My Blog List

Wednesday, December 19, 2007

ZUMA AANZA HARAKATI ZA KUWA RAISI WA BONDENI

The image “http://www.mg.co.za/ContentImages/328066/zuma.jpg” cannot be displayed, because it contains errors.

Bado nina hisia mchanganyiko manake kuchaguliwa kwa Zuma kuiongoza ANC ni matokeo ya demokrasia. Ila mara nyingine demokrasia ina matatizo yake; hili ni tatizo kwa Afrika ya kusini kabisa.

Vijana wa ANC nao wana mashaka sana na uchaguzi wa Zuma kwani hana haiba nzuri ya kiongozi.

Wednesday, December 12, 2007

SIASA ZA BONDENI ZINACHEKESHA

Yaani mara nyingine inafikia wakati mtu anaamini kuwa siasa zetu zimebakwa na wanasiasa. Pia huko somalia, amechaguliwa waziri mkuu mpya je, ataweza kazi yake?

UHURU NA AKILI MGANDO ZA BAADHI YA WATAWALA

Taifa letu lilitimiza miaka arobaini na sita (46) tangu lizaliwe; jumapili iliyopita ilikuwa ni kumbukumbu ya siku ya uhuru kwa maana nyingine. Kama mtanzania, na mzalendo sina budi kuchukua kalamu na kutafakari kwa kina miongo kadhaa kama Taifa ni changamoto gani tumezikabili na zipi inatubidi tupandishe soksi (pull up socks) ili kuendeleza nchi yetu. Binafsi, naamini kama tutafanyia kazi changamoto ya “Utawala Bora” basi uhuru wetu utakuwa na maana sana. Mada yangu itaegemea sana hapa tu.

Kabla ya kujadili, nitoe pongezi kwa watanzania wote tangu raisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete na kwa ujumla watu wa kada zote hapa nchini kwa kuadhimisha siku hii.

Bila ubishi kabisa, nchi yetu imefanikiwa sana katika nyanja mbalimbali tangu uhuru hasa ukilinganisha na nchi nyingine za dunia ya tatu. Hapa ieleweke hata kama tungekuwa tumefanikiwa kiuchumi kama vile Wachina ama Wajapan bado kungekuwa tu na matatizo. Hivyo si vyema kubeza kuwa labda kila kitu ni mrama; yapo mafanikio kama vile umoja wa kitaifa ambao ni mfano dunia nzima. Binafsi nimekutana wa watu kadhaa kutoka pande mbalimbali za dunia wanaposikia umetoka Tanzania watasifia Umoja wetu. Hii yote ni heshima za mwasisi wa Taifa, hayati Mwalimu Nyerere.

Kuendana na mfumo wa kiutawala duniani, yapo mapungufu mengi ambayo nadhani ni vigumu kujikwamua nayo hasa ukizingatia mfumo mzima wa biashara ulimwenguni ni wa upendeleo na ukandamizaji kwa sera za mashirika makubwa ya kiuchumi na kibiashara ulimwenguni. Hapa nazungumzia sera za Mfuko wa Kimataifa wa Fedha (IMF), Benki ya Dunia (WB) na Shirika la Biashara Ulimwenguni (WTO) mwanzoni likijulikana kama GATT.

Ndio maana kama mtu anafuatilia hata yale majadiliano kibiashara ya kule DOHA yamekwama kabisa na ni wazi watawala wa dunia hawataki kabisa kukubali baadhi ya hoja ambazo zitalikwamua bara la Afrika kutoka umasikini usiokwisha. Hata hivi majuzi, Taifa letu limesaini makubaliano mapya ya mashirikiano ya kiuchumi na Jumuiya ya Ulaya (EU) yajulikanayo kama (EPA) kwa kutumia mgongo wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ambayo ni wazi yameshinikizwa na hayatailetea nchi yetu tija sana kinyume na inavyodhaniwa na wale waliosaini. Inajulikana wazi tumelazimishwa kwa kuharakisha kusaini kabla ya ule mkataba wa Cotonou kumalizika hapo December 31 mwaka huu. Nisijadili hili zaidi labda siku nyingine.

Ni katika mchakato huu wa changamoto hizi za mabepari basi hata kama watawala wetu wanao utashi inakuwa vigumu kuweza kusimamia maslahi yenye tija kwa nchi zetu. Kwani mara nyingine watawala wetu wanapokuwa na utashi wa dhati basi mambo kama yanayomkuta Robert Mugabe hayazuiliki kwani wanaishia kufanya maamuzi kwa pupa, bila kufikiri kwa mpangilio na kwa logiki ambayo yanagharimu maisha na uchumi wa nchi zao. Ndio changamoto za “Uhuru” ambazo kwangu ni jinamizi tu; kwani, tunaposherehekea siku hii lazima tuelewe inawezekana kabisa siku ile ilikuwa ni mwanzo wa kipindi cha giza. Ningependa nielezwe hivi Mwalimu Nyerere alipokwenda kule Lancaster alikwenda kusaini mambo gani? Manake inatia shaka huenda ndio ulikuwa wakati wa kujitia kitanzi badala ya kuwa huru. Kwani nina mashaka sana kama kweli tuko huru.

Na ndio maana bado tuna changamoto nyingi sana za kutafakari na kujiuliza tufanye nini? Kwa mtizamo wa serikali ya awamu ya nne, ni wazi changamoto kuu ambayo lazima ifanyiwe kazi ni hii ya “utawala bora”. Hii imebaki kuwa ngonjera na kama hatubadiliki kwa hili basi kamwe hatutapiga hatua yeyote. Nasema hivi kwani naamini pamoja na changamoto za jinamizi la uhuru linaloongozwa na sera dhalimu za kimataifa bado tuna mengi ya kufanya kwa hapa nyumbani ambayo yatatuwezesha tuwe bora tu mbali na mashinikizo dhalimu ya mabepari.

JE TUFANYE NINI?

Tunahitaji kufikiri zaidi ya kuongea sana; hii itatuwezesha kuwekeza katika kuwajibika kwa bidii (hardworking) badala ya kupiga siasa kwa muda mrefu zaidi. Ni wazi hadi leo hii, bado utendaji wetu umetawaliwa na mashiko ya kisiasa zaidi kuliko nidhamu ya kazi katika nyanja mbalimbali. Hasa katika chombo kama Bunge, ni lazima tubadilike; miaka arobaini na sita itufanye tuamue sasa ni mwisho wa siasa za upande mmoja usiozingatia maslahi ya umma. Njozi za chama kushika hatamu zisipoachwa basi hatufiki popote kama Taifa la miongo hii minne na ushehe.

Kwa watawala wetu, lazima kung’amua kuwa kama mhimili wa utawala (executive) unakuwa na nguvu kubwa dhidi ya mihimili mingine basi hatufiki. Pamoja na nguvu ya kikatiba ya taasisi ya uraisi, Uhuru unakuwa na maana kama kiongozi mkuu wa nchi atang’amua hili na kuruhusu utendaji unaoruhusu majadiliano ya vyama vyote vya mitizamo tofauti ndani ya bunge badala ya kuzingatia tu upitishaji wa maamuzi yenye kuegemea uchama na si umma.

Ingawa demokrasia inasema ‘wengi wape’, lakini nadhani pia tuangalie mfumo wetu wa upigaji kura na maamuzi ya upitishaji sheria ama maamuzi bungeni ukoje? Je unaruhusu upigaji kura wa wabunge wa chama tawala unaozingatia uhuru wa mawazo ya mbunge au ni kushurutisha kwa kuegemea maslahi ya chama yaliyofichwa ili kulinda maslahi ya vigogo wa chama tawala bila kutoa sababu za msingi kuhusu jambo fulani ili kulinda maslahi ya nchi.Uhuru unaweza usiwe na maana sana kama mfumo wa maamuzi ndani ya chombo kama Bunge unambana mbunge mwenye mawazo tofauti.

Hata ndani ya vyama vya siasa, ni changamoto pia kujiuliza hivi kuna uhuru wa mawazo wa mbunge katika kujadili mambo na hata kuhoji ndani ya chama? Yaani kwa miaka yote hii arobaini na sita, bado ni kosa la jinai ndani ya chama tawala kwa mtu kujadili hisia zake kwa uwazi inavyoonekana na hata kupinga ama kupiga kura ni udikteta tu (intra-party disagreement, debate and even voting is still a crime). Hapa lazima watawala wakumbuke hili ndilo linalokwamisha maendeleo yetu na hapana budi tuweke mizani ya usawa (strike a balance) katika utendaji wa serikali dhidi ya mihimili mingine miwili hasa ule wa Bunge tukianzia ndani ya vyama vya siasa.

Kwa mfano, kama tutazingatia utawala bora, basi lazima tubadili mitizamo yetu (mentality): yaani serikali iwe kwa ajili ya umma na si kama jamvi la kuficha mafisadi kama ilivyokwishajidhihirisha kwa watuhumiwa wa ufisadi kutajwa hadharani na wao kuamua kukaa kimya bila kujisafisha. Hata mamlaka yenye uwezo wa kuwawajibisha nayo haikuchukua hatua zozote. Ndio hapa bado inaonesha tunawaza zaidi katika kulinda maslahi ya kisiasa kuliko ya umma. Yote hii inashawishi mtu mwenye akili timamu kuwaza na kuamini labda ni kwa sababu ya utawala mbovu. Mfumo wa “Check and Balance” uko likizo ili tu kulinda maslahi ya kisiasa ya chama kinachotawala. Huu ni ugonjwa mkubwa barani Afrika na kama hatubadili mtizamo “Uhuru” unakuwa hauna maana.

Ninaamini kama watanzania, tuna bahati ya kuwa na raisi wa nchi ambaye ana karama ya kuongoza kwa kujali demokrasia; kwani anajitahidi kujumuisha pande na hisia mbalimbali za kisiasa katika utendaji wake. Mashaka yangu bado nadhani waliomzunguka raisi wetu mitizamo yao imepitwa na wakati na si endelevu. Ni mitizamo ya kusisitiza zaidi ‘umilele-chama’ (party-omnipresence) kuwa na woga labda chama kitaangushwa madarakani kwa kile wasichokijua. Na hii ndio chanzo cha madhila kadhaa zinazoisumbua serikali ya awamu hii.

Ni changamoto nzuri za kumfanya raisi na wasaidizi wake kuliona hili na kuamua kubadilika. La sivyo tuna hatari ya kubakiwa na “Kiongozi mwenye karama asiye na mwelekeo” (a charismatic leader without a cause). Mwelekeo wa sasa kwa nchi huru unatia shaka kwani uwezo wa kufikiri wa vigogo wengi ni mdogo sana na ni wazi unasababishwa na tamaa ya fedha na ulafi wa kila aina. Kitu woga kwa viongozi wetu ndio chanzo cha udhaifu wa viongozi wetu kuanzia juu.

Siku ya leo tujiulize ni kwa jinsi gani utawala wa shaghala baghala ulivyogharimu taifa letu kwa kipindi chote cha uhuru. Tunaweza tukalaumu sana na kusingizia mfumo wa kidunia (world order) ambao nimeuelezea awali, lakini kama tuna akili timamu ni wazi kwa nafasi yetu kwa mambo ya hapa nyumbani tuna mapungufu pia ambayo lazima tuamue kwa dhati kuyafanyia kazi. Ndio maana hata Raisi wetu majuzi alisikika akisema na kukiri hata hii mikataba ya madini ni sisi wenyewe wa kujilaumu mbele ya Waziri Mkuu wa Canada mheshimiwa Stephen Harper.

Kama Taifa, miaka arobaini na sita ya Uhuru haina maana sana kwani tumeshindwa kukabili changamoto za ndani kabisa. Inakuwa vigumu kukabili zile za nje manake watawala wa dunia wanatumia udhaifu wetu huu kutulaghai kwa kila hali. Kama hatubadiliki kwa kuruhusu kukosoana ndani ya vyama vyetu, bunge letu na kila mahali ili kulinda maslahi ya umma basi kamwe sioni maana sana ya uhuru. Ninachokiona ni sana sana ni juhudi kubwa tena hasi (highest retrogressive endeavour) za watawala na wanasiasa katika kuirudisha nyuma nchi yetu kwa kasi.

Uhuru bila ‘utawala bora’ ni kwa wachache na si kwa umma wa watanzania. Kama siku ya Jumapili, leo nitamwomba Mungu aizindue akili ya watawala na wanasiasa kwa ujumla wao kubadili mitizamo. Tuachane na akili mgando ndio uhuru utakuwa na maana. Miaka arobaini na sita ya Uhuru ije na mtimzamo (mentality) mpya kuhusu utawala wa Taifa hili. Hii ndio tafakuri yangu ya siku hii ya uhuru kwa leo.

MAWAZIRI NAO HAWALIPI BILI YA MAJI MPAKA WAKATIWE?

Kama unataka kuamini kuwa ni vigumu kwa nchi ya Tanzania kuendelea basi amini kwa haya ya vigogo wa serikali tena mawaziri eti hawalipii kodi ya maji mpaka wakatiwe.
Ni wazi hatuwezi kuendelea kama hata mawaziri hawako makini kiasi hiki. Sasa kama waziri halipi bili ya maji je wananchi wa kawaida watalipa? Nakwambia bado tuko kwenye lepe la ujamaa ambapo kila kitu kilifanywa na serikali.
Hebu soma habari hii alafu ushangae ni vigogo gani hao?

Mawaziri wasiolipia maji watajwa

::Yumo Waziri wa Maji, Msola, Hawa Ghasia
::jumbe wa vitisho watumwa DAWASCO


na yasmine protace

MAJINA ya mawaziri sita, ambao ni miongoni mwa wateja wa Kampuni ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASCO), waliokatiwa maji baada kushindwa kulipia ankara, yametajwa.

Mawaziri hao wanaoishi eneo la Masaki, jijini Dar es Salaam, pamoja na wakazi wengine wa eneo hilo, walikatiwa maji wiki iliyopita.

Kabla ya kuwakatia maji, DAWASCO kupitia Ofisa Mtendaji Mkuu wake, Alex Kaaya, iliwaomba wateja wanaodaiwa kulipia ankara wanazodai.

Katika maombi hayo kwa wateja, DAWASCO ilitoa siku tatu wateja hao kulipia ankara hizo, hata hivyo ni wachache tu waliotii.

MTANZANIA imefanikiwa kupata baadhi ya majina ya mawaziri wanaodaiwa ankara, ambao ni pamoja na Waziri wa Maji, Dk. Shukuru Kawambwa.

Wengine wanaodaiwa ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mizengo Pinda na Waziri wa Maendeleo ya Mifugo, Anthony Diallo.

Katika orodha hiyo, Waziri wa Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Peter Msolla, naye ametajwa, pamoja na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Hawa Ghasia, naye ni mmoja wa mawaziri hao.

Akizungumzia kilichomsibu hadi kushindwa kulipia ankara zake kwa kipindi kirefu, Waziri Ghasia alidai kuwa tangu aanze kuishi katika nyumba hiyo amekuwa hapati huduma ya maji.

Alisema amekuwa akinunua maji kutoka kwa wafanyabiashara binafsi na si kampuni ya DAWASCO.

“Kwa hili jambo ni la binafsi mno. Lakini hata hivyo, lakini sikuwahi kupata huduma ya maji ya DAWASCO na zaidi sikuwahi kupata hizo bili. Sikuwahi kuletewa bili hadi leo,” alidai Waziri Ghasia.

MTANZANIA pia iliwasiliana na Waziri Msolla kwa simu, ambaye alikiri kudaiwa, lakini akadai kuwa hakuwa akifahamu taratibu za kupata ankara na malipo.

“Ni kweli kwamba hilo suala (la kudaiwa) lilikuwapo, nami sikuwapo nchini… lakini last week (wiki iliyopita) tulipata bili na tumekwishalipia,” alisema Prof. Msolla, ambaye hakuwa tayari kuzungumza zaidi kutokana na kile alichodai yupo katika mkutano.

Waziri Simba hakuweza kupatikana, baada ya kuwasiliana naye kupitia simu yake ya mkononi. Majibu kutoka kwa aliyepokea simu hiyo yalieleza kuwa waziri huyo yuko safarini Marekani.

Waziri wa Maji, Dk. Shukuru Kawambwa, Waziri wa Maendeleo ya Mifugo, Anthony Diallo, Waziri wa TAMISEMI, Mizengo Pinda, hawakupatikana, baada ya simu zao za mkononi kuita kwa muda mrefu bila kujibiwa.

Hata hivyo, katika hali ya kushangaza, DAWASCO imesita kuzungumzia majaliwa ya viongozi hao kurejeshewa huduma ya maji.

Meneja Uhusiano wa kampuni hiyo, Badra Masoud, alisisitiza kwamba, walichokifanya ni kukata maji kwa wadaiwa.

“Tunadai fedha nyingi sana Masaki, hivyo tunataka tuendelee kutoa huduma bora kwa wateja wetu ambao wanalipa na wasiolipa tumewakatia mpaka hapo watakapolipa,’’ alisema.

Eneo jingine lililokatiwa maji mbali na Masaki ni Mbezi Beach. Hata hivyo, tofauti na Masaki, wateja wa Mbezi Beach wamekuwa wakijitokeza kulipia ankara zao.

Katika hatua nyingine, DAWASCO imedai kupokea vitisho baada ya kuwapo kwa operesheni hiyo ya ukataji maji.

“Watu wananipigia simu na kunitaka niwarudishie maji eti sijafanya vizuri, lakini mimi nimesema kwamba maji yatarudishwa kama watumiaji watalipia ankara zao,’’ alisema.

Aliongeza kwamba pamoja na kupigiwa simu, pia amekuwa akitumiwa ujumbe wa maneno ya kashfa kutoka kwa watu asiowafahamu.

Takwimu za DAWASCO zinabainisha kuwa, eneo la Masaki lenye wateja 1,270 linadaiwa Sh milioni 574, wakati Mbezi Beach kuna wateja 1,271 wanaodaiwa Sh milioni 578.

Eneo la Ada Estate lenye wateja 475 wanadaiwa Sh milioni 527, Mwenge wateja 733 wakiwa wanadaiwa Sh milioni 463 na Regent kwenye wateja 222 wanadaiwa Sh milioni 200,’’ alisema.

Ni kwa misingi hii jamani tutaendelea kama tunakuwa na viongozi makupe?Yaani kwao kila kitu bure tuu? Ni wazi hata kodi nyingine nadhani hawalipi?Pafanyike uchunguzi hapa.

Saturday, December 01, 2007

TANZANIA BILA UKIMWI INAWEZEKANA?

Siku ya Ukimwi duniani; ni wakati wa kila mtu hasa mwafrika kutafakari juu ya balaa hili ambalo limeshachukua roho za watu lukuki. Wakati naandika makala hii mara nasikia redioni kuwa huko Mbagala Kizuiani kuna jamaa mmoja kaamua kujiua baada ya kuthibitishiwa kuwa ana virusi mwilini mwakeMwingine kaamua kumuua mkewe huko Mbeya baada ya kusikia mkewe kapima bila ruhusa yake

.Ni habari za kusikitisha lakini ni lazima tujiulize hivi kweli hizi kampeni za upimaji ndio jibu la dhahama hili? Na pia tujiulize kwanini tunahofu juu ya kuambiwa tumeathirika?Je hatupo tayari kuwajibika na matokeo ya tabia zetu za ngono zembe?

Napenda niseme kuwa hizi kampeni za upimaji ukimwi zinanitia wasiwasi kama kweli ndio muarobaini wa gonjwa hili. Nasema hivi kwani ni zaidi ya miaka ishirini sasa tangu nimeanza kusikia habari za ugonjwa huu. Na kwa muda wote huo kampeni mbalimbali za kuhamasisha na kuelimisha kuhusu ugonjwa huu zimekuwepo. Ndio maana leo hii katika kampeni hizi za rais Jakaya Kikwete, hakuna jipya linalosemwa. Nimesikiliza, kutizama na hata kuhudhuria semina juu ya gonjwa hili kwa kweli sijaona kipya chochote juu ya elimu ya gonjwa hili.

Nikirejea kwenye mafunzo yatolewayo shuleni: msingi, sekondari na hata katika vyuo kupitia mitaala mbalimbali, nadhani watanzania kama jamii tuna tatizo. Ni jamii isiyojishughulisha kabisa kusoma na kujielimisha binafsi. Habari juu ya gonjwa hili zimesambaa kila kona kwa miaka ishirini iliyopita: vitabuni, majarida, vibwagizo, kwenye mitandao ya intaneti na magazetini, lakini watanzania hatujishughulishi kupata mafunzo lakini tunataka semina, makongamano na hata vipindi vya redio na televisheni visivyo na jipya juu ya gonjwa hili kila kukicha. Kuna haja ya watanzania kuamka katika kujali umuhimu wa kujua mambo yanayohusu maisha yao. Bila hivyo sidhani kama tutafika popote katika vita ya gonjwa hili.

Hivi kweli inaingia akilini kuwa hadi leo hii watanzania watu wazima kwa vijana hatuna uelewa wa gonjwa hili?Miaka yote tumeishi na gonjwa hili yaani hatulifahamu? Nisingetegemea tuwe na kampeni kubwa kama ya sasa na ambayo hatima yake bado ni kutokupungua kwa maambukizi kwani kuna kila dalili watu wengi wameziba masikio.

Nashangazwa na upimaji kwa siri: mosi, hivi kama napima kama nina virusi alafu nasema ni siri yangu, na sitaki watu wajue kama nimeathirika, si kuwa ninataka kuendelea kujichanganya visivyo na watu wengine ili niwaambukize? Kwanini tusiwe na utaratibu wa kistaarabu wa waathirika kuhimizwa kwa ushauri nasaha ili wajiweka wazi na hata kujiunga kwa uwazi na taasisi za waathirika kwani kwa sasa wengi wao ni kwa siri sana. Hapa siongelei unyanyapaa, ila ni vyema watu wawe huru kutambuliwa kwani kama usiri utaendelea kutiliwa maanani zaidi, basi hii kampeni haitatusaidia sana kwani kuna kila shaka ya kuendeleza uambukizi zaidi.

Uwazi huu pia ungeoneshwa hata kwa wanajamii vinara: wabunge, mawaziri, na viongozi mbalimbali wa jamii. Kwa mfano, kama tungejulishwa angalau taarifa za upimaji kule bungeni, je wangapi walipima, wangapi walionekana kuathirika ama kutoathirika. Lakini kupambana na ukimwi kwa usiri hakutakomesha ukimwi kamwe.

Pia nashangazwa na hizi juhudi za upimaji hazijaonekana sana katika taasisi za elimu hasa elimu ya juu. Huku kuna vijana lukuki na ingekuwa vyema hapa watu wapimwe manake ndio viongozi wa kesho tunaowatarajia na tukiwaacha ngono mbele kwa mbele basi tujue kuna mahali ambapo paangaliwe manake kwa muono wa karibu ni sehemu ambapo maambukizi yanawezekana kuwa kwa kasi sana.

Linalonishangaza sana ni kuwa Ukimwi umekuwa ni mradi mkubwa kwa baadhi ya watu flani na vitaasisi vyao vyenye utegemezi wa wafadhili. Ni wazi kuna watu wanafurahi sana ongezeko la wagonjwa wa ukimwi na hata yatima. Bila gonjwa hili watu wengi hawataajiriwa na wengine wangekuwa masikini kabisa. Najua siku hizi imani za kidini ni kiini macho kwa wengi kutokana na matendo yao. Ni kwa misingi hii vita ya gonjwa la Ukimwi inaonesha kama vile hakuna Mungu.

Ukimwi bado ni kiini macho kupambana nao kwani hadi leo bado watu wanaugua gonjwa hili lakini utasikia eti wamekufa kwa vigonjwa vingine ama wamelogwa na mambo mengine ambayo mtu mwenye akili inashangaza sana. Kuna haja mtu anaugua gonjwa hili awe tayari kusema nilikuwa naugua gonjwa hili bila aibu. Tunazika watu wengi hata wasomi kabisa ambao wakati wa kuugua anaonekana anaugua Ukimwi ila siku ya kufa utasikia eti anaumwa sijui kansa, presha na kadhalika. Ni usiri wa kijinga tunauendekeza na ambao hatima yake ni kiini macho cha vita ya ukimwi. Umefika wakati tuache usiri bila hivyo ni vifo bila mabadiliko.

Mwisho, nadhani kwa mwenendo wa sasa, “Tanzania bila Ukimwi” haitawezekana kama raisi wetu anavyotusihi. Usiri huu kwa kisingizio cha kuzuia unyanyapaa ni chanzo cha janga hili kuendelea. Siamini nchi yetu inaweza kuendelea, ni wazi gonjwa hili litaendelea kudumaza na kuwamaliza wasomi wa nchi yetu. Ni mwaka wa ishirini na saba tangu gonjwa hili livamie nchi yetu na bado watanzania wengi hawajaamua kuacha ngono zembe, ni mwanzo wa kiama Tanzania.