My Blog List

Thursday, May 22, 2008

BALALI – MWISHO WA SINEMA LA BOT?

Ni saa nane za mchana, siku ya tarehe 21/5/2008 mara napokea meseji ya simu inasema hivi: “Hatimaye picha la BoT lafikia patamu! Balali amefariki! Watatuchezea usanii kuwa huu ndio mwisho wa sinema maana stelingi kafa, ila ukweli wenyewe sinema hii haikuwa na stelingi mmoja tu! Nipe mawazo yako.” Habari hii ilinishtua kidogo kwani nilishatarajia huyu bwana angekufa kwani awali iliripotiwa alitiliwa sumu na mamafia wa kibongo. Akili yangu ilikwenda kwenye hisia za sumu na mara moja nikajenga kanuni za kidhahania (conspiracy theories) kadhaa:

Kwanza kabisa ni muhimu sana kuzungumzia na kuchambua kifo mara kitokeapo. Mara nyingi tunapozungumzia kifo inatusaidia kumchambua aliyekufa weledi wake kimaadili. Yaani ni jinsi gani aliishi wakati wa uhai wake. Kifalsafa, na pia kwa kuzingatia mtizamo wa kikristo, kifo ni utengano kati ya raha na mwili. Kwa maana nyingine, ni kusimama (cessation) kwa uhai katika kiumbe chochote kama hayati Balali. Kwa mtizamo wangu nina maswali kadhaa bila majibu ambayo ni kidhahania zaidi.

Pili, hebu wote wenye akili timamu tujiulize kuwa Gavana aliyeomba kujiuzulu akakataliwa na baadaye uteuzi wake ukatenguliwa (kufukuzwa) hatimaye anakufa baada ya hisia kuwa aliwahi kutiliwa sumu. Huyu ndiye shahidi muhimu sana katika sakata la BoT na nadhani kwa mafisadi sasa wanapumua sana. Ndie mtu pekee ambaye kama Gavana alijua michezo yote michafu katika skandali hili kwani yeye alikuwa stelingi kama nilivyokwisha elezwa na mtuma meseji ya simu awali.

Kwa wapenda picha, filamu,kuna msemo kuwa, kwa kawaida stelingi hauawi, akiuawa sinema imeisha; sitarajii tena kama kutakuwa na lolote la maana kuhusu sakata la BoT. Kifo hiki ni pigo kubwa kwa wale wote tuliodhani vita ya mafisadi ni rahisi. Ni vita ngumu sana kwani mara nyingine mafisadi wanawamaliza wale wote watakaoweza kusaidia michezo yao kugundulika ili kupoteza ushahidi.

Tatu, nategemea ile kamati ya kuchunguza dhahama la BoT imalize miezi sita ije na madai kuwa haikuwahi kumuhoji hayati Balali. Nina wasiwasi inawezekana kupewa muda wa miezi sita ilikuwa ni kuvuta muda ili huyu bwana afe kama ni kweli aliwahi kupewa sumu. Na kama niko sahihi basi sitasita kukubali madai ya mwandishi mmoja kuwa dola yetu sasa ni kimafiamafia hivi; yaani inatumikia mafia. Si hili tu ninalolidhania ila niseme tu kifo hiki kimenishangaza sana; yaani kilitokea ijumaa (16/5/2008). Siku tano baada ya kifo habari zake ndipo zinafika nchini yaani jumatano ya tarehe 21/5/2008. Huu mficho wa nini?

Swali lingine la kidhahania ni kuwa hivi huyu Balali alikuwa mtumishi wa serikali au la? Alishafukuzwa (kutenguliwa uteuzi), sasa inakuwaje kifo chake kiwe ni wajibu wa serikali kukitangaza kwa umma? Waandishi wa habari pia walijazana benki kuu kutaka kujua ni vipi kuhusu kifo cha mtu ambaye hakuwa na uhusiano na taasisi ya benki kuu. Inanishangaza kidogo labda nifafanuliwe maana ya kutenguliwa kama si sawa na kufukuzwa. Mtu ambaye alishajiuzulu kwa barua na kujiweka pembeni ingawa baadaye kuonesha kuwa hatakiwi kabisa alitenguliwa uteuzi wake. Jamani naomba nijulishwe maana ya kutenguliwa uteuzi ni kufukuzwa ama vingine? Kwani kifo hiki kinaonesha wazi si kufukuzwa ndio maana BoT waliwajibika kutoa taarifa maalum kama vile huyu bado mtumishi wao.
Kanuni nyingine ya kidhahania: Najiuliza zaidi eti hayati Balali kafia Marekani na mazishi yake hatujui ni wapi japo inaonekana hata familia yake iko huko. Tetesi ni kuwa alikuwa ni raia wa Marekani zinapata ukweli manake huyu mtu kama hata mazishi yatafanyika huko Marekani basi serikali iliyopita itapata doa. Yaani iliajiri Gavana ambaye si raia? Je huu uoza wote wa BoT si inawezekana umechangiwa na kutokuwa raia? Kwani tangu lini nchi yetu ina sheria ya uraia wa nchi mbili? Kiuzalendo mtu ambaye si raia ataweza kujali uzalendo katika maamuzi yake kwa kusimamia sheria na taratibu za nchi? Mamlaka iliyomteua na nyingine ikaendelea naye ina deni kubwa kwa watanzania.
Binafsi, inanishawishi niamini ile sheria ya uraia wa nchi mbili (dual citizenship) kumbe tayari inatumiwa na wateule wachache hapa Tanzania kama akina Jeetu Patel na mwenzie Vithlani pamoja na hayati Balali. Na kama niko sahihi basi si hayati Balali tu anayefaidika na sheria hii bali tutarajie kuwajua wengine wanaofaidika na sheria kama hii vita dhidi ya mafisadi itaendelezwa. Waziri wa fedha kipindi cha uborongaji wa BoT, mama Zakia Meghji ameripotiwa akimsifia marehemu ete alikuwa mchapakazi hodari. Imenishangaza yaani unakuwa kiongozi alafu mafisadi wanajichotea fedha hazina ya serikali ukiangalia tu alafu mambo yakiharibika unaandika barua kujiuzulu eti huo ni uhodari.

Mwisho, kifo cha mtu yeyote ni ukumbusho wa jinsi gani mtu aliishi kimaadili au la. Na kwa Balali ni wazi kama Gavana, uoza wake ulifichuka pale ukaguzi wa Ernst & Young ulipoanika ufisadi wa EPA. Kimaadili namwondoa katika kundi na huyu anatuachia kumbukumbu ya ufisadi. Kama si fisadi basi wanafamilia wake wamsafishe na kutujuza nini hasa zilikuwa hisia zake kabla ya kuondoka. Ila kama wataendelea kushiriki huu usiri wa serikali kuhusu kifo chake ni wazi yeye pamoja na familia yake hawatalikwepa hili limzimu la ufisadi.
Binafsi nadhani hayati Balali kafa kama mtu pekee Tanzania ambaye hakuwahi kufukuzwa kazi ila uteuzi wake ulitenguliwa. La kushangaza kwanini kujiuzulu kwake kukataliwe? Aliogopwa sana? Ama mamlaka ya uteuzi ni ya kishikaji sana na kufukuza wavunja sheria na taratibu ni vigumu kwayo au ina woga kumtia mkosaji kwenye aibu? Sina jibu hapa ila kifo hiki kwa kiasi fulani kinatupa picha halisi ya udhaifu ama uimara wa mamlaka kuu ya utawala wa nchi hii. Na kwa mwono wangu mdogo nadhani kama shahidi muhimu katika suala la BoT basi skandali hiyo imepoteza mwelekeo na ni furaha kwa mafisadi wengi waliohusika.
Mungu amlaze hayati Balali mahali pema peponi, Amina.

Thursday, May 08, 2008

UTAPELI WA WALOKOLE

Watu wanadai eti kuna walokole wenye uwezo wa kutibu Ukimwi kwa sala!Mama wee!, huyu katumiwa na walokole kudanganya aliponywa kwa miaka kadhaa.
Malimwengu bwana, yaani kumbe tunadanganywa sana, lazima tuwe macho sasa na haya madini yaliyoongezeka sana.

Friday, May 02, 2008

MEI MOSI MAONESHO


Jamaa wa zimamoto kutoka uwanja wa ndege KIA nao walikuwepo kuonesha mambo yao:

Thursday, May 01, 2008

MEI MOSI ILIVYOFANA MOSHI


Niliamua nijumuike na wafanyakazi Mkoa wa Kilimanjaro; picha zitakuonesha mambo yalivyokuwa.


Hapa jamaa wanaonesha jinsi shughuli za kilimo cha kahawa zinavyoendeshwa:

Sunday, April 27, 2008

HAPA NI WAPI?


Kama unajua hili ni jengo gani mjini Moshi sema.

MASALIA YA AJALI YA NDEGE



Haya ni masalia ya ndege ndogo iliyoanguka Moshi miezi kadhaa.

AJALI YA NDEGE - MOSHI

Nilikuwepo ndege ilipoanguka Moshi maeneo ya jirani na kiwanda cha mafuta BP. Watu wawili walipoteza maisha yao: Rubani (Mbongo) na Mzungu mmoja. Wengine wawili walijeruhiwa.Ilikuwa ni Januari mwaka huu.

VYOO VYA USWAHILINI

Hiki choo kimebomoka lakini kinatumika, ndio mambo ya walalaho wa kitanzania. Nusu kimetoboka na jamaa akija kujisevu hapa inabidi awe makini asije tumbukia.

HILI NALO BAFU


TUONE NA MABAFU YA KUOGEA YA MTANZANIA WA KAWAIDA

Mtanzania wa kawaida ambaye kwake maisha ni magumu na haoni vijisenti hata kidogo. Yeye huwa anaoga mahali kama hapa. Chini ni mchanga tu, hakuna mlango na ujenzi wa bafu ni makaratasi na magunia. Haya yakitokea, wengine wanakomba mafedha "vijisenti" na wala hawachukuliwi hatua. Wanalazimishwa kujiuzulu tu.

HEBU TUJIONEE VYOO VYA WATANZANIA

Hapo chini ni hali halisi ya vyoo vya mtanzania wa kawaida ambaye vijisenti kwake ni ndoto. Mambo ya uswahilini hayo.

Saturday, April 05, 2008

UFISADI HADI JESHINI UGANDA

Wakati ufisadi umetawala Tanzania,kule Uganda hakuna tena woga, mafisadi ambao zamani walikuwa jeuri sasa mkono wa sheria unawakumba. Kuna Jemedari wa jeshi sasa kawekwa jela kwa kosa la ufisadi jeshini. Hebu msome anavyojitetea dhidi ya ufisadi alioufanya.
Majenerali wengine wanaendelea kukanusha ufisadi. Wakati jeshi letu liko Comoro, Waganda nao wako Somalia na kuna tetesi za ufisadi zaidi jeshini.

Tuesday, April 01, 2008

MAJENERALI UGANDA MATUMBO MOTO

Kwa wale masekretary wa vibosile basi wajifunze ni jinsi gani kazi hiyo imejaa ufisadi kutoka kwa sekretary wa Museveni.
Kuna skandali kubwa dhidi ya maafsa wa jeshi la Uganda kwa kuajiri askari hewa: unalijua? Msome pia kinara wa skandali hilo Jenerali James Kazini, ni yule aliyewahi kushtakiwa na Umoja wa Mataifa kwa kuibia DRC rasilimali.

Tuesday, March 18, 2008

YOWERI MUSEVENI NA AJENDA YA KIFALME

Muammar Ghadafi amemuhimiza Museveni aendelee kuitawala Uganda milele.

Saturday, March 15, 2008

NRM NA MADHILA KWA WAGANDA

Unataka kuijua NRM, ni chama dume, tawala kama kilivyo CCM, lakini madhara yake ni makubbwa sana kwa watu wake.

Thursday, March 13, 2008

TANZANIA NA MFUMO WA KIOLIGACHI KAMA URUSI

TANZANIA NA MFUMO WA KIOLIGACHI KAMA URUSI

Wiki hii nimeshawishika kuchangia juu ya mwono wangu kuhusu hili skandali la wizi wa fedha kule benki kuu: BoT maarufu kama EPA. Kwanza nimevutwa na mchango wa jumapili iliyopita kutokana na makala ya Bw. Tambwe Hiza: “Fedha zetu ni muhimu kuliko mashitaka” Tanzania Daima, Jumapili, Machi 09, 2008. uk. 21. Kwangu makala ile imenifanya nijiulize hivi kweli elimu ya Tanzania inafundisha watu kufikiri hasa?

Kwanza niseme tu nampongeza mwandishi kwa mtizamo wake huu ambao una tija moja tu: nayo ni fedha zote kurudishwa. Haya ni mawazo mazuri sana ambayo kwangu yananipa wasiwasi kama tunafurahia kurudishwa kwa fedha kwa kuwabembeleza wahalifu. Siamini kuwa kashfa hii imetufikisha mahali tuwaogope hawa mafisadi hadi kuwalinda na kuwahakikishia usalama wao mara watakaporudisha dhidi ya mkono wa sheria.

Pili, mwandishi alitumia mifano hai kuonesha jinsi gani matatizo katika nchi mbalimbali yalivyotatuliwa kwa njia nje ya mkondo wa kisheria. Nina wasiwasi kuwa kama tunawaepusha mafisadi na mkondo wa kisheria basi tunajenga mustakabali mbaya (wrong precedence) kwa mwelekeo wa Taifa hili changa kidemokrasia. Mwandishi alitahadharisha eti kama tutafuata mkondo wa kisheria basi itatugharimu sana kuwapata mafisadi ambao watakimbilia ughaibuni. Hili si kweli kabisa: moja, mfano jirani zetu Kenya kumekuwa na kashfa kubwa kama ile ya Anglo Leasing ambapo mabilioni ya dola yalichotwa kama EPA.

Baada ya watuhumiwa kujulikana hasa vigogo, tumeona serikali kama za Marekani na hata Uingereza zikiwanyima hata visa (hati za kusafiri na kuzuru nchi zao). Matokeo yake baadhi ya vigogo wa serikali ya Kibaki hawaruhusiwi kuitembelea Marekani. Mbili, sisi hapa hata kuwataja tunaogopa na hii inawaruhusu wawe huru kutoroka huko ambako Bw. Tambwe anakohofu itatugharimu kuwapata. Usiri huu kwa nia ya kubembelezana wahalifu nadhani ndio utakaotugharimu zaidi kuliko tungeamua kukazia kwenye mkondo wa kisheria.

Tatu, mwandishi wa makala ile alidai kuwa: “Binafsi nitafurahi endapo rais atashauriwa kusaini ‘Presidential Decree’ ya kuwasamehe waliorejesha fedha na watakaozirejesha”. Hii inanirejesha pale awali niliposema juu ya ‘wrong precedence’. Kama kweli ndio mawazo ya serikali yetu basi ni kusema kuwa Taifa letu limetupwa kwa mambwa. (thrown to the dogs). Ni kielelezo tosha cha tatizo la kielimu na kifikra miongoni mwa watanzania walio wengi hasa katika nyadhifa za juu. Haingii akilini eti watu Flani wanachukua kiasi cha fedha cha Taifa na kuzifanyia biashara zao alafu uchumi wan chi unaathirika vibaya hasa thamani ya shilingi yake nab ado kuna watu wana mawazo eti tuwasamehe na kuwapa upendeleo Fulani dhidi ya mkono wa sheria.

Ni wazi woga wote huu wa serikali katika kupambana na hili ni kwasababu tu Taifa letu limejaa mafisadi wa hali ya juu. Watu wasioshikika kirahisi wenye mitandao hadi ikulu na hata katika idara zote nyeti za nchi. Kule Urusi ya Putin wanawaita hawa watu ni “Oligarchy”. Ni watu wenye hila, wasio na huruma na maisha ya binadamu wenzao hata kidogo. Kwa kawaida hawa wanalindwa na dola katika ufisadi wao. Hawa hukamatwa tu pale ambapo wameamua kuwa maadui wa dola kwa kuanzisha harakati dhidi ya dola. Na ndio maana watu kama “Khodokosky” yule tajiri wa kampuni ya mafuta ya ‘Yukos’ anaozea jela baada ya kuanza kumpinga Putin.

Hapa kwetu kile anachotetea Bw. Tambwe ni katika kuendeleza mfumo wa kioligarchy kama ilivyo kule Urusi. Kama alivyokiri mwenyewe hajatumwa na mtu; lakini kama mtu una akili inayojali kuwajibika kimaadili kwa kila utendalo basi kwa Bw. Tambwe nadhani kwake maadili si hoja maadam hela zinarudi zote. Hivi kuna maana gani kuwa na Taifa ambalo watu ama viongozi wake wanakuwa huru kuiba fedha na baadae kuzirudisha baada ya kuzitumia kwa matumizi yao binafsi? Tena wanazirudisha wakati zimeshapoteza thamani ya kipindi walipozichota alafu tunasema hela imerudi.

Alafu pia tunajenga Taifa ambalo viongozi wake hawana mfumo maalum wa kitabia katika ofisi za umma (code of conduct). Ni hatari manake ni lazima tuwe na taratibu za kisheria za kuadhibu makosa na wala si kubembelezana.

Ningependa pia nipinge mifano kadhaa ambayo Bw. Tambwe aliitoa katika kuhimiza hoja zake; na hasa ni juu ya jinsi kule Kenya mfumo wa kisheria ulivyoachwa na mazungumzo yakaleta faraja. Naamini kama tunafananisha na Kenya kwa hili la BoT basi ile naiona kama mfanano usio sahihi (wrong analogy). Labda tu nimkumbushe Bw. Tambwe kuwa kwa Kenya bado ni mapema sana kudhani kuwa siasa za Kenya zitatulia. Kuna suala moja nyeti sana wakenya wameliacha nalo ni Haki (justice). Ni usanii tu pale kwani haiwezekani mtu ashinde kwa kuiba kura alafu wafanye kazi pamoja na aliyeibiwa kirahisi. Ni usanii tu; kwani siamini kuwa miaka mitano serikali hii ya Muungano (grand coalition) itadumu. Kuna tofauti za kimsingi kati ya ODM na PNU ambazo bila kuzingatia haki haziwezi kusawazishwa.

Ni katika mfanano huo wa Kenya ambao siamini unatufaa katika hili la EPA. Masuala ya kimaadili hayawezi kutatuliwa kwa kisiasa; haya ni mambo yenye kuathiri uchumi na maendeleo ya nchi na kama tunafanya makubaliano na hawa maoligarchy wa kitanzania basi ni kutangaza Tanzania kama Taifa la viongozi kuwa huru kuiba kwani watarudisha. Kwa mtizamo wa Bw. Tambwe, kitaalamu ni kuwa hii ni nchi ya ustahimivu wa maovu wa hali ya juu (highest impunity) kwa watawala.

Mawazo ya Bw. Tambwe yalikuwa ni mazuri kusikiliza na kihisia (emotionally) lakini unapoyaingiza ndani ya ubongo ni ya hatari kwani ni kweli fedha zitarudi lakini ndio utakuwa ni mwanzo wa kuwaruhusu watawala kutumia ofisi za umma kuiba bila kushtakiwa kwani wanarudisha. Na kwa mantiki hiyo, serikali itatumika kama mkopeshaji bila riba kwa vigogo kama ilivyokwisha jionesha kwani pesa zinarudishwa bila riba. Hii ni hasara kwa nchi; na i ikiachwa iendelee basi zitaibiwa nyingi sana kitu ambacho ni hatari sana.

Mwisho niseme ni vyema tukumbuke kila mtu ana haki ya kutoa maoni ila tukae chini tufikiri kwa mapana kimantiki na si kihisia kabla hatujazungumza. Nalisema hili kwani umasikini mkubwa unaoikumba Tanzania na hata Afrika ni kwasababu tumegeuka kuwa watu wa mashiko ya kihisia zaidi kuliko kufikiri. Tanzania ya leo hakuna tofauti ya kimawazo kati ya msomi wa hadhi ya mwanasheria mkuu dhidi ya msomi wa elimu ya msingi linapokuja suala la kuwajibika na kutoa mawazo ya kifikra yanayohitaji kufikiri hasa.

Kwani wenye mawazo kama haya ya Tambwe basi kuna tatizo la ubinafsi hasa pale mtu anapochagua hatua ambazo hazitamuumiza panapohitaji kuwajibika. Kimaadili tunasema ni ‘ethical relativism’. Kuepukana na hili zinahitajika bongo kufanya kazi kwelikweli. Na kwasababu kwa Tanzania hili ni tatizo kubwa basi ufisadi na mafisadi wataendelea kutesa hasa.

Saturday, March 08, 2008

SIKU YA AKINA MAMA TANZANIA

Ni siku ya wanawake duniani; na hatuna budi kutafakari.

Ulimwengu wa leo umejaa “ngano” nyingi sana ambazo kwa kiasi kikubwa ni chanzo cha tamaduni na ustaarabu usio makini miongoni mwa waafrika na hasa watanzania kwa ujumla wetu. Katika siku hii ya wanawake duniani, nasema hivi huku nikijiuliza bila majibu maswali kadhaa:

Mosi, hivi siku hii ya wanawake duniani ni changamoto zipi tulizonazo kama watanzania? Kwangu nadhani ni wakati muafaka kwa jamii ya wanawake kujiuliza hivi ni kwa vipi bado wanaishi katika “ngano”: yaani bado kuamini wao si bora zaidi ya wanaume? Badala yake mwelekeo wa uongozi wa nchi hii umebakia na wanawake wasindikizaji, yaani wanaoridhika na vyeo tu. (sycophants). Hawa hawana hoja mbadala kwa bwana mkubwa; na ndio maana katika hii dhahama yote ya ufisadi (ufisadizesheni) iliyoikumba nchi yetu hakuna wanawake hasa wasomi wakionesha hisia zao kimaandishi ama kimdomo.

Pili, ni wakati akina mama kujiuliza hivi ni lini wataamua kukataa kutumiwa kama chombo cha kustarehesha (enticing object)? Hili naliona kwani ni ukweli halisi kuwa ufisadi mwingi nchini Tanzania unachangiwa sana na tamaa ya akina baba wengi kutamani mafedha katika kile kuwaridhisha wapenzi ama wake wao waishi raha mustarehe. Ni wakati akina mama waamue la sivyo ufisadi hautakwisha.

Tatu, kuna huu upendeleo maalum kuwainua wanawake (affirmative action): nakumbuka tamko la Beijing (Platform for Action) ilihimiza kuwainua wanawake katika nyadhifa za kiuongozi dhidi ya mfumo dume (partriarchy). Kwa Tanzania nadhani rais Jakaya Kikwete katimiza hili. Ila nadhani kaenda mbali sana manake kuna wanawake wengi tu nchini mwetu wana nyadhifa zisizolingana na kiwango cha elimu walichonacho na wanapwaya sana pale mambo yanayohitaji mtu atumie bongo hasahasa. Hili nalisema wazi kuwa nadhani upendeleo maalum naukubali lakini usitumiwe kama zawadi kwa mtu ama ahsante kama tunavyoshuhudia kwa sasa.

Kwa Tanzania, nimeshangazwa sana kuona bunge letu limejaa hawa wabunge wa viti maalum ambao wengine hata elimu ya sekondari hawana ama wameishia kidato cha nne na vikozi kama vya vyeti vya utunzaji ofisi (secretary). Siamini kabisa katika ulimwengu wa leo, mbunge wa aina hii anaweza kutoa mijadala ya kimantiki katika kujenga nchi yetu; wengi wao hawajui hata sera za kiuchumi za nchi zikoje ama hata mpangilio wa kidunia ukoje (World Order). Ni katika mtizamo wa aina hii hata hizi kashfa kama za Richmond, EPA – BoT na zingine nyingi zimetufikisha hapa tulipo leo bila kuhojiwa huko Bungeni. Ni wazi wabunge wengi wa viti maalum ni mzigo kwa walipa kodi wa nchi hii.

Tufike pahali tukomeshe huu mfumo wa uwakilishi wa viti maalum. Ikibidi tuige nchi kama Uganda kwa mfano, wabunge wanawake wote ni lazima wagombee na wapigiwe kura na wananchi na si kama hapa kwetu ambapo mara nyingi njia chafu kama rushwa za kila aina mara nyingine hata za ngono zinatumika miongoni mwa vigogo wa vyama vya siasa ili mabibi warembo fulani wawe wabunge. Pia hata Kenya hivi majuzi tumeona ni jinsi gani wanawake wamejikakamua kