My Blog List

Wednesday, January 30, 2008

KIIZA BESIGYE NA MWAKA 2008

Kiiza Besyige anajulikana sana Uganda. Leo bado ni mwiba mkubwa kwa jeshi la uganda na anadai analijua wazi. Hivi tunajua ilimbidi amwache rafiki wake wa kike ili kujiunga na Museveni msituni na kuacha fani ya udaktari?
Kama unataka kujua madhara ya kupingana na Museveni, basi ona haya yaliyowakumba hawa waliojaribu.

MLIMA KILIMANJARO



Hii ndio Moshi, unauona mlima Kilimanjaro? Wanadai eti karibu theluji yake itakwisha. Ndivyo unavyoonekana leo hii.

Saturday, January 26, 2008

NIKIWA NGORONGORO NASHINO PAKI



Hapa nimesimama katika lango kuu la kuingilia Mbuga ya Ngorongoro.Mara nyingine hata mie natembea kidogo kama akina Majjid.Ilikuwa novemba mwaka jana.

NIKIWA SERENGETI

Hapa niko na wanafunzi wa BENDEL SECONDARY, huko mbuga za Serengeti november mwaka jana katika ziara ya mafunzo.

Friday, January 25, 2008

ODM INAWEZEKANA WAMEPOTEA NJIA KUANDAMANA

Raila Odinga na vigogo wenzake wa chama cha upinzani wamejaribu wiki iliyopita kuitisha maandamano mfulilizo katika juhudi za kutaka kumng’oa madarakani Raisi anayesemekana hakuchaguliwa kihalali—Mwai Emilio Stanley Kibaki. Muungano wa harakati za chama cha Chungwa (ODM) unajaribu kuiga yale maandamano ya wafuasi wa harakati za Chungwa kule Ukraine mwaka 2004 ambayo yalifanikiwa kuiondoa serikali batili madarakani baada ya kuiba kura.

Pamoja na juhudi hizi bado haionekani kama itawezekana kwani nadhani kuna sababu za msingi ambazo kwa wanaharakati hata wa hapa nchini hatuna budi tuzing’amue:

Kwanza kabisa, ODM inakosa kuungwa mkono katika maandamano na tabaka la juu pamoja na lile la kati. Hawa ni wale watu wanaojihusisha na biashara kubwa na za kati pamoja na wengine wengi ambao ni wafanyakazi katika serikali (Civil Servants) pamoja na sekta binafsi. Hawa ni watu wanaojiweza ambao kimtizamo wanaunga mkono ODM lakini kivitendo haiwezekani kabisa hata siku moja kujitokeza mitaani na kushiriki maandamano mitaani. Sana sana wanachofanya ni kuchanga fedha kuunga mkono waandamanaji kwa chakula, vinywaji na hata matibabu kwa wale wanaoumia. Wanafanya hivi kwani wanalinda mali na hata ajira zao nono zisipotee pale watakapogundulika wanaunga mkono upinzani.

Pili, ni raia masikini waishio kwenye mitaa ya mabanda (slums): Tofauti na tabaka la kati na matajiri, wakazi wa mitaa ya mabanda (slums) ambao ni masikini kila kukicha; hawana cha kupoteza ila wanabaki wakiamini labda ODM ikichukua madaraka wanaweza kubadili hali zao za maisha kitu ambacho ni vigumu kubashiri kama kitatokea. Tabaka hili la raia ndio wanaoandamana kila kukicha katika nchi nyingi za Afrika zilizojaa udikteta wa kila aina. Masikini ni vijana ambao wengi wao hawana elimu bora; wengine miongoni mwao wana elimu lakini kwasababu hawana ndugu (God fathers) ndani ya serikali ama hata ndani ya sekta binafsi basi ajira kwao ni ndoto.

Wamechanganyikiwa na kila ahadi kwao ni lazima waiamini hasa inapotolewa na wanasiasa mbadala kama Raila Amolo Odinga. Hili ni kundi kubwa katika miji ya Kenya kama Nairobi, Eldoret, Kisumu na Mombasa. Inakadiriwa ni nusu ya wakazi wa miji hii; lakini zaidi ya robo iliyobakia ni tabaka la kati na la juu na hawapo tayari kuhatarisha maisha yao kuingia mitaani kuunga mkono maandamano dhidi ya serikali batili. Wanachofanya hawa wanaojiweza ingawa hawaridhiki na serikali batili ni kukaa majumbani mwao wakiangalia runinga zao ni jinsi gani polisi wanavyopambana na waandamanaji; pia ni hawa wanaoandika sana barua kwa wahariri wa magazeti na hata kupiga simu redioni kushutumu serikali batili. Kamwe hawatashiriki maandamano au hatua yeyote ya harakati kivitendo ndani ya uwanja wa mapambano. Na ndio hapa Kibaki inawezekana kabisa akawa Raisi hadi miaka mingine mitano.

Kama tabaka la kati na la juu lingeshiriki maandamano haya basi ndani ya siku tatu polisi wa Kenya wasingeweza kuzuia waandamanaji kwani wangekuwa wengi sana hasa ukizingatia muundo wa miji ulivyo. Ila kwasababu maandamano yanatarajiwa yaanzishwe na masikini wa mitaa ya mabanda; na kwa mipango miji ilivyo, mitaa ya mabanda iko mbali na miji ama katikati ya miji (central business street) basi inakuwa ni rahisi kwa askari kwenda huko nje ya jiji na kuwazuia kuingia mijini. Wanafanya haya wakati wamewaacha matajiri na watu wa tabaka la kati wakiwa wamejifungia ndani ya nyumba zao zilizo mijini. Ni wazi kama watu wote wa tabaka zote wangejitokeza basi polisi watapata shida sana kuwazuia kwani itakuwa vigumu ukizingati kila kona ya jiji itabidi iwekewe ulinzi kitu ambacho si rahisi kwa askari kuhimili wingi wa watu kutoka kila upande.

