Baadhi ya wanaofuatilia mtizamo wangu ni wazi nimekuwa napinga Shirikisho la Afrika Mashariki ila nikiunganga mkono hatua ya Jumuiya tu kwani naamini Shirikisho la Afrika Mashariki itakuwa ni hatua ya kisiasa isiyokuwa na manufaa yeyote kwa mwanachi wa kawaida.
Moja, mwaka 1958, Osagyefo Kwame Nkrumah alifanya juhudi sana kuinganisha Afrika kwa kuanzia na Ghana na Guinea, ikafuatiwa na Ghana-Guinea-Mali ambazo zote hazikudumu. Pili, kukaja Shirikisho la Senegambia kati ya mwaka 1981 na 1989. Zote hizi hazikudumu sana wala kuweza kusimama; kwa ujumla mashirikisho ya kisiasa yaliyojaribiwa katika karne iliyopita hayakufanikiwa pia si tu Afrika bali hata sehemu nyingine za ulimwengu na mifano ipo mingi: kwa mfano, Shirikisho la India Magharibi (West Indies Federation) kati ya mwaka 1952 hadi 1962.
Nyingine ikawa ni Shirikisho la Kijamaa la Mataifa ya Kiarabu (Federation of Socialist Arab States) kati ya mwaka 1972 hadi 1977 ambapo msisitizo ulikuwa wa kizalendo yaani Pan Arabinism; alafu likawepo lile shirikisho la Yugoslavia kati ya mwaka 1945 hadi 1992; na mfano wa mwisho kabisa ni lile shirikisho kubwa kubwa kabisa la kisiasa wakati wa vita baridi la Urusi ( Union of Socialist States of Russia) la mwaka 1922 hadi 1991.
Unaweza kuona mashirikisho niliyoyataja hapo juu yalianza na kufa kwa sababu mbalimbali ambazo pia zipo hapa Afrika Mashariki. Lakini pia mtu anaweza kujiuliza mbona yapo mashirikisho ya kisiasa ambayo bado wamo na yanaendelea? kwa mfano, Shirikisho la Nigeria lenye watu takriban millioni mia moja na kumi (110) au lile la Ethiopia lenye wakazi takriban milioni sabini na nane (78). Kama kweli Mashirikisho haya mawili ya kiafrika yana tija hasa kwa wananchi wa kawaida ni kwanini basi nchi zote hizi mbili bado ziko katika kundi la nchi zinazoendelea na si nchi zilizoendelea?
Hii ni sababu inayonifanya mimi kutokuunga mkono wazo la Shirikisho la Kisiasa la Afrika Mashariki. Nikihakikishiwa ni dawa ya kutuondoa kutoka katika nchi zinazoendelea, au zile masikini sana ulimwenguni (LDCs) basi nitaunga mkono; ila kwa hali ya sasa nafikiri shirikisho halina maslahi makini ukiacha matakwa binafsi ya wachache.
Nimejaribu kutizama pia lile shirikisho ambalo nadhani ni mfano wa mafanikio ulimwenguni, nalo ni ule Muungano wa Mataifa ya Amerika ( United States of America) ambalo kisiasa ni mfano wa kuigwa kimafanikio. Je hiki ni kielelezo cha Shirikisho la Afrika Mashariki kufikiwa? Mimi sioni kama ni kweli kabisa: nikumbushe kihistoria ilihitajika takriban miaka mia moja (100)--1776 hadi 1865 pamoja na vita kali na kubwa ya kiraia ya mwaka 1861 hadi 1865 ndipo Marekani ikakomaa na kuweza hata kustawi kama taifa lenye nguvu kabisa ulimwenguni.
Ni wazi kuundwa kwa Shirikisho sio mchakato wa kuharakishwa kama akina Museveni, Kibaki na Kikwete wanavyotaka. Kuna mambo mengi ya kuzingatia hasa ukiangalia EAC ni jumuiya yenye nchi zenye historia ya kupiganapigana katika kila jambo la kisiasa.
Labda nisisitize kuwa si Marekani tu ambapo mambo hayakuwa rahisi kama vile maraisi wetu wanavyotaka tuharakishe kufikia Shirikisho. Niwapeleke katika jumuiya ya Ulaya--(European Union). Kuanzia juhudi za mwanzo kabisa pale uliposainiwa mkataba wa Roma- 1957, kuanzisha Jumuiya ambayo mpaka leo mchakato wa kuunda Shirikisho la Kisiasa umebaki kiini macho. Mwaka juzi tu wanachi wa Ufaransa na Uholanzi walikataa kuunga mkono Katiba mpya ya Jumuiya ya Ulaya kwenye kura ya maoni, ambapo lilikuwa ni pigo katika kukwamisha mchakato mzima wa kufikia Shirikisho la Kisiasa. Tunaweza kuona ni miaka zaidi ya hamsini sasa Ulaya inashindwa kuunda Shirikisho la Kisiasa.
Mambo yote haya niliyoyataja yananifanya niamini kuwa muungano ya kiuchumi ni hatua muafaka ambayo itatufaidisha kiuchumi baada ya kipindi fulani. Nionavyo, Shirikisho la Kisiasa halitaweza kwa jinsi yeyote kuleta faida yeyote kwa mwananchi wa kawaida zaidi ya kuwafaidisha wanasiasa wetu. Wanasiasa wetu waache mawazo eti ile kuwa tu na idadi kubwa ya watu basi utakuwa na soko kubwa ambayo ni kielelezo cha nguvu za kiuchumi. Kwa Jumuiya yetu kweli soko litakuwa kubwa ila ni dhaifu sana kiuchumi; ni soko la wateja wengi ila ni masikini sana na ndio hapa nadhani zifanyike juhudi kuendeleza wananchi kielimu na kiuchumi hasa kiujasiriamali (entreprenuership) ndipo tutegemee soko lenye tija. Kinyume chake, hii "uharakishaji" ni usanii mwingine wa watawala kama walivyowahi kujaribu hapo nyuma na kutofanikiwa.
Mwisho ni vyema tuangalie historia ya mashirikisho ya kisiasa katika sehemu kadhaa za dunia ili tuweze kung'amu tufanye nini katika juhudi zetu za kujumuika kimataifa; lisiwe suala la kuharakisha bila kujiuliza je ni kwa maslahi ya nani? Je watawala wanawaza juu ya mwananchi wa kawaida katika jumuiya? Mimi nashangazwa sana na hili zoezi la kukusanya maoni juu ya Shirikisho kufanyika wakati tayari wameshatia saini kuruhusu "kuharakisha mchakato" mzima wa kuunda Shirikisho. Zoezi zima la kukusanya maoni naamini ilikuwa ni ufujaji wa fedha kwani viongozi wetu walishaamua jambo walilotaka kutuuliza; sasa sijue kwanini wanakusanya maoni kwa kitu walichokwisha kitolea maamuzi. Ama kweli tusipokuwa makini tutaburuzwa bila kutafakari.