My Blog List

Saturday, March 08, 2008

SIKU YA AKINA MAMA TANZANIA

Ni siku ya wanawake duniani; na hatuna budi kutafakari.

Ulimwengu wa leo umejaa “ngano” nyingi sana ambazo kwa kiasi kikubwa ni chanzo cha tamaduni na ustaarabu usio makini miongoni mwa waafrika na hasa watanzania kwa ujumla wetu. Katika siku hii ya wanawake duniani, nasema hivi huku nikijiuliza bila majibu maswali kadhaa:

Mosi, hivi siku hii ya wanawake duniani ni changamoto zipi tulizonazo kama watanzania? Kwangu nadhani ni wakati muafaka kwa jamii ya wanawake kujiuliza hivi ni kwa vipi bado wanaishi katika “ngano”: yaani bado kuamini wao si bora zaidi ya wanaume? Badala yake mwelekeo wa uongozi wa nchi hii umebakia na wanawake wasindikizaji, yaani wanaoridhika na vyeo tu. (sycophants). Hawa hawana hoja mbadala kwa bwana mkubwa; na ndio maana katika hii dhahama yote ya ufisadi (ufisadizesheni) iliyoikumba nchi yetu hakuna wanawake hasa wasomi wakionesha hisia zao kimaandishi ama kimdomo.

Pili, ni wakati akina mama kujiuliza hivi ni lini wataamua kukataa kutumiwa kama chombo cha kustarehesha (enticing object)? Hili naliona kwani ni ukweli halisi kuwa ufisadi mwingi nchini Tanzania unachangiwa sana na tamaa ya akina baba wengi kutamani mafedha katika kile kuwaridhisha wapenzi ama wake wao waishi raha mustarehe. Ni wakati akina mama waamue la sivyo ufisadi hautakwisha.

Tatu, kuna huu upendeleo maalum kuwainua wanawake (affirmative action): nakumbuka tamko la Beijing (Platform for Action) ilihimiza kuwainua wanawake katika nyadhifa za kiuongozi dhidi ya mfumo dume (partriarchy). Kwa Tanzania nadhani rais Jakaya Kikwete katimiza hili. Ila nadhani kaenda mbali sana manake kuna wanawake wengi tu nchini mwetu wana nyadhifa zisizolingana na kiwango cha elimu walichonacho na wanapwaya sana pale mambo yanayohitaji mtu atumie bongo hasahasa. Hili nalisema wazi kuwa nadhani upendeleo maalum naukubali lakini usitumiwe kama zawadi kwa mtu ama ahsante kama tunavyoshuhudia kwa sasa.

Kwa Tanzania, nimeshangazwa sana kuona bunge letu limejaa hawa wabunge wa viti maalum ambao wengine hata elimu ya sekondari hawana ama wameishia kidato cha nne na vikozi kama vya vyeti vya utunzaji ofisi (secretary). Siamini kabisa katika ulimwengu wa leo, mbunge wa aina hii anaweza kutoa mijadala ya kimantiki katika kujenga nchi yetu; wengi wao hawajui hata sera za kiuchumi za nchi zikoje ama hata mpangilio wa kidunia ukoje (World Order). Ni katika mtizamo wa aina hii hata hizi kashfa kama za Richmond, EPA – BoT na zingine nyingi zimetufikisha hapa tulipo leo bila kuhojiwa huko Bungeni. Ni wazi wabunge wengi wa viti maalum ni mzigo kwa walipa kodi wa nchi hii.

Tufike pahali tukomeshe huu mfumo wa uwakilishi wa viti maalum. Ikibidi tuige nchi kama Uganda kwa mfano, wabunge wanawake wote ni lazima wagombee na wapigiwe kura na wananchi na si kama hapa kwetu ambapo mara nyingi njia chafu kama rushwa za kila aina mara nyingine hata za ngono zinatumika miongoni mwa vigogo wa vyama vya siasa ili mabibi warembo fulani wawe wabunge. Pia hata Kenya hivi majuzi tumeona ni jinsi gani wanawake wamejikakamua kuhakikisha wanagombea na wanaume na kushindana kwa hoja badala ya kusubiri kuhonga kamati za chama / vyama ili vikupitishe kupitia vitandani na hongo nyingine nyingi za kila aina hasa za aibu.

Nne, tukiacha mambo ya mustakabali wa nchi yetu kisiasa, pia kifamilia tayari tujiulize mambo kadhaa: mojawapo ni hili la wanawake kujikomboa katika mtizamo wa kujilinganisha na wanaume ukiachilia mbali tofauti za kimaumbile (anatomy) na hata kimajukumu (roles). Katika hili kundi (radical feminists) naliona kama hatari sana katika Tanzania ya leo. Hawa ni wale wanawake wasomi kabisa na kwa mantiki hiyo ubinafsi umewajaa kwa kiwango kikubwa (highest ego) na matokeo yake hawawezi kudumu katika ndoa ama hata kama wanadumu wanaishi katika ndoa zilizofeli (failed marriages). Hawa ndio walioshindwa kuwa mifano bora kwa jamii; na wengi wana nafasi kubwa katika jamii wakibadilisha wanaume – vigogo kama njugu ili kuhakikisha wanaishi raha mustarehe. Wengi wao wanaishi wakiwa wamechanganyikiwa (frustrated).

Nimalizie kwa kumbushia nasaha za wanafalsafa wawili: mmoja ni Jeremy Benthamy, ambaye alikataa kata kata kuwa hatambui nafasi yeyote ya mwanamke katika jamii. Alisema: “Wife should submit to husband”, yaani mke shuruti awe chini ya utawala wa mume. Wako wanawake wengi ambao bado wana hisia za bwana huyu na ndio maana wamewafanya wanaume ni miradi yao. Mwanafalsafa wa pili ni John Stuart Mills, yeye anajulikana kama “Male feminist” yaani mwanaume – mke. Alipinga mwanamke kunyanyaswa kabisa. Alishawishi sana kwa wanawake kuruhusiwa kupiga kura nchini Uingereza wakati wa maisha yake. Tunaweza kurejea pale alipoandika juu ya mke wake – Harriet Taylor.

Basi siku hii ya leo itufanye hasa kwa wale wanawake kufuata mawazo ya wanafalsafa hawa wawili kwa kuchagua mmoja. Kazi kwenu sijui mtachagua yupi kwani tukikosea tuataendelea kuishi maisha yaliyojaa hisia na imani potofu za kijinsia (stereotypes). Tufike pahali wanawake waamue kikwelikweli na si kimzaha mzaha kushiriki katika nyanja mbalimbali za maisha nchini Tanzania na kuachana na kuishi kwa unafiki ilimradi wanapata upendeleo kuwawezesha kupata mkate wa kila siku. Nashangazwa sana hadi leo bado wanawake wengi sana nchini mwetu na Afrika kwa ujumla wako tayari kujidhalilisha ilimradi wapate vyeo, upendeleo, na raha za kila aina kutoka kwa wanaume.

Ni katika mtizamo huu; bado wanawake wa Tanzania bado wako kizani hasa kama wanafikiri wameshajikomboa. Manake hata wengi wa wanaharakati si mfano bora kimaadili linapokuja swali la mahusiano bora ya kijinsia. Tujiulize je siku ya wanawake imetusaidia kubadili mwelekeo wetu? Au ni usanii kama kawaida?

Wednesday, February 27, 2008

ZIARA YA BUSH—NA UFISADI WA FIKRA ZETU

Mwezi wa februari utabakia wa kukumbukwa kwangu binafsi kwa matukio kadhaa ya kukumbukwa. Kwanza, tarehe ya pili tu nilimpoteza bibi yangu, Emilia aliyefariki akiwa na umri wa miaka tisini na sita (96). Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi. Tarehe saba wakati nikiwa nimesimama pembeni ya jeneza la bibi siku ya mazishi, ndugu yangu mmoja ananiuma sikio kuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa amejiuzulu.

Ukiacha hayo mawili, lingine ambalo kwangu naliona la kukumbuka ni ziara ya Rais George Bush nchini Tanzania. Imenishangaza sana huyu bwana kapata mapokezi makubwa sana barani Afrika kitu ambacho ni tofauti katika mabara mengine ambapo anachukiwa sana. Kwangu nadhani ina mafunzo mengi sana kwetu kama wananchi na hasa kwa viongozi wetu. Labda niseme pia siungi mkono hata kidogo kelele na pingamizi nyingi ambazo zilioneshwa na baadhi ya watanzania—waislamu wachache na jumuiya ya wasomi wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam. Nasema hivi kwani siamini kabisa kuwa rais Bush anazo sera zake binafsi ila kila kinachofanywa na serikali ya Bush ni matokeo ya sera ya nje ya serikali ya Marekani ikihanikizwa na imani za kihafidhina za Chama cha Republican.

Tatu, sijui kama Magaidi wasingeivamia Marekani September kumi na moja kama kweli leo majeshi ya Marekani yangekuwa Iraq na Afghanistan. Lakini pia sijui kama kweli kuna njia gani ya mazungumzo ingetumika kuleta mabadiliko ya kiutawala ya kidhalimu chini ya Matalebani ama Saddam Hussein. Si kura hata kidogo ingeumaliza udikteta wa Saddam ila kujitoa mhanga wa maisha ya watu—yaani damu kumwagika ili kuleta mabadiliko kutoka mfumo dhalimu. Kama hatutaki kuamini hivyo, basi tuangalie Kenya kama itatulia iwapo Kibaki atakuwa rais kwa miaka mitano ijayo. Kuna nyakati vita haiepukiki ili kuleta mabadiliko kwani hata nchi yetu ilibidi ipigane vita kumng’oa Iddi Amin ili kuung’oa udikteta wa Amin Uganda.

Kwa kuzingatia mwelekeo wa uchumi wa kileo duniani, na hata kihistoria, Taifa kubwa limejiimarisha kwa njia nyingi mojawapo ikiwa ni vita. Hivyo basi, Bush si wa kwanza kuendesha vita. Hata Nyerere aliendesha vita kwa maslahi ya nchi yake (Tanzania) kitu ambacho anafanya Bush. Hivyo basi, kumkataa Bush asitembelee nchi yetu si hoja yenye mashiko sana kiuhalisia leo hii; kwani kama asingekuja na hata alivyokuja, hakuna kitu amepoteza. Nguvu ya kujieneza ya Taifa kubwa kama Marekani haizuiliki; hivyo basi kimtizamo kelele za pale Mlimani zilikuwa zimejaa mantiki ya kitaaluma ambayo kwangu sina hoja kupinga uhalali wake kimaadili na katika suala zima la uadilifu unaotakikana kwa mwanadamu.

Lakini katika hali halisi ya dunia si hoja muafaka manake inaonekana maisha ya mwanadamu na mtanzania wa leo yamejaa matendo mengi ambayo si ya kimaadili lakini ndiyo yamefanywa haswa kama utamaduni. Hata Raisi Kikwete alimwambia Bush kuwa kwetu watanzania hatuana shida nae japo zipo serikali nyingine ambazo zina mitizamo tofauti na sera zake.

Kwa maana nyingine mtanzania anaongozwa na mbinu nyingi za kifisadi kufikia malengo yake; na ndio maana ziara ya Bush ilikuwa ya mapokezi mazuri sana sidhani kama amewahi kufanyiwa hivyo ugenini hata siku moja. Tanzania ni Taifa linalojiendesha kifisadi fisadi sana na ndio maana ni wananchi wachache sana waliokuwa na muda wa kutafakari hoja za wasomi wetu kule Mlimani. Watanzania na serikali yao hawajali jambo fulani linapatikana kwa njia gani ilimradi tu lina tija katika kutatua matatizo yao. Ni nchi ambayo kama kweli una elimu yako nzuri na ya juu kama vile Dr. Msabaha alivyofanya kwenye skandali ya Richmond, lazima uachane na kile unachokiamini ndio sahihi na ufuate matakwa ya utawala. Labda nieleze ni kwanini watanzania na serikali yao hawakuona haja ya kusikiliza busara za kisomi:

Moja, ziara hii imetoa msaada mkubwa kwa nchi yetu katika sekta ya afya na miundombinu. Japo nina mashaka na mafisadi hawataziacha salama, ila ni kielelezo kuwa Bush ana nia njema na nchi yetu. Na katika kutia shime vita dhidi ya ufisadi, Bush alisema baada ya kusaini mkataba kuwa fedha za Marekani si kwa mafisadi. Na kusisitiza kuwa moja ya masharti ya Mfuko wa Millenia ni serikali yetu kuzingatia “Utawala Bora”, vita dhidi ya ufisadi na kwa ujumla serikali inayojali watu wake.

Pili, ziara hii imeonesha ni jinsi gani Raisi Bush na mkewe walivyo watu wa kujitolea (compassionate)hata huruma ya kujali watu wa kawaida. Kwa viongozi wetu wamejifunza ni jinsi gani wanapaswa kuishi na kujichanganya na watu hohehahe kama walivyo watanzania wengi. Viongozi wetu wengi wa Afrika, kwa mfano, si rahisi mtu atembelee hospitali na umwone akikumbatiana na kukaa karibu kabisa kwa kujichanganya na wagonjwa. Hili Bush katoa funzo; nilitegemea kule hospitali ya Mount Meru nione makachero wakiwa karibu na Raisi wakimwongoza wapi apite na ashikane na nani mkono au hata kuwazuia watu wasimkaribie bwana mkubwa. Hili sikuliona ila niliona Raisi Bush akijiweka sawa na binadamu wengine na kukaa hata karibu nao kabisa, wala si kwenye kiti maalum bali viti vya kawaida wanavyokalia wagonjwa kwenye foleni. Wakubwa wetu watataka sofa maalum tofauti na walalahoi.