Ingawa polisi wanaweza kuamua kuua kwa risasi za moto lakini kama watu wote niliotaja wataingia mitaani si rahisi kwa serikali ya Kibaki kuamrisha polisi kuua (shoot to kill) manake shinikizo la jumuiya ya kimataifa halitawaacha salama. Na ndio maana hadi sasa siku ya pili ya maandamano, silaha kuu ya polisi imekuwa ni maji yenye presha kali (water canon) katika kupambana na waandamanaji. Pia serikali haitakuwa na utashi na thubutu ya kuua wafanyakazi (Civil Servants) wake yenyewe ambao wengi wao ni kundi la tabaka la kati.

Kinachokwaza harakati ni kuwa tabaka la kati (middle class) hawana mwamko na uthubutu wa kushiriki maandamano wala harakati za mapinduzi moja kwa moja. Hawako tayari kupoteza kazi zao zenye malipo mazuri, mali zao kama nyumba zingine labda wamekopeshwa na serikali; pia la msingi kwao laweza kuwa ni wasiwasi kuwapoteza wapendwa wao: waume na wake zao wazuri pamoja na watoto wao wenye afya nzuri.

JE MAPINDUZI YATOKEE WAPI?

Naamini kama kweli ODM itafanikiwa basi ni kutokana na jitihada za masikini wa kutupwa (makabwela) ambao hawana cha kupoteza kama vile vibanda vyao vilivyojengwa kwa maboksi pamoja na wake zao wasiotamanisha na hata watoto wao wengi wao wenye utapiamlo. Inawezekana hatimaye wakafanikiwa; ila kama Raila atafanikiwa kumlazimisha Kibaki ampishe basi mshangao mkubwa utawakumba walalahoi wanaoandamana leo hii:

Mosi, lile tabaka la kati pamoja na matajiri wachache ambao ni waoga na wamejichimbia ndani sasa hivi wakitizama televisheni zao jinsi makabwela wakipambana na polisi ndio watakuwa wa kwanza kujitokeza na kupangiwa nyadhifa kadhaa na serikali mpya ya Raila kama itatukia. Hii itakuwa ni katika kuthibitisha maneno ya biblia takatifu: “Aliyenacho ataongezewa na asiyenacho atanyang’wanywa kabisa”.

Pili, kama mapinduzi hayatafanikiwa, tabaka la kati (middle class) hawajali sana kwani maisha yao yasiyo na kero nyingi yataendelea kama kawaida tena watajiona kama vile hakuna kilichotokea kwani wataendelea na kazi zao; mishahara yao minono na yenye ongezeko la asilimia 3% hadi 5% kila mwaka. Ni hawa hawa kila jioni baada ya saa za kazi wanajumuika kupata kinywaji wakijadili juu ya mapinduzi ambayo yatakuwa yamefeli.

Tatu, kwa upande wa masikini ambao tunawashuhudia wakipambana na polisi; iwapo harakati zitafeli basi wanajirudia vibandani mwao; maisha ya msoto yataendelea yaani kuamka alfajiri na kurudi majumbani usiku baada ya kazi za kitumwa kama vile: kazi za utarishi, ulinzi, utunzaji bustani za maua na pia kazi za viwandani ambazo zinazalisha asilimia tisini 90% ya uchumi wa nchi ilihali wao wanapata vipato vidogo na vya aibu sana.

Nne, pia ikiwa harakati za ODM zitashindwa basi wakati masikini wanateseka, matajiri pamoja na tabaka la kati wataendelea na maisha bila kujali; kwa kujiweka karibu na wanasiasa batili ambao wamewashinda masikini. Zaidi kila jioni watakutana katika sehemu za starehe kupiga soga na hata kucheza gofu.

Napenda pia tukae chini: lazima tujiulize hadi sasa kwanini ODM haijaweza kufanya maandamano licha ya nia yao ya dhati? Ukichukulia nini kilitokea kule Ukraine kama nilivyotaja awali, basi ni wazi jumuiya ya kimataifa haijaamua kuwaunga mkono. Kule Ukraine, Marekani iliwaunga mkono wanaharakati wa chungwa (Orange Revolution) kifedha kitu ambacho inaonekana Marekani inasita kwani pia haiamini kama kweli ODM ina jipya. Pia kule Ukraine, polisi walitambua kuwa nao pia ni sehemu ya tabaka dhalili dhidi ya ufisadi wa wanasiasa. Ila kwa Kenya na hata nchi nyingi za Afrika si polisi wala askari jeshi ambao wametambua hili: kuwa maisha magumu kwa baadhi yao yanachangiwa na serikali batili wanayoilinda kimabavu.

Kule Ukraine, polisi hawakupambana na waandamanaji hata kidogo kwani walitaka pia mabadiliko. Hapa Afrika hatujafika hatua hiyo na ndio maana nadhani ODM kufanikiwa kuiondoa serikali batili ni vigumu sana ingawa naamini juhudi zao zapaswa kuungwa mkono zaidi.

Tayari kuna tetesi kuwa kama hali ya maandamano itaendelea hivi, basi iko siku wanajeshi watapindua serikali ya kibaki na ndipo itakuwa mwanzo na mwisho wa kadhia hii. Ndio njia pekee ya kuanzisha upya mchakato mzima wa kuiepusha Kenya kuwa Taifa lililofeli (failed state). La sivyo yaliyowahi kutokea Liberia ama Ivory Coast yatatokea hapa. Na ndipo hapo wanasiasa wetu fedhuli na fisadi huku wakilindwa na vyombo vya usalama kwa kodi ya wananchi watang’amua kuwa raia wa kawaida anayo nguvu kubwa kuliko majeshi na bunduki zao.

TANZANIA IMETEKWA NYARA NA CCM

Miezi kadhaa imepita sasa baada ya mwanasaikolojia na mshindi wa nishani ya Nobel kuja na wazo lake kuwa “Waafrika ni dhaifu katika kufikiri ukiwalinganisha na wazungu ama watu wasio weusi”. Si mwingine bali ni daktari James Watson, mtaalam maarufu wa Saikolojia na mgunduzi wa sayansi ya chembe hai ( DNA) nchini Marekani na duniani kwa ujumla. Mawazo yake yalipokewa kwa machungu sana na watu weusi wengi kila kona ya dunia; lakini kwangu nilijaribu kuona hili kama changamoto hasa nikizingati mambo kadha wa kadha yanayotukia hapa nchini mwetu Tanzania na Afrika kwa ujumla.

Naye David Landes kaja na kitabu chake “The Wealth and Poverty of Nations: Why Some are so Rich and Some are So Poor”, akijaribu kutuonesha kwanini waafrika wako nyuma ya wazungu kiuchumi. Tatizo ni utamaduni anadai kwani anasema wazi utamaduni wa mwafrika ni dhaifu ama ni wa kiwango cha chini sana ukiulinganisha na ule wa wazungu. Kwa mfano anadai utamaduni wa mwafrika unakosa vikolezo kama kufanya kazi kwa bidii (hard working), uaminifu (honest), uwazi (open mindedness), na utashi wa dhati katika demokrasia (commitment to democracy)

Landes anasisitiza pia maendeleo ya kiuchumi yanategemea sana hisia (attitudes) za wananchi wake hasa uwezo wao katika kutumia au kutokutumia sayansi na teknolojia na hata fursa za kiuchumi pindi zinapojitokeza. Ni wazi utamaduni una nafasi kubwa sana katika kuendelea ama kutoendelea kwa jamii Fulani. Kwa mfano, Wajapan wanaamini kuwa utamaduni wao ndio chanzo cha mafanikio yao tunayoyaona leo hii. Yoshihara Kunio, kwa mfano ameandika kuwa: “Sababu moja kuendelea kwa Japan ni kuwa ina utamaduni wa maendeleo”. Wajapan wameweka msisitizo katika utafutaji mali (material pursuit), kufanya kazi kwa bidii, kuweka akiba ya siku zijazo( serving for future), kuwekeza katika elimu na kujali jamii (community value).

Tukirejea kwa Landes, anatuonya kuwa kuna tamaduni fulani ambazo ni sumu na mtu akiziamini na kuziishi basi ni umasikini. Kwa mfano, utamaduni wa wazungu/ magharibi ni wa ubinafsi (individualistic) zaidi wakati ule wa kiafrika ni wa kijamii zaidi ama tunaweza kusema kiasili ni utamaduni wa kijamaa unaojali wengi katika migawanyiko ya aina mbalimbali hasa kikabila. Ni katika msingi huu naweza kusema kuwa nadhani ni wazi utamaduni wetu hasa watanzania ni wa kijamii ambao leo hii umehama kutoka ukabila hadi kufikia kikundi cha watu ama jamii kisiasa: namaanisha vyama vya siasa vinavyowakutanisha makabila mbalimbali yenye maslahi yao ikiwa ni pamoja na kuing’ata nchi yetu bila huruma.

Kwa mfano, watanzania na waafrika kwa ujumla wao wamekuwa wakiamini ni lazima watumikie maslahi ya makabila yao. Hali si Kenya tu ila hata hapa kwetu mambo ni hayo tu. Katika kutumikia maslahi ya kikabila ndipo kwa mfano watanzania tunajikuta tukijirudisha nyuma sana kimaendeleo. Utamaduni huu mara nyingi hauruhusu kukosoana hasa pale viongozi ama wakuu wa kaya ama makabila mbalimbali wanapokiuka taratibu za kijamii. Kwa kawaida, wakuu wa familia ama jamii za kiafrika mara nyingi hawaadhibiwi; hakuna mfumo wa udhibiti kwao. Hawa ni sawa na miungu watu wanaotenda visivyo bila kuadhibiwa (impunity).

Maadam waafrika na watanzania tuna kasumba ya kutumikia jamii ama makabila yetu zaidi, basi leo hii tabia hii imejipenyeza hadi katika sehemu za kazi. Angalia hata siasa zetu sasa zimegeuka kuwa ni watu ndani ya vyama mbalimbali kama kikundi kwa maslahi yao na wala si maslahi ya pamoja (common interests) kama ilivyo Japan. Ni katika hili ambapo suala “uzalendo” limekufa na sasa ni maslahi ya kivikundi. Kwa mfano, unaposikia Taifa linakumbwa na upotevu wa fedha nyingi alafu serikali kuanzia Raisi hadi mawaziri wanashindwa kuweka mambo wazi juu ya wapi Gavana Ballali anakotibiwa, basi mtu unapata picha ni jinsi gani serikali ya CCM haiko tayari kuwa wazi kwa suala hili.

Hii yote ni kuonesha jinsi gani utamaduni wa kutoadhibu ama kutowajibisha wakuu wa kaya ama makabila ya kiafrika unavyoitafuna nchi yetu. Ni utamaduni wa karne kadhaa zilizopita ambao CCM inahakikisha utadumishwa ili watu fulani waitafune nchi yetu kwa maslahi yao na chama chao. Ukienda Bungeni na jinsi ambavyo hadi leo hii tangu kashfa ya BOT iibuliwe hakuna mbunge wa CCM aliyethubutu kusema jambo kuonesha kukerwa na hili. Nasubiri nione jinsi watakavyojiuma huko bungeni kuanzia wiki ijayo watakapokuwa wanachambua uchunguzi wa ripoti ya uchunguzi wa kashfa ya Richmond.

Tuna tatizo kubwa kitaifa: yaani mentalite (fikra) za viongozi wengi wa Tanzania ni mzigo mkubwa kwa Taifa. Kizazi cha uongozi cha sasa ni balaa kubwa sana kwa taifa hili kwani hawana tofauti sana na mababu zetu zamani enzi za ukoloni ambao hawakujua kufikiri kwa dhati. Naamini kama Rais Kikwete atatawala kwa miaka kumi basi utakuwa ndio mwisho wa mawazo mgando. Siku za kizazi cha mawazo mgando zinahesabika; kizazi kipya cha sasa chenye mawazo ya kisasa ya kuivusha nchi kutoka umasikini kinakuja taratibu. Ni kizazi ambacho kinawaza zaidi “utaifa” na si maslahi binafsi kama akina Balali na wenzake ambao wanajifanya wametengua uteuzi wake ilihali wengi wao ndio chanzo cha madudu aliyoyafanya.

Ninasema haya kwani hata yaliyotukia Kenya situ ni ukabila bali ni utamaduni huu wa watu katika vikundi vyao vya kikabila na kisiasa wanang’ang’ania madaraka ili kulinda maslahi yao. Chunguza kashfa kubwa kama Goldernberg alafu kama unalijua kundi la “ Mount Kenyan Mafians” ujiulize kwanini Kibaki anang’ang’ania madaraka? Ni hii tabia ya makundi fulani ya viongozi wetu ambao wataiibia nchi huku wakilindwa na wabunge wa chama chao dhidi ya ufisadi wao; kwani kwao bunge ni muhuri (rubber stump) wa kupitisha uchafu wao kwa maslahi yao. Ni tabia kama hii naiona ndani ya CCM ambapo ‘kupitia wingi wa wabunge wao ni wazi Tanzania imetekwa nyara na CCM’.

Kama kweli CCM kingekuwa ni chama cha kuiendeleza nchi yetu basi leo hii hizi kashfa za BOT, Richmond, Buzwagi zisingechukua muda na kutumia muda mrefu bila wahusika kuchukuliwa hatua za kuwajibishwa namna tuonavyo leo. Chama chochote kinapokubali kutumika kama muhuri wa kupitisha wizi na utapeli wa baadhi ya watawala basi ujue ni kwa ajili ya utamaduni mbovu wa kiafrika umekimeza.

Na kwa maana nyingine ni kuwa uwezo wa kufikiri wa wengi walioshikilia hatamu za chama hicho ni mdogo kama alivyosema daktari Watson anavyomwona mwafrika. Jamii kama hii haishangazi hata kidogo sera za kishikaji zinawekwa mbele sana; na jamii hii kufikia maendeleo ya kweli ni vigumu sana ukiacha maendeleo ya wachache wenye mashiko ya kikabila, dini, rangi na kisiasa hasa ukada wa chama. Ni kwa msingi huu naiona Tanzania, nchi yangu kama Taifa lililotekwa nyara na kikundi cha watu Fulani wachache lakini wanaoungwa mkono na watu wenye wajibu wa kuwawajibisha lakini hawataki. Hawa ni wabunge fulani ambao ama kwa makusudi kabisa ama kwa ufinyu wa kufikiri kama ule aliouelezea Dr. Watson basi wanaamua kuhakikisha Mafioso wa Tanzania wanashamiri.

Ni wazi CCM ndio pekee kwa uwingi wa wabunge wao wakiamua wataisafisha nchi yetu na kupambana na mafisadi wa Taifa hili. Mafisadi wengi wa nchi hii ni wanachama wa chama hicho; na ndio hapa pagumu kutegua kitendawili. Mungu wangu: mara nyingine mtu unajuta kuzaliwa katika Taifa lisilopenda kufikirisha bongo ilihali likijiita eti ni Bongo land.

Tuesday, January 15, 2008

MKASA WA BALALI--WASOMI WANAPOCHEZA NGOMA YA WANASIASA

Balali kafukuzwa kazi na Raisi Jakaya Kikwete; ni habari ambayo ilinishangaza manake tayari nilikuwa najua alikuwa ameshaandika barua ya kujiuzulu lakini inasemekana rais akamkatalia. Mimi nilidhani alimkatalia kwa kuwa ni msafi sana; na, hata ile tu kutuhumiwa katika ile listi ya aibu (list of shame) ya mtanzania makini na mzalendo wa hali ya juu, daktari Wilbroad Slaa, kuwa yeye ni kati ya mafisadi wa Taifa letu naamini ilitosha kwa mtu mwenye akili timamu kukaa kando achunguzwe ili asafishwe.

Balali pamoja na vigogo wengine waliziba masikio na kutufanya tumwone Dr Slaa kama vile ni msanii tu. Nchi yetu sasa inadhihirisha kuwa imekumbwa na ugonjwa mbaya sana wa kimaadili. Nakumbuka baadhi ya watuhumiwa wa listi ile ya aibu walitishia kwenda mahakamani lakini hadi leo wamekaa kimya na hata hawajathubutu kujiuzulu angalau. Yaani angalau wangeandika barua angalau basi wakataliwe tujue raisi ana imani na mafisadi.

Leo nataka nizungumzie suala la uwajibikaji; yaani mtu akichafuliwa asiendelee kukalia madaraka bali ajiuzulu ili aruhusu kusafishwa au awapishe wengine ambao wataweza kuendeleza nchi yetu kwa uadilifu. Labda nikumbushie tu hali tete kama hii ambayo ilijitokeza kule Ghana mara tu raisi John Kuffour alipoingia madarakani. Waziri wake mmoja wa mawasiliano na uchukuzi, ndugu Richard Anane, alituhumiwa kufuja fedha chini ya wizara yake. Ilipoundwa tume ya uchunguzi iligundulika ni kweli zaidi ya dola laki moja ziliibwa na mara moja akafukuzwa kazi. Nchini Uganda mawaziri wawili wa afya, Waziri Jim Muhwezi na naibu waziri, Mike Mukula waliamua kung’ang’ania madarakani licha ya tuhuma nzito za ufujaji wa fedha za Global Fund. Ilipoundwa tume baada ya shinikizo la vyombo vya habari, tume ilipendekeza wafunguliwe mashtaka mahakamani. Kesi yao bado inaendelea hadi leo.

Ni wazi kashfa inapoibuliwa kuna ukweli na ni vyema tujenge utaratibu wa kujiuzulu ili kuruhusu uchunguzi. Na kama hatufanyi hivyo ina maana kazi za umma zimegeuzwa kama za kifalme; yaani mtu hadi afe. Sasa yaliyomkuta Balali ndio kuanguka kwa mfalme.

Nimetoa mifano miwili kuonesha jinsi baadhi ya nchi za Afrika zinavyozingatia vita juu ya ufisadi. Hapa kwetu hata pale madai makubwa yanapotolewa bungeni,haindwi hata tume ya bunge na yanabezwa. Bado najiuliza ni kwanini tufanye uchunguzi kwa kutegemea kampuni za nje ilihali kamati ya bunge ama ya raisi ingeweza pia kuchunguza hili? Nina mashaka sana kama kweli jeshi la polisi, mwanasheria mkuu na hata Takukuru kama kweli wana utashi wa kimaadili (moral authority) kuweza kuchukua hatua kwa wahusika wa dhahama hili. Watanzania hatuna utamaduni wa kuwashughulikia watu wazito hasa wenye fedha na vigogo serikalini. Huu ni ugonjwa wa kitaifa na ndipo hapa nadhani Balali kaenda na maji kilichobaki baada ya miezi sita sidhani kama tutawajua zaidi waliohusika na sidhani kama kutakuwa na hatua kali zozote. Tanzania imejaa vigogo wasioshikika (untouchables) na sidhani kama tuna watu mashujaa kuwashughulikia mafisadi. Manake kama si utamaduni huu basi tangu wizi huu uanze ungekuta idara nilizozitaja zimeshughulikia lakini wapi.

Mara kwa mara nagusia sana juu ya “utawala bora”: serikali haieshimu sana taasisi zake (institutions) katika utendaji ila tunaamini zaidi katika watu (people). Unafikiri Balali angethubutu kuweka kapuni maadili ya utendaji ya gavana na aamue kuruhusu maamuzi ya watu binafsi yatawale utendaji wa Bot? Ni wazi gavana hawezi kufanya hasara kubwa hivyo kwa nchi kama kweli baadhi ya watu wa ngazi za juu hawashiriki katika maamuzi hayo. Ndio maana tumesikia eti baadhi ya fedha hizo zilitolewa kufanya “malipo nyeti”.

Serikali zetu za kiafrika zinaegemea zaidi katika utashi ama uswahiba unaozingatia mashiko ya kisiasa; yaani watendaji wetu pamoja na taaluma zao lakini wanacheza ngoma za wanasiasa. (pandering to the whims of politicians). Hii kwa kiasi kikubwa inasababishwa na mhimili mmoja wa serikali umekufa. Bunge letu, niliwahi kusema inawezekana kabisa ni Jumba la Sanaa la Taifa (National Theatre). Manake tukumbuke wakati madai haya yalitolewa bungeni yalibezwa sana kitu kilichowafanya wapinzani waamue kupeleka hasira zao kwa wananchi katika mikutano ya hadhara.

Bunge letu limedumaa na ndio maana watu kama akina Balali wanajifanyia watakavyo wakishurutishwa na wanasiasa kwani wanajua Bungeni hakuna mtu hajali kuhoji. Kama Bunge letu lingekuwa la nguvu na la viwango kama tulivyodanganywa wakati linazinduliwa Balali na mafisadi wenzake ungekuta wameshashughulikiwa siku nyingi sana. Ila jamii yenye bunge dhaifu (feeble parliament) wabunge walio wengi (majority) wataitetea serikali hata kwenye maovu. Mfumo mbovu wa bunge unamfanya mbunge wa chama tawala kuogopa kutengwa pindi atakapokwenda kinyume na maslahi ya chama chake pale yanapokinzana na utashi wake (conscience). Bunge halina sheria za kumlinda katika kuihoji serikali na kwa maana hiyo wabunge wengi wa chama tawala wanalazimika kuziasi akili zao na kunyamaza ama kuongea pumba pale hoja nzito kama ya Bot ilipoletwa bungeni.

Kucheza ngoma ya wanasiasa unakwenda mbali zaidi ya bungeni hadi katika taasisi mbalimbali za serikali. Naamini kabisa wakubwa wengi wa ngazi mbalimbali za serikali hawana uwezo wa kuzuia wimbi la kutumiwa (manipulation), kufanya maamuzi chini ya vitisho (threats) pamoja na mashinikizo au mibinyo (pressure) mbalimbali. Ni katika mtizamo huu ndio maana nakuwa na mashaka kama kweli polisi ama ofisi ya mwanasheria mkuu ina ubavu wa kuwashughulikia mafisadi.

Tunahitaji kuimarisha taasisi ya Bunge (legislature) ili kashfa kubwa kama hizi za ufisadi zisipigwe danadana kama ilivyokuwa kwa skandali hili la Bot. Ninaamini kabisa kama Bunge lingekuwa la viwango wala tusingefika leo; siku nyingi wahusika wangeadabishwa. Namaliza kwa kumsikitikia gavana Balali kwani sasa imethibitika kumbe yeye ni fisadi haswa; lakini nataka nihoji wasomaji: kuna tetesi kuwa jamaa haumwi, eti kazamia ughaibuni kama mkakati maalum wa mafisadi kupambana na skandali hili. Je kama ni kweli tutawashinda mafisadi?

Mwisho, ni wazi huu ndio mwanzo wa ukweli wa aliyokuwa akiyasema mheshimiwa Dr. Slaa. Hili la Bot limedhihiri; lakini maswali bila majibu vipi mafisadi wengine waliobakia katika ile listi ya aibu? Nasikitika hata mkuu wa nchi alitajwa. Kweli maneno ya meseji ya simu ya rafiki yangu juu ya kunijulisha Balali katimuliwa yana kila sababu ya kuaminiwa; aliandika hivi: “Jk amecharuka!Hapo kuna wengi wataguswa, ila sijui kama sheria itafanya kazi yake maana hilo ndio muhimu. Kwa jamii yenye taasisi zisizo huru (independent) sina mategemeo sana kama sheria itafuata mkondo kwa skandali hili.

Nabakia nikiamini inawezekana lakini tusipoona “mapapa” wakishughulikiwa kwa hili bali “kambale” sitashangaa kabisa. Demokrasia yetu bado hairuhusu kufika huko labda tuamue kwa dhati kabisa kubadilika. Na si kizazi hiki cha akina JK na wenzake. Nina wasiwasi sana kama kuna utashi wa kutosha kukabili hili. Eti kumbe Balali na wenzake ndani ya serikali wametuibia kiasi cha fedha kinachotosha kujenga shule za sekondari 1000? Jamani kumbe Tanzania inang’atwa haswa na mafisadi.

Monday, January 07, 2008

UTATA WA KENYA

Chanzo cha machafuko Kenya ni hiki;machafuko haya yanafananishwa na hali ya Pakistan. Pia Yesu kristu kagusiwa juu ya utata wa Kenya. Kutokuwa na machafuko haina maana eti kuna amani kama tunavodhani. Unajua madaraka yanapendwa sana na vigogo ila pia hata masikini imedhihirika Kenya.

Lakini Kibaki alisahau amani bila haki haiwezekani. Lazima tukubali demokrasia ni gharama.

Tunamwonea Kibaki, tatizo ni Kivuitu

SAMUEL Kivuitu, Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Kenya (ECK) ndiye chanzo cha machafuko yaliyojitokeza nchini Kenya baada ya kumtangaza Mwai Emilio Kibaki kuwa mshindi katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika mwishoni mwa mwaka jana, huku hana uhakika iwapo Kibaki alikuwa ameshinda kweli au la.

Baada ya kumtangaza kuwa mshindi, Kibaki aliapishwa chapuchapu kuwa Rais wa Kenya katika kipindi kingine cha miaka mitano ijayo.

Nilifuatilia matangazo ya moja kwa moja ya radio na televisheni, tangu uchaguzi hadi siku ya kutangazwa mshindi; mwenendo mzima wa uchaguzi huo ulithibitisha kuwepo dalili za matokeo ya kura za urais kuchezewa yalipofika katika ofisi ya Kivuitu kutoka vituoni.

Kabla hajatangaza matokeo hayo, Kivuitu alionekana kuwalaumu maofisa wasimamizi wa baadhi ya vituo vya uchaguzi kwa kuchelewesha kuleta matokeo.

Hii ilikuwa dalili ya kwanza ya kuwepo kwa mchezo mchafu, na hata alipofika mbele ya waandishi wa habari kutangaza mshindi, siku ya Jumapili iliyopita, alianza kutaja matokeo ya vituo vilivyochelewa na alipofikia kituo cha Molo, alisoma kura za Kibaki akitaja namba ya juu zaidi ya kura alizopata.

Kwa ushujaa kabisa, William Ruto, mmoja wa viongozi wa ODM, alisimama akihoji hesabu ya kura hizo, alimtaka ofisa aliyesimamia na kusaini fomu ya matokeo (form 16A) aliyekuwepo eneo hilo, athibitishe kama kilichokuwa kikisemwa na Kivuitu mbele ya hadhara ni kweli.

Lakini kwa bahati mbaya, katika kile kinachoweza kutafsiriwa kuwa kunyongwa kwa demokrasia, maofisa usalama walimdaka Ruto haraka haraka, wakamwondoa na kumpeleka ndani huku wakiacha zogo ndani ya ukumbi, matokeo yalipokuwa yakitangazwa.

Wakati nashuhudia zogo hilo likiendelea, mara Kivuitu alionekana katika kituo cha taifa cha televisheni akitangaza matokeo ya jumla ya kura za urais na kubatiza ushindi wa Kibaki na baadaye kidogo, redio na televisheni zikawa zikitangaza tukio la kuapishwa kwake Ikulu. Ilikuwa ni kama sinema vile, na nilijikuta nikiifurahia kwa kicheko maana yake muandaaji wake alifanikiwa sana.

Mara moja mawazo yalinijia na nikamkumbuka dikteta wa zamani wa Urusi: Joseph Stalin. Alijulikana kama bingwa wa mizengwe ya kisiasa. Aliwahi kusema kuwa: “Not the voters decide the winner in an election, but those who counts votes will decide everything.” Alikuwa akimaanisha kuwa katika uchaguzi, mshindi apangwi na wapiga kura, bali wale wanaohesabu kura.

Binafsi huwa sipigi kura katika chaguzi zetu kwa sababu naamini ni sawa na kupoteza muda na kuchafua kidole changu wakati mtu huwa tayari keshachaguliwa.

Mambo yanayotokea Kenya hayakuanzia hapo na wala si mageni barani Afrika. Mambo kama hayo yameshawahi kutokea katika nchi nyingi, tuna mfano mzuri kwetu sisi, ni yale yaliyowahi kutokea Zanzibar katika chaguzi kuanzia mwaka 1995.

Kwani tatizo hapa ni mgombea mmojawapo kutotakiwa na wanaoamini wao ni wazalendo zaidi ya wengine.

Hawa wamejipa kazi ya kuwachagulia wenzao viongozi. Kwao si kila mtu anayechagulika ni kiongozi, hivyo huamua kulifanya zoezi la uchaguzi kama kupoteza muda na fedha.

Kwa uchaguzi wa Kenya, Kivuitu ndiye tatizo baada ya kutangaza matokeo yenye hila na shaka. Alitangaza matokeo yaliyopikwa katika ofisi za makao makuu ya ECK. Baadhi ya makamishna wenzake walianza kuthibitisha hilo na hata yeye mwenyewe, alipoona maji yamefika shingoni aliibuka na kuthibitisha.

Kivuitu kama alivyokiri mwenyewe, ana dhambi dhidi ya wananchi wa Kenya: Mosi, wiki hii amenukuliwa na gazeti la The Standard, akidai hana hakika ni mgombea yupi alishinda urais. Inashangaza! Ilikuwaje akatangaza ni Kibaki?

Pili, ameamsha hasira ya wananchi kwa kudhani kwamba uelewa wake ni mkubwa kuliko wa Wakenya wote juu ya haki yao kikatiba ya kuchagua na kuchaguliwa.

Hasira za Wakenya zilizosababishwa na Kivuitu ambaye naamini kabisa kuwa aliyafanya hayo aliyoyafanya akijua madhara yake na matokeo yake, ndiyo mauaji kama yanavyoripotiwa katika vyombo vya habari kwa wiki yote iliyopita.

Dhambi ya tatu ya Kivuitu ni kushindwa kutenda kazi inavyopaswa; kwa uaminifu na kwa wakati muafaka. Dhambi hii inamfanya achorwe kama mhusika mbaya (sad character) katika sinema hii ya uchaguzi wa Kenya.

Wiki hii kawaeleza waandishi wa habari kuwa, eti alitaka kujiuzulu lakini akaona si muafaka kwa vile angeonekana mwoga (coward).

Kivuitu ameyatamka haya bila kujua yanadhihirisha jinsi asivyokuwa mzalendo wa kweli kwa kukubali taasisi anayoiongoza kuruhusu mapinduzi yasiyo halali nchini Kenya.

Huo ndio ukweli kwa sababu baada ya kuapishwa Kibaki, ilitolewa amri kuwa redio na televisheni ziache kurusha matangazo ya moja kwa moja. Udhibiti wa vyombo vya habari, hasa vya elektroniki, ni moja ya sifa za wapinduaji wa serikali. Mara wanapokamata madaraka, au wakiwa katika hatua za mwisho mwisho kufanikisha kukamata madaraka, wanakimbilia kudhibiti vyombo vya habari.

Amri ya kupiga marufuku vyombo vya habari Kenya ilitolewa na Waziri wa Usalama wa Taifa, John Michuki, akidhihirisha kwa nmna nyingine kuwa naye ni mshiriki katika mapinduzi hayo.

Hili liliwanyima wananchi haki ya kuhabarishwa juu ya kilichokuwa kinatokea na ni wazi hata matumizi makubwa ya nguvu za dola kudhibiti wananchi waliokuwa wanadai haki yao, ni sifa nyingine ya mapinduzi.

Haina ubishi kuwa wanausalama hawakuheshimu matokeo ya uchaguzi, ila waliamua kumuweka mtu wamtakaye atawale. Na kama nionavyo ni sahihi, basi Kibaki atakuwa rais asiye na maamuzi sana kwa vile amewekwa pale na kikundi cha watu wakishirikiana na baadhi ya maofisa wa usalama.

Kivuitu pia kama mwanasheria ambaye anafanya kazi baada ya kuapa, aliamua kwa makusudi kabisa au kwa kulazimishwa kutoheshimu majukumu yake ya kutenda kwa haki.

Hata hivyo, kwa kuangalia rekodi yake ya kusimamia chaguzi mbili: mwaka 2002 na kura ya maoni 2005 kwa ufanisi kabisa, inawezekana kabisa Kivuitu alishinikizwa chini ya mtutu wa bunduki kumtangaza mshindi.

Angalia jinsi alivyotaka kuporwa cheti cha ushindi na watu ambao nia yao ilikuwa ni kuona kuwa Kibaki anaapishwa. Hata alipofika Ikulu kupeleka cheti hicho, alikuta maandalizi ya rais kuapishwa yameshakamilika!

Mwenyewe ametamka kuwa alishinikizwa atangaze mshindi, vinginevyo jukumu hilo lingechukuliwa na mtu mwingine. Kama mazingira haya yalikuwepo ni wazi kuwa maisha yake yalikuwa hatarini na tunaweza kumuelewa, lakini kama hivyo ndivyo kwanini hasemi wazi? Hii nayo ni dhambi, dhambi ya kutokuwa mkweli!

Dhambi nyingine mbaya kabisa inayomuangukia Kivuitu ni chanzo cha machafuko haya kubadilika kutoka kwenye upingaji wa matokeo hadi kwenye mtazamo wa kikabila.

Hisia za watu wengi hivi sasa juu ya sinema hii ya uchaguzi wa Kenya ni kwamba, Raila ni mkabila na hafai kuwa rais. Haya ni madai ya kushangaza kwa sababu ukiiangalia ODM, haijakaa katika mtazamo wa kikabila hata chembe.

Hata ilivyosukwa hasa viongozi wake wakuu (pentagon) ni wa uwakilishi mpana wa jamii mbalimbali za Kenya. Wengine nimeongea nao wanaenda mbali zaidi na kuegemea katika ngano (myth) kuwa ‘Mjaluo hawezi kutawala Kenya hata siku moja.’

Nakubaliana na ngano hizi kwa sababu nimezisikia muda mrefu sasa kwamba Wakikuyu wanawadharau Wajaluo kama watoto wadogo ambao hawajakua kwa sababu tu hawaendi jando!

Hapa unadhihirika ushahidi mwingine kuwa Kibaki na watu wake wanaomzunguka wanaogopa kivuli chao na wana wasiwasi na utawala wa Raila kwamba unaweza kulipa kisasi kwa Wakikuyu ambao wamekuwa wakifanya hila ili wasitawale Kenya.

Katika mazingira kama haya, yapaswa kutafuta jibu zuri kwa swali la nani ni mkabila kati ya Kibaki na kundi lake na Raila?

Jambo la muhimu kuzingatiwa katika utata huu uliosababishwa na Kivuitu ni kwamba, matatizo ya uhesabuji kura sasa yamekuwa mazoea Afrika Mashariki.

Mwaka 1995 kule Zanzibar yalitokea, 2001 na 2006 kule Uganda pia yalitokea. Ni wazi bado tu wachanga sana kwenye suala la utawala bora.

Yaani, taasisi zetu hazifanyi kazi kwa uhuru bali zinamtumikia mtawala (rais). Ni katika msingi huu tatizo la Kenya haliwezi kutatuliwa kwa majadiliano wala kwa kwenda mahakamani.

Haliwezi kutatuliwa mahakamani kwa sababu ni mahakama hiyo hiyo iliyomuapisha Kibaki kupitia kwa Jaji Mkuu, haraka haraka baada tu ya Kivuitu kumtangaza kuwa mshindi.

Hapa napo Jaji Mkuu wa Kenya, Moses Gicheru, naye keshapoteza mamlaka ya kimaadili katika kusimamia kesi yeyote dhidi ya uovu wa Kivuitu.

Itashangaza sana iwapo Raila akiamua kwenda mahakamani kulalamikia ushindi wa Kibaki, halafu mahakama hiyo hiyo, ambayo ndiyo iliyomuapisha Kibaki, iamue kuwa ushindi wa Kibaki ni batili. Lakini hawa wote wameingizwa dhambini na Kivuitu ambaye kama asingekubali kupindua matokeo, hali ya Kenya isingekuwa kama ilivyo sasa. Kama Kivuitu asingekubali kutangaza matokeo kwa shinikizo, angesubiri mpaka uhakiki ukafanyika na kila mmoja akawa na imani na matokeo, wala haya yasingetokea.

Waafrika tunapaswa kuwa makini zaidi sasa na watu wa aina ya Kivuitu ambaye historia yake inaonyesha kuwa hata wakati akisoma Chuo Kikuu cha Dar es Salaam aliwahi kumkorofisha Mwalimu Nyerere hadi akaitwa ikulu.

Utukutu wake wa utotoni ndiyo matokeo ya machafuko yanayoendelea nchini Kenya.

Kwa sababu hizo, kuna kila sababu ya kuchagua watendaji na wasimamizi wa shughuli mbalimbali za kitaifa kwa kuangalia historia zao.

MJUE UNDANI WA JOSEPH KONY

Leo nataka watu wamjue Joseph Kony ni mtu wa aina gani kutoka kwa mtu aliyesoma naye. Pia tujue ili Afrika iendelee, kuna mengi zaidi ya viwanda ya kufanya.

Wednesday, January 02, 2008

ETI KIVUITU ALISHINIKIZWA?

Imedhihirika kuwa mwenyekiti wa tume ya Taifa ya uchaguzi alishinikizwa kutangaza matokeo ya uchaguzi. Je hii si ndio chanzo cha uoza wa dhahama na mauaji?

KIU YA UONGOZI TATIZO LA WAZEE KAMA KIBAKI

Uchaguzi Kenya umekwisha kwa mizengwe lakini mambo ni mabaya kabisa. Ni wakati wa viongozi wa Kenya kufikiri sana. Mwanazuoni mmoja anatoa ni kwa vipi wanasiasa walikuwa wamejisahau.
Pia vurugu za Kenya ni chanzo cha madhara eneo zima la Afrika Mashariki. Kwa waganda wanajiuliza je ni Uganda ina demokrasia zaidi ya Kenya?