (Status Quo) yaani kuzuia mabadiliko ya kifikra na hata jinsi mpya ya kiutendaji ili kuikwamua nchi yetu katika umasikini wa kujitakia.

Kwa mwendo huu kama viongozi wa bara la Afrika hawataki kuruhusu mfumo wa utawala bora ufanye kazi basi katu haisaidii juhudi za kujikwamua na umasikini. Haya ndio yananifanya niwe na wasiwasi na tume ya raisi; hebu tusubiri tuone kama itakuwa na tija. Lakini ningekumbusha mbona tunaizika kashfa ya Buzwagi? Hii ni sarakasi ya raisi; je itafanikiwa? Tusubiri tuone.

Saturday, November 17, 2007

LEO JUMAMOSI

Profesa Mazrui kaandika juu ya mapambano ya mwafrika; na pia kama kawaida napenda sana kujijuza mambo ya nyakati za Iddi Amin.

Wednesday, November 14, 2007

RAIS KIKWETE ADHIHIRISHA JINSI BUNGE LISIVYOJALI MASLAHI YA NCHI

Sijui niuite ni ukinyonga au niseme nini ila kama kuna siku rais Kikwete kanichekesha ni pale niliposikia kuwa ameunda tume ya kuchunguza na kupitia mikataba ya madini. Mshangao ulinipata baada ya kusikia eti na mheshimiwa Zito Kabwe nae ni miongoni mwa wajumbe wa tume. Kwangu hii ilikuwa ni faraja kusikia hili la kumjumuisha mpinzani ndani ya shughuli kama hii. Zaidi kumjumuisha Zito Kabwe lilinichekesha sana.

Zitto Kabwe ndie mwaanzilishi na mpiga filimbi mkuu aliyethubutu kujitoa mhanga na hatimaye kupewa adhabu ya kutohudhuria kikao cha Bunge kinachoendelea sasa ili kutaka tume ya Bunge iundwe kuchunguza haya rais anayoyaundia tume. Kama mtu unafikiri na si kimgandomgando, unapata hisia kuwa raisi Jakaya Kikwete amelipiga bunge mwereka kimawazo. Ni katika msingi huu Bunge letu hasa vinara wake: Waziri Mkuu na Spika pamoja na wabunge wote waliounga mkono Zitto apewe adhabu wanafanywa ni wajinga ajabu.

Saturday, November 10, 2007

MSONGO WA MAWAZO TATIZO KUBWA UGANDA

Jamani watu wengi wana msongo mkubwa w a mawazo au wana tatizo la kisaikolojia; Uganda eti watu wengi wamechanganyikiwa. Pia ziara y a Museveni Marekani imekuwa gumzo juu ya uswahiba m p ya na Joji Kichaka.

MUSEVENI NA UTUNZI WA VITABU

Museveni ni rais mahiri kwani huwa anaandika vitabu na hata makala magazetini. Karibuni kaandika kitabu na kimeshangaza kidogo kimtazamo. M useveni anaaminika kama kiongozi bora ila kuna haja ya mabadiliko kwa mujibu wa jaji maarufu. Pia tujiulize je Big Brother ni muhimu sana?Pia benki zimeanza kuhimiza ndoa unazijua?
Pia tunajuzwa zaidi ni vipi Iddi A min alivyowapendelea watu wa kabila lake.

Kumbe John Garang aliuawa na serikali ya Uganda? Kumbe pia uzazi bila mpango ni chanzo cha Ukimwi kuenea kwa kasi? Mwisho kabisa hii ni kali yaani kuna kesi kubwa ya aina yake nchini Uganda.Unamjua mtuhumiwa wa wizi wa f edha za Gl obal Fund?Na ugonjwa wa m araisi wa Afrika je?

Monday, November 05, 2007

KWANINI VIGOGO WANAPENDA HOSPITALI ZA MAJUU?

Ama kweli bongo kuna vituko, huwezi amini eti madaktari wanaweza kosea namna hii; mambo kama haya yanawezekana bongo tu. Inawezekana ndio maana vigogo wanaziogopa hospitali za bongo.

Saturday, November 03, 2007

IDDI AMIN MZIMU BADO HAI

Kwanza kabisa leo tukumbushane juu ya Iddi Amin; alafu tutizame waasi wa LRA Uganda wanavyojaribu kujirudi.
Alafu kuna hili gonjwa la kisukari linakuwa sugu, hali ni mbaya Uganda.

Na kwa wale mapedeje, mnajua gharama zake?

Saturday, October 27, 2007

DR. JAMES WATSON NA MALUMBANO YA AKILI ZA MTU MWEUISI

Je akili za waafrika ni sawa na za wazungu? Ushindi wa urais bora kwa Chisano una ujumbe gani kwa maraisi wengine?
Mambo ya siasa ni kuwa eti kiranja wa bunge la Uganda ni mvunjaji sheria mkubwa.

Thursday, October 25, 2007

KWAHERI MAMA MBATIA

Ni habari za kusikitisha Naibu waziri wa wizara ya Maendeleo ya Wanawake, Jinsia na Watoto amefariki kwa ajali ya gari jana huko mkoani Iringa. Picha hii ni dhihirisho la ubaya wa ajali hiyo.
Huu ni mwaka wa ajali nyingi sana hasa kwa viongozi wetu, ni wazi kuna tatizo kubwa katika matumizi bora dhidi ya watumiaji wa vyombo vya moto.

Saturday, October 20, 2007

DUBE MWANAMAPINDUZI HALISI

Lucky Dube katutoka; ni jambo la kusikitisha sana. Mungu amlaze pema peponi. Dube alifahamika kila kona ya Afrika hasa wakati wa kipindi cha makaburu. Aliimba kuhamasisha dhidi ya ukaburu; sitamsahau.
\Pia tunakumbushwa kujali njia ya ABC dhidi ya Ukimwi na pia je unawajua Waganda wenye akili sana?