Kimavazi pia imekuwa ni funzo kwa viongozi na vigogo wetu. Unakwenda kuwatembelea watu masikini ni lazima angalau ufanane nao. Kwa Bush hili alilizingatia hasa na wala sikuona akiwa ndani ya suti, siku ile yenye joto ambalo lingemfanya achemke kwa joto na aogope kujichanganya. Nadhani ndio maana kulikuwa hamna haja ya wanausalama kumzuia kuwa karibu na watu kwani vigogo wetu inabidi makachero kuzuia watu ili bwana mkubwa apate hewa kwani mara nyingi unakuta watu wamevaa misuti. Hapa katukumbusha mavazi rahisi (simplistic). Hili nalo ni funzo gumu kwa vigogo wa kiafrika kulimeza.

Wakati akiitembelea shule ya sekondari maalum kwa wasichana wa kimasai kutoka mazingira magumu alinigusa hasa. Labda niseme mwaka jana Raisi Jakaya Kikwete alifungua shule moja ya sekondari kule Moshi. Ilikuwa ni ziara ya saa moja kufungua shule rasmi; na mara alipowasili pale shuleni si walimu wala wanafunzi waliopata muda wa kumfariji na kumpokea rais wao. Kilichotokea nilishangaa kuona makada kibao wa CCM pamoja na vigogo wa serikali kutoka mkoani na wilaya za jirani wakihangaika kugombania kujipanga mstari ili tu kushikana mkono na bwana mkubwa. Walimu waliokuwa wamejipanga sehemu maalum walifunikwa na wala hawakuweza kupata nafasi hiyo. Wala raisi hakuwa na muda wa kusalimiana ama kuzungumza sana na wanafunzi zaidi ya kupiga kejeli za kisiasa katika hotuba yake. Nadhani angeteta na wanafunzi kadhaa na kusikia hisia zao ingependeza zaidi.

Lakini kwa Bush tumeoneshwa nini maana ya kuwa kiongozi na nini cha kujali wakati unapotembelea sehemu. Raisi Bush alisalimiana na watoto wote wa shule ile pale Arusha; pia alisalimiana na hata kucheza ngoma na wamasai waliokuwa wakiburudisha ikiwa ni pamoja na kuwakumbatia baadhi yao. Hapa kwetu na Afrika kwa ujumla sivyo inavyokuwa, wanausalama hawaruhusu hili kabisa. Hivi huwa najiuliza kila Rais wetu anapokuwa mahali utaona mlinzi wake/ msaidizi wake kasimama nyuma. Hivi hiyo ndio kumaanisha ulinzi wa rais ni imara? Mbona watu kama akina Bush si hivyo na ulinzi ni imara? Nadhani ziara hii iwe mwanzo wa kuiga jambo kwa wanausalama na kwa ujumla wale watu wa karibu wa bwana mkubwa.

Labda niungane na waziri Dr. Jumanne Maghembe aliponukuliwa na ITV katika ziara ya Bush kule Arusha: “Marekani ni Taifa kubwa na tajiri na lina fursa nyingi. Ni vizuri tukashirikiana nayo na kudumisha urafiki na udugu na Taifa hili”. Nikiwarudia wale walionesha kutokutaka ziara hii: Hasa wasomi wa Mlimani, wajameni hivi tunajua kuwa wahenga waliwahi kusema kwa kiingereza tafsiri isiyo rasmi: “Every black has its white”, kuwa kila cheusi kina weupe wake pia”. Hapa namaanisha pamoja na uovu na unyama unaoambatanishwa na haiba ya Raisi George Bush, huyu ni mwanadamu mwenye pande mbili. Na kwa kutilia mkazo kwenu mabaya yake naamini mlighafilika tu; na mashiko ya kihisia yalitawala zaidi ya busara, mbona hamkutizama upande wa pili wa Bush?. La sivyo wala msingefikia hatua hiyo ya kutaka kuandamana.

Ziara ya Bush imetuonesha upande wa pili Bush mwanadamu. Mpaka kaondoka sijasikia akiongelea habari za Africom kama wasomi wetu walivyokazia kuwa anatafuta mahali pa kujenga kambi za kijeshi. Pia nadhani kilio chenu kingine kuwa kumkaribisha Bush ni kuonesha serikali yetu imeamua kuacha marafiki wa zamani na kufuata mabepari kama hatua isiyo muafaka si sahihi. Tumefuata sera za marafiki zetu kama Cuba, China na wengine wengi kwa miongo minne kwa mafanikio sana ya kiuchumi. Dunia ya leo tusiogope sana juu ya hali ya baadaye ila tutumie fursa zinazojitokeza hasa kama zina mwelekeo wa kukuza uchumi wetu.

Tukiwa bado tuna marafiki zetu wa zamani hakuna ubaya kama tunaongeza mwingine bila kuwapoteza wa zamani. Hii ndio hisia ninayoipata kwa ugeni wa Bush. Ziara hii kupitia mkataba wa Millenium Challenge naamini ni fursa ambayo tusingepaswa tuiache kwani ina tija sana hasa kama “mafisadi” watadhibitiwa wasiweke pua zao hapa. Tukumbuke hata jirani yetu Yoweri Museveni alikuwa na uswahiba na Bush na hata enzi za Clinton na kwa sasa wamemtupa kiana na kwa kipindi chote Uganda haikuwahi kuathiriwa kijeshi na Marekani ingawa kwa sasa kuna makampuni kibao ya Marekani yakianza kuchimba mafuta nchini humo.

Funzo lingine la ziara ya Bush kwangu ni pale kung’amua kuwa kweli nchi yetu ni masikini sana. Yaani bado hatuna uwezo wa kujikinga na Malaria? Yaani Bush anatununulia chandarua watanzania? Yaani watanzania walio wengi hawana uwezo wa kununua chandarua? Kwa maana nyingine watanzania wengi tu wachafu hatuwezi kuishi kwenye mazingira safi yasiyoruhusu mbu kuzaliana. Hatujui wajibu wa kiafya kusafisha mazingira yetu ili kuondoa mazalia ya mbu. Ni aibu lakini tufanyeje? Mpaka aje Bush atununulie chandarua. Hili linanipa shida sana kwani nadhani fedha ya malaria ni nyingi na ingefaa itumike kwenye sekta kama ya elimu. Sidhani kama unamzuia mtu asiugue malaria lakini hapo hapo humpi elimu bora kama unamsaidia sana. Bado umasikini hautoki kwa njia hii.

Ukimwi pia ingawa ni janga ambalo binafsi limeniathiri sana; ila ni wakati tujiulize kuwa hivi kama tukiweza kujihadhari na maambukizi, hizi fedha zote za Bush si zingefanya mambo mengine? Napata mashaka sana kama tunaendelea kupata ufadhili hasa wa kurefusha maisha na kwa wakati huo huo hatuna utaratibu wa kuwalinda wale ambao hawajaambukizwa ambao kwa kujichanganya kwao na waathirika wengi ni hatari.Ni wazi waathirika Fulani wana hasira sana na lengo lao kubwa ni kuondoka na wengine. Sisemi hili kwa kunyanyapaa ila ni lazima tufike mahali tujiulize hii misaada mikubwa ya kulinda maisha ya waathirika ina matokeo mazuri? Ni kwa vipi tuifanye tuwe na mazingira mapya kiutaratibu wa maisha ili tupate tija. La sivyo Taifa zima litaangamia na mamilioni ya dola za Bush.

Mwisho, nimalizie kama nilivyoanza: wakati nikiwa pale pembeni ya jeneza la bibi yangu baada tu ya kunong’onezwa na ndugu yangu kuwa Waziri Mkuu kajiuzulu, mara moja nilichoropoka nikaingia ndani nikafungua kiredio changu kidogo, radio sauti ya Ujerumani na nikakutana na sauti yake ikisema: Nimefadhaishwa, nimesononeshwa, …..mengine nimeyasahau manake yalinishangaza kwanini sasa kaamua kujiuzulu. Taifa linapotekwa nyara na mafisadi mtu hushangai pale hata busara za wasomi kama wale wa pale Mlimani zinapoonekana ni kejeli.

Nilisikitika tu pale jeshi la polisi lilipokataa kiaina kutoa ulinzi kwa maandamano ya wasomi wa mlimani kupinga ziara ya Bush. Ingawa sikuwa naunga mkono hoja zao, nadhani walinyimwa haki yao ya msingi kuandamana kupinga ujio wa Bush. Kweli February sitaisahau kama wakati muafaka wa mapinduzi ambayo sina imani sana kama yatabadilisha mwelekeo wa Taifa letu dhidi ya ufisadi. Hii ni nchi inaathiriwa na tabia na hulka ya kubebana, kupendeleana na utapeli wa kila aina. Na ndio maana baada ya Raisi kukabidhiwa ripoti ya Ernst & Young iliyokwishagundua kila ufisadi ndani ya BoT bado anaunda kamati nyingine ya uchunguzi. Lengo ni kulindana tu. Nimeshangazwa pia na mtuhumiwa mmojawapo wa ufisadi karudi kwa wapiga kura wake na kupokewa kwa shangwe na hata kupewa baraka za Askofu wa kanisa lake. Kweli kwa Tanzania ya leo bila ufisadi labda maisha ya wengi yatasimama.

Wednesday, January 30, 2008

KIIZA BESIGYE NA MWAKA 2008

Kiiza Besyige anajulikana sana Uganda. Leo bado ni mwiba mkubwa kwa jeshi la uganda na anadai analijua wazi. Hivi tunajua ilimbidi amwache rafiki wake wa kike ili kujiunga na Museveni msituni na kuacha fani ya udaktari?
Kama unataka kujua madhara ya kupingana na Museveni, basi ona haya yaliyowakumba hawa waliojaribu.

MLIMA KILIMANJARO



Hii ndio Moshi, unauona mlima Kilimanjaro? Wanadai eti karibu theluji yake itakwisha. Ndivyo unavyoonekana leo hii.

Saturday, January 26, 2008

NIKIWA NGORONGORO NASHINO PAKI



Hapa nimesimama katika lango kuu la kuingilia Mbuga ya Ngorongoro.Mara nyingine hata mie natembea kidogo kama akina Majjid.Ilikuwa novemba mwaka jana.

NIKIWA SERENGETI

Hapa niko na wanafunzi wa BENDEL SECONDARY, huko mbuga za Serengeti november mwaka jana katika ziara ya mafunzo.

Friday, January 25, 2008

ODM INAWEZEKANA WAMEPOTEA NJIA KUANDAMANA

Raila Odinga na vigogo wenzake wa chama cha upinzani wamejaribu wiki iliyopita kuitisha maandamano mfulilizo katika juhudi za kutaka kumng’oa madarakani Raisi anayesemekana hakuchaguliwa kihalali—Mwai Emilio Stanley Kibaki. Muungano wa harakati za chama cha Chungwa (ODM) unajaribu kuiga yale maandamano ya wafuasi wa harakati za Chungwa kule Ukraine mwaka 2004 ambayo yalifanikiwa kuiondoa serikali batili madarakani baada ya kuiba kura.

Pamoja na juhudi hizi bado haionekani kama itawezekana kwani nadhani kuna sababu za msingi ambazo kwa wanaharakati hata wa hapa nchini hatuna budi tuzing’amue:

Kwanza kabisa, ODM inakosa kuungwa mkono katika maandamano na tabaka la juu pamoja na lile la kati. Hawa ni wale watu wanaojihusisha na biashara kubwa na za kati pamoja na wengine wengi ambao ni wafanyakazi katika serikali (Civil Servants) pamoja na sekta binafsi. Hawa ni watu wanaojiweza ambao kimtizamo wanaunga mkono ODM lakini kivitendo haiwezekani kabisa hata siku moja kujitokeza mitaani na kushiriki maandamano mitaani. Sana sana wanachofanya ni kuchanga fedha kuunga mkono waandamanaji kwa chakula, vinywaji na hata matibabu kwa wale wanaoumia. Wanafanya hivi kwani wanalinda mali na hata ajira zao nono zisipotee pale watakapogundulika wanaunga mkono upinzani.

Pili, ni raia masikini waishio kwenye mitaa ya mabanda (slums): Tofauti na tabaka la kati na matajiri, wakazi wa mitaa ya mabanda (slums) ambao ni masikini kila kukicha; hawana cha kupoteza ila wanabaki wakiamini labda ODM ikichukua madaraka wanaweza kubadili hali zao za maisha kitu ambacho ni vigumu kubashiri kama kitatokea. Tabaka hili la raia ndio wanaoandamana kila kukicha katika nchi nyingi za Afrika zilizojaa udikteta wa kila aina. Masikini ni vijana ambao wengi wao hawana elimu bora; wengine miongoni mwao wana elimu lakini kwasababu hawana ndugu (God fathers) ndani ya serikali ama hata ndani ya sekta binafsi basi ajira kwao ni ndoto.

Wamechanganyikiwa na kila ahadi kwao ni lazima waiamini hasa inapotolewa na wanasiasa mbadala kama Raila Amolo Odinga. Hili ni kundi kubwa katika miji ya Kenya kama Nairobi, Eldoret, Kisumu na Mombasa. Inakadiriwa ni nusu ya wakazi wa miji hii; lakini zaidi ya robo iliyobakia ni tabaka la kati na la juu na hawapo tayari kuhatarisha maisha yao kuingia mitaani kuunga mkono maandamano dhidi ya serikali batili. Wanachofanya hawa wanaojiweza ingawa hawaridhiki na serikali batili ni kukaa majumbani mwao wakiangalia runinga zao ni jinsi gani polisi wanavyopambana na waandamanaji; pia ni hawa wanaoandika sana barua kwa wahariri wa magazeti na hata kupiga simu redioni kushutumu serikali batili. Kamwe hawatashiriki maandamano au hatua yeyote ya harakati kivitendo ndani ya uwanja wa mapambano. Na ndio hapa Kibaki inawezekana kabisa akawa Raisi hadi miaka mingine mitano.

Kama tabaka la kati na la juu lingeshiriki maandamano haya basi ndani ya siku tatu polisi wa Kenya wasingeweza kuzuia waandamanaji kwani wangekuwa wengi sana hasa ukizingatia muundo wa miji ulivyo. Ila kwasababu maandamano yanatarajiwa yaanzishwe na masikini wa mitaa ya mabanda; na kwa mipango miji ilivyo, mitaa ya mabanda iko mbali na miji ama katikati ya miji (central business street) basi inakuwa ni rahisi kwa askari kwenda huko nje ya jiji na kuwazuia kuingia mijini. Wanafanya haya wakati wamewaacha matajiri na watu wa tabaka la kati wakiwa wamejifungia ndani ya nyumba zao zilizo mijini. Ni wazi kama watu wote wa tabaka zote wangejitokeza basi polisi watapata shida sana kuwazuia kwani itakuwa vigumu ukizingati kila kona ya jiji itabidi iwekewe ulinzi kitu ambacho si rahisi kwa askari kuhimili wingi wa watu kutoka kila upande.

Ingawa polisi wanaweza kuamua kuua kwa risasi za moto lakini kama watu wote niliotaja wataingia mitaani si rahisi kwa serikali ya Kibaki kuamrisha polisi kuua (shoot to kill) manake shinikizo la jumuiya ya kimataifa halitawaacha salama. Na ndio maana hadi sasa siku ya pili ya maandamano, silaha kuu ya polisi imekuwa ni maji yenye presha kali (water canon) katika kupambana na waandamanaji. Pia serikali haitakuwa na utashi na thubutu ya kuua wafanyakazi (Civil Servants) wake yenyewe ambao wengi wao ni kundi la tabaka la kati.

Kinachokwaza harakati ni kuwa tabaka la kati (middle class) hawana mwamko na uthubutu wa kushiriki maandamano wala harakati za mapinduzi moja kwa moja. Hawako tayari kupoteza kazi zao zenye malipo mazuri, mali zao kama nyumba zingine labda wamekopeshwa na serikali; pia la msingi kwao laweza kuwa ni wasiwasi kuwapoteza wapendwa wao: waume na wake zao wazuri pamoja na watoto wao wenye afya nzuri.

JE MAPINDUZI YATOKEE WAPI?

Naamini kama kweli ODM itafanikiwa basi ni kutokana na jitihada za masikini wa kutupwa (makabwela) ambao hawana cha kupoteza kama vile vibanda vyao vilivyojengwa kwa maboksi pamoja na wake zao wasiotamanisha na hata watoto wao wengi wao wenye utapiamlo. Inawezekana hatimaye wakafanikiwa; ila kama Raila atafanikiwa kumlazimisha Kibaki ampishe basi mshangao mkubwa utawakumba walalahoi wanaoandamana leo hii:

Mosi, lile tabaka la kati pamoja na matajiri wachache ambao ni waoga na wamejichimbia ndani sasa hivi wakitizama televisheni zao jinsi makabwela wakipambana na polisi ndio watakuwa wa kwanza kujitokeza na kupangiwa nyadhifa kadhaa na serikali mpya ya Raila kama itatukia. Hii itakuwa ni katika kuthibitisha maneno ya biblia takatifu: “Aliyenacho ataongezewa na asiyenacho atanyang’wanywa kabisa”.

Pili, kama mapinduzi hayatafanikiwa, tabaka la kati (middle class) hawajali sana kwani maisha yao yasiyo na kero nyingi yataendelea kama kawaida tena watajiona kama vile hakuna kilichotokea kwani wataendelea na kazi zao; mishahara yao minono na yenye ongezeko la asilimia 3% hadi 5% kila mwaka. Ni hawa hawa kila jioni baada ya saa za kazi wanajumuika kupata kinywaji wakijadili juu ya mapinduzi ambayo yatakuwa yamefeli.

Tatu, kwa upande wa masikini ambao tunawashuhudia wakipambana na polisi; iwapo harakati zitafeli basi wanajirudia vibandani mwao; maisha ya msoto yataendelea yaani kuamka alfajiri na kurudi majumbani usiku baada ya kazi za kitumwa kama vile: kazi za utarishi, ulinzi, utunzaji bustani za maua na pia kazi za viwandani ambazo zinazalisha asilimia tisini 90% ya uchumi wa nchi ilihali wao wanapata vipato vidogo na vya aibu sana.

Nne, pia ikiwa harakati za ODM zitashindwa basi wakati masikini wanateseka, matajiri pamoja na tabaka la kati wataendelea na maisha bila kujali; kwa kujiweka karibu na wanasiasa batili ambao wamewashinda masikini. Zaidi kila jioni watakutana katika sehemu za starehe kupiga soga na hata kucheza gofu.

Napenda pia tukae chini: lazima tujiulize hadi sasa kwanini ODM haijaweza kufanya maandamano licha ya nia yao ya dhati? Ukichukulia nini kilitokea kule Ukraine kama nilivyotaja awali, basi ni wazi jumuiya ya kimataifa haijaamua kuwaunga mkono. Kule Ukraine, Marekani iliwaunga mkono wanaharakati wa chungwa (Orange Revolution) kifedha kitu ambacho inaonekana Marekani inasita kwani pia haiamini kama kweli ODM ina jipya. Pia kule Ukraine, polisi walitambua kuwa nao pia ni sehemu ya tabaka dhalili dhidi ya ufisadi wa wanasiasa. Ila kwa Kenya na hata nchi nyingi za Afrika si polisi wala askari jeshi ambao wametambua hili: kuwa maisha magumu kwa baadhi yao yanachangiwa na serikali batili wanayoilinda kimabavu.

Kule Ukraine, polisi hawakupambana na waandamanaji hata kidogo kwani walitaka pia mabadiliko. Hapa Afrika hatujafika hatua hiyo na ndio maana nadhani ODM kufanikiwa kuiondoa serikali batili ni vigumu sana ingawa naamini juhudi zao zapaswa kuungwa mkono zaidi.

Tayari kuna tetesi kuwa kama hali ya maandamano itaendelea hivi, basi iko siku wanajeshi watapindua serikali ya kibaki na ndipo itakuwa mwanzo na mwisho wa kadhia hii. Ndio njia pekee ya kuanzisha upya mchakato mzima wa kuiepusha Kenya kuwa Taifa lililofeli (failed state). La sivyo yaliyowahi kutokea Liberia ama Ivory Coast yatatokea hapa. Na ndipo hapo wanasiasa wetu fedhuli na fisadi huku wakilindwa na vyombo vya usalama kwa kodi ya wananchi watang’amua kuwa raia wa kawaida anayo nguvu kubwa kuliko majeshi na bunduki zao.

TANZANIA IMETEKWA NYARA NA CCM

Miezi kadhaa imepita sasa baada ya mwanasaikolojia na mshindi wa nishani ya Nobel kuja na wazo lake kuwa “Waafrika ni dhaifu katika kufikiri ukiwalinganisha na wazungu ama watu wasio weusi”. Si mwingine bali ni daktari James Watson, mtaalam maarufu wa Saikolojia na mgunduzi wa sayansi ya chembe hai ( DNA) nchini Marekani na duniani kwa ujumla. Mawazo yake yalipokewa kwa machungu sana na watu weusi wengi kila kona ya dunia; lakini kwangu nilijaribu kuona hili kama changamoto hasa nikizingati mambo kadha wa kadha yanayotukia hapa nchini mwetu Tanzania na Afrika kwa ujumla.

Naye David Landes kaja na kitabu chake “The Wealth and Poverty of Nations: Why Some are so Rich and Some are So Poor”, akijaribu kutuonesha kwanini waafrika wako nyuma ya wazungu kiuchumi. Tatizo ni utamaduni anadai kwani anasema wazi utamaduni wa mwafrika ni dhaifu ama ni wa kiwango cha chini sana ukiulinganisha na ule wa wazungu. Kwa mfano anadai utamaduni wa mwafrika unakosa vikolezo kama kufanya kazi kwa bidii (hard working), uaminifu (honest), uwazi (open mindedness), na utashi wa dhati katika demokrasia (commitment to democracy)

Landes anasisitiza pia maendeleo ya kiuchumi yanategemea sana hisia (attitudes) za wananchi wake hasa uwezo wao katika kutumia au kutokutumia sayansi na teknolojia na hata fursa za kiuchumi pindi zinapojitokeza. Ni wazi utamaduni una nafasi kubwa sana katika kuendelea ama kutoendelea kwa jamii Fulani. Kwa mfano, Wajapan wanaamini kuwa utamaduni wao ndio chanzo cha mafanikio yao tunayoyaona leo hii. Yoshihara Kunio, kwa mfano ameandika kuwa: “Sababu moja kuendelea kwa Japan ni kuwa ina utamaduni wa maendeleo”. Wajapan wameweka msisitizo katika utafutaji mali (material pursuit), kufanya kazi kwa bidii, kuweka akiba ya siku zijazo( serving for future), kuwekeza katika elimu na kujali jamii (community value).

Tukirejea kwa Landes, anatuonya kuwa kuna tamaduni fulani ambazo ni sumu na mtu akiziamini na kuziishi basi ni umasikini. Kwa mfano, utamaduni wa wazungu/ magharibi ni wa ubinafsi (individualistic) zaidi wakati ule wa kiafrika ni wa kijamii zaidi ama tunaweza kusema kiasili ni utamaduni wa kijamaa unaojali wengi katika migawanyiko ya aina mbalimbali hasa kikabila. Ni katika msingi huu naweza kusema kuwa nadhani ni wazi utamaduni wetu hasa watanzania ni wa kijamii ambao leo hii umehama kutoka ukabila hadi kufikia kikundi cha watu ama jamii kisiasa: namaanisha vyama vya siasa vinavyowakutanisha makabila mbalimbali yenye maslahi yao ikiwa ni pamoja na kuing’ata nchi yetu bila huruma.

Kwa mfano, watanzania na waafrika kwa ujumla wao wamekuwa wakiamini ni lazima watumikie maslahi ya makabila yao. Hali si Kenya tu ila hata hapa kwetu mambo ni hayo tu. Katika kutumikia maslahi ya kikabila ndipo kwa mfano watanzania tunajikuta tukijirudisha nyuma sana kimaendeleo. Utamaduni huu mara nyingi hauruhusu kukosoana hasa pale viongozi ama wakuu wa kaya ama makabila mbalimbali wanapokiuka taratibu za kijamii. Kwa kawaida, wakuu wa familia ama jamii za kiafrika mara nyingi hawaadhibiwi; hakuna mfumo wa udhibiti kwao. Hawa ni sawa na miungu watu wanaotenda visivyo bila kuadhibiwa (impunity).

Maadam waafrika na watanzania tuna kasumba ya kutumikia jamii ama makabila yetu zaidi, basi leo hii tabia hii imejipenyeza hadi katika sehemu za kazi. Angalia hata siasa zetu sasa zimegeuka kuwa ni watu ndani ya vyama mbalimbali kama kikundi kwa maslahi yao na wala si maslahi ya pamoja (common interests) kama ilivyo Japan. Ni katika hili ambapo suala “uzalendo” limekufa na sasa ni maslahi ya kivikundi. Kwa mfano, unaposikia Taifa linakumbwa na upotevu wa fedha nyingi alafu serikali kuanzia Raisi hadi mawaziri wanashindwa kuweka mambo wazi juu ya wapi Gavana Ballali anakotibiwa, basi mtu unapata picha ni jinsi gani serikali ya CCM haiko tayari kuwa wazi kwa suala hili.

Hii yote ni kuonesha jinsi gani utamaduni wa kutoadhibu ama kutowajibisha wakuu wa kaya ama makabila ya kiafrika unavyoitafuna nchi yetu. Ni utamaduni wa karne kadhaa zilizopita ambao CCM inahakikisha utadumishwa ili watu fulani waitafune nchi yetu kwa maslahi yao na chama chao. Ukienda Bungeni na jinsi ambavyo hadi leo hii tangu kashfa ya BOT iibuliwe hakuna mbunge wa CCM aliyethubutu kusema jambo kuonesha kukerwa na hili. Nasubiri nione jinsi watakavyojiuma huko bungeni kuanzia wiki ijayo watakapokuwa wanachambua uchunguzi wa ripoti ya uchunguzi wa kashfa ya Richmond.

Tuna tatizo kubwa kitaifa: yaani mentalite (fikra) za viongozi wengi wa Tanzania ni mzigo mkubwa kwa Taifa. Kizazi cha uongozi cha sasa ni balaa kubwa sana kwa taifa hili kwani hawana tofauti sana na mababu zetu zamani enzi za ukoloni ambao hawakujua kufikiri kwa dhati. Naamini kama Rais Kikwete atatawala kwa miaka kumi basi utakuwa ndio mwisho wa mawazo mgando. Siku za kizazi cha mawazo mgando zinahesabika; kizazi kipya cha sasa chenye mawazo ya kisasa ya kuivusha nchi kutoka umasikini kinakuja taratibu. Ni kizazi ambacho kinawaza zaidi “utaifa” na si maslahi binafsi kama akina Balali na wenzake ambao wanajifanya wametengua uteuzi wake ilihali wengi wao ndio chanzo cha madudu aliyoyafanya.

Ninasema haya kwani hata yaliyotukia Kenya situ ni ukabila bali ni utamaduni huu wa watu katika vikundi vyao vya kikabila na kisiasa wanang’ang’ania madaraka ili kulinda maslahi yao. Chunguza kashfa kubwa kama Goldernberg alafu kama unalijua kundi la “ Mount Kenyan Mafians” ujiulize kwanini Kibaki anang’ang’ania madaraka? Ni hii tabia ya makundi fulani ya viongozi wetu ambao wataiibia nchi huku wakilindwa na wabunge wa chama chao dhidi ya ufisadi wao; kwani kwao bunge ni muhuri (rubber stump) wa kupitisha uchafu wao kwa maslahi yao. Ni tabia kama hii naiona ndani ya CCM ambapo ‘kupitia wingi wa wabunge wao ni wazi Tanzania imetekwa nyara na CCM’.

Kama kweli CCM kingekuwa ni chama cha kuiendeleza nchi yetu basi leo hii hizi kashfa za BOT, Richmond, Buzwagi zisingechukua muda na kutumia muda mrefu bila wahusika kuchukuliwa hatua za kuwajibishwa namna tuonavyo leo. Chama chochote kinapokubali kutumika kama muhuri wa kupitisha wizi na utapeli wa baadhi ya watawala basi ujue ni kwa ajili ya utamaduni mbovu wa kiafrika umekimeza.

Na kwa maana nyingine ni kuwa uwezo wa kufikiri wa wengi walioshikilia hatamu za chama hicho ni mdogo kama alivyosema daktari Watson anavyomwona mwafrika. Jamii kama hii haishangazi hata kidogo sera za kishikaji zinawekwa mbele sana; na jamii hii kufikia maendeleo ya kweli ni vigumu sana ukiacha maendeleo ya wachache wenye mashiko ya kikabila, dini, rangi na kisiasa hasa ukada wa chama. Ni kwa msingi huu naiona Tanzania, nchi yangu kama Taifa lililotekwa nyara na kikundi cha watu Fulani wachache lakini wanaoungwa mkono na watu wenye wajibu wa kuwawajibisha lakini hawataki. Hawa ni wabunge fulani ambao ama kwa makusudi kabisa ama kwa ufinyu wa kufikiri kama ule aliouelezea Dr. Watson basi wanaamua kuhakikisha Mafioso wa Tanzania wanashamiri.

Ni wazi CCM ndio pekee kwa uwingi wa wabunge wao wakiamua wataisafisha nchi yetu na kupambana na mafisadi wa Taifa hili. Mafisadi wengi wa nchi hii ni wanachama wa chama hicho; na ndio hapa pagumu kutegua kitendawili. Mungu wangu: mara nyingine mtu unajuta kuzaliwa katika Taifa lisilopenda kufikirisha bongo ilihali likijiita eti ni Bongo land.

Tuesday, January 15, 2008

MKASA WA BALALI--WASOMI WANAPOCHEZA NGOMA YA WANASIASA

Balali kafukuzwa kazi na Raisi Jakaya Kikwete; ni habari ambayo ilinishangaza manake tayari nilikuwa najua alikuwa ameshaandika barua ya kujiuzulu lakini inasemekana rais akamkatalia. Mimi nilidhani alimkatalia kwa kuwa ni msafi sana; na, hata ile tu kutuhumiwa katika ile listi ya aibu (list of shame) ya mtanzania makini na mzalendo wa hali ya juu, daktari Wilbroad Slaa, kuwa yeye ni kati ya mafisadi wa Taifa letu naamini ilitosha kwa mtu mwenye akili timamu kukaa kando achunguzwe ili asafishwe.

Balali pamoja na vigogo wengine waliziba masikio na kutufanya tumwone Dr Slaa kama vile ni msanii tu. Nchi yetu sasa inadhihirisha kuwa imekumbwa na ugonjwa mbaya sana wa kimaadili. Nakumbuka baadhi ya watuhumiwa wa listi ile ya aibu walitishia kwenda mahakamani lakini hadi leo wamekaa kimya na hata hawajathubutu kujiuzulu angalau. Yaani angalau wangeandika barua angalau basi wakataliwe tujue raisi ana imani na mafisadi.

Leo nataka nizungumzie suala la uwajibikaji; yaani mtu akichafuliwa asiendelee kukalia madaraka bali ajiuzulu ili aruhusu kusafishwa au awapishe wengine ambao wataweza kuendeleza nchi yetu kwa uadilifu. Labda nikumbushie tu hali tete kama hii ambayo ilijitokeza kule Ghana mara tu raisi John Kuffour alipoingia madarakani. Waziri wake mmoja wa mawasiliano na uchukuzi, ndugu Richard Anane, alituhumiwa kufuja fedha chini ya wizara yake. Ilipoundwa tume ya uchunguzi iligundulika ni kweli zaidi ya dola laki moja ziliibwa na mara moja akafukuzwa kazi. Nchini Uganda mawaziri wawili wa afya, Waziri Jim Muhwezi na naibu waziri, Mike Mukula waliamua kung’ang’ania madarakani licha ya tuhuma nzito za ufujaji wa fedha za Global Fund. Ilipoundwa tume baada ya shinikizo la vyombo vya habari, tume ilipendekeza wafunguliwe mashtaka mahakamani. Kesi yao bado inaendelea hadi leo.

Ni wazi kashfa inapoibuliwa kuna ukweli na ni vyema tujenge utaratibu wa kujiuzulu ili kuruhusu uchunguzi. Na kama hatufanyi hivyo ina maana kazi za umma zimegeuzwa kama za kifalme; yaani mtu hadi afe. Sasa yaliyomkuta Balali ndio kuanguka kwa mfalme.

Nimetoa mifano miwili kuonesha jinsi baadhi ya nchi za Afrika zinavyozingatia vita juu ya ufisadi. Hapa kwetu hata pale madai makubwa yanapotolewa bungeni,haindwi hata tume ya bunge na yanabezwa. Bado najiuliza ni kwanini tufanye uchunguzi kwa kutegemea kampuni za nje ilihali kamati ya bunge ama ya raisi ingeweza pia kuchunguza hili? Nina mashaka sana kama kweli jeshi la polisi, mwanasheria mkuu na hata Takukuru kama kweli wana utashi wa kimaadili (moral authority) kuweza kuchukua hatua kwa wahusika wa dhahama hili. Watanzania hatuna utamaduni wa kuwashughulikia watu wazito hasa wenye fedha na vigogo serikalini. Huu ni ugonjwa wa kitaifa na ndipo hapa nadhani Balali kaenda na maji kilichobaki baada ya miezi sita sidhani kama tutawajua zaidi waliohusika na sidhani kama kutakuwa na hatua kali zozote. Tanzania imejaa vigogo wasioshikika (untouchables) na sidhani kama tuna watu mashujaa kuwashughulikia mafisadi. Manake kama si utamaduni huu basi tangu wizi huu uanze ungekuta idara nilizozitaja zimeshughulikia lakini wapi.

Mara kwa mara nagusia sana juu ya “utawala bora”: serikali haieshimu sana taasisi zake (institutions) katika utendaji ila tunaamini zaidi katika watu (people). Unafikiri Balali angethubutu kuweka kapuni maadili ya utendaji ya gavana na aamue kuruhusu maamuzi ya watu binafsi yatawale utendaji wa Bot? Ni wazi gavana hawezi kufanya hasara kubwa hivyo kwa nchi kama kweli baadhi ya watu wa ngazi za juu hawashiriki katika maamuzi hayo. Ndio maana tumesikia eti baadhi ya fedha hizo zilitolewa kufanya “malipo nyeti”.

Serikali zetu za kiafrika zinaegemea zaidi katika utashi ama uswahiba unaozingatia mashiko ya kisiasa; yaani watendaji wetu pamoja na taaluma zao lakini wanacheza ngoma za wanasiasa. (pandering to the whims of politicians). Hii kwa kiasi kikubwa inasababishwa na mhimili mmoja wa serikali umekufa. Bunge letu, niliwahi kusema inawezekana kabisa ni Jumba la Sanaa la Taifa (National Theatre). Manake tukumbuke wakati madai haya yalitolewa bungeni yalibezwa sana kitu kilichowafanya wapinzani waamue kupeleka hasira zao kwa wananchi katika mikutano ya hadhara.

Bunge letu limedumaa na ndio maana watu kama akina Balali wanajifanyia watakavyo wakishurutishwa na wanasiasa kwani wanajua Bungeni hakuna mtu hajali kuhoji. Kama Bunge letu lingekuwa la nguvu na la viwango kama tulivyodanganywa wakati linazinduliwa Balali na mafisadi wenzake ungekuta wameshashughulikiwa siku nyingi sana. Ila jamii yenye bunge dhaifu (feeble parliament) wabunge walio wengi (majority) wataitetea serikali hata kwenye maovu. Mfumo mbovu wa bunge unamfanya mbunge wa chama tawala kuogopa kutengwa pindi atakapokwenda kinyume na maslahi ya chama chake pale yanapokinzana na utashi wake (conscience). Bunge halina sheria za kumlinda katika kuihoji serikali na kwa maana hiyo wabunge wengi wa chama tawala wanalazimika kuziasi akili zao na kunyamaza ama kuongea pumba pale hoja nzito kama ya Bot ilipoletwa bungeni.

Kucheza ngoma ya wanasiasa unakwenda mbali zaidi ya bungeni hadi katika taasisi mbalimbali za serikali. Naamini kabisa wakubwa wengi wa ngazi mbalimbali za serikali hawana uwezo wa kuzuia wimbi la kutumiwa (manipulation), kufanya maamuzi chini ya vitisho (threats) pamoja na mashinikizo au mibinyo (pressure) mbalimbali. Ni katika mtizamo huu ndio maana nakuwa na mashaka kama kweli polisi ama ofisi ya mwanasheria mkuu ina ubavu wa kuwashughulikia mafisadi.

Tunahitaji kuimarisha taasisi ya Bunge (legislature) ili kashfa kubwa kama hizi za ufisadi zisipigwe danadana kama ilivyokuwa kwa skandali hili la Bot. Ninaamini kabisa kama Bunge lingekuwa la viwango wala tusingefika leo; siku nyingi wahusika wangeadabishwa. Namaliza kwa kumsikitikia gavana Balali kwani sasa imethibitika kumbe yeye ni fisadi haswa; lakini nataka nihoji wasomaji: kuna tetesi kuwa jamaa haumwi, eti kazamia ughaibuni kama mkakati maalum wa mafisadi kupambana na skandali hili. Je kama ni kweli tutawashinda mafisadi?

Mwisho, ni wazi huu ndio mwanzo wa ukweli wa aliyokuwa akiyasema mheshimiwa Dr. Slaa. Hili la Bot limedhihiri; lakini maswali bila majibu vipi mafisadi wengine waliobakia katika ile listi ya aibu? Nasikitika hata mkuu wa nchi alitajwa. Kweli maneno ya meseji ya simu ya rafiki yangu juu ya kunijulisha Balali katimuliwa yana kila sababu ya kuaminiwa; aliandika hivi: “Jk amecharuka!Hapo kuna wengi wataguswa, ila sijui kama sheria itafanya kazi yake maana hilo ndio muhimu. Kwa jamii yenye taasisi zisizo huru (independent) sina mategemeo sana kama sheria itafuata mkondo kwa skandali hili.

Nabakia nikiamini inawezekana lakini tusipoona “mapapa” wakishughulikiwa kwa hili bali “kambale” sitashangaa kabisa. Demokrasia yetu bado hairuhusu kufika huko labda tuamue kwa dhati kabisa kubadilika. Na si kizazi hiki cha akina JK na wenzake. Nina wasiwasi sana kama kuna utashi wa kutosha kukabili hili. Eti kumbe Balali na wenzake ndani ya serikali wametuibia kiasi cha fedha kinachotosha kujenga shule za sekondari 1000? Jamani kumbe Tanzania inang’atwa haswa na mafisadi.

Monday, January 07, 2008

UTATA WA KENYA

Chanzo cha machafuko Kenya ni hiki;machafuko haya yanafananishwa na hali ya Pakistan. Pia Yesu kristu kagusiwa juu ya utata wa Kenya. Kutokuwa na machafuko haina maana eti kuna amani kama tunavodhani. Unajua madaraka yanapendwa sana na vigogo ila pia hata masikini imedhihirika Kenya.

Lakini Kibaki alisahau amani bila haki haiwezekani. Lazima tukubali demokrasia ni gharama.

Tunamwonea Kibaki, tatizo ni Kivuitu

SAMUEL Kivuitu, Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Kenya (ECK) ndiye chanzo cha machafuko yaliyojitokeza nchini Kenya baada ya kumtangaza Mwai Emilio Kibaki kuwa mshindi katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika mwishoni mwa mwaka jana, huku hana uhakika iwapo Kibaki alikuwa ameshinda kweli au la.

Baada ya kumtangaza kuwa mshindi, Kibaki aliapishwa chapuchapu kuwa Rais wa Kenya katika kipindi kingine cha miaka mitano ijayo.

Nilifuatilia matangazo ya moja kwa moja ya radio na televisheni, tangu uchaguzi hadi siku ya kutangazwa mshindi; mwenendo mzima wa uchaguzi huo ulithibitisha kuwepo dalili za matokeo ya kura za urais kuchezewa yalipofika katika ofisi ya Kivuitu kutoka vituoni.

Kabla hajatangaza matokeo hayo, Kivuitu alionekana kuwalaumu maofisa wasimamizi wa baadhi ya vituo vya uchaguzi kwa kuchelewesha kuleta matokeo.

Hii ilikuwa dalili ya kwanza ya kuwepo kwa mchezo mchafu, na hata alipofika mbele ya waandishi wa habari kutangaza mshindi, siku ya Jumapili iliyopita, alianza kutaja matokeo ya vituo vilivyochelewa na alipofikia kituo cha Molo, alisoma kura za Kibaki akitaja namba ya juu zaidi ya kura alizopata.

Kwa ushujaa kabisa, William Ruto, mmoja wa viongozi wa ODM, alisimama akihoji hesabu ya kura hizo, alimtaka ofisa aliyesimamia na kusaini fomu ya matokeo (form 16A) aliyekuwepo eneo hilo, athibitishe kama kilichokuwa kikisemwa na Kivuitu mbele ya hadhara ni kweli.

Lakini kwa bahati mbaya, katika kile kinachoweza kutafsiriwa kuwa kunyongwa kwa demokrasia, maofisa usalama walimdaka Ruto haraka haraka, wakamwondoa na kumpeleka ndani huku wakiacha zogo ndani ya ukumbi, matokeo yalipokuwa yakitangazwa.

Wakati nashuhudia zogo hilo likiendelea, mara Kivuitu alionekana katika kituo cha taifa cha televisheni akitangaza matokeo ya jumla ya kura za urais na kubatiza ushindi wa Kibaki na baadaye kidogo, redio na televisheni zikawa zikitangaza tukio la kuapishwa kwake Ikulu. Ilikuwa ni kama sinema vile, na nilijikuta nikiifurahia kwa kicheko maana yake muandaaji wake alifanikiwa sana.

Mara moja mawazo yalinijia na nikamkumbuka dikteta wa zamani wa Urusi: Joseph Stalin. Alijulikana kama bingwa wa mizengwe ya kisiasa. Aliwahi kusema kuwa: “Not the voters decide the winner in an election, but those who counts votes will decide everything.” Alikuwa akimaanisha kuwa katika uchaguzi, mshindi apangwi na wapiga kura, bali wale wanaohesabu kura.

Binafsi huwa sipigi kura katika chaguzi zetu kwa sababu naamini ni sawa na kupoteza muda na kuchafua kidole changu wakati mtu huwa tayari keshachaguliwa.

Mambo yanayotokea Kenya hayakuanzia hapo na wala si mageni barani Afrika. Mambo kama hayo yameshawahi kutokea katika nchi nyingi, tuna mfano mzuri kwetu sisi, ni yale yaliyowahi kutokea Zanzibar katika chaguzi kuanzia mwaka 1995.

Kwani tatizo hapa ni mgombea mmojawapo kutotakiwa na wanaoamini wao ni wazalendo zaidi ya wengine.

Hawa wamejipa kazi ya kuwachagulia wenzao viongozi. Kwao si kila mtu anayechagulika ni kiongozi, hivyo huamua kulifanya zoezi la uchaguzi kama kupoteza muda na fedha.

Kwa uchaguzi wa Kenya, Kivuitu ndiye tatizo baada ya kutangaza matokeo yenye hila na shaka. Alitangaza matokeo yaliyopikwa katika ofisi za makao makuu ya ECK. Baadhi ya makamishna wenzake walianza kuthibitisha hilo na hata yeye mwenyewe, alipoona maji yamefika shingoni aliibuka na kuthibitisha.

Kivuitu kama alivyokiri mwenyewe, ana dhambi dhidi ya wananchi wa Kenya: Mosi, wiki hii amenukuliwa na gazeti la The Standard, akidai hana hakika ni mgombea yupi alishinda urais. Inashangaza! Ilikuwaje akatangaza ni Kibaki?

Pili, ameamsha hasira ya wananchi kwa kudhani kwamba uelewa wake ni mkubwa kuliko wa Wakenya wote juu ya haki yao kikatiba ya kuchagua na kuchaguliwa.

Hasira za Wakenya zilizosababishwa na Kivuitu ambaye naamini kabisa kuwa aliyafanya hayo aliyoyafanya akijua madhara yake na matokeo yake, ndiyo mauaji kama yanavyoripotiwa katika vyombo vya habari kwa wiki yote iliyopita.

Dhambi ya tatu ya Kivuitu ni kushindwa kutenda kazi inavyopaswa; kwa uaminifu na kwa wakati muafaka. Dhambi hii inamfanya achorwe kama mhusika mbaya (sad character) katika sinema hii ya uchaguzi wa Kenya.

Wiki hii kawaeleza waandishi wa habari kuwa, eti alitaka kujiuzulu lakini akaona si muafaka kwa vile angeonekana mwoga (coward).

Kivuitu ameyatamka haya bila kujua yanadhihirisha jinsi asivyokuwa mzalendo wa kweli kwa kukubali taasisi anayoiongoza kuruhusu mapinduzi yasiyo halali nchini Kenya.

Huo ndio ukweli kwa sababu baada ya kuapishwa Kibaki, ilitolewa amri kuwa redio na televisheni ziache kurusha matangazo ya moja kwa moja. Udhibiti wa vyombo vya habari, hasa vya elektroniki, ni moja ya sifa za wapinduaji wa serikali. Mara wanapokamata madaraka, au wakiwa katika hatua za mwisho mwisho kufanikisha kukamata madaraka, wanakimbilia kudhibiti vyombo vya habari.

Amri ya kupiga marufuku vyombo vya habari Kenya ilitolewa na Waziri wa Usalama wa Taifa, John Michuki, akidhihirisha kwa nmna nyingine kuwa naye ni mshiriki katika mapinduzi hayo.

Hili liliwanyima wananchi haki ya kuhabarishwa juu ya kilichokuwa kinatokea na ni wazi hata matumizi makubwa ya nguvu za dola kudhibiti wananchi waliokuwa wanadai haki yao, ni sifa nyingine ya mapinduzi.

Haina ubishi kuwa wanausalama hawakuheshimu matokeo ya uchaguzi, ila waliamua kumuweka mtu wamtakaye atawale. Na kama nionavyo ni sahihi, basi Kibaki atakuwa rais asiye na maamuzi sana kwa vile amewekwa pale na kikundi cha watu wakishirikiana na baadhi ya maofisa wa usalama.

Kivuitu pia kama mwanasheria ambaye anafanya kazi baada ya kuapa, aliamua kwa makusudi kabisa au kwa kulazimishwa kutoheshimu majukumu yake ya kutenda kwa haki.

Hata hivyo, kwa kuangalia rekodi yake ya kusimamia chaguzi mbili: mwaka 2002 na kura ya maoni 2005 kwa ufanisi kabisa, inawezekana kabisa Kivuitu alishinikizwa chini ya mtutu wa bunduki kumtangaza mshindi.

Angalia jinsi alivyotaka kuporwa cheti cha ushindi na watu ambao nia yao ilikuwa ni kuona kuwa Kibaki anaapishwa. Hata alipofika Ikulu kupeleka cheti hicho, alikuta maandalizi ya rais kuapishwa yameshakamilika!

Mwenyewe ametamka kuwa alishinikizwa atangaze mshindi, vinginevyo jukumu hilo lingechukuliwa na mtu mwingine. Kama mazingira haya yalikuwepo ni wazi kuwa maisha yake yalikuwa hatarini na tunaweza kumuelewa, lakini kama hivyo ndivyo kwanini hasemi wazi? Hii nayo ni dhambi, dhambi ya kutokuwa mkweli!

Dhambi nyingine mbaya kabisa inayomuangukia Kivuitu ni chanzo cha machafuko haya kubadilika kutoka kwenye upingaji wa matokeo hadi kwenye mtazamo wa kikabila.

Hisia za watu wengi hivi sasa juu ya sinema hii ya uchaguzi wa Kenya ni kwamba, Raila ni mkabila na hafai kuwa rais. Haya ni madai ya kushangaza kwa sababu ukiiangalia ODM, haijakaa katika mtazamo wa kikabila hata chembe.

Hata ilivyosukwa hasa viongozi wake wakuu (pentagon) ni wa uwakilishi mpana wa jamii mbalimbali za Kenya. Wengine nimeongea nao wanaenda mbali zaidi na kuegemea katika ngano (myth) kuwa ‘Mjaluo hawezi kutawala Kenya hata siku moja.’

Nakubaliana na ngano hizi kwa sababu nimezisikia muda mrefu sasa kwamba Wakikuyu wanawadharau Wajaluo kama watoto wadogo ambao hawajakua kwa sababu tu hawaendi jando!

Hapa unadhihirika ushahidi mwingine kuwa Kibaki na watu wake wanaomzunguka wanaogopa kivuli chao na wana wasiwasi na utawala wa Raila kwamba unaweza kulipa kisasi kwa Wakikuyu ambao wamekuwa wakifanya hila ili wasitawale Kenya.

Katika mazingira kama haya, yapaswa kutafuta jibu zuri kwa swali la nani ni mkabila kati ya Kibaki na kundi lake na Raila?

Jambo la muhimu kuzingatiwa katika utata huu uliosababishwa na Kivuitu ni kwamba, matatizo ya uhesabuji kura sasa yamekuwa mazoea Afrika Mashariki.

Mwaka 1995 kule Zanzibar yalitokea, 2001 na 2006 kule Uganda pia yalitokea. Ni wazi bado tu wachanga sana kwenye suala la utawala bora.

Yaani, taasisi zetu hazifanyi kazi kwa uhuru bali zinamtumikia mtawala (rais). Ni katika msingi huu tatizo la Kenya haliwezi kutatuliwa kwa majadiliano wala kwa kwenda mahakamani.

Haliwezi kutatuliwa mahakamani kwa sababu ni mahakama hiyo hiyo iliyomuapisha Kibaki kupitia kwa Jaji Mkuu, haraka haraka baada tu ya Kivuitu kumtangaza kuwa mshindi.

Hapa napo Jaji Mkuu wa Kenya, Moses Gicheru, naye keshapoteza mamlaka ya kimaadili katika kusimamia kesi yeyote dhidi ya uovu wa Kivuitu.

Itashangaza sana iwapo Raila akiamua kwenda mahakamani kulalamikia ushindi wa Kibaki, halafu mahakama hiyo hiyo, ambayo ndiyo iliyomuapisha Kibaki, iamue kuwa ushindi wa Kibaki ni batili. Lakini hawa wote wameingizwa dhambini na Kivuitu ambaye kama asingekubali kupindua matokeo, hali ya Kenya isingekuwa kama ilivyo sasa. Kama Kivuitu asingekubali kutangaza matokeo kwa shinikizo, angesubiri mpaka uhakiki ukafanyika na kila mmoja akawa na imani na matokeo, wala haya yasingetokea.

Waafrika tunapaswa kuwa makini zaidi sasa na watu wa aina ya Kivuitu ambaye historia yake inaonyesha kuwa hata wakati akisoma Chuo Kikuu cha Dar es Salaam aliwahi kumkorofisha Mwalimu Nyerere hadi akaitwa ikulu.

Utukutu wake wa utotoni ndiyo matokeo ya machafuko yanayoendelea nchini Kenya.

Kwa sababu hizo, kuna kila sababu ya kuchagua watendaji na wasimamizi wa shughuli mbalimbali za kitaifa kwa kuangalia historia zao.

MJUE UNDANI WA JOSEPH KONY

Leo nataka watu wamjue Joseph Kony ni mtu wa aina gani kutoka kwa mtu aliyesoma naye. Pia tujue ili Afrika iendelee, kuna mengi zaidi ya viwanda ya kufanya.

Wednesday, January 02, 2008

ETI KIVUITU ALISHINIKIZWA?

Imedhihirika kuwa mwenyekiti wa tume ya Taifa ya uchaguzi alishinikizwa kutangaza matokeo ya uchaguzi. Je hii si ndio chanzo cha uoza wa dhahama na mauaji?

KIU YA UONGOZI TATIZO LA WAZEE KAMA KIBAKI

Uchaguzi Kenya umekwisha kwa mizengwe lakini mambo ni mabaya kabisa. Ni wakati wa viongozi wa Kenya kufikiri sana. Mwanazuoni mmoja anatoa ni kwa vipi wanasiasa walikuwa wamejisahau.
Pia vurugu za Kenya ni chanzo cha madhara eneo zima la Afrika Mashariki. Kwa waganda wanajiuliza je ni Uganda ina demokrasia zaidi ya Kenya?

Wednesday, December 19, 2007

ZUMA AANZA HARAKATI ZA KUWA RAISI WA BONDENI

The image “http://www.mg.co.za/ContentImages/328066/zuma.jpg” cannot be displayed, because it contains errors.

Bado nina hisia mchanganyiko manake kuchaguliwa kwa Zuma kuiongoza ANC ni matokeo ya demokrasia. Ila mara nyingine demokrasia ina matatizo yake; hili ni tatizo kwa Afrika ya kusini kabisa.

Vijana wa ANC nao wana mashaka sana na uchaguzi wa Zuma kwani hana haiba nzuri ya kiongozi.

Wednesday, December 12, 2007

SIASA ZA BONDENI ZINACHEKESHA

Yaani mara nyingine inafikia wakati mtu anaamini kuwa siasa zetu zimebakwa na wanasiasa. Pia huko somalia, amechaguliwa waziri mkuu mpya je, ataweza kazi yake?

UHURU NA AKILI MGANDO ZA BAADHI YA WATAWALA

Taifa letu lilitimiza miaka arobaini na sita (46) tangu lizaliwe; jumapili iliyopita ilikuwa ni kumbukumbu ya siku ya uhuru kwa maana nyingine. Kama mtanzania, na mzalendo sina budi kuchukua kalamu na kutafakari kwa kina miongo kadhaa kama Taifa ni changamoto gani tumezikabili na zipi inatubidi tupandishe soksi (pull up socks) ili kuendeleza nchi yetu. Binafsi, naamini kama tutafanyia kazi changamoto ya “Utawala Bora” basi uhuru wetu utakuwa na maana sana. Mada yangu itaegemea sana hapa tu.

Kabla ya kujadili, nitoe pongezi kwa watanzania wote tangu raisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete na kwa ujumla watu wa kada zote hapa nchini kwa kuadhimisha siku hii.

Bila ubishi kabisa, nchi yetu imefanikiwa sana katika nyanja mbalimbali tangu uhuru hasa ukilinganisha na nchi nyingine za dunia ya tatu. Hapa ieleweke hata kama tungekuwa tumefanikiwa kiuchumi kama vile Wachina ama Wajapan bado kungekuwa tu na matatizo. Hivyo si vyema kubeza kuwa labda kila kitu ni mrama; yapo mafanikio kama vile umoja wa kitaifa ambao ni mfano dunia nzima. Binafsi nimekutana wa watu kadhaa kutoka pande mbalimbali za dunia wanaposikia umetoka Tanzania watasifia Umoja wetu. Hii yote ni heshima za mwasisi wa Taifa, hayati Mwalimu Nyerere.

Kuendana na mfumo wa kiutawala duniani, yapo mapungufu mengi ambayo nadhani ni vigumu kujikwamua nayo hasa ukizingatia mfumo mzima wa biashara ulimwenguni ni wa upendeleo na ukandamizaji kwa sera za mashirika makubwa ya kiuchumi na kibiashara ulimwenguni. Hapa nazungumzia sera za Mfuko wa Kimataifa wa Fedha (IMF), Benki ya Dunia (WB) na Shirika la Biashara Ulimwenguni (WTO) mwanzoni likijulikana kama GATT.

Ndio maana kama mtu anafuatilia hata yale majadiliano kibiashara ya kule DOHA yamekwama kabisa na ni wazi watawala wa dunia hawataki kabisa kukubali baadhi ya hoja ambazo zitalikwamua bara la Afrika kutoka umasikini usiokwisha. Hata hivi majuzi, Taifa letu limesaini makubaliano mapya ya mashirikiano ya kiuchumi na Jumuiya ya Ulaya (EU) yajulikanayo kama (EPA) kwa kutumia mgongo wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ambayo ni wazi yameshinikizwa na hayatailetea nchi yetu tija sana kinyume na inavyodhaniwa na wale waliosaini. Inajulikana wazi tumelazimishwa kwa kuharakisha kusaini kabla ya ule mkataba wa Cotonou kumalizika hapo December 31 mwaka huu. Nisijadili hili zaidi labda siku nyingine.

Ni katika mchakato huu wa changamoto hizi za mabepari basi hata kama watawala wetu wanao utashi inakuwa vigumu kuweza kusimamia maslahi yenye tija kwa nchi zetu. Kwani mara nyingine watawala wetu wanapokuwa na utashi wa dhati basi mambo kama yanayomkuta Robert Mugabe hayazuiliki kwani wanaishia kufanya maamuzi kwa pupa, bila kufikiri kwa mpangilio na kwa logiki ambayo yanagharimu maisha na uchumi wa nchi zao. Ndio changamoto za “Uhuru” ambazo kwangu ni jinamizi tu; kwani, tunaposherehekea siku hii lazima tuelewe inawezekana kabisa siku ile ilikuwa ni mwanzo wa kipindi cha giza. Ningependa nielezwe hivi Mwalimu Nyerere alipokwenda kule Lancaster alikwenda kusaini mambo gani? Manake inatia shaka huenda ndio ulikuwa wakati wa kujitia kitanzi badala ya kuwa huru. Kwani nina mashaka sana kama kweli tuko huru.

Na ndio maana bado tuna changamoto nyingi sana za kutafakari na kujiuliza tufanye nini? Kwa mtizamo wa serikali ya awamu ya nne, ni wazi changamoto kuu ambayo lazima ifanyiwe kazi ni hii ya “utawala bora”. Hii imebaki kuwa ngonjera na kama hatubadiliki kwa hili basi kamwe hatutapiga hatua yeyote. Nasema hivi kwani naamini pamoja na changamoto za jinamizi la uhuru linaloongozwa na sera dhalimu za kimataifa bado tuna mengi ya kufanya kwa hapa nyumbani ambayo yatatuwezesha tuwe bora tu mbali na mashinikizo dhalimu ya mabepari.

JE TUFANYE NINI?

Tunahitaji kufikiri zaidi ya kuongea sana; hii itatuwezesha kuwekeza katika kuwajibika kwa bidii (hardworking) badala ya kupiga siasa kwa muda mrefu zaidi. Ni wazi hadi leo hii, bado utendaji wetu umetawaliwa na mashiko ya kisiasa zaidi kuliko nidhamu ya kazi katika nyanja mbalimbali. Hasa katika chombo kama Bunge, ni lazima tubadilike; miaka arobaini na sita itufanye tuamue sasa ni mwisho wa siasa za upande mmoja usiozingatia maslahi ya umma. Njozi za chama kushika hatamu zisipoachwa basi hatufiki popote kama Taifa la miongo hii minne na ushehe.

Kwa watawala wetu, lazima kung’amua kuwa kama mhimili wa utawala (executive) unakuwa na nguvu kubwa dhidi ya mihimili mingine basi hatufiki. Pamoja na nguvu ya kikatiba ya taasisi ya uraisi, Uhuru unakuwa na maana kama kiongozi mkuu wa nchi atang’amua hili na kuruhusu utendaji unaoruhusu majadiliano ya vyama vyote vya mitizamo tofauti ndani ya bunge badala ya kuzingatia tu upitishaji wa maamuzi yenye kuegemea uchama na si umma.

Ingawa demokrasia inasema ‘wengi wape’, lakini nadhani pia tuangalie mfumo wetu wa upigaji kura na maamuzi ya upitishaji sheria ama maamuzi bungeni ukoje? Je unaruhusu upigaji kura wa wabunge wa chama tawala unaozingatia uhuru wa mawazo ya mbunge au ni kushurutisha kwa kuegemea maslahi ya chama yaliyofichwa ili kulinda maslahi ya vigogo wa chama tawala bila kutoa sababu za msingi kuhusu jambo fulani ili kulinda maslahi ya nchi.Uhuru unaweza usiwe na maana sana kama mfumo wa maamuzi ndani ya chombo kama Bunge unambana mbunge mwenye mawazo tofauti.

Hata ndani ya vyama vya siasa, ni changamoto pia kujiuliza hivi kuna uhuru wa mawazo wa mbunge katika kujadili mambo na hata kuhoji ndani ya chama? Yaani kwa miaka yote hii arobaini na sita, bado ni kosa la jinai ndani ya chama tawala kwa mtu kujadili hisia zake kwa uwazi inavyoonekana na hata kupinga ama kupiga kura ni udikteta tu (intra-party disagreement, debate and even voting is still a crime). Hapa lazima watawala wakumbuke hili ndilo linalokwamisha maendeleo yetu na hapana budi tuweke mizani ya usawa (strike a balance) katika utendaji wa serikali dhidi ya mihimili mingine miwili hasa ule wa Bunge tukianzia ndani ya vyama vya siasa.

Kwa mfano, kama tutazingatia utawala bora, basi lazima tubadili mitizamo yetu (mentality): yaani serikali iwe kwa ajili ya umma na si kama jamvi la kuficha mafisadi kama ilivyokwishajidhihirisha kwa watuhumiwa wa ufisadi kutajwa hadharani na wao kuamua kukaa kimya bila kujisafisha. Hata mamlaka yenye uwezo wa kuwawajibisha nayo haikuchukua hatua zozote. Ndio hapa bado inaonesha tunawaza zaidi katika kulinda maslahi ya kisiasa kuliko ya umma. Yote hii inashawishi mtu mwenye akili timamu kuwaza na kuamini labda ni kwa sababu ya utawala mbovu. Mfumo wa “Check and Balance” uko likizo ili tu kulinda maslahi ya kisiasa ya chama kinachotawala. Huu ni ugonjwa mkubwa barani Afrika na kama hatubadili mtizamo “Uhuru” unakuwa hauna maana.

Ninaamini kama watanzania, tuna bahati ya kuwa na raisi wa nchi ambaye ana karama ya kuongoza kwa kujali demokrasia; kwani anajitahidi kujumuisha pande na hisia mbalimbali za kisiasa katika utendaji wake. Mashaka yangu bado nadhani waliomzunguka raisi wetu mitizamo yao imepitwa na wakati na si endelevu. Ni mitizamo ya kusisitiza zaidi ‘umilele-chama’ (party-omnipresence) kuwa na woga labda chama kitaangushwa madarakani kwa kile wasichokijua. Na hii ndio chanzo cha madhila kadhaa zinazoisumbua serikali ya awamu hii.

Ni changamoto nzuri za kumfanya raisi na wasaidizi wake kuliona hili na kuamua kubadilika. La sivyo tuna hatari ya kubakiwa na “Kiongozi mwenye karama asiye na mwelekeo” (a charismatic leader without a cause). Mwelekeo wa sasa kwa nchi huru unatia shaka kwani uwezo wa kufikiri wa vigogo wengi ni mdogo sana na ni wazi unasababishwa na tamaa ya fedha na ulafi wa kila aina. Kitu woga kwa viongozi wetu ndio chanzo cha udhaifu wa viongozi wetu kuanzia juu.

Siku ya leo tujiulize ni kwa jinsi gani utawala wa shaghala baghala ulivyogharimu taifa letu kwa kipindi chote cha uhuru. Tunaweza tukalaumu sana na kusingizia mfumo wa kidunia (world order) ambao nimeuelezea awali, lakini kama tuna akili timamu ni wazi kwa nafasi yetu kwa mambo ya hapa nyumbani tuna mapungufu pia ambayo lazima tuamue kwa dhati kuyafanyia kazi. Ndio maana hata Raisi wetu majuzi alisikika akisema na kukiri hata hii mikataba ya madini ni sisi wenyewe wa kujilaumu mbele ya Waziri Mkuu wa Canada mheshimiwa Stephen Harper.

Kama Taifa, miaka arobaini na sita ya Uhuru haina maana sana kwani tumeshindwa kukabili changamoto za ndani kabisa. Inakuwa vigumu kukabili zile za nje manake watawala wa dunia wanatumia udhaifu wetu huu kutulaghai kwa kila hali. Kama hatubadiliki kwa kuruhusu kukosoana ndani ya vyama vyetu, bunge letu na kila mahali ili kulinda maslahi ya umma basi kamwe sioni maana sana ya uhuru. Ninachokiona ni sana sana ni juhudi kubwa tena hasi (highest retrogressive endeavour) za watawala na wanasiasa katika kuirudisha nyuma nchi yetu kwa kasi.

Uhuru bila ‘utawala bora’ ni kwa wachache na si kwa umma wa watanzania. Kama siku ya Jumapili, leo nitamwomba Mungu aizindue akili ya watawala na wanasiasa kwa ujumla wao kubadili mitizamo. Tuachane na akili mgando ndio uhuru utakuwa na maana. Miaka arobaini na sita ya Uhuru ije na mtimzamo (mentality) mpya kuhusu utawala wa Taifa hili. Hii ndio tafakuri yangu ya siku hii ya uhuru kwa leo.

MAWAZIRI NAO HAWALIPI BILI YA MAJI MPAKA WAKATIWE?

Kama unataka kuamini kuwa ni vigumu kwa nchi ya Tanzania kuendelea basi amini kwa haya ya vigogo wa serikali tena mawaziri eti hawalipii kodi ya maji mpaka wakatiwe.
Ni wazi hatuwezi kuendelea kama hata mawaziri hawako makini kiasi hiki. Sasa kama waziri halipi bili ya maji je wananchi wa kawaida watalipa? Nakwambia bado tuko kwenye lepe la ujamaa ambapo kila kitu kilifanywa na serikali.
Hebu soma habari hii alafu ushangae ni vigogo gani hao?

Mawaziri wasiolipia maji watajwa

::Yumo Waziri wa Maji, Msola, Hawa Ghasia
::jumbe wa vitisho watumwa DAWASCO


na yasmine protace

MAJINA ya mawaziri sita, ambao ni miongoni mwa wateja wa Kampuni ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASCO), waliokatiwa maji baada kushindwa kulipia ankara, yametajwa.

Mawaziri hao wanaoishi eneo la Masaki, jijini Dar es Salaam, pamoja na wakazi wengine wa eneo hilo, walikatiwa maji wiki iliyopita.

Kabla ya kuwakatia maji, DAWASCO kupitia Ofisa Mtendaji Mkuu wake, Alex Kaaya, iliwaomba wateja wanaodaiwa kulipia ankara wanazodai.

Katika maombi hayo kwa wateja, DAWASCO ilitoa siku tatu wateja hao kulipia ankara hizo, hata hivyo ni wachache tu waliotii.

MTANZANIA imefanikiwa kupata baadhi ya majina ya mawaziri wanaodaiwa ankara, ambao ni pamoja na Waziri wa Maji, Dk. Shukuru Kawambwa.

Wengine wanaodaiwa ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mizengo Pinda na Waziri wa Maendeleo ya Mifugo, Anthony Diallo.

Katika orodha hiyo, Waziri wa Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Peter Msolla, naye ametajwa, pamoja na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Hawa Ghasia, naye ni mmoja wa mawaziri hao.

Akizungumzia kilichomsibu hadi kushindwa kulipia ankara zake kwa kipindi kirefu, Waziri Ghasia alidai kuwa tangu aanze kuishi katika nyumba hiyo amekuwa hapati huduma ya maji.

Alisema amekuwa akinunua maji kutoka kwa wafanyabiashara binafsi na si kampuni ya DAWASCO.

“Kwa hili jambo ni la binafsi mno. Lakini hata hivyo, lakini sikuwahi kupata huduma ya maji ya DAWASCO na zaidi sikuwahi kupata hizo bili. Sikuwahi kuletewa bili hadi leo,” alidai Waziri Ghasia.

MTANZANIA pia iliwasiliana na Waziri Msolla kwa simu, ambaye alikiri kudaiwa, lakini akadai kuwa hakuwa akifahamu taratibu za kupata ankara na malipo.

“Ni kweli kwamba hilo suala (la kudaiwa) lilikuwapo, nami sikuwapo nchini… lakini last week (wiki iliyopita) tulipata bili na tumekwishalipia,” alisema Prof. Msolla, ambaye hakuwa tayari kuzungumza zaidi kutokana na kile alichodai yupo katika mkutano.

Waziri Simba hakuweza kupatikana, baada ya kuwasiliana naye kupitia simu yake ya mkononi. Majibu kutoka kwa aliyepokea simu hiyo yalieleza kuwa waziri huyo yuko safarini Marekani.

Waziri wa Maji, Dk. Shukuru Kawambwa, Waziri wa Maendeleo ya Mifugo, Anthony Diallo, Waziri wa TAMISEMI, Mizengo Pinda, hawakupatikana, baada ya simu zao za mkononi kuita kwa muda mrefu bila kujibiwa.

Hata hivyo, katika hali ya kushangaza, DAWASCO imesita kuzungumzia majaliwa ya viongozi hao kurejeshewa huduma ya maji.

Meneja Uhusiano wa kampuni hiyo, Badra Masoud, alisisitiza kwamba, walichokifanya ni kukata maji kwa wadaiwa.

“Tunadai fedha nyingi sana Masaki, hivyo tunataka tuendelee kutoa huduma bora kwa wateja wetu ambao wanalipa na wasiolipa tumewakatia mpaka hapo watakapolipa,’’ alisema.

Eneo jingine lililokatiwa maji mbali na Masaki ni Mbezi Beach. Hata hivyo, tofauti na Masaki, wateja wa Mbezi Beach wamekuwa wakijitokeza kulipia ankara zao.

Katika hatua nyingine, DAWASCO imedai kupokea vitisho baada ya kuwapo kwa operesheni hiyo ya ukataji maji.

“Watu wananipigia simu na kunitaka niwarudishie maji eti sijafanya vizuri, lakini mimi nimesema kwamba maji yatarudishwa kama watumiaji watalipia ankara zao,’’ alisema.

Aliongeza kwamba pamoja na kupigiwa simu, pia amekuwa akitumiwa ujumbe wa maneno ya kashfa kutoka kwa watu asiowafahamu.

Takwimu za DAWASCO zinabainisha kuwa, eneo la Masaki lenye wateja 1,270 linadaiwa Sh milioni 574, wakati Mbezi Beach kuna wateja 1,271 wanaodaiwa Sh milioni 578.

Eneo la Ada Estate lenye wateja 475 wanadaiwa Sh milioni 527, Mwenge wateja 733 wakiwa wanadaiwa Sh milioni 463 na Regent kwenye wateja 222 wanadaiwa Sh milioni 200,’’ alisema.

Ni kwa misingi hii jamani tutaendelea kama tunakuwa na viongozi makupe?Yaani kwao kila kitu bure tuu? Ni wazi hata kodi nyingine nadhani hawalipi?Pafanyike uchunguzi hapa.

Saturday, December 01, 2007

TANZANIA BILA UKIMWI INAWEZEKANA?

Siku ya Ukimwi duniani; ni wakati wa kila mtu hasa mwafrika kutafakari juu ya balaa hili ambalo limeshachukua roho za watu lukuki. Wakati naandika makala hii mara nasikia redioni kuwa huko Mbagala Kizuiani kuna jamaa mmoja kaamua kujiua baada ya kuthibitishiwa kuwa ana virusi mwilini mwakeMwingine kaamua kumuua mkewe huko Mbeya baada ya kusikia mkewe kapima bila ruhusa yake

.Ni habari za kusikitisha lakini ni lazima tujiulize hivi kweli hizi kampeni za upimaji ndio jibu la dhahama hili? Na pia tujiulize kwanini tunahofu juu ya kuambiwa tumeathirika?Je hatupo tayari kuwajibika na matokeo ya tabia zetu za ngono zembe?

Napenda niseme kuwa hizi kampeni za upimaji ukimwi zinanitia wasiwasi kama kweli ndio muarobaini wa gonjwa hili. Nasema hivi kwani ni zaidi ya miaka ishirini sasa tangu nimeanza kusikia habari za ugonjwa huu. Na kwa muda wote huo kampeni mbalimbali za kuhamasisha na kuelimisha kuhusu ugonjwa huu zimekuwepo. Ndio maana leo hii katika kampeni hizi za rais Jakaya Kikwete, hakuna jipya linalosemwa. Nimesikiliza, kutizama na hata kuhudhuria semina juu ya gonjwa hili kwa kweli sijaona kipya chochote juu ya elimu ya gonjwa hili.

Nikirejea kwenye mafunzo yatolewayo shuleni: msingi, sekondari na hata katika vyuo kupitia mitaala mbalimbali, nadhani watanzania kama jamii tuna tatizo. Ni jamii isiyojishughulisha kabisa kusoma na kujielimisha binafsi. Habari juu ya gonjwa hili zimesambaa kila kona kwa miaka ishirini iliyopita: vitabuni, majarida, vibwagizo, kwenye mitandao ya intaneti na magazetini, lakini watanzania hatujishughulishi kupata mafunzo lakini tunataka semina, makongamano na hata vipindi vya redio na televisheni visivyo na jipya juu ya gonjwa hili kila kukicha. Kuna haja ya watanzania kuamka katika kujali umuhimu wa kujua mambo yanayohusu maisha yao. Bila hivyo sidhani kama tutafika popote katika vita ya gonjwa hili.

Hivi kweli inaingia akilini kuwa hadi leo hii watanzania watu wazima kwa vijana hatuna uelewa wa gonjwa hili?Miaka yote tumeishi na gonjwa hili yaani hatulifahamu? Nisingetegemea tuwe na kampeni kubwa kama ya sasa na ambayo hatima yake bado ni kutokupungua kwa maambukizi kwani kuna kila dalili watu wengi wameziba masikio.

Nashangazwa na upimaji kwa siri: mosi, hivi kama napima kama nina virusi alafu nasema ni siri yangu, na sitaki watu wajue kama nimeathirika, si kuwa ninataka kuendelea kujichanganya visivyo na watu wengine ili niwaambukize? Kwanini tusiwe na utaratibu wa kistaarabu wa waathirika kuhimizwa kwa ushauri nasaha ili wajiweka wazi na hata kujiunga kwa uwazi na taasisi za waathirika kwani kwa sasa wengi wao ni kwa siri sana. Hapa siongelei unyanyapaa, ila ni vyema watu wawe huru kutambuliwa kwani kama usiri utaendelea kutiliwa maanani zaidi, basi hii kampeni haitatusaidia sana kwani kuna kila shaka ya kuendeleza uambukizi zaidi.

Uwazi huu pia ungeoneshwa hata kwa wanajamii vinara: wabunge, mawaziri, na viongozi mbalimbali wa jamii. Kwa mfano, kama tungejulishwa angalau taarifa za upimaji kule bungeni, je wangapi walipima, wangapi walionekana kuathirika ama kutoathirika. Lakini kupambana na ukimwi kwa usiri hakutakomesha ukimwi kamwe.

Pia nashangazwa na hizi juhudi za upimaji hazijaonekana sana katika taasisi za elimu hasa elimu ya juu. Huku kuna vijana lukuki na ingekuwa vyema hapa watu wapimwe manake ndio viongozi wa kesho tunaowatarajia na tukiwaacha ngono mbele kwa mbele basi tujue kuna mahali ambapo paangaliwe manake kwa muono wa karibu ni sehemu ambapo maambukizi yanawezekana kuwa kwa kasi sana.

Linalonishangaza sana ni kuwa Ukimwi umekuwa ni mradi mkubwa kwa baadhi ya watu flani na vitaasisi vyao vyenye utegemezi wa wafadhili. Ni wazi kuna watu wanafurahi sana ongezeko la wagonjwa wa ukimwi na hata yatima. Bila gonjwa hili watu wengi hawataajiriwa na wengine wangekuwa masikini kabisa. Najua siku hizi imani za kidini ni kiini macho kwa wengi kutokana na matendo yao. Ni kwa misingi hii vita ya gonjwa la Ukimwi inaonesha kama vile hakuna Mungu.

Ukimwi bado ni kiini macho kupambana nao kwani hadi leo bado watu wanaugua gonjwa hili lakini utasikia eti wamekufa kwa vigonjwa vingine ama wamelogwa na mambo mengine ambayo mtu mwenye akili inashangaza sana. Kuna haja mtu anaugua gonjwa hili awe tayari kusema nilikuwa naugua gonjwa hili bila aibu. Tunazika watu wengi hata wasomi kabisa ambao wakati wa kuugua anaonekana anaugua Ukimwi ila siku ya kufa utasikia eti anaumwa sijui kansa, presha na kadhalika. Ni usiri wa kijinga tunauendekeza na ambao hatima yake ni kiini macho cha vita ya ukimwi. Umefika wakati tuache usiri bila hivyo ni vifo bila mabadiliko.

Mwisho, nadhani kwa mwenendo wa sasa, “Tanzania bila Ukimwi” haitawezekana kama raisi wetu anavyotusihi. Usiri huu kwa kisingizio cha kuzuia unyanyapaa ni chanzo cha janga hili kuendelea. Siamini nchi yetu inaweza kuendelea, ni wazi gonjwa hili litaendelea kudumaza na kuwamaliza wasomi wa nchi yetu. Ni mwaka wa ishirini na saba tangu gonjwa hili livamie nchi yetu na bado watanzania wengi hawajaamua kuacha ngono zembe, ni mwanzo wa kiama Tanzania.

Thursday, November 29, 2007

MALKIA ALIVYOFURAHIA UGANDA

Leo nataka tuone ni wapi Malkia Elizabeth alilala na ni jinsi gani aliandaliwa na kufurahi maisha ya kiafrika alipokuwa nchini Uganda.

KAMATI YA MADINI--NI SARAKASI ZA KISIASA ZISIZO NA TIJA SANA

Katika makala yangu ya mwezi September, tarehe 9, mwaka huu,katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili: “Bunge letu ni jumba la Sanaa”, ukurasa wa 12—13 , nilieleza kuwa demokrasia ya Tanzania ni ya kipekee duniani na kusema hivi: “kwa misingi kwamba tuna serikali isiyozingatia mihimili mitatu: Watawala, Bunge na Mahakama. Tanzania ya leo, serikali inaendeshwa kwa mihimili miwili: watawala na mahakama.” Hapa nilionesha wasiwasi wangu jinsi gani Bunge linafanya kazi ya kubariki na kuisemea serikali (rubber stamping) mijadala ya serikali badala ya kuihoji.

Hii niliona kama chanzo cha Bunge, kupitia wabunge wengi (majority) wa CCM walivyohakikisha wanaizima hoja ya Zito Kabwe na kumfungia kama adhabu kwa kile walichodai ni uzushi na utafutaji wa umaarufu kirahisi (cheap popularity).

Leo nataka niendelee nilipokomea kwani kutokana na mada ile ile ya Zitto Kabwe, rais Kikwete kaja na mpya. Kuunda kamati ya raisi kuchunguza ama kuipitia mikataba ya madini ni jambo zuri japo ninapata wasiwasi na utashi wa kweli wa hatua yake. Yaani raisi kama mkuu wa mhimili wa utawala na pia sehemu ya Bunge, ni wazi maamuzi ya awali ya kumuadhibu Zitto hayakuanzia tu kwa wabunge bali yalipangwa na raisi pia kupitia baraza la mawaziri, alafu waziri mkuu akawafunda wabunge wa CCM na maamuzi yakawa jinsi ilivyokuwa.

Mpango mzima wa kuzima madai yale ulishindwa na ukaleta matokeo isivyotarajiwa (backfire) na ikadhihirisha aibu kubwa ya kifikra kwa wabunge wa CCM na serikali kwa ujumla. Raisi anapong’amua hili alafu anawageuka wabunge baada ya kuwaaibisha kwa kuwashurutisha wafikiri visivyo. Ni kichekesho kikubwa; hebu fikiri Bunge letu limejaa wasomi, maprofesa, madaktari wa falsafa lukuki wa fani mbalimbali. Ni hatari kwa nchi kubwa kama yetu yaani mafanikio yote haya ya kitaaluma hawawezi kufikiri sahihi wala kusoma alama za nyakati.

Ukiacha hilo, raisi anajaribu kukiuka ahadi yake ya Ari Mpya, Nguvu Mpya na Kasi Mpya. Raisi anaturudisha kulekule kufanya mambo kwa mazoea kitu ambacho amekuwa akikipinga. Uundwaji wa tume ya raisi wala si ya Bunge unanifanya nianze kukosa imani na raisi kwa hili. Swali: Inakuwaje Bunge, linaamua kufanya kazi ya mhimili wa watawala na kuacha wajibu wake wa kuhoji au kuchunguza madai halali ya Zitto kwa kisingizio cha Spika eti tungepoteza pesa bure baada ya kupoteza zile za tume ya madai ya Mengi awali. Pili, hivi hii tume ya raisi ya leo hii haitumii pesa?

Wajuzi wa masuala ya kiuchunguzi wanasema tume ya raisi haina meno kisheria kama ile ya kibunge. Ni wazi raisi anajaribu kutuchezea mchezo wa kisiasa katika kujaribu kuifuta ile kashfa ya Buzwagi. Hoja ya Kabwe ilikuwa juu ya uvunjaji wa taratibu kusaini mkataba wa Buzwagi kule hotelini Churchil. Raisi kaiteka nyara ile hoja na akageuza kuunda kamati kuchunguza mapitio ya mikataba yote ya madini. Hapa nashangazwa na utashi wa kupambana na ufisadi kama ni kiini macho tu. Najiuliza: hivi zile juhudi zote sa Spika na Wabunge wa CCM kutumia kanuni halali za Bunge na kuzima kwa msisitizo mkubwa hoja ya Buzwagi zilikuwa za kuwalinda akina nani?

Kuna harufu ya rushwa hapa, kwani kama tunapitia sheria zote za madini basi labda tunataka kuondoa akili ya watanzania wote kutoka Buzwagi na kuzika madai ambayo Spika ama kwa utashi wake ama kwa maagizo hakutaka kabisa iundwe kamati ya Bunge.

Hata hii kamati ya Bunge ya kuchunguza mkataba wa Richmond inatia wasiwasi sana juu ya utashi wa kweli kama upo. Ukifikiri sana unajiuliza: kwanini imeundwa leo hii na si wakati ule ambapo ilipingwa kwa nguvu zote? Hata taasisi nyeti ya uchunguzi wa rushwa (Takukuru) ilishaisafisha Richmond lakini mara tunaona mabadiliko ya bunge letu (U-turn) na sasa bunge linakubali kamati ya Bunge iundwe. Hapa nina wasiwasi sasa wahusika wameshaandaa nakala-vielelezo mpya za kufuta ushahidi wa rushwa na maadam wameshajihami basi wana hakika Kamati ya bunge itawakuta ni wasafi.

Jambo lingine kwenye hii kamati ya raisi kupitia sheria za madini: vipi miongoni mwa wajumbe wa tume ya raisi ni wabunge wawili wa CCM ambao kwa nguvu kubwa walipiga makelele kwa kupiga meza katika kuzima kabisa hoja ya Buzwagi? Kama hawakuona kabisa utata katika mkataba ule hivi kweli ni watu wenye utashi wa kuchunguza mikataba ya madini? Hapa ndio pananitoa imani na uamuzi huu wa kuunda kamati ya raisi.

Wasiwasi wangu mwingine, nakumbuka wakati anaongea na Sauti ya Amerika (VOA) akihojiwa na Shaka Sally kupitia kipindi cha Straight Talk Afrika kutoka Chamwino Dodoma, raisi alisema mikataba yote ya madini imeshapitiwa na sasa inaendana na viwango vinavyokubalika kimataifa. Nakumbuka alizungumzia mambo kama ya mirabaha inayolipwa na kampuni za madini na hata lile suala nyeti la mgawanyo wa kodi wa asilimia 3% kwa 97% na akasema sasa ni 30% kwa 60% kama sijakosea kukunukuu. Sasa kuunda kamati kupitia tena sheria za mikataba kunamaanisha alikuwa anadanganya? Nilitegemea raisi aunde kamati kuchunguza Buzwagi—kiini cha madai ya Zitto. Sasa hii upitiaji wa mikataba ambayo raisi amewahi kusema imepitiwa na wataalamu ni nini tena?

Hapa raisi mimi binafsi nadhani tumwamini kwa maamuzi yake japo utashi unatutia wasiwasi. Nampa imani ya kidhahania tu (benefit of doubt) na tusubiri tuone kweli kama tume yake itapendekeza nini na kama atafanyia kazi mapendekezo hayo. Mambo haya ya kufunikafunika ni mbinu za kisiasa zilizopitwa na wakati. Nina wasiwasi raisi hajui kuwa nchi yetu ipo katika kipindi cha kiongozi mkuu kufanya maamuzi magumu la sivyo umaarufu wa chama na serikali yako utagharimika sana. Ni wakati wa “Utawala Bora” kuachiwa ufanye kazi. Mihimili mitatu ya dola isipoachiwa ifanye kazi kwa kujitegemea bila kuingiliwa na watawala basi ndio tunashuhudia usanii kila kukicha hasa tangu awamu ya nne ianze.

Ule wakati wa kuwachukulia watanzania kama watu wa mawazo finyu (gullible) umekwisha. Ni wazi kama rais na chama chake hawakutaka kamati ya bunge kuchunguza Buzwagi ila anaamua kuunda kamati chini ya mamlaka yake. Lengo linaweza kuwa ni kuweza kudhibiti uchafu wote utakaoibuliwa usishughulikiwe kwa mujibu wa sheria. Tume aliyoiunda inawajibika kwake na wala haina nguvu za kisheria kuwezesha mapendekezo yake yafuate mkondo wa kisheria iwapo itathibitika kuna haja ya kuwawajibisha vigogo fulani.

Ndio maana ikiwa tume itawakilisha ripoti kinyume na matarajio ya Raisi, tusishangae yale yaliwahi kumkumba Jaji Robert Kisanga wakati wa enzi za uwazi na ukweli yakamkumba pia Jaji Mark Bomani. Binafsi nimeitafakari hatua ya kuunda kamati ya raisi na si ya Bunge kama sarakasi za raisi katika kufunika kashfa ya Buzwagi. Ni dhihirisho jinsi Bunge lilivyotekwa na mhimili wa watawala (executive’s hijack of the legislature). Raisi anafanya kila juhudi kuendeleza hali tata iliyopo (Status Quo) yaani kuzuia mabadiliko ya kifikra na hata jinsi mpya ya kiutendaji ili kuikwamua nchi yetu katika umasikini wa kujitakia.

Kwa mwendo huu kama viongozi wa bara la Afrika hawataki kuruhusu mfumo wa utawala bora ufanye kazi basi katu haisaidii juhudi za kujikwamua na umasikini. Haya ndio yananifanya niwe na wasiwasi na tume ya raisi; hebu tusubiri tuone kama itakuwa na tija. Lakini ningekumbusha mbona tunaizika kashfa ya Buzwagi? Hii ni sarakasi ya raisi; je itafanikiwa? Tusubiri tuone.

Saturday, November 17, 2007

LEO JUMAMOSI

Profesa Mazrui kaandika juu ya mapambano ya mwafrika; na pia kama kawaida napenda sana kujijuza mambo ya nyakati za Iddi Amin.

Wednesday, November 14, 2007

RAIS KIKWETE ADHIHIRISHA JINSI BUNGE LISIVYOJALI MASLAHI YA NCHI

Sijui niuite ni ukinyonga au niseme nini ila kama kuna siku rais Kikwete kanichekesha ni pale niliposikia kuwa ameunda tume ya kuchunguza na kupitia mikataba ya madini. Mshangao ulinipata baada ya kusikia eti na mheshimiwa Zito Kabwe nae ni miongoni mwa wajumbe wa tume. Kwangu hii ilikuwa ni faraja kusikia hili la kumjumuisha mpinzani ndani ya shughuli kama hii. Zaidi kumjumuisha Zito Kabwe lilinichekesha sana.

Zitto Kabwe ndie mwaanzilishi na mpiga filimbi mkuu aliyethubutu kujitoa mhanga na hatimaye kupewa adhabu ya kutohudhuria kikao cha Bunge kinachoendelea sasa ili kutaka tume ya Bunge iundwe kuchunguza haya rais anayoyaundia tume. Kama mtu unafikiri na si kimgandomgando, unapata hisia kuwa raisi Jakaya Kikwete amelipiga bunge mwereka kimawazo. Ni katika msingi huu Bunge letu hasa vinara wake: Waziri Mkuu na Spika pamoja na wabunge wote waliounga mkono Zitto apewe adhabu wanafanywa ni wajinga ajabu.

Saturday, November 10, 2007

MSONGO WA MAWAZO TATIZO KUBWA UGANDA

Jamani watu wengi wana msongo mkubwa w a mawazo au wana tatizo la kisaikolojia; Uganda eti watu wengi wamechanganyikiwa. Pia ziara y a Museveni Marekani imekuwa gumzo juu ya uswahiba m p ya na Joji Kichaka.

MUSEVENI NA UTUNZI WA VITABU

Museveni ni rais mahiri kwani huwa anaandika vitabu na hata makala magazetini. Karibuni kaandika kitabu na kimeshangaza kidogo kimtazamo. M useveni anaaminika kama kiongozi bora ila kuna haja ya mabadiliko kwa mujibu wa jaji maarufu. Pia tujiulize je Big Brother ni muhimu sana?Pia benki zimeanza kuhimiza ndoa unazijua?
Pia tunajuzwa zaidi ni vipi Iddi A min alivyowapendelea watu wa kabila lake.

Kumbe John Garang aliuawa na serikali ya Uganda? Kumbe pia uzazi bila mpango ni chanzo cha Ukimwi kuenea kwa kasi? Mwisho kabisa hii ni kali yaani kuna kesi kubwa ya aina yake nchini Uganda.Unamjua mtuhumiwa wa wizi wa f edha za Gl obal Fund?Na ugonjwa wa m araisi wa Afrika je?

Monday, November 05, 2007

KWANINI VIGOGO WANAPENDA HOSPITALI ZA MAJUU?

Ama kweli bongo kuna vituko, huwezi amini eti madaktari wanaweza kosea namna hii; mambo kama haya yanawezekana bongo tu. Inawezekana ndio maana vigogo wanaziogopa hospitali za bongo.

Saturday, November 03, 2007

IDDI AMIN MZIMU BADO HAI

Kwanza kabisa leo tukumbushane juu ya Iddi Amin; alafu tutizame waasi wa LRA Uganda wanavyojaribu kujirudi.
Alafu kuna hili gonjwa la kisukari linakuwa sugu, hali ni mbaya Uganda.

Na kwa wale mapedeje, mnajua gharama zake?