My Blog List

Saturday, November 08, 2008

JANET MUSEVENI MWANAMAMA SHUJAA?


Huko Uganda kuna skandali kubwa juu ya ufisadi wa mawaziri wawili ambao ni watu wa karibu wa Bwana Museveni. Jamaa kaamua lazima wasafishwe na wabunge wa chama tawala hivyo akaitisha wabunge wa NRM ili kuwekwe mkakati wa kuwasafisha mafisadi. Kilichotokea ni kituko kwani Mke wa Museveni ambaye ni mbunge wa chama tawala alipinga maamuzi na ushawishi wa mumewe kuwasafisha mafisadi. Je unajua kwanini?
Pia baada ya Obama kuchaguliwa Rais wa Marekani, sasa ni wakati wa kupambana na chumi zinazokuwa kwa kasi huko Asia.

Tuesday, November 04, 2008

OBAMA RAISI MPYA MAREKANI

Seneta Obama hatimaye ameshinda urais wa Marekani na anakuwa rais wa Kwanza Mweusi kwa historia. John Mc Cain amekuwa wa kwanza kukiri kuwa ameshindwa kiungwana na kumpongeza mwenzake Obama. Hili limekuwa funzo lingine kwa wagombea wetu wa kiafrika na kitanzania wanaposhindwa si kukimbilia mahakamani bali ni kukubali.
Seneta Obama ndio anatoa hotuba ya shukrani kwa sasa ninapoandika hii makala.

Tuesday, October 21, 2008

FURAHA KWA MADIKTETA WA AFRICA

Ni kipindi cha mataifa ya kibepari kupata dhoruba la kiuchumi lakini ni kipindi cha fuaraha kwa madikteta wa Afrika.
Si hayo tu hata wengine wanakumbuka enzi za Iddi Amin kama demokrasia.

Wednesday, October 08, 2008

JAJI KAPOTEZA KIBARUA

Mjue Jaji alilyepoteza kibarua kwa kutimiza wajibu wake.

KUVUJA MITIHANI - MAPROFESA WIZARA YA ELIMU WAACHIE NGAZI

Ni hivi majuzi tu Raisi Jakaya Mrisho Kikwete alikwenda nchini Marekani na kutembeza bakuli na akafanikiwa kuahidiwa misaada lukuki ya vitabu mbalimbali kusaidia sekta ya elimu nchini Tanzania. Nilitizama picha za runinga zikimuonesha Raisin a Waziri wake wa Elimu ambaye walifuatana naye wakishukuru kwa moyo wa ukunjufu misaada hiyo. Kwa kweli nilifarijika angalau na aina ya msaada ambao Raisi alifanikiwa kushawishi wamarikani na kuupata.

Mara mtihani wa kidato cha nne ukaanza siku ya tarehe 6/10/2008 na mtihani wa kwanza wa Hisabati ukafutwa eti umevuja. Yaani ilimaanisha kuwa walioandaa na kuhifadhi mtihani huo hawakuwa makini katika kuutunza na sasa mtihani huo tayari uliwafikia watahiniwa kabla ya mtihani. Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu alionekana akidai eti ni mtihani mmoja tu umevuja na hivyo mitihani mingine iendelee. Alisahau kuwa ile tu mtihani mmoja ambao unaandaliwa na taasisi moja tu umevuja ilitosha kuifuta mitihani yote? Huyu bwana ni Professa, kwa kweli alinishangaza sana na kwa mwendo huu Katibu Mkuu alikosea kabisa. Haiingii akilini eti mtu aibe mtihani mmoja tu na aache mingine.

Mitaani katika sehemu mbalimbali za Tanzania kuna taarifa kuwa mitihani yote iko nje nje na inauzwa kama vile ulivyouzwa ule wa Hisabati. Napenda ieleweke wazi kuwa ni dhahiri kabisa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi imeshindwa kabisa kusimamia shughuli nzima ya Mitihani ya kidato cha nne. Katibu Mkuu wa Elimu anaeleza vyombo vya habari eti kushuka kwa maadili miongoni mwa watendaji wa Necta kumechangia hili dhahama. Kwa maoni yangu naamini kuwa pia kuna tatizo la kimaadili kwa Waziri wa Elimu na Naibu Wake pamoja na Katibu Mkuu vilevile.

Haiwezekani tatizo la msingi kama la kuvuja kwa mitihani linatokea alafu mtu anabakia akiendelea na kazi yake kama vile hakuna jambo lolote. Msingi wa kimaadili (Moral Fibre) wa viongozi hawa niliowataja una mashaka sana. Jamani kama tunaruhusu wanafunzi wa kidato cha nne waendelee na mitihani hii basi kwa maana nyingine Tanzania inakufa. Katika dunia ya leo ambayo elimu imebakia kama nguzo kuu nay a msingi katika maisha ya mwanadamu, wizara inaachia wanafunzi wanaoiibia mtihani ndio waendelee na masomo yao bila kupimwa sawasawa? Tunaandaa Taifa gani?

Tunaanda Taifa la wataalam mbumbumbu ambao watakuwa wataalam katika kipindi ambacho nadhani Maprofesa hawa wawili wanaoongoza Wizara ya Elimu labda hawatakuwepo na hivyo hawajali lolote. Kwao kila mtu na lake. Sijui Profesa Maghembe na Profesa Dihenga wana taaluma gani ila nabakia nikiamini kama kweli Uprofesa wao ni wa halali basi wasingelivumilia hili la kuvuja mitihani na kubaki kimya. Kama mitihani hii inayoendelea itaachwa imalizike na itumike kama kipimo cha wanafunzi basi itamaanisha katika Tanzania ya leo hakuna tofauti kati ya profesa na mkulima ambaye hajaenda shule.

Maprofesa hawa wanatupeleka kuwa na Taifa ambalo litakuwa na wasomi wasioiva ama waliokamilika nusu (half baked), matokeo yake ni kuwa na wasomi feki. Kama kweli maprofesa wawili wanaiongoza Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi wangekuwa makini, wasingeichukulia hii hali kimzahamzaha namna hii. Elimu sio kama haya mambo ya EPA na Richmond ambayo yameamuliwa kisaniisanii tu, bali ni sekta ambayo kama utalegeza udhibiti wake basi maana yake matokeo yake yatabakia kwenye jamii husika kwa miongo kadhaa. Ndio maana napendekeza kuwa Maprofesa hawa waifute mitihani hii mara moja na kama si hivyo wapime wenyewe waamue ama kuachia ngazi au kung’ang’ania mkate ikimaanisha watakuwa wameidhinisha vitendo vyote vya wizi wa mitihani. Watakuwa pia wanatekeleza kile alichowahi kunena mwanafalsafa Niccolo Machiaveli: “The End Justifies the Means”. Yaani unapofanya jambo hakuna haja ya kujali unafikiaje malengo yako ila la msingi ni matokeo”.

Baada ya kuwasihi viongozi wakuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, pia nisisahau juu ya huyu Katibu Mkuu wa Baraza la Mitihani (Necta) naye sijui anangoja nini. Yaani kuna madai tumeyasikia karibuni kama vile wizi wa vyeti mbalimbali pamoja na sasa kuvuja kwa mitihani lakini bado anathubutu kukaa kimya nab ado anathubutu kuingia ofisini bila aibu ama hisia za ukosaji wa usimamizi imara. Napenda nishauri huyu Katibu Mkuu apime hili jambo na aamue mwenyewe. Siamini kama nchi yetu tumefika mahali mtu anavurunda lakini hawajibiki.

Hivi nchi yetu ni njaa zinatusumbua ama ni nini? Lakini lazima tumshangae Raisi wa nchi inapata tatizo zito kama hili lakini bado Raisi anawaonea haya wateule hawa wanaosimamia Wizara ya Elimu. Hivi jamani huyu Raisi anakwenda nje ya nchi kuomba misaada ya elimu alafu hapo hapo anaendelea kuwachekea wateule wake ambao wameshindwa kuhakikisha mitihani haivuji. Umefika wakati kama baadhi ya watendaji hawawajibiki pale uoza unapojitokeza katika taasisi zao basi Raisi kama Mtendaji Mkuu wa Serikali achukue hatua, kinyume chake inamaanisha Tanzania inazikwa taratibu kwa Ari Mpya na Kasi Mpya.

Naliona Baraza la Mitihani pamoja na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kama ndio chanzo cha kuifanya Tanzania siku za usoni imezwe na utandawazi. Hebu fikiria tu katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, je watanzania hawa wanaofanya mitihani ya kununua mitaani na kwenye mitandao ya kompyuta wataweza kushindana na wenzao wa Kenya na Uganda ama Rwanda? Nashauri Baraza la Mitihani livunjwe kabisa ikiwezekana kwa maana ya utawala mzima na watendaji wake wote waondolewe. Inahitajika damu mpya yenye mawazo mapya yenye utashi wa kujali hatima ya jamii na si hii habari ya kutokujali na kujifanyia mambo kama vile hakuna kizazi kijacho nchini mwetu.

Umefika wakati vyombo vyote vya habari viamue kuwavalia njuga hawa viongozi wa elimu ili wang’oke katika vyeo vyao kwani nadhani wamepoteza mamlaka ya kimaadili (Moral Authority) ya kuongoza sekta husika. Vyombo vya habari navisihi vichukue uamuzi wa dhati kabisa katika kuhakikisha hatuendelei kuishi kwa njia za wizi wa mitihani kwani hiki ni kiama kwa Taifa.

Tuesday, September 16, 2008

TANZANIA INAHITAJI AKINA YOHANA MBATIZAJI

Jumapili ya tarehe 07/0009/2008, nilihudhuria ibada katika kanisa katoliki la “Kristu Mfalme, mjini Moshi. Katika ibada hiyo mara padri aliyekuwa akihubiri kwa kuoanisha na masomo yaliyosomwa siku hiyo alitumia mfano wa kashfa ya EPA kufikisha ujumbe kwa waumini.
Alilaani tabia ya waumini wa siku hizi kuona maovu au watu waovu wakifanya jambo la uvunjaji wa sheria alafu wananyamaza pale wanapotakiwa kuripoti jambo hilo. Padri huyu alikwenda mbali kabisa akadai kuwa hii ni kwasababu ya tabia ya kila mtu kudai “hayo hayanihusu, mimi najali mambo yangu”. Mtizamo huu, padri alidai ndio chanzo cha kukua kwa ufisadi ambao unaliua taifa letu na bara letu la Afrika kwa ujumla.
Padri alidai kuwa wakati mafisadi walipokuwa wanachukua fedha zile za EPA kuna watu wengi waliwaona lakini wamenyamaza na hata sasa hivi wakati mambo yamewekwa hadharani pia wameamua kunyamaza na wala hawatasema. Aliwachekesha waumini kuwa tabia hii ni kwasababu watu tunaogopa tukisema maovu ya mafisadi basi watakuja kutuchoma moto majumbani kwetu ama watatuchinja. Padri alitoa mfano jinsi Yohana Mbatizaji alivyouawa kwa kukatwa kichwa chake na Mfalme Herode kwa kujaribu kumkemea Mfalme alipojaribu kuishi na mjane wa kaka yake alipofariki. Yohana mbatizaji alimkemea Herode na hatima yake ikawa ni kukatwa kichwa chake na kufa.
Padri akasisitiza tuwe tayari kusema ukweli, kumwambia mtu ukweli anapokosea bila woga. Waumini wengi ndani ya kanisa walicheka manake kwa watanzania kwa sasa si rahisi kutekeleza hili.
Mimi kama muumini mahubiri ya padri yalinikuna sana ila nilipata hisia kuwa kwa Tanzania ya leo ni vigumu sana kuweza kuwa wakweli. Mila na desturi za watanzania karibu wote zinakazia zaidi kuficha mambo na kuchukulia kila kitu kinachomhusu mtu mkubwa au mwenye hadhi ni siri. Ni katika mtizamo huu nadhani elimu ya nchi yetu ina changamoto sana kuweza kuwafanya vijana wetu waje na mentalite ya kisasa ambayo ni ya uwazi na ukweli bila kujali ni nani mkosaji. Kama tutaendelea na haya mambo ya kizazi cha kizamani basi tujue haya mambo ya kupiga kelele kuhusu EPA yataendelea kutusumbua bila kupata jibu.
Naamini umefika wakati tuache kubebea bango hili kashfa la EPA na tuanze mchakato mpya wa kufunza watu wetu kwa ujumla wao juu ya suala la kusema ukweli na nini umuhimu wa kusema na kupenda ukweli. Nasema hivi si kwamba ninaunga mkono kashfa ya EPA ilivyozikwa kwa juhudi kubwa na Rais wetu Jakaya Kikwete pamoja na kamati yake ya uchunguzi. Ninaamini kuwa ukweli ni suala tete ambalo ni tatizo letu kama watanzania kwa ujumla wao. Tungekuwa tunapenda ukweli basi usingetarajia kuona makashfa yanafichwa fichwa kama tunavyoshuhudia leo.
Ninasema kutokupenda ukweli ni tabia za kizamani kwasababu mimi binafsi nimepata bahati kufundisha wanafunzi katika shule mbalimbali za msingi na sekondari hapa nchini. Basi inapotokea mwanafunzi kakosea jambo kinyume na sheria za shule na mwalimu umemwona mkosaji akifanya jambo mbele ya wanafunzi bila wao kujua, unapowauliza watakujibu hatujui. Hata uwabane kwa adhabu za aina gain, hutapata jibu kabisa. Ni tabia ambayo watoto wa siku hizi wameirithi kutoka kwa wazazi wao na ni vigumu kuiondoa. Kwa maana nyingine tunayoyashuhudia leo hii ya kuficha ukweli ni matokeo ya aina ya maisha familia nyingi za kitanzania zinavyoishi. Waswahili walisema: “Mtoto umleavyo ndivyo akuavyo”. Basi kwa hali ilivyo umefika wakati kwanza tufundishane kama jamii umuhimu wa kuheshimu na kupenda ukweli. Bila hivyo, kashfa zitaendelea kwani watenda kashfa hizo wanajua kabisa kashfa zitafichwa kabisa.
Nitoe mifano michache: angalia vyama vyetu vya siasa kwa mfano utaona huku CCM haya mambo ya akina Nape na Lowasa, ukienda Chadema hii kusimamishwa kwa uongozi kwa Chacha Wangwe na hatimaye kufa kuna mambo yanayogusa kusema na kupenda kutenda mambo kwa ukweli ndio yanayosumbua na kusababisha kashfa na mabishano yasiyokuwa na maana utadhani viongozi wetu ni watoto.
Kwa mtizamo wangu, kwa tabia hii ya kutokupenda ukweli basi tusishangae tutaendelea kupata kashfa ambazo kamwe hazitafanyiwa utatuzi wa kitaalamu ili kuficha ukweli kama tulivyoona kwenye EPA, Richmond, na hata mikataba mingi ambayo serikali yetu haitaki watu waichokonoe na inawaona wachokonozi kama ni watu wenye wivu.
Hata hii habari ya Nape Nnaye kuadhibiwa kwa alichokifanya; yaani kuhoji mambo yaliyofanywa na wakubwa ni dalili nyingine ya kutopenda ukweli. Bila kukubali ukosoaji, naamini nchi yetu haifiki popote. Ni kwa mfano wa mahubiri ya Padri wa Kristo Mfalme kwa jumapili iliyopita ambayo kwangu naamini yalilenga nyakati hasahasa. Basi tuamue kuupenda ukweli, la sivyo tusilalamike juu ya mafisadi.
Kutokupenda ukweli imekuwa ni tabia ya watanzania katika nyanja zote. Kwa mfano, hili dhahama la UVCCM, utaona kijana Nape amevuliwa uanachama wa UVCCM, kama adhabu ya kusema uwongo. Mimi kidogo napata taabu sana kuona wachokonozi kama Nape wanapodai jambo na wanaadhibiwa alafu wanaamua kunyamaza kimya. Hii ndio kielelezo cha viongozi wa leo ambao kwao ni bora “status quo” kuliko kuleta mapinduzi. Kwao mapinduzi si hoja ila ni ile wazungu wanaita: “Business as usual”, yaani mambo kama kawaida, hakuna kubadilika.
Mimi naamini viongozi wa aina ya akina Nape tunao wengi ndani ya CCM. Utashangaa bungeni mbunge wa CCM kupiga kelele nyingi dhidi ya ufisadi unaofanywa na viongozi wenzake ndani ya chama. Lakini anabakia kama mwanachama mwaminifu ndani ya chama anachokilalamikia. Yote hii ni kwasababu tumefikia mahali wote ama wengi wetu tunaamini eti bila kuwa mwanachama au mfuasi wa CCM basi hakuna maisha. Hii ni kasumba ambayo ninaiona inawakabili wengi wa tabaka jipya la viongozi linaloibuka kwa sasa. Nadhani ingekuwa vyema kwa watu kama akina Nape waanzishe vyama vipya vya kisiasa ambavyo vitaruhusu mawazo kama yao ili kuleta mabadiliko. Naamini pamoja na CCM na hata vyama vyetu vya upinzani vilivyopo, vyote ni bure tu kama unakuwa mwanasiasa ndani yake na una hii tabia ya uchokonozi au kuhoji mambo yanapokuwa yanakwenda kombo.
Na kwasababu Nape hayuko tayari kuwa kama Yohana Mbatizaji basi tutegemee kuwa hakuna mabadiliko na wala yeye si tabaka jipya la viongozi wanamapinduzi ambao wanaweza kuitoa nchi hapa ilipo katika kipindi hiki. Ni wasanii tuu ambao wanajaribu kufanya kile ambacho mtaani watu wanakiita: kutest zari.

Sunday, September 14, 2008

Rais Museveni anajaribu kutumia viongozi wa kijadi katika kuhakikisha serikali ya NRM inapata sapoti ya karibu kutoka kwa makabila yote Uganda. Hii kwa wachunguzi wa mambo inaonekana ni mbinu isiyo sahihi.http://www.monitor.co.ug/artman/publish/Golooba-Mutebi/Cultural_leaders_shouldn_t_be_political_tools_71486.shtml

Friday, August 22, 2008

VITA YA UKIMWI UGANDA YASHINDIKANA

Uganda ile nchi iliyokuwa inasifiwa vizuri kuwa ndio bingwa wa kudhibiti Ukimwi nayo imeshindwa vita hii.

Thursday, August 21, 2008

KIKWETE AHUTUBIA BUNGE

Hatimaye Kikwete kahutubia Bunge na kama ilivyotarajiwa na wengi wanaomfahamu, hakuna la maana aliloteta sana ukiacha machache.

Tuesday, August 19, 2008

MWANAWASA HATUNAYE DUNIANI

Rais wa Zambia, Levy Mwanawasa amefariki dunia.
Kifo hiki nilikitarajia tangu jana usiku.

Sunday, August 10, 2008

CHACHA WANGWE LABDA HAKUFAA KUWA MWANASIASA

CHACHA WANGWE HAKUFAA KUWA MWANASIASA

Mara baada ya mazishi ya mbunge wa Tarime kufanyika, nimejiuliza mambo mengi sana kuhusu jamii ya kitanzania. Yaliyotokea Tarime kwa hali ya kawaida yamenifanya nishindwe kujua hivi kweli mtu anaweza kufa alafu wafiwa waamue kuwa mazishi yasifanyike dakika za mwisho? Sina hakika kama hali imewahi kutokea Tanzania hasa kwa watu waheshimiwa kama mbunge. Ila nadhani umefika wakati tuutizame kwa kina mfumo mzima wa uendeshaji wa siasa zetu.

Nimesema hivyo kwani naamini kabisa hisia za mbunge Chacha Wangwe kuuawa zilijitokeza kwa sababu kuna mazingira yanayoonesha kwa sasa jamii ya kitanzania haina imani na mfumo mzima wa uendeshaji siasa. Hii inaweza kujidhihirisha kama ifuatavyo:
Kwanza, kupitia vyombo vya habari vyote viliiripoti habari ya kuwa Chacha aliuawa kwa kushabikia hasa. Hali hii inaonesha ni jinsi gani Tanzania ya leo baadhi ya viongozi wanapokufa basi moja kwa moja kuna kuwa na hisia za kifo cha kupangwa. Tumshukuru rais Kikwete kwa ulegezaji wa sheria za kubana uhuru wa magazeti na vyombo vya habari kwa ujumla, hii inatupa wasaa mzuri kupima na kujua nini hisia za watanzania juu ya matukio mbalimbali nchini Tanzania.

Pili, wanatarime na hasa wanafamilia ya Chacha Wangwe waliamua kwa dhati kabisa kutia shaka kifo kile. Sijui walitaka Chacha afe vipi ama labda walikuwa wanajua kuwa Chacha atakufa je, ila napata mashaka sana kama watanzania tumeamua kuishi kwa kuamini kila jambo lina mchezo mchafu. Kwa maana nyingine nchi yetu imegeuzwa jamvi la wapiga ramli ama watu wasioaminiana kwa jambo lolote. Hila ndio umebaki mchezo pekee katika masuala ya kisiasa.

Tatu, tujiulize alipokufa Amina Chifupa (RIP) yalisemwa mengi na hata baadhi ya wakubwa fulani walihusishwa na kifo kile. Mwisho wa siku mtu alikufa na mpaka leo kifo kile kimebaki na maswali mengi kwa watu wenye akili timamu. Matukio kama haya ya vifo vya viongozi wa kijamii katika utata yanalidhalilisha bunge letu sana na hata jamii nzima ya Tanzania. Inapofikia mahali jamii kwa kiasi kikubwa inapoteza imani na serikali na hata chombo chake kama bunge basi ujue kuna kila dalili za mpasuko.

Kwa upande mwingine, kifo cha Mbunge Chacha kimenifanya nijiulize hivi inakuwaje Mbunge anasafiri safari ya usiku tena na rafiki yake na wala si dereva. Na hata kama itathibitika yule Bwana aliyesafiri naye alikuwa dereva, inakuwaje mbunge aendeshwe na dereva asiyekuwa na sifa kama vile leseni ya udereva. Hii inanipa taabu sana ya umakini wa viongozi wetu. Hebu nikumbushe kuwa Mh. Mudhihir Mudhihir alipata ajali wala hakuwa na dereva; Mh. Kapuya alipata ajali akiwa na dereva, lakini mazingira ya ajali dhahiri yanaonesha ilikuwa kwasababu ya mwendo kasi wa dereva na labda dereva kutozingatia uendeshaji salama wa gari katika barabara ambayo nina hakika hakuwa ameizoea. Ni katika mazingira haya mtu mwenye akili timamu najiuliza : hivi kweli hizi ajira za kuendesha viongozi wetu zinafuata weledi wa dereva ama ni haya masuala ya kuendeshwa na marafiki ama ndugu tu kama alivyokuwa marehemu Wangwe?

Jambo lingine ambalo nadhani kifo cha Wangwe kimetuachia kulidurusu ni juu ya muundo wa vyama vya siasa Tanzania. Inasemwa kuwa aliwahi kutuhumu kuwa Chadema ni chama cha wachaga. Nimeshuhudia mheshimiwa Zitto Kabwe akijitutumua na kuwalaumu wahariri mbalimbali wa vyombo vya habari kwa kuripoti vibaya juu ya vitisho alivyofanyiwa mwenyekiti wa Chadema kule Tarime. Anafananisha uandishi ule kama ule wa Rwanda ambao ulichangia kwa mauaji ya kimbari kwa kusema kuwa wachaga kule Mara sasa wanatishwa.

Kuna kitu ningependa Mheshimiwa Zitto na wapenda demokrasia wajiulize kwa kina: Nacho ni hivi kauli ile ya Chacha ilikuwa na ukweli wowote? Nilipomsikia Wangwe akidai kuwa ni chama cha wachaga sikupata taabu kabisa. Nilimwelewa akimaanisha kuwa ile safu ya uongozi ya juu kabisa, safu ya wadhamini wa chama ndicho alichokuwa analenga. Nani anaweza kubisha kwa muundo wa vyama vya siasa hapa Afrika tangu mageuzi yaanzishwe vimeegemea kwenye nguvu ya kiuchumi ya ama mtu mmoja au kikundi cha watu ambao ndio wenye ushawishi katika Chama? Hili lipo karibu kila nchi ya Afrika kwa mfano: Uganda, NRM ilianzishwa na watu wa magharibi ya Uganda alikozaliwa Museveni. PNU ya Kibaki kule Kenya imeegemea zaidi kabila la Wakikuyu ambako Kibaki katokea. Hapa Tanzania mambo ni hay ohayo, hebu tizama chama kama UDP iko chini ya John Cheyo na yeye ndie mshika dau mkuu pamoja na ukoo wa Cheyo.

Ni katika hali kama hii ambapo nadhani kwa mwanademokrasia wa dhati kama marehemu Wangwe asingeweza kuwa ndani ya Chadema ambacho mhimili wake mkuu ni watu wa kabila la mwenyekiti . Na hata uongozi wa Chadema nani asiyejua kwa mfano wabunge wa kuteuliwa wengi wao ni wa kabila moja na ama wamepata nafasi hizo kwa kigezo cha urafiki ama undugu na baadhi ya wadhamini wa chama? Isitoshe, wabunge baadhi wa kuteuliwa ni ndugu wa karibu wa baadhi ya wadhamini? Ni katika mtizamo huu ambapo ninaamini marehemu Wangwe alikosea mwenyewe kutambua juu ya mifumo ya uundaji wa vyama vya siasa. Nani atakayebisha kuwa kama hao wote ambao Wangwe aliwatuhumu kabla ya kusimamishwa kuwa ni wa kabila fulani ndio mhimili wa Chama? Na kama wakiamua waondoke katika chama hicho na wamwachie marehemu akiendeshe basi chama kitayumba?

Wazungu wana msemo “to go too far” yaani kwenda mbali zaidi. Kwa marehemu Chacha kutuhumu Chama ni cha Kabila fulani ilikuwa sio hatua muafaka kufanywa na mbunge kama yeye ingawa alilotetea ni la ukweli. Matokeo yake Chama kimepatwa na mitikisiko ambayo kwa vyovyote vile kama marehemu Chacha angetafakari kwa kina, nadhani hata kifo chake kisingehusishwa na Chadema. Mara nyingine binadamu ana kasumba tofauti lakini kwa wale wote wenye tabia na kasumba za akina Wangwe; yaani misimamo thabiti isiyoyumbishwa kwa hali yeyote ile inakuwa vigumu sana kuelewana na watu wengi. Watu kama akina Wangwe hawafai kuwa wanasiasa kwani siasa ni mchezo uliojaa unafiki. Na Wangwe na jamii ya watu kama yeye si wanafiki sasa inakuwa taabu sana kuweza kuhimili mizengwe ya kisiasa. Kama Wangwe angekuwa mwanasiasa nina hakika kabisa asingeliwahi kuzua mambo ambayo yalipelekea kusimamishwa uongozi.

Katika hali kama niliyoielezea nadhani tatizo la vyama vyetu ni la kimfumo tulioamua kujiwekea wenyewe ambapo demokrasia ya kweli kwa maana ya kutoa maoni yako mbele ya viongozi wako hayaruhusiwi na yanaonekana ni dharau. Mpaka hapo tutakapoamua kuendesha vyama vya siasa ambavyo havitegemei ruzuku kutoka kwa wenye chama kama kikundi basi tujue migogoro ya aina ya Chacha itaendelea. Ni katika hali hiyo basi umefika wakati tujitizame kama jamii ya watanzania makini na tuamue kuwa na kanuni za kuendesha siasa ambazo zitawekwa kama sheria. Hii itasaidia sana kuwa na vyama kwa maslahi ya nchi na wala si chombo cha kutetea maslahi ya wananchi kijujuu huku wakati huo huo vyama vya siasa vikitumika kama vyombo ama nyenzo za kusaidia ndugu na jamaa ya viongozi kujipatia maslahi ya kazi na maisha yao.

Na tunapokuwa na vyama hivi tulivyonavyo leo hii basi watu wote wa aina ya Wangwe kamwe hawataweza kuishi bila kukumbana na mikasa ya kusimamishwa, kufukuzwa na hata kuonywa mara kwa mara. Si hayo tu, pia kwa zile nchi zenye udikteta watu wa aina hii huuawa ( elimination) ili kuwaondoa katika uso wa kisiasa wa nchi husika. Na ndio maana hadi leo kuna watu wamefariki na kuacha maswali bila majibu. Hawa ni kama vile: Horace Kolimba, Imran Kombe, Amina Chifupa, Ipyana Malecela kwa hapa Tanzania na akina Litvnenko kule Russia, Robert Ouko kule Kenya na wengine wengi ambao wamekufa na watu wakawa na hisia wemeuawa bila kuwa na ushahidi wa dhati kabisa.

Mwisho, binafsi ninaamini kabisa kuwa Wangwe amekufa na baada ya kushindwa kuthibitisha risasi ilitumika basi ni wakati wa kukubali kuwa ilikuwa kazi ya Mungu kwani pamoja na maadui wengi aliokuwa nao bado tumeshindwa kuthibitisha. Lililo mbele yetu ni kuwa umefika wakati kuhakikisha tunaimarisha taasisi za mfumo wa kisiasa Tanzania hasa jinsi gani vyama vya siasa vinapaswa kuendesha shughuli zake kwa kuzingatia misingi ya demokrasia ya kweli bila kuweka uzandiki. Tukishindwa haya basi tujue kuwa kila mwaka hasa wakati wa bajeti tutarajie mbunge fulani mwenye misimamo isiyoyumba atatutoka hapa duniani katika mazingira tata ambayo mara nyingi tutashindwa kuthibitisha kama kweli ni kazi ya Mungu.

Thursday, July 31, 2008

CHACHA WANGWE ALIUAWA KWA RISASI?

MAZISHI YA CHACHA HAYAKUFANYIKA!

Huwezi amini lakini ndio hivyo, ndugu wa marehemu Chacha Wangwe walizuia mazishi yasifanyike kwa kile kilichoitwa kuwa hawaamini kama kuna ajali bali alipigwa risasi. Kwa mujibu wa redio free Afrika jana usiku, inasemekana familia ilimualika rafiki wa familia kutoka Kenya ambaye ni daktari na akawaambia kuwa jeraha lililopo kisogoni kwa marehemu ni la risasi.
Makubwa ndio haya inaonekana marehemu alipigwa risasi mdomoni na ikatokea kisogoni. Maoni yangu ni kuwa kama hii ni kweli basi marehemu alikuwa anafuatwa na maadui zake ambao naweza kuwaita (firing squad) ambao watakuwa walitumwa. Na inavyoelekea hawa jamaa watakuwa walilipita gari la marehemu na kumpiga risasi wakiwa mbele yake. Hii ndio itakayokuwa sababu ya ajali kwani kishindo ambacho Dennis Mallya alikisikia kabla gari halijabiringika ilikuwa ni risasi.
Kama hiyo sivyo, basi kwa vyovyote vile Dennis Mallya atakuwa ndie muuaji wa mbunge wetu mpendwa. Atakuwa ndie anahusika na mauaji haya na ashughulikiwe ikithibitika ni risasi imemuua Chacha.
Pia ni vyema gari lichunguzwe kama tairi zake zimepasuka kweli.
Nadhani baada ya mafisadi wa kisiasa Tanzania kuzidi kuwaua viongozi bora wa Tanzania sasa mwisho umefika. Alikufa Amina Chifupa alafu tukakaa kimya tu hatukuhoji lakini leo napenda niwapongeze ndugu wa Chacha Wangwe kwa walichokifanya kwani wameonesha kuwa wana akili na wanapenda nchi hii iwe na viongozi wenye weledi.
Mwisho nikumbushie kuwa kabla marehemu hajafariki, alikuwa ametoa maneno mazito dhidi ya hali ya “Ukabila ndani ya chama cha Chadema” na kuanzia hapo amepata misukosuko mingi hata kusimamishwa uongozi. Ni vyema wapenda amani wote Tanzania tujiulize hivi inawezekana maneno haya aliyoyasema ndio chanzo cha kifo chake? Wenye chama chao wamemuua? Je kwa kipindi hiki Chacha alikuwa ni tishio kwa CCM au Chadema? Iwe iwavyo, mojawapo ya hivi viwili ndio chanzo cha kifo hiki.

Tuesday, July 29, 2008

UGANDA VS MENGO - UNAIJUA KASHESHE?

Kwa sasa Uganda ina mgogoro mkubwa wa kisiasa na himaya ya Baganda, unajua chanzo chake?

Monday, July 28, 2008

MSIBA BUNGE LA TANZANIA TENA

TANZIA – SASA IMEKUWA ZAMU YA CHACHA WANGWE


Ni saa nne na dakika arobaini na saba, mara nikitizama taarifa ya habari ya ITV usiku nashanga mstari mweusi wa maneno unakatiza katika runinga na maneno: “mbunge wa Tarime, mheshimiwa Chacha Wangwe amefariki dunia usiku kwa ajali ya Gari” habari zaidi fuatilia redio one.

Na kweli ninazima runinga yangu na kuanza kusikiliza redio one. Ninakutana na mahojiano kati ya watangazaji: Asia Mohamed na Jerry Muro akiripoti kutoka Dodoma. Wanahojiwa waheshimiwa mbalimbali kwa masikitiko bado wanaonekana kutaharuki. Mtangazaji anadai eti nyakati za mchana mheshimiwa Chacha alionekana akiteta na mheshimiwa Mudhihir, hii inanikumbusha huyu ni mhanga mwingine wa ajali katika bunge hili. Hisia fulani zinanijia akilini lakini sisemi kitu najinyamazia.

Nikiwa nimekwishaamini kuwa mheshimiwa huyu katutoka, navuta hisia kadhaa juu ya bwana huyu na mara moja nautambua Umachachari wake, ubishi wake hata pale pasipo na Mantiki lakini kwa yote , kauli ya John Cheyo inanikuna akihojiwa na Jerry Muro. Anasema: “Chacha alikuwa na msimamo ambao wengi wetu hatunao” . Nakubaliana na mheshimiwa Cheyo na ninaendelea kusikitika.

Mara ninaamua kumtumia mtu wangu wa karibu sms akiwa Dar es salaam nikimsihi afuatilie habari kuna tukio la kifo cha mbunge mashuhuri. Pia katika message yangu nampa hisia yangu kuwa sasa “ Chadema itachafuka hasa kwani kifo hiki kitatumiwa na wanazi kuonesha kukolimbana hakuko tu CCM”. Ninapoituma message ile mara napata message kutoka kwa rafiki mwingine akinihabarisha juu ya kifo cha Chacha. Ninamrudishia nikimsihi kuwa “Siasa za Afrika ni mchezo mchafu, nina hisia lazima kuna mkono wa mtu awe wa kambi ya marehemu ama kule tulikozoea kukolimba watu wabishi kama Wangwe”.

Hapo hapo napokea message nyingine ambayo inanijibu ile niliyotuma Dar es salaam: “Sio Chadema ni CCM walileta mgogoro alafu wamemuua ili tuone Chadema nao wana mchezo kama wao! Tunaelekea pazuri sana. Tutashuhudia mengi na ukweli utadhihirika mwisho”. Mie sijui kwanini watu wana maoni ya aina hiyo ila ndio jamii ya kitanzania ilipofikia sasa.

Inapofika saa sita na dakika kumi na sita usiku hisia zangu zinashangaa: Jerry Muro, mwandishi wa ITV anaongea na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, mheshimiwa Lukuvi ambaye anasema kuwa gari la Wangwe limepata ajali ya kuanguka baada ya kupasuka gurudumu. Lukuvi anamnukuu rafiki wa Wangwe ambaye alikuwa ndani ya gari la Wangwe na amepata michubuko tu. Anasema gari lenyewe lilibiringika mara nyingi sana na ndipo Israel akachukua roho ya mheshimiwa Chacha. Moja kwa moja hapa ninajenga kanuni za kihisia na chonganishi (conspiracy theories) kadhaa:

Moja, kwanini gari la mbunge kama tuyajuavyo ni magari imara , mazuri na nina hakika yanafanyiwa matengenezo bora, itakuwaje lipasuke tairi tena nyakati za usiku pasipo na joto sana la kupasha hiyo chubu? Inawezekana kirahisi namna hiyo? Au tuseme Chacha anatembelea ulimu?
Pili, hili Bunge letu lina matatizo gani? Ni balaa ama ni nini? Kwanini kila kikao kinapokutana hasa cha bajeti lazima Mbunge afe?
Tatu, kwanini katika bunge hili ukiacha mbunge mmoja tu, wote waliokufa kulikuwa na hali ya kuwa na maadui hasa juu ya misimamo ya marehemu hawa?
Nne, kwanini wabunge wa bunge hili wanapatwa na madhila kama ajali ama vifo mara baada ya kuwa ni watu wenye misimamo yenye kutetea maslahi ya umm a sana ama kudhoofisha maslahi ya umma?

SHUHUDA WA AJALI

Saa sita na dakika thelathini na sita, redio one inaripoti kuwa ndio mwili wa Chacha Unaingia hospitali ya Dodoma kutoka eneo la ajali huko Kongwa. Gari ni Land Cruiser namba: SM.4297 la Halmashauri ya Kongwa. Jerry Muro anaongea na Rafiki wa mheshimiwa Chacha ambaye alikuwa akisafiri na mheshimiwa Chacha, ndugu Deus Mallya, rafiki wa karibu wa Chacha, anaeleza walitoka Dodoma wakienda Dar, anasema alisikia kishindo kikubwa sana kabla ya ajali, ninapata hisia sio ajabu inawezekana gari hilo lilikuwa limetegwa bomu labda, na gari liliruka juu na kufuatiwa na mbiringiko mkubwa sana.

Kuhusu mwendo wa gari Deus Mallya anasema kuwa Mheshimiwa Wangwe hana hakika kama alifunga mkanda. Yeye alifunga mkanda, lakini kimazingira inaonekana marehemu alibanwa kwa hiyo napata hisia alikuwa amefunga mkanda la sivyo kwa mbiringiko huo lazima angerushwa nje.
Je mheshimiwa Wangwe alikuwa kwenye hali gani? Mwanzoni nilidhani ni Land Cruiser, kumbe sio, ila ni gari dogo. Alikuwa anaendesha gari aina ya Corola na anapoulizwa kama marehemu alikuwa mlevi anasema hadhani ila asubuhi alisema alikuwa na malaria.
Je hali ya gari ilikuwaje? Gari limekuwa kama kopo lililofinyangwa. Mheshimiwa Wangwe alikuwa katika hali gani baada ya ajali? Aliumia maeneo ya kichwani na kifuani.
Deus Mallya yeye anasema ameumia mguu wa kushoto kama ameteguka tu na ana maumivu kichwani. Haamini kama amepona, ndio maajabu ya Mungu.

Mwisho, Mkuu wa mkoa wa Dodoma anasema baada ya mwili kuingia Dodoma tusubiri maelezo ya Spika kesho asubuhi. Nami naamua kwenda kulala nitamsubiri Spika aseme zaidi asubuhi.

Binafsi niseme tu, kifo hiki kimenisikitisha na ndio maana nikaamua kuandika makala hii usiku huu wakati nikufuatilia habari zaidi za kifo hiki. Nimalizie kwa maneno ya rafiki yangu katika message yake ambayo yameingia sasa hivi wakati namaliza : “ Aise inasikitisha ubunge sio kazi nzuri kwa sasa afrika hakuna la maana wanalofanya bali kuadhibiana kiainaaina, ngoja tuone mengi yanaweza kufichuka”. Mie nabaki nikijiuliza sijui ni nani atafuata manake nina hakika kabisa kwa mtiririko huu basi kuna mbunge mwingine atakufa kikao kijacho cha bajeti. Kazi kwenu wabunge.

Nimalizie kwa kusema: “ Chacha tulimpenda sana lakini Mafisadi walimchukia sana”. Mungu amlaze mahali pema peponi, Amina.

Saturday, July 26, 2008

HABARI ZA JUMAPILI

Kutatokea kupatwa kwa jua wiki ijayo. Kupatwa kwa jua nusu hakutaonekana Afrika siku hiyo.

Kumbe udikteta na ubabe uongozini una faida? Je kuna faida gani kuweka maafisa wa Jeshi kama ndio mabosi wa jeshi la polisi?
Huko Kenya wanafunzi wa sekondari wanagoma, kumbe ni halali kugoma.
ICC imeamua kulia na dikteta wa Sudan, je kwanini ICC inadili na madikteta wa nchi masikini tu?

Monday, July 21, 2008

MAKAMU WA RAIS ANAPOINGILIA NDOA YA DEREVA

Profesa Bukenya ni makama wa rais Uganda. Ana vituko, hebu vione.

MUGABEISM – FALSAFA ILIYOZINDULIWA NA NYERERE

Robert Mugabe hatimaye jana alikutana na hasimu wake wa kisiasa na kusaini makubaliano ya kuanza kujadiliana ili kutanzua mgogoro mkubwa wa kisiasa wa Zimbabwe. Ni hatua ambayo imeendelea kunishangaza juu ya mwenendo mzima wa siasa za Kiafrika kama kweli zinafuata demokrasia ya Kimagharibi au ni demokrasia mpya ya Kiafrika. Morgan Tsavingarai yeye jana kasema ni siku ya kihistoria kukutana na Mugabe tangu miaka kumi.

Kwangu nimeona tukio la hili la kukubali kuzungumza kwa watu hawa wawili kama mwelekeo tata wa siasa za Zimbabwe na pia kama hatua mpya kwa waafrika kujiuliza mambo kadhaa: Moja, nianze na Mugabe mwenyewe ni mtu wa aina yake. Kati ya maraisi wote wanaoitawala Afrika kwa sasa na hata wale waliowahi kutawala bara hili ndiye msomi sana kuliko wote. Mugabe ana shahada (degree) saba za chuo kikuu na wala sio zile zilizoeleka kwa vigogo wetu kutunikiwa za heshima. Huwa nafurahi kumsikiliza kila anapoongea kwa ufasaha lugha ya kiingereza huku akionekana hata kwa umri mkubwa bado ana uwezo mkubwa wa kufikiri.

Pili Mugabe pamoja na akili zote za darasani alizonazo amekosa busara za umri alionao. Nasema hivi kwani nadhani Mugabe ni mwanamapinduzi hasa wa harakati za kiafrika (Pan Africanist) ambaye kateleza sana kwa kile anachokitetea ama labda hajateleza basi ndio mwanzo wa Uwanamapinduzi mpya wa kiafrika. Namfananisha Mugabe na Mwalimu Nyerere ambaye naye alikuwa ni mwanamapinduzi halisi wa kiafrika ambaye hakuwa tayari kuwaruhusu mabepari waimeze nchi yetu chini ya utawala wake. Aliamua aanzishe mfumo wa kisiasa wa kiafrika hasa kwa kutumia mfumo wa kijamaa ambao asili yake ilikuwa ni mfumo mama wa sera za mwanafalsafa wa kijerumani Marx (Marxism).
Mfumo huu wa Ujamaa kwa kiasi fulani haukufanikiwa hadi pale Mwalimu Nyerere alipoamua ang’atuke (1985) kwani alijua wazi hawezi kushindana na mabepari kwa njia yeyote. Kwa kipindi kile nilikuwa nasoma shule ya msingi darasa la tatu nakumbuka jinsi maisha yalivyokuwa magumu kukikosekana hata bidhaa muhimu kama sukari ama sabuni za kuogea ama kufulia na biashara za magendo kushamiri hasa mpakani na Kenya. Nadhani Nyerere hakuwa tayari kuvumilia haya na akaamua akapumzike kwao Butiama.

Tatu, Mugabe pia alikuwa katika imani moja na Nyerere lakini yeye akaamua atofautiane kidogo na Nyerere kwa kuamua kupigana na maadui wakuu yaani mabepari. Ni vita ngumu sana na kuishinda hii mimi binafsi kama mwafrika na mzalendo siamini inawezekana hata kidogo kwa sasa. Nasema hivi kwani naona mfumo wa dunia kwa sasa ni wa unyonyaji kwa nchi kubwa kuzilazimisha nchi masikini kufuata matakwa yao na hata kwa kuruhusu rasilimali zetu kuchukuliwa kwa visingizio vya uwekezaji ama ukosefu wa teknolojia kwa nchi masikini.

Ni katika mtizamo wangu huu nadhani ndio maana Mwalimu Nyerere aliliona hili na ndio maana alikuwa kila akifanya hotuba anakumbushia eti siku zijazo kutakuwa na hali fulani na ambayo ndio tunaiona leo hii hapa Tanzania. Kwa Mugabe yeye ni tofauti na haoni sababu kuwaruhusu mabepari kuzikalia ardhi ya Zimbabwe na kufanya shughuli zao. Hivyo kwake aliona ni bora kuwanyang’anya ardhi na hapo ikawa ndio mwanzo wa dhahama lote hadi leo. Mwenzake Tsavingarai kwa kuona jinsi ambavyo unyang’anyi huo wa ardhi kutoka kwa walowezi ulivyoleta dhahama yeye akaamua kukubali kutumiwa na mabepari. Ni wazi Tsavingarai ni kibaraka (puppet) wa Waingereza; lakini pia naamini anatekeleza matakwa ya mfumo wa kidunia kwa sasa bila kujali ni kiasi gani Wazimbabwe wengi watakavyoumizwa na mfumo wa serikali itakayokuwa chini ya utawala wake kama angelishinda uchaguzi.

Nakubali kuwa Mugabe ndie mwanamapinduzi halisi anayetakiwa Afrika kwa wakati huu. Kwani yeye kaamua ajaribu kuendeleza pale akina Nyerere, Nkrumah, Sekou Toure na Thomas Sankara walipoachia baada ya tawala zao kushindwa kabisa kuhimili mitetemo ya mabepari. Mugabe aliamua avuruge uchaguzi unaoendeshwa kwa taratibu za kimagharibi zilizoanzia kule Athens Ugiriki karne nyingi zilizopita. Yeye kaja na demokrasia mpya kabisa ya kiafrika kwa kuhakikisha watu wanatishwa, kupigwa marungu, na hata kuuawa ili mradi tu wasivutwe na kutekwa na hisia za kupenda sera za mabepari. Hali hii ilifanya uchaguzi uharibike na mpinzani mkuu akaamua kujitoa nah ii ikamruhusu Mugabe kushinda kwa ulaini uchaguzi wa Zimbabwe.

Demokrasia ya Kiafrika haina vigezo vingi; yaani haina mambo ya taratibu za upigaji kura kama kujiandikisha, taratibu za kampeni, uhuru wa kutumia vyombo vya habari kwa wapinzani hauna nafasi kabisa. Ni uchaguzi ambao unazingatia tu ni nani tume ya uchaguzi itamtangaza kama ni mshindi. Hii ni mbinu ambayo hata hapa Tanzania imekuwa ikitumika hasa kule Zanzibar katika chaguzi kadhaa chini ya uasisi wa Mwalimu Nyerere tangu mwaka 1995.

Mugabe alifanikiwa kwa njia hii na hata pale jumuiya ya kimataifa ilipojaribu kuweka vikwazo iligonga mwamba pale Wachina na Warusi walipoamua kupiga kura ya turufu katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa. Huu ukawa ushindi mkubwa kwa Mugabe na sasa ameamua kuanza mazungumzo na Tsavingirai, kwa kiasi fulani ni hatua moja mbele zaidi ya watangulizi waliowahi kupingana na mabepari lakini wakashindwa. Ninasema hivi kwani naamini kwa hotuba aliyoitoa baada ya kusaini na hasimu wake Tsvangira, kuwa sasa “Tuanze kuwaza na kutenda kizimbabwe” ilionesha kuwa hataki mawazo ya kibepari na hii ndio imekuwa shida yake kubwa. Anataka mambo yafanyike Kiafrika kwa kuzingatia mashiko ya kiafrika.

Kufikia hapa ndipo napata maswali ambayo siku zijazo nitayajengea hoja zaidi: Kwanza, Je Mugabe kama atakubali kuunda serikali ya umoja wa kitaifa na Tsvangira, je ataweza kuwafanya hawa jamaa wa MDC kuwaza na kutenda “Kizimbabwe” ? Hapa nina mashaka sana, sijui itakuwaje.
Pili, je kwa hatua iliyofikiwa hadi leo ya chuki dhidi ya Waingereza na Wamarekani, itawezekana Zimbabwe chini ya Mugabe iwe na ushirikiano wowote wenye manufaa na nchi hizo? Na je nchi zingine zitachukuliaje hatua hii ya maelewano kati ya mafahali hawa wawili, wataweza kuanzisha mashirikiano mapya?

Tatu, Je inawezekana nchi za Kiafrika zikaendelea na utengamano ikiwa hazifuati matakwa ya kiutandawazi ambayo kwayo lengo lake ni “utandawizi” ambao Mugabe na akina Nyerere hawautaki? Na je kama kweli Zimbabwe itatulia je mapinduzi haya mapya ya Mugabe (Mugabeism) yataenea barani Afrika ili kumkomboa mwafrika dhidi ya Utandawizi?
Labda niseme tu ni maoni yangu kuwa sina imani kama kweli hii “Mugabeism” ina tija sana kwa bara letu. Ni falsafa ambayo ni tamu sana kimatamshi lakini kiutekelezaji nadhani ni chanzo cha migogoro hasa ikizingatiwa bado bara letu hatujawekeza ipasavyo katika sekta ya elimu kuweza kuwa na wanataaluma hasa wahandisi ambao wangewezesha nchi zetu kuweza kujitengenezea na kufaidi rasilimali zake kwa asilimia mia moja bila kuibiwa kwa kutumia utandawizi. Ni wazi Zimbabwe na hii “Mugabeism” haitakuwa na tija yeyote ingawa ni tamu masikioni miongoni mwa wazalendo wa kiafrika lakini mtu ukifikiri sana ni bure tu. Ni falsafa inayojaribu kugeuza mwenendo wa dunia pale pasipowezekana.

Naiona Zimbabwe kama ilivyokuwa Kenya kwani mara baada ya Kibaki kukubaliana na Raila, imekuwa kama kuahirisha mwelekeo mpya wa siasa za Kenya na kuendelea mawazo ya kale ( status quo). Mugabe alipaswa atumie busara kwa kuiga wenzake akina Nyerere ama Moi walipoamua kujing’atua pale upepo ulipoonesha wazi kuwa wimbi la dunia lilikuwa dhidi ya falsafa zao na kama wangelijaribu kushinikiza falsafa zao basi wananchi wengi wangeumia sana. Kwa akina Mugabe na Kibaki wao si tija watu kufa ama kuumia ilimradi falsafa zao zinabaki madarakani.

Huku haya yote yakitokea nitabaki najiuliza bila jibu inakuwaje mtu msomi wa shahada saba ang’ang’ane na falsafa potofu (Mugabeism) yake huku uchumi mzima wa nchi ukiangamia? Ni wazi Mugabe atabakia kama mwanamapinduzi halisi ila ameshindwa kuelewa kuwa katika dunia ya utandawizi kamwe mtu huwezi kuwashinda mabepari. Huu ndio ukweli mchungu kwetu wote tunaoipenda Afrika. Na si Wachina wala Warusi ambao watairejesha Zimbabwe katika mafanikio ya kiuchumi kama zamani bali ni hao Waingereza ama Wamarekani ndio tu wanaoweza kurekebisha mambo ya Zimbabwe.
Mwisho, hapa nataka wote tujiulize hivi Ali Hasan Mwinyi kama angeliamua kufuata sera za Nyerere alipopewa jukumu la kuliongoza Taifa la Tanzania je nchi yetu ingelifika hapa ilipo leo? Umefika wakati kwa watawala wetu kujua mipaka ya sera wanazozitetea la sivyo wataharibu kabisa nchi wanazopigania na kujitoa mhanga kuzipigania. Nina mashaka sana bila kufuata kile Watandawizi wanataka basi ni kiama kwa nchi zetu. Kama nimekosea basi naomba nipewe wazo mbadala.

Saturday, July 19, 2008

Bashiri Kukamatwa?

Wiki hii ilikuwa siku ya Kupanga Uzazi je unajua kupanga uzazi ni vizuri sana? Pia jambo lililosemwa sana ni hii hatua ya Mahakama ya ICC kutaka kumkamata Rais Bashir.

Friday, July 04, 2008

MUSEVENI KAMA MUGABE?

Saa nyingine serikali za Kiafrika zinajiabisha sana pale zinapowatumia wahuni tu wa mtaani katika shughuli zake. Ona hili la Uganda jinsi lilivyo. Uganda ya Museveni sasa imeanza kumchoka; kuna kila dalili kuwa wapo watu tena wengine wa karibu na Museveni wameanza kupanga jinsi ya kuondokana naye. Hii inachangiwa na kukuwa kwa rushwa na pia jeuri ya baadhi ya maswahiba wa Rais Museveni ambao kwao hata mkaguzi mkuu wa serikali si kitu.
Si hayo tu, kuna hili la Mugabe kufananishwa na Mobutu.

Friday, June 27, 2008

UGANDA YAMPOTEZA MSOMI MWANASIASA

Wiki hii Chama cha Upinzani nchini Uganda kimempoteza Mwenyekiti wake Dr. Kiggundu ambaye amewahi kuwa gavana wa benki kuu.

BARACK OBAMA NA MATUMAINI FEKI YA WAAFRIKA NA WEUSI

Mapema mwezi wa Juni, tarehe 3 mwaka huu, Barack Obama alifikia hatua kubwa katika harakati zake za kuteuliwa mgombea wa Chama cha Democratic. Ni hatua ambayo Wamarekani wanaiita (Nominee designate) mgombea mtarajiwa. Siku hiyo hapa Tanzania mkutano wa nane wa Taasisi ya Sullivan ulikuwa ukifanyika. Aliyewahi kujaribu harakati za kuchaguliwa, Mchungaji Jesse Jackson alinena kwa furaha akijivunia ni ushindi kwa weusi. Karibu waongeaji wote walizungumza juu ya hili kwa maono ya ushindi wa weusi.

Nikiwa kama mtanzania, mtu mweusi, nimefarijika pia kwa ushindi wa Seneta Barack Obama. Kufarijika kwangu si kwa mashiko ya rangi; yaani mweusi kashinda basi nami nifurahi. Kwangu nimeshangazwa karibu weusi wote wanamshabikia Obama eti kwa kuwa ni mweusi. Nina mashaka kama kweli hisia zetu zinaegemea zaidi rangi basi nadiriki kusema kuwa tusipokuwa makini nasi pia ni wabaguzi wa rangi wakubwa.
Nina wasiwasi: wote wanaouchukulia ushindi wa Obama kama ushindi kwasababu ni mweusi basi wamepotea njia. Ni lazima watu tufikiri kwa kina na si kushabikia tu ilihali inawezekana kabisa Obama hatakuwa na maslahi yoyote kwa waafrika na hata kwa watu weusi sehemu mbalimbali za dunia.

Labda niwarejeshe kwenye historia: Raisi wa zamani wa Marekani, Ruthirford Hayes aliwahi kunena kuwa “Us government is a government of the corporations, by corporations for the corporations”. Alimaanisha kuwa serikali ya Marekani ni serikali ya Makampuni, kwa maslahi ya Makampuni na inaendeshwa na Makampuni. Hapa alikuwa anajaribu kutanzua kiza kinene (illusion) kwenye maana ya demokrasia kama ilivyokuwa imeelezwa awali na mtangulizi wake Lincoln pale alipoweka maneno: “Government of the People for the People by the People” yaani: “serikali ya watu, kwa watu na maslahi yao” katika katiba ya nchi hiyo.

Ni katika msingi wa kuingalia serikali ya Marekani kama inayoongozwa na mtizamo wa Katiba kuheshimiwa bila ubazazi wa aina yeyote kama tunavyoshuhudia hapa kwetu, basi kama Obama atachaguliwa kuwa raisi wa Marekani tujue kabisa atafanya kazi kwa misingi ya Rais wa zamani Ruthirford Hayes. Hapa ndipo panaponifanya nisiwe na matumaini kama kweli mtu mweusi kuwa Rais wa Marekani basi tutafaidika na lolote tofauti na marasi wengine weupe waliokwishapita na kutawala Marekani. Ni vyema tumfurahie Seneta Obama kutokana na wajihi wake: ni jinsi gani ameweza kuchambua masuala mbalimbali kwa ufasaha na kuonesha jinsi gani anavyoweza kufikiri. Ni kigezo hiki tu naweza kufurahia ushindi wa Obama na wala kamwe si rangi yake. Kinyume na hapo naona ni mtizamo wa kibaguzi ambao hauna nafasi katika dunia ya kileo.

USHINDI HARAKATI ZA MTU MWEUSI

Kuna wengine wanauona ushindi wa Seneta Obama kama vile ni ushindi wa harakati za kutafuta haki za mtu mweusi. Hebu nikumbushie harakati za kumkomboa mtu mweusi nadhani zilianza siku nyingi chini ya watu kama akina Willium Du Bois, Marcus Garvey, George Padmore, Malcolm X, Martin Luther King, Nelson Mandela, Julius Nyerere, Jomo Kenyatta, Kenneth Kaunda, Robert Nesta Marley hadi akina Jesse Jackson na Luis Farhani wa leo hii Marekani.

Nimejaribu kupiga picha na nimeona hadi leo hii mtu mweusi kafikia mafanikio mengi katika nyanja nyingi. Kwa mfano, miongo mitatu iliyopita tunaweza kung’amua mafanikio ya mtu mweusi kama ifuatavyo:
Mosi, mwishoni mwa miaka ya 1970, waafrika weusi wa Marekani waliweza kutawala fani ya muziki kimataifa pale mziki aina ya kufokafoka ulikuwa sana kuanzia New York na kuua kabisa muziki wa Rock uliokuwa ukitawala.
Pili, baada ya mafanikio ya muziki, mwafrika asilia alianza kuonesha mafanikio duniani katika mchezo wa soka. Mwaka 1990, timu ya Taifa ya soka ya Cameroon (Indomitable Lions) ilifikia hatua ya robo fainali ya Kombe la dunia kule Italia chini ya Roger Milla. Baadaye mwaka 2002 kule Korea na Japan timu nyingine ya Senegal nayo ilifika hatua kama hiyo.

Jambo la tatu, katika miaka hiyo hiyo ya 1990, kule Afrika ya Kusini, Nelson Mandela na wafungwa wenzake kama akina Govan Mbeki, Walter Sisulu waliachiwa huru. Baadaye mwaka 1994 waafrika walio wengi wakafanikiwa kuunda serikali ndani ya nchi ambayo walinyimwa haki hiyo kwa miongo kadhaa. Si hapa Afrika tu mtu mweusi kafanikiwa, kwa mfano, mwaka 1997, kijana mweusi wa Marekani: Eldrick ‘Tiger’ Woods akaweka historia kushinda mashindano makubwa ya mchezo wa gofu “US Masters” na ametawala mchezo huo kidunia hadi ninapoandika makala hii. Mchezo wa kikapu ndio usiseme, mtu mweusi katawala hasa.

TIJA YA MAFANIKIO YA MTU MWEUSI

Kwa ujumla mtu mweusi kafanikiwa sana kwa miaka ishirini iliyopita si kwenye fani ya sanaa na michezo tu. Bali hata kwenye mambo ya uongozi wa taasisi nyeti za kimataifa, mwafrika tayari anajivunia kuweza kuongoza katika nyadhifa za juu kabisa. Kwa mfano, Umoja wa Mataifa (UN) , mwaka 1991 – 1994 ulikuwa chini ya Butros Butros Ghali raia wa Misri, baadaye akarithiwa na mweusi hasa Koffi Atta Annan wa Ghana mwaka 1995. Ni kipindi hichohicho, Jumuiya ya Madola ilikuwa chini ya Chief Emeka Anyaoku wa Nigeria kama Katibu Mkuu. Haya yote ilikuwa ni kuionesha dunia kuwa mtu mweusi anaweza na anatambulika. Lakini tujiulize: Je kulikuwa na msaada gani mkubwa kwa waafrika pale yote haya yalipojitokeza? Nakumbuka tulifurahi na kushangilia kutokana na hisia zenye mashiko ya rangi.

Watu wengine wanaweza kujiuliza labda mafanikio mengi ya mtu mweusi niliyoyaelezea hayakutokea Marekani bali hapa Afrika chini ya waafrika. Lakini kwa sasa yanatokea kule Marekani, ambalo ndilo Taifa linalotoa mwongozo wa dunia basi hatuna budi kuwa na matarajio. Na hii ndio hisia ninayoiona miongoni mwetu wengi kama “matumaini feki”. Kwangu siamini hivyo na kamwe sitaamini. Labda nikumbushie tu pale Raisi George Bush alipoingia madarakani na kumteua Collin Luther Powel kama mweusi wa kwanza kuwa Waziri wa Mambo ya Nje, yaani cheo cha juu kabisa baada ya Raisi na Makamu wake Marekani. Raisi Bush alimteua baadaye mweusi mwingine Condoleza Rice katika nafasi hiyo ya juu kabisa hadi wakati naandaa makala hii.
Pia ni miaka si chini ya mitatu iliyopita, mwafrika mzaliwa wa Uganda John Sentamu alichaguliwa kuwa Askofu wa jimbo la York huko Uingereza. Hii ni nafasi ya pili kwa cheo ndani ya kanisa la Anglikana duniani. Katika haya yote yanayohusu ukombozi wa mwafrika ni mafanikio ambayo wanaharakati wanatumia mara nyingi neno la kiingereza “African Renaissance” yaani kuzaliwa upya kwa mwafrika.
Kwangu hili naliona pia kwa mtizamo huo kwani mwafrika ameweza kuondokana na kadhia za kibaguzi za zamani. Lakini tujiulize swali: Hivi mafanikio yote hayo yamesaidiaje weusi wa dunia hii? Tuache ukichaa, hebu angalia hata kule Afrika ya Kusini sasa mtu mweusi anapinga mweusi mwenzake kuishi nchini mwake. Umasikini wa mtu mweusi uliosababishwa na ufisadi wa wanaharakati wa zamani umetufikisha hapa tulipo. African Reinassance imepoteza mwelekeo huko Afrika Kusini kwa Madiba. Yote ni kwasababu mtu mweusi amekubali awe mtumishi na wakala wa mfumo wa kiutawala wa aina ya: “ corporate by corporation for the corporation”. Akina Raisi Mbeki na wapigania uhuru wenzake wamegeuka umma wa weusi na kuacha kuwatumikia na kuyatumikia makampuni.

Vivyo hivyo, nadhani hata Seneta Barack Obama atafuata mwelekeo huohuo kwa kuitumikia katiba ya Marekani ambayo imejaa lugha ya giza ikimaanisha mambo ambayo kimatendo ni kinyume na maneno. Yaani ikifuata mwelekeo wa Raisi Hayes badala ya ule sahihi wa Lincoln.
Ndio maana nilishangazwa sana mara baada ya Obama kuthibitisha kuwa ni mgombea mtarajiwa, hotuba yake ya kwanza mjini Washington ilikuwa ni mbele ya umati wa watu 7000 uliojumuisha “Kamati ya Mambo ya Waisraiel – Wamarekani ( Jewish American Israel Public Affairs Committee – AIPAC. Tujiulize ikiwa weusi wengi ndio waliompigia kura ilikuwaje aanze na shukrani kwa Wayahudi?

Dhahiri mwelekeo hapa wa dunia lazima tutumie bongo kufikiri na si kufuata hisia tu. Barack Obama hana njia nyingine ila ataungana na wale wengine niliowataja awali kama alama ya “African Reinassance” ambao wamemtangulia katika kuwatumikia wazungu. Kwani katika demokrasia ya leo, ule mtizamo wa Raisi Lincoln ndivyo sivyo. Mambo ya ‘Serikali ya watu, kwa watu na maslahi yao’ ni hadithi ya alinacha. Democrasia leo ni kutumikia makampuni makubwa yenye ushawishi. Haya ndiyo yenye kupenyeza rupia kusaidia kampeni za akina Seneta Obama ili wayatumikie pindi watakaposhinda. Ni kama vile hapa kwetu Tanzania vigogo fulani walivyojiundia vikampuni kwa mgongo wa EPA ili kupata fedha za kampeni. Obama yeye hakutumia mbinu za kibazazi za kujiundia vijikampuni feki ila anafadhiliwa na makampuni ambayo lazima alipe fadhila.

Mwisho, Seneta Obama ataungana na waliomtangulia: Koffi Annan, Colin Powel, Condoleza Rice, Chief Emeka Anyaoku na hata mama yetu mpendwa Asha Rose Migiro ambao walitumika na wengine wanatumika kwa sasa kama kielelezo feki cha kioo cha ubinadamu wa serikali za Marekani na Ulaya kukubalika ulimwenguni mbele ya umma wa watu weusi. Kwa mtizamo wangu huu ni lazima wale wote wenye mawazo kuwa Obama atasaidia weusi na hasa sisi waafrika waandike maumivu na masikitiko. Kwani akishakuwa Rais, kipaumbele kitakuwa ni maslahi ya Marekani kwanza kwa kufuata maneno ya Raisi Rutherford Hayes. Yaani kutumikia makampuni mbalimbali kabla ya kutumikia wapiga kura. Je tutarajie kama Raisi wa Marekani hatumikii watu wake, je atatumikia watu walio mbali naye kama sisi waafrika? Tuache ubaguzi tufikiri sana na tuangalie kwa bongo zetu na si kwa mioyo.

AFRIKA MATATIZO YASIYOKWISHA

Umeyasikia haya ya wapigania uhuru (freedom fighters) wa jamii ya akina Mugabe? kwao demokrasia ikifanya kazi yake haina maana kabisa. Mmojawao huko Uganda anadai kuwa hata kama wakishindwa uchaguzi hawataachia wapinzani watawale.
Ndio maana tusishangae kama Uganda itageuka Zimbabwe siku chache zijazo baada ya Museveni maji kumfika shingoni. Saa nyingine tunadhani matatizo ya Afrika ni Ukoloni, je ni kweli? Lakini Museveni anadai tatizo ni IMF na World Bank.

Thursday, May 22, 2008

BALALI – MWISHO WA SINEMA LA BOT?

Ni saa nane za mchana, siku ya tarehe 21/5/2008 mara napokea meseji ya simu inasema hivi: “Hatimaye picha la BoT lafikia patamu! Balali amefariki! Watatuchezea usanii kuwa huu ndio mwisho wa sinema maana stelingi kafa, ila ukweli wenyewe sinema hii haikuwa na stelingi mmoja tu! Nipe mawazo yako.” Habari hii ilinishtua kidogo kwani nilishatarajia huyu bwana angekufa kwani awali iliripotiwa alitiliwa sumu na mamafia wa kibongo. Akili yangu ilikwenda kwenye hisia za sumu na mara moja nikajenga kanuni za kidhahania (conspiracy theories) kadhaa:

Kwanza kabisa ni muhimu sana kuzungumzia na kuchambua kifo mara kitokeapo. Mara nyingi tunapozungumzia kifo inatusaidia kumchambua aliyekufa weledi wake kimaadili. Yaani ni jinsi gani aliishi wakati wa uhai wake. Kifalsafa, na pia kwa kuzingatia mtizamo wa kikristo, kifo ni utengano kati ya raha na mwili. Kwa maana nyingine, ni kusimama (cessation) kwa uhai katika kiumbe chochote kama hayati Balali. Kwa mtizamo wangu nina maswali kadhaa bila majibu ambayo ni kidhahania zaidi.

Pili, hebu wote wenye akili timamu tujiulize kuwa Gavana aliyeomba kujiuzulu akakataliwa na baadaye uteuzi wake ukatenguliwa (kufukuzwa) hatimaye anakufa baada ya hisia kuwa aliwahi kutiliwa sumu. Huyu ndiye shahidi muhimu sana katika sakata la BoT na nadhani kwa mafisadi sasa wanapumua sana. Ndie mtu pekee ambaye kama Gavana alijua michezo yote michafu katika skandali hili kwani yeye alikuwa stelingi kama nilivyokwisha elezwa na mtuma meseji ya simu awali.

Kwa wapenda picha, filamu,kuna msemo kuwa, kwa kawaida stelingi hauawi, akiuawa sinema imeisha; sitarajii tena kama kutakuwa na lolote la maana kuhusu sakata la BoT. Kifo hiki ni pigo kubwa kwa wale wote tuliodhani vita ya mafisadi ni rahisi. Ni vita ngumu sana kwani mara nyingine mafisadi wanawamaliza wale wote watakaoweza kusaidia michezo yao kugundulika ili kupoteza ushahidi.

Tatu, nategemea ile kamati ya kuchunguza dhahama la BoT imalize miezi sita ije na madai kuwa haikuwahi kumuhoji hayati Balali. Nina wasiwasi inawezekana kupewa muda wa miezi sita ilikuwa ni kuvuta muda ili huyu bwana afe kama ni kweli aliwahi kupewa sumu. Na kama niko sahihi basi sitasita kukubali madai ya mwandishi mmoja kuwa dola yetu sasa ni kimafiamafia hivi; yaani inatumikia mafia. Si hili tu ninalolidhania ila niseme tu kifo hiki kimenishangaza sana; yaani kilitokea ijumaa (16/5/2008). Siku tano baada ya kifo habari zake ndipo zinafika nchini yaani jumatano ya tarehe 21/5/2008. Huu mficho wa nini?

Swali lingine la kidhahania ni kuwa hivi huyu Balali alikuwa mtumishi wa serikali au la? Alishafukuzwa (kutenguliwa uteuzi), sasa inakuwaje kifo chake kiwe ni wajibu wa serikali kukitangaza kwa umma? Waandishi wa habari pia walijazana benki kuu kutaka kujua ni vipi kuhusu kifo cha mtu ambaye hakuwa na uhusiano na taasisi ya benki kuu. Inanishangaza kidogo labda nifafanuliwe maana ya kutenguliwa kama si sawa na kufukuzwa. Mtu ambaye alishajiuzulu kwa barua na kujiweka pembeni ingawa baadaye kuonesha kuwa hatakiwi kabisa alitenguliwa uteuzi wake. Jamani naomba nijulishwe maana ya kutenguliwa uteuzi ni kufukuzwa ama vingine? Kwani kifo hiki kinaonesha wazi si kufukuzwa ndio maana BoT waliwajibika kutoa taarifa maalum kama vile huyu bado mtumishi wao.
Kanuni nyingine ya kidhahania: Najiuliza zaidi eti hayati Balali kafia Marekani na mazishi yake hatujui ni wapi japo inaonekana hata familia yake iko huko. Tetesi ni kuwa alikuwa ni raia wa Marekani zinapata ukweli manake huyu mtu kama hata mazishi yatafanyika huko Marekani basi serikali iliyopita itapata doa. Yaani iliajiri Gavana ambaye si raia? Je huu uoza wote wa BoT si inawezekana umechangiwa na kutokuwa raia? Kwani tangu lini nchi yetu ina sheria ya uraia wa nchi mbili? Kiuzalendo mtu ambaye si raia ataweza kujali uzalendo katika maamuzi yake kwa kusimamia sheria na taratibu za nchi? Mamlaka iliyomteua na nyingine ikaendelea naye ina deni kubwa kwa watanzania.
Binafsi, inanishawishi niamini ile sheria ya uraia wa nchi mbili (dual citizenship) kumbe tayari inatumiwa na wateule wachache hapa Tanzania kama akina Jeetu Patel na mwenzie Vithlani pamoja na hayati Balali. Na kama niko sahihi basi si hayati Balali tu anayefaidika na sheria hii bali tutarajie kuwajua wengine wanaofaidika na sheria kama hii vita dhidi ya mafisadi itaendelezwa. Waziri wa fedha kipindi cha uborongaji wa BoT, mama Zakia Meghji ameripotiwa akimsifia marehemu ete alikuwa mchapakazi hodari. Imenishangaza yaani unakuwa kiongozi alafu mafisadi wanajichotea fedha hazina ya serikali ukiangalia tu alafu mambo yakiharibika unaandika barua kujiuzulu eti huo ni uhodari.

Mwisho, kifo cha mtu yeyote ni ukumbusho wa jinsi gani mtu aliishi kimaadili au la. Na kwa Balali ni wazi kama Gavana, uoza wake ulifichuka pale ukaguzi wa Ernst & Young ulipoanika ufisadi wa EPA. Kimaadili namwondoa katika kundi na huyu anatuachia kumbukumbu ya ufisadi. Kama si fisadi basi wanafamilia wake wamsafishe na kutujuza nini hasa zilikuwa hisia zake kabla ya kuondoka. Ila kama wataendelea kushiriki huu usiri wa serikali kuhusu kifo chake ni wazi yeye pamoja na familia yake hawatalikwepa hili limzimu la ufisadi.
Binafsi nadhani hayati Balali kafa kama mtu pekee Tanzania ambaye hakuwahi kufukuzwa kazi ila uteuzi wake ulitenguliwa. La kushangaza kwanini kujiuzulu kwake kukataliwe? Aliogopwa sana? Ama mamlaka ya uteuzi ni ya kishikaji sana na kufukuza wavunja sheria na taratibu ni vigumu kwayo au ina woga kumtia mkosaji kwenye aibu? Sina jibu hapa ila kifo hiki kwa kiasi fulani kinatupa picha halisi ya udhaifu ama uimara wa mamlaka kuu ya utawala wa nchi hii. Na kwa mwono wangu mdogo nadhani kama shahidi muhimu katika suala la BoT basi skandali hiyo imepoteza mwelekeo na ni furaha kwa mafisadi wengi waliohusika.
Mungu amlaze hayati Balali mahali pema peponi, Amina.

Thursday, May 08, 2008

UTAPELI WA WALOKOLE

Watu wanadai eti kuna walokole wenye uwezo wa kutibu Ukimwi kwa sala!Mama wee!, huyu katumiwa na walokole kudanganya aliponywa kwa miaka kadhaa.
Malimwengu bwana, yaani kumbe tunadanganywa sana, lazima tuwe macho sasa na haya madini yaliyoongezeka sana.

Friday, May 02, 2008

MEI MOSI MAONESHO


Jamaa wa zimamoto kutoka uwanja wa ndege KIA nao walikuwepo kuonesha mambo yao:

Thursday, May 01, 2008

MEI MOSI ILIVYOFANA MOSHI


Niliamua nijumuike na wafanyakazi Mkoa wa Kilimanjaro; picha zitakuonesha mambo yalivyokuwa.


Hapa jamaa wanaonesha jinsi shughuli za kilimo cha kahawa zinavyoendeshwa:

Sunday, April 27, 2008

HAPA NI WAPI?


Kama unajua hili ni jengo gani mjini Moshi sema.

MASALIA YA AJALI YA NDEGE



Haya ni masalia ya ndege ndogo iliyoanguka Moshi miezi kadhaa.

AJALI YA NDEGE - MOSHI

Nilikuwepo ndege ilipoanguka Moshi maeneo ya jirani na kiwanda cha mafuta BP. Watu wawili walipoteza maisha yao: Rubani (Mbongo) na Mzungu mmoja. Wengine wawili walijeruhiwa.Ilikuwa ni Januari mwaka huu.

VYOO VYA USWAHILINI

Hiki choo kimebomoka lakini kinatumika, ndio mambo ya walalaho wa kitanzania. Nusu kimetoboka na jamaa akija kujisevu hapa inabidi awe makini asije tumbukia.

HILI NALO BAFU


TUONE NA MABAFU YA KUOGEA YA MTANZANIA WA KAWAIDA

Mtanzania wa kawaida ambaye kwake maisha ni magumu na haoni vijisenti hata kidogo. Yeye huwa anaoga mahali kama hapa. Chini ni mchanga tu, hakuna mlango na ujenzi wa bafu ni makaratasi na magunia. Haya yakitokea, wengine wanakomba mafedha "vijisenti" na wala hawachukuliwi hatua. Wanalazimishwa kujiuzulu tu.

HEBU TUJIONEE VYOO VYA WATANZANIA

Hapo chini ni hali halisi ya vyoo vya mtanzania wa kawaida ambaye vijisenti kwake ni ndoto. Mambo ya uswahilini hayo.

Saturday, April 05, 2008

UFISADI HADI JESHINI UGANDA

Wakati ufisadi umetawala Tanzania,kule Uganda hakuna tena woga, mafisadi ambao zamani walikuwa jeuri sasa mkono wa sheria unawakumba. Kuna Jemedari wa jeshi sasa kawekwa jela kwa kosa la ufisadi jeshini. Hebu msome anavyojitetea dhidi ya ufisadi alioufanya.
Majenerali wengine wanaendelea kukanusha ufisadi. Wakati jeshi letu liko Comoro, Waganda nao wako Somalia na kuna tetesi za ufisadi zaidi jeshini.

Tuesday, April 01, 2008

MAJENERALI UGANDA MATUMBO MOTO

Kwa wale masekretary wa vibosile basi wajifunze ni jinsi gani kazi hiyo imejaa ufisadi kutoka kwa sekretary wa Museveni.
Kuna skandali kubwa dhidi ya maafsa wa jeshi la Uganda kwa kuajiri askari hewa: unalijua? Msome pia kinara wa skandali hilo Jenerali James Kazini, ni yule aliyewahi kushtakiwa na Umoja wa Mataifa kwa kuibia DRC rasilimali.

Tuesday, March 18, 2008

YOWERI MUSEVENI NA AJENDA YA KIFALME

Muammar Ghadafi amemuhimiza Museveni aendelee kuitawala Uganda milele.

Saturday, March 15, 2008

NRM NA MADHILA KWA WAGANDA

Unataka kuijua NRM, ni chama dume, tawala kama kilivyo CCM, lakini madhara yake ni makubbwa sana kwa watu wake.

Thursday, March 13, 2008

TANZANIA NA MFUMO WA KIOLIGACHI KAMA URUSI

TANZANIA NA MFUMO WA KIOLIGACHI KAMA URUSI

Wiki hii nimeshawishika kuchangia juu ya mwono wangu kuhusu hili skandali la wizi wa fedha kule benki kuu: BoT maarufu kama EPA. Kwanza nimevutwa na mchango wa jumapili iliyopita kutokana na makala ya Bw. Tambwe Hiza: “Fedha zetu ni muhimu kuliko mashitaka” Tanzania Daima, Jumapili, Machi 09, 2008. uk. 21. Kwangu makala ile imenifanya nijiulize hivi kweli elimu ya Tanzania inafundisha watu kufikiri hasa?

Kwanza niseme tu nampongeza mwandishi kwa mtizamo wake huu ambao una tija moja tu: nayo ni fedha zote kurudishwa. Haya ni mawazo mazuri sana ambayo kwangu yananipa wasiwasi kama tunafurahia kurudishwa kwa fedha kwa kuwabembeleza wahalifu. Siamini kuwa kashfa hii imetufikisha mahali tuwaogope hawa mafisadi hadi kuwalinda na kuwahakikishia usalama wao mara watakaporudisha dhidi ya mkono wa sheria.

Pili, mwandishi alitumia mifano hai kuonesha jinsi gani matatizo katika nchi mbalimbali yalivyotatuliwa kwa njia nje ya mkondo wa kisheria. Nina wasiwasi kuwa kama tunawaepusha mafisadi na mkondo wa kisheria basi tunajenga mustakabali mbaya (wrong precedence) kwa mwelekeo wa Taifa hili changa kidemokrasia. Mwandishi alitahadharisha eti kama tutafuata mkondo wa kisheria basi itatugharimu sana kuwapata mafisadi ambao watakimbilia ughaibuni. Hili si kweli kabisa: moja, mfano jirani zetu Kenya kumekuwa na kashfa kubwa kama ile ya Anglo Leasing ambapo mabilioni ya dola yalichotwa kama EPA.

Baada ya watuhumiwa kujulikana hasa vigogo, tumeona serikali kama za Marekani na hata Uingereza zikiwanyima hata visa (hati za kusafiri na kuzuru nchi zao). Matokeo yake baadhi ya vigogo wa serikali ya Kibaki hawaruhusiwi kuitembelea Marekani. Mbili, sisi hapa hata kuwataja tunaogopa na hii inawaruhusu wawe huru kutoroka huko ambako Bw. Tambwe anakohofu itatugharimu kuwapata. Usiri huu kwa nia ya kubembelezana wahalifu nadhani ndio utakaotugharimu zaidi kuliko tungeamua kukazia kwenye mkondo wa kisheria.

Tatu, mwandishi wa makala ile alidai kuwa: “Binafsi nitafurahi endapo rais atashauriwa kusaini ‘Presidential Decree’ ya kuwasamehe waliorejesha fedha na watakaozirejesha”. Hii inanirejesha pale awali niliposema juu ya ‘wrong precedence’. Kama kweli ndio mawazo ya serikali yetu basi ni kusema kuwa Taifa letu limetupwa kwa mambwa. (thrown to the dogs). Ni kielelezo tosha cha tatizo la kielimu na kifikra miongoni mwa watanzania walio wengi hasa katika nyadhifa za juu. Haingii akilini eti watu Flani wanachukua kiasi cha fedha cha Taifa na kuzifanyia biashara zao alafu uchumi wan chi unaathirika vibaya hasa thamani ya shilingi yake nab ado kuna watu wana mawazo eti tuwasamehe na kuwapa upendeleo Fulani dhidi ya mkono wa sheria.

Ni wazi woga wote huu wa serikali katika kupambana na hili ni kwasababu tu Taifa letu limejaa mafisadi wa hali ya juu. Watu wasioshikika kirahisi wenye mitandao hadi ikulu na hata katika idara zote nyeti za nchi. Kule Urusi ya Putin wanawaita hawa watu ni “Oligarchy”. Ni watu wenye hila, wasio na huruma na maisha ya binadamu wenzao hata kidogo. Kwa kawaida hawa wanalindwa na dola katika ufisadi wao. Hawa hukamatwa tu pale ambapo wameamua kuwa maadui wa dola kwa kuanzisha harakati dhidi ya dola. Na ndio maana watu kama “Khodokosky” yule tajiri wa kampuni ya mafuta ya ‘Yukos’ anaozea jela baada ya kuanza kumpinga Putin.

Hapa kwetu kile anachotetea Bw. Tambwe ni katika kuendeleza mfumo wa kioligarchy kama ilivyo kule Urusi. Kama alivyokiri mwenyewe hajatumwa na mtu; lakini kama mtu una akili inayojali kuwajibika kimaadili kwa kila utendalo basi kwa Bw. Tambwe nadhani kwake maadili si hoja maadam hela zinarudi zote. Hivi kuna maana gani kuwa na Taifa ambalo watu ama viongozi wake wanakuwa huru kuiba fedha na baadae kuzirudisha baada ya kuzitumia kwa matumizi yao binafsi? Tena wanazirudisha wakati zimeshapoteza thamani ya kipindi walipozichota alafu tunasema hela imerudi.

Alafu pia tunajenga Taifa ambalo viongozi wake hawana mfumo maalum wa kitabia katika ofisi za umma (code of conduct). Ni hatari manake ni lazima tuwe na taratibu za kisheria za kuadhibu makosa na wala si kubembelezana.

Ningependa pia nipinge mifano kadhaa ambayo Bw. Tambwe aliitoa katika kuhimiza hoja zake; na hasa ni juu ya jinsi kule Kenya mfumo wa kisheria ulivyoachwa na mazungumzo yakaleta faraja. Naamini kama tunafananisha na Kenya kwa hili la BoT basi ile naiona kama mfanano usio sahihi (wrong analogy). Labda tu nimkumbushe Bw. Tambwe kuwa kwa Kenya bado ni mapema sana kudhani kuwa siasa za Kenya zitatulia. Kuna suala moja nyeti sana wakenya wameliacha nalo ni Haki (justice). Ni usanii tu pale kwani haiwezekani mtu ashinde kwa kuiba kura alafu wafanye kazi pamoja na aliyeibiwa kirahisi. Ni usanii tu; kwani siamini kuwa miaka mitano serikali hii ya Muungano (grand coalition) itadumu. Kuna tofauti za kimsingi kati ya ODM na PNU ambazo bila kuzingatia haki haziwezi kusawazishwa.

Ni katika mfanano huo wa Kenya ambao siamini unatufaa katika hili la EPA. Masuala ya kimaadili hayawezi kutatuliwa kwa kisiasa; haya ni mambo yenye kuathiri uchumi na maendeleo ya nchi na kama tunafanya makubaliano na hawa maoligarchy wa kitanzania basi ni kutangaza Tanzania kama Taifa la viongozi kuwa huru kuiba kwani watarudisha. Kwa mtizamo wa Bw. Tambwe, kitaalamu ni kuwa hii ni nchi ya ustahimivu wa maovu wa hali ya juu (highest impunity) kwa watawala.

Mawazo ya Bw. Tambwe yalikuwa ni mazuri kusikiliza na kihisia (emotionally) lakini unapoyaingiza ndani ya ubongo ni ya hatari kwani ni kweli fedha zitarudi lakini ndio utakuwa ni mwanzo wa kuwaruhusu watawala kutumia ofisi za umma kuiba bila kushtakiwa kwani wanarudisha. Na kwa mantiki hiyo, serikali itatumika kama mkopeshaji bila riba kwa vigogo kama ilivyokwisha jionesha kwani pesa zinarudishwa bila riba. Hii ni hasara kwa nchi; na i ikiachwa iendelee basi zitaibiwa nyingi sana kitu ambacho ni hatari sana.

Mwisho niseme ni vyema tukumbuke kila mtu ana haki ya kutoa maoni ila tukae chini tufikiri kwa mapana kimantiki na si kihisia kabla hatujazungumza. Nalisema hili kwani umasikini mkubwa unaoikumba Tanzania na hata Afrika ni kwasababu tumegeuka kuwa watu wa mashiko ya kihisia zaidi kuliko kufikiri. Tanzania ya leo hakuna tofauti ya kimawazo kati ya msomi wa hadhi ya mwanasheria mkuu dhidi ya msomi wa elimu ya msingi linapokuja suala la kuwajibika na kutoa mawazo ya kifikra yanayohitaji kufikiri hasa.

Kwani wenye mawazo kama haya ya Tambwe basi kuna tatizo la ubinafsi hasa pale mtu anapochagua hatua ambazo hazitamuumiza panapohitaji kuwajibika. Kimaadili tunasema ni ‘ethical relativism’. Kuepukana na hili zinahitajika bongo kufanya kazi kwelikweli. Na kwasababu kwa Tanzania hili ni tatizo kubwa basi ufisadi na mafisadi wataendelea kutesa hasa.

Saturday, March 08, 2008

SIKU YA AKINA MAMA TANZANIA

Ni siku ya wanawake duniani; na hatuna budi kutafakari.

Ulimwengu wa leo umejaa “ngano” nyingi sana ambazo kwa kiasi kikubwa ni chanzo cha tamaduni na ustaarabu usio makini miongoni mwa waafrika na hasa watanzania kwa ujumla wetu. Katika siku hii ya wanawake duniani, nasema hivi huku nikijiuliza bila majibu maswali kadhaa:

Mosi, hivi siku hii ya wanawake duniani ni changamoto zipi tulizonazo kama watanzania? Kwangu nadhani ni wakati muafaka kwa jamii ya wanawake kujiuliza hivi ni kwa vipi bado wanaishi katika “ngano”: yaani bado kuamini wao si bora zaidi ya wanaume? Badala yake mwelekeo wa uongozi wa nchi hii umebakia na wanawake wasindikizaji, yaani wanaoridhika na vyeo tu. (sycophants). Hawa hawana hoja mbadala kwa bwana mkubwa; na ndio maana katika hii dhahama yote ya ufisadi (ufisadizesheni) iliyoikumba nchi yetu hakuna wanawake hasa wasomi wakionesha hisia zao kimaandishi ama kimdomo.

Pili, ni wakati akina mama kujiuliza hivi ni lini wataamua kukataa kutumiwa kama chombo cha kustarehesha (enticing object)? Hili naliona kwani ni ukweli halisi kuwa ufisadi mwingi nchini Tanzania unachangiwa sana na tamaa ya akina baba wengi kutamani mafedha katika kile kuwaridhisha wapenzi ama wake wao waishi raha mustarehe. Ni wakati akina mama waamue la sivyo ufisadi hautakwisha.

Tatu, kuna huu upendeleo maalum kuwainua wanawake (affirmative action): nakumbuka tamko la Beijing (Platform for Action) ilihimiza kuwainua wanawake katika nyadhifa za kiuongozi dhidi ya mfumo dume (partriarchy). Kwa Tanzania nadhani rais Jakaya Kikwete katimiza hili. Ila nadhani kaenda mbali sana manake kuna wanawake wengi tu nchini mwetu wana nyadhifa zisizolingana na kiwango cha elimu walichonacho na wanapwaya sana pale mambo yanayohitaji mtu atumie bongo hasahasa. Hili nalisema wazi kuwa nadhani upendeleo maalum naukubali lakini usitumiwe kama zawadi kwa mtu ama ahsante kama tunavyoshuhudia kwa sasa.

Kwa Tanzania, nimeshangazwa sana kuona bunge letu limejaa hawa wabunge wa viti maalum ambao wengine hata elimu ya sekondari hawana ama wameishia kidato cha nne na vikozi kama vya vyeti vya utunzaji ofisi (secretary). Siamini kabisa katika ulimwengu wa leo, mbunge wa aina hii anaweza kutoa mijadala ya kimantiki katika kujenga nchi yetu; wengi wao hawajui hata sera za kiuchumi za nchi zikoje ama hata mpangilio wa kidunia ukoje (World Order). Ni katika mtizamo wa aina hii hata hizi kashfa kama za Richmond, EPA – BoT na zingine nyingi zimetufikisha hapa tulipo leo bila kuhojiwa huko Bungeni. Ni wazi wabunge wengi wa viti maalum ni mzigo kwa walipa kodi wa nchi hii.

Tufike pahali tukomeshe huu mfumo wa uwakilishi wa viti maalum. Ikibidi tuige nchi kama Uganda kwa mfano, wabunge wanawake wote ni lazima wagombee na wapigiwe kura na wananchi na si kama hapa kwetu ambapo mara nyingi njia chafu kama rushwa za kila aina mara nyingine hata za ngono zinatumika miongoni mwa vigogo wa vyama vya siasa ili mabibi warembo fulani wawe wabunge. Pia hata Kenya hivi majuzi tumeona ni jinsi gani wanawake wamejikakamua kuhakikisha wanagombea na wanaume na kushindana kwa hoja badala ya kusubiri kuhonga kamati za chama / vyama ili vikupitishe kupitia vitandani na hongo nyingine nyingi za kila aina hasa za aibu.

Nne, tukiacha mambo ya mustakabali wa nchi yetu kisiasa, pia kifamilia tayari tujiulize mambo kadhaa: mojawapo ni hili la wanawake kujikomboa katika mtizamo wa kujilinganisha na wanaume ukiachilia mbali tofauti za kimaumbile (anatomy) na hata kimajukumu (roles). Katika hili kundi (radical feminists) naliona kama hatari sana katika Tanzania ya leo. Hawa ni wale wanawake wasomi kabisa na kwa mantiki hiyo ubinafsi umewajaa kwa kiwango kikubwa (highest ego) na matokeo yake hawawezi kudumu katika ndoa ama hata kama wanadumu wanaishi katika ndoa zilizofeli (failed marriages). Hawa ndio walioshindwa kuwa mifano bora kwa jamii; na wengi wana nafasi kubwa katika jamii wakibadilisha wanaume – vigogo kama njugu ili kuhakikisha wanaishi raha mustarehe. Wengi wao wanaishi wakiwa wamechanganyikiwa (frustrated).

Nimalizie kwa kumbushia nasaha za wanafalsafa wawili: mmoja ni Jeremy Benthamy, ambaye alikataa kata kata kuwa hatambui nafasi yeyote ya mwanamke katika jamii. Alisema: “Wife should submit to husband”, yaani mke shuruti awe chini ya utawala wa mume. Wako wanawake wengi ambao bado wana hisia za bwana huyu na ndio maana wamewafanya wanaume ni miradi yao. Mwanafalsafa wa pili ni John Stuart Mills, yeye anajulikana kama “Male feminist” yaani mwanaume – mke. Alipinga mwanamke kunyanyaswa kabisa. Alishawishi sana kwa wanawake kuruhusiwa kupiga kura nchini Uingereza wakati wa maisha yake. Tunaweza kurejea pale alipoandika juu ya mke wake – Harriet Taylor.

Basi siku hii ya leo itufanye hasa kwa wale wanawake kufuata mawazo ya wanafalsafa hawa wawili kwa kuchagua mmoja. Kazi kwenu sijui mtachagua yupi kwani tukikosea tuataendelea kuishi maisha yaliyojaa hisia na imani potofu za kijinsia (stereotypes). Tufike pahali wanawake waamue kikwelikweli na si kimzaha mzaha kushiriki katika nyanja mbalimbali za maisha nchini Tanzania na kuachana na kuishi kwa unafiki ilimradi wanapata upendeleo kuwawezesha kupata mkate wa kila siku. Nashangazwa sana hadi leo bado wanawake wengi sana nchini mwetu na Afrika kwa ujumla wako tayari kujidhalilisha ilimradi wapate vyeo, upendeleo, na raha za kila aina kutoka kwa wanaume.

Ni katika mtizamo huu; bado wanawake wa Tanzania bado wako kizani hasa kama wanafikiri wameshajikomboa. Manake hata wengi wa wanaharakati si mfano bora kimaadili linapokuja swali la mahusiano bora ya kijinsia. Tujiulize je siku ya wanawake imetusaidia kubadili mwelekeo wetu? Au ni usanii kama kawaida?

Wednesday, February 27, 2008

ZIARA YA BUSH—NA UFISADI WA FIKRA ZETU

Mwezi wa februari utabakia wa kukumbukwa kwangu binafsi kwa matukio kadhaa ya kukumbukwa. Kwanza, tarehe ya pili tu nilimpoteza bibi yangu, Emilia aliyefariki akiwa na umri wa miaka tisini na sita (96). Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi. Tarehe saba wakati nikiwa nimesimama pembeni ya jeneza la bibi siku ya mazishi, ndugu yangu mmoja ananiuma sikio kuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa amejiuzulu.

Ukiacha hayo mawili, lingine ambalo kwangu naliona la kukumbuka ni ziara ya Rais George Bush nchini Tanzania. Imenishangaza sana huyu bwana kapata mapokezi makubwa sana barani Afrika kitu ambacho ni tofauti katika mabara mengine ambapo anachukiwa sana. Kwangu nadhani ina mafunzo mengi sana kwetu kama wananchi na hasa kwa viongozi wetu. Labda niseme pia siungi mkono hata kidogo kelele na pingamizi nyingi ambazo zilioneshwa na baadhi ya watanzania—waislamu wachache na jumuiya ya wasomi wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam. Nasema hivi kwani siamini kabisa kuwa rais Bush anazo sera zake binafsi ila kila kinachofanywa na serikali ya Bush ni matokeo ya sera ya nje ya serikali ya Marekani ikihanikizwa na imani za kihafidhina za Chama cha Republican.

Tatu, sijui kama Magaidi wasingeivamia Marekani September kumi na moja kama kweli leo majeshi ya Marekani yangekuwa Iraq na Afghanistan. Lakini pia sijui kama kweli kuna njia gani ya mazungumzo ingetumika kuleta mabadiliko ya kiutawala ya kidhalimu chini ya Matalebani ama Saddam Hussein. Si kura hata kidogo ingeumaliza udikteta wa Saddam ila kujitoa mhanga wa maisha ya watu—yaani damu kumwagika ili kuleta mabadiliko kutoka mfumo dhalimu. Kama hatutaki kuamini hivyo, basi tuangalie Kenya kama itatulia iwapo Kibaki atakuwa rais kwa miaka mitano ijayo. Kuna nyakati vita haiepukiki ili kuleta mabadiliko kwani hata nchi yetu ilibidi ipigane vita kumng’oa Iddi Amin ili kuung’oa udikteta wa Amin Uganda.

Kwa kuzingatia mwelekeo wa uchumi wa kileo duniani, na hata kihistoria, Taifa kubwa limejiimarisha kwa njia nyingi mojawapo ikiwa ni vita. Hivyo basi, Bush si wa kwanza kuendesha vita. Hata Nyerere aliendesha vita kwa maslahi ya nchi yake (Tanzania) kitu ambacho anafanya Bush. Hivyo basi, kumkataa Bush asitembelee nchi yetu si hoja yenye mashiko sana kiuhalisia leo hii; kwani kama asingekuja na hata alivyokuja, hakuna kitu amepoteza. Nguvu ya kujieneza ya Taifa kubwa kama Marekani haizuiliki; hivyo basi kimtizamo kelele za pale Mlimani zilikuwa zimejaa mantiki ya kitaaluma ambayo kwangu sina hoja kupinga uhalali wake kimaadili na katika suala zima la uadilifu unaotakikana kwa mwanadamu.

Lakini katika hali halisi ya dunia si hoja muafaka manake inaonekana maisha ya mwanadamu na mtanzania wa leo yamejaa matendo mengi ambayo si ya kimaadili lakini ndiyo yamefanywa haswa kama utamaduni. Hata Raisi Kikwete alimwambia Bush kuwa kwetu watanzania hatuana shida nae japo zipo serikali nyingine ambazo zina mitizamo tofauti na sera zake.

Kwa maana nyingine mtanzania anaongozwa na mbinu nyingi za kifisadi kufikia malengo yake; na ndio maana ziara ya Bush ilikuwa ya mapokezi mazuri sana sidhani kama amewahi kufanyiwa hivyo ugenini hata siku moja. Tanzania ni Taifa linalojiendesha kifisadi fisadi sana na ndio maana ni wananchi wachache sana waliokuwa na muda wa kutafakari hoja za wasomi wetu kule Mlimani. Watanzania na serikali yao hawajali jambo fulani linapatikana kwa njia gani ilimradi tu lina tija katika kutatua matatizo yao. Ni nchi ambayo kama kweli una elimu yako nzuri na ya juu kama vile Dr. Msabaha alivyofanya kwenye skandali ya Richmond, lazima uachane na kile unachokiamini ndio sahihi na ufuate matakwa ya utawala. Labda nieleze ni kwanini watanzania na serikali yao hawakuona haja ya kusikiliza busara za kisomi:

Moja, ziara hii imetoa msaada mkubwa kwa nchi yetu katika sekta ya afya na miundombinu. Japo nina mashaka na mafisadi hawataziacha salama, ila ni kielelezo kuwa Bush ana nia njema na nchi yetu. Na katika kutia shime vita dhidi ya ufisadi, Bush alisema baada ya kusaini mkataba kuwa fedha za Marekani si kwa mafisadi. Na kusisitiza kuwa moja ya masharti ya Mfuko wa Millenia ni serikali yetu kuzingatia “Utawala Bora”, vita dhidi ya ufisadi na kwa ujumla serikali inayojali watu wake.

Pili, ziara hii imeonesha ni jinsi gani Raisi Bush na mkewe walivyo watu wa kujitolea (compassionate)hata huruma ya kujali watu wa kawaida. Kwa viongozi wetu wamejifunza ni jinsi gani wanapaswa kuishi na kujichanganya na watu hohehahe kama walivyo watanzania wengi. Viongozi wetu wengi wa Afrika, kwa mfano, si rahisi mtu atembelee hospitali na umwone akikumbatiana na kukaa karibu kabisa kwa kujichanganya na wagonjwa. Hili Bush katoa funzo; nilitegemea kule hospitali ya Mount Meru nione makachero wakiwa karibu na Raisi wakimwongoza wapi apite na ashikane na nani mkono au hata kuwazuia watu wasimkaribie bwana mkubwa. Hili sikuliona ila niliona Raisi Bush akijiweka sawa na binadamu wengine na kukaa hata karibu nao kabisa, wala si kwenye kiti maalum bali viti vya kawaida wanavyokalia wagonjwa kwenye foleni. Wakubwa wetu watataka sofa maalum tofauti na walalahoi.

Kimavazi pia imekuwa ni funzo kwa viongozi na vigogo wetu. Unakwenda kuwatembelea watu masikini ni lazima angalau ufanane nao. Kwa Bush hili alilizingatia hasa na wala sikuona akiwa ndani ya suti, siku ile yenye joto ambalo lingemfanya achemke kwa joto na aogope kujichanganya. Nadhani ndio maana kulikuwa hamna haja ya wanausalama kumzuia kuwa karibu na watu kwani vigogo wetu inabidi makachero kuzuia watu ili bwana mkubwa apate hewa kwani mara nyingi unakuta watu wamevaa misuti. Hapa katukumbusha mavazi rahisi (simplistic). Hili nalo ni funzo gumu kwa vigogo wa kiafrika kulimeza.

Wakati akiitembelea shule ya sekondari maalum kwa wasichana wa kimasai kutoka mazingira magumu alinigusa hasa. Labda niseme mwaka jana Raisi Jakaya Kikwete alifungua shule moja ya sekondari kule Moshi. Ilikuwa ni ziara ya saa moja kufungua shule rasmi; na mara alipowasili pale shuleni si walimu wala wanafunzi waliopata muda wa kumfariji na kumpokea rais wao. Kilichotokea nilishangaa kuona makada kibao wa CCM pamoja na vigogo wa serikali kutoka mkoani na wilaya za jirani wakihangaika kugombania kujipanga mstari ili tu kushikana mkono na bwana mkubwa. Walimu waliokuwa wamejipanga sehemu maalum walifunikwa na wala hawakuweza kupata nafasi hiyo. Wala raisi hakuwa na muda wa kusalimiana ama kuzungumza sana na wanafunzi zaidi ya kupiga kejeli za kisiasa katika hotuba yake. Nadhani angeteta na wanafunzi kadhaa na kusikia hisia zao ingependeza zaidi.

Lakini kwa Bush tumeoneshwa nini maana ya kuwa kiongozi na nini cha kujali wakati unapotembelea sehemu. Raisi Bush alisalimiana na watoto wote wa shule ile pale Arusha; pia alisalimiana na hata kucheza ngoma na wamasai waliokuwa wakiburudisha ikiwa ni pamoja na kuwakumbatia baadhi yao. Hapa kwetu na Afrika kwa ujumla sivyo inavyokuwa, wanausalama hawaruhusu hili kabisa. Hivi huwa najiuliza kila Rais wetu anapokuwa mahali utaona mlinzi wake/ msaidizi wake kasimama nyuma. Hivi hiyo ndio kumaanisha ulinzi wa rais ni imara? Mbona watu kama akina Bush si hivyo na ulinzi ni imara? Nadhani ziara hii iwe mwanzo wa kuiga jambo kwa wanausalama na kwa ujumla wale watu wa karibu wa bwana mkubwa.

Labda niungane na waziri Dr. Jumanne Maghembe aliponukuliwa na ITV katika ziara ya Bush kule Arusha: “Marekani ni Taifa kubwa na tajiri na lina fursa nyingi. Ni vizuri tukashirikiana nayo na kudumisha urafiki na udugu na Taifa hili”. Nikiwarudia wale walionesha kutokutaka ziara hii: Hasa wasomi wa Mlimani, wajameni hivi tunajua kuwa wahenga waliwahi kusema kwa kiingereza tafsiri isiyo rasmi: “Every black has its white”, kuwa kila cheusi kina weupe wake pia”. Hapa namaanisha pamoja na uovu na unyama unaoambatanishwa na haiba ya Raisi George Bush, huyu ni mwanadamu mwenye pande mbili. Na kwa kutilia mkazo kwenu mabaya yake naamini mlighafilika tu; na mashiko ya kihisia yalitawala zaidi ya busara, mbona hamkutizama upande wa pili wa Bush?. La sivyo wala msingefikia hatua hiyo ya kutaka kuandamana.

Ziara ya Bush imetuonesha upande wa pili Bush mwanadamu. Mpaka kaondoka sijasikia akiongelea habari za Africom kama wasomi wetu walivyokazia kuwa anatafuta mahali pa kujenga kambi za kijeshi. Pia nadhani kilio chenu kingine kuwa kumkaribisha Bush ni kuonesha serikali yetu imeamua kuacha marafiki wa zamani na kufuata mabepari kama hatua isiyo muafaka si sahihi. Tumefuata sera za marafiki zetu kama Cuba, China na wengine wengi kwa miongo minne kwa mafanikio sana ya kiuchumi. Dunia ya leo tusiogope sana juu ya hali ya baadaye ila tutumie fursa zinazojitokeza hasa kama zina mwelekeo wa kukuza uchumi wetu.

Tukiwa bado tuna marafiki zetu wa zamani hakuna ubaya kama tunaongeza mwingine bila kuwapoteza wa zamani. Hii ndio hisia ninayoipata kwa ugeni wa Bush. Ziara hii kupitia mkataba wa Millenium Challenge naamini ni fursa ambayo tusingepaswa tuiache kwani ina tija sana hasa kama “mafisadi” watadhibitiwa wasiweke pua zao hapa. Tukumbuke hata jirani yetu Yoweri Museveni alikuwa na uswahiba na Bush na hata enzi za Clinton na kwa sasa wamemtupa kiana na kwa kipindi chote Uganda haikuwahi kuathiriwa kijeshi na Marekani ingawa kwa sasa kuna makampuni kibao ya Marekani yakianza kuchimba mafuta nchini humo.

Funzo lingine la ziara ya Bush kwangu ni pale kung’amua kuwa kweli nchi yetu ni masikini sana. Yaani bado hatuna uwezo wa kujikinga na Malaria? Yaani Bush anatununulia chandarua watanzania? Yaani watanzania walio wengi hawana uwezo wa kununua chandarua? Kwa maana nyingine watanzania wengi tu wachafu hatuwezi kuishi kwenye mazingira safi yasiyoruhusu mbu kuzaliana. Hatujui wajibu wa kiafya kusafisha mazingira yetu ili kuondoa mazalia ya mbu. Ni aibu lakini tufanyeje? Mpaka aje Bush atununulie chandarua. Hili linanipa shida sana kwani nadhani fedha ya malaria ni nyingi na ingefaa itumike kwenye sekta kama ya elimu. Sidhani kama unamzuia mtu asiugue malaria lakini hapo hapo humpi elimu bora kama unamsaidia sana. Bado umasikini hautoki kwa njia hii.

Ukimwi pia ingawa ni janga ambalo binafsi limeniathiri sana; ila ni wakati tujiulize kuwa hivi kama tukiweza kujihadhari na maambukizi, hizi fedha zote za Bush si zingefanya mambo mengine? Napata mashaka sana kama tunaendelea kupata ufadhili hasa wa kurefusha maisha na kwa wakati huo huo hatuna utaratibu wa kuwalinda wale ambao hawajaambukizwa ambao kwa kujichanganya kwao na waathirika wengi ni hatari.Ni wazi waathirika Fulani wana hasira sana na lengo lao kubwa ni kuondoka na wengine. Sisemi hili kwa kunyanyapaa ila ni lazima tufike mahali tujiulize hii misaada mikubwa ya kulinda maisha ya waathirika ina matokeo mazuri? Ni kwa vipi tuifanye tuwe na mazingira mapya kiutaratibu wa maisha ili tupate tija. La sivyo Taifa zima litaangamia na mamilioni ya dola za Bush.

Mwisho, nimalizie kama nilivyoanza: wakati nikiwa pale pembeni ya jeneza la bibi yangu baada tu ya kunong’onezwa na ndugu yangu kuwa Waziri Mkuu kajiuzulu, mara moja nilichoropoka nikaingia ndani nikafungua kiredio changu kidogo, radio sauti ya Ujerumani na nikakutana na sauti yake ikisema: Nimefadhaishwa, nimesononeshwa, …..mengine nimeyasahau manake yalinishangaza kwanini sasa kaamua kujiuzulu. Taifa linapotekwa nyara na mafisadi mtu hushangai pale hata busara za wasomi kama wale wa pale Mlimani zinapoonekana ni kejeli.

Nilisikitika tu pale jeshi la polisi lilipokataa kiaina kutoa ulinzi kwa maandamano ya wasomi wa mlimani kupinga ziara ya Bush. Ingawa sikuwa naunga mkono hoja zao, nadhani walinyimwa haki yao ya msingi kuandamana kupinga ujio wa Bush. Kweli February sitaisahau kama wakati muafaka wa mapinduzi ambayo sina imani sana kama yatabadilisha mwelekeo wa Taifa letu dhidi ya ufisadi. Hii ni nchi inaathiriwa na tabia na hulka ya kubebana, kupendeleana na utapeli wa kila aina. Na ndio maana baada ya Raisi kukabidhiwa ripoti ya Ernst & Young iliyokwishagundua kila ufisadi ndani ya BoT bado anaunda kamati nyingine ya uchunguzi. Lengo ni kulindana tu. Nimeshangazwa pia na mtuhumiwa mmojawapo wa ufisadi karudi kwa wapiga kura wake na kupokewa kwa shangwe na hata kupewa baraka za Askofu wa kanisa lake. Kweli kwa Tanzania ya leo bila ufisadi labda maisha ya wengi yatasimama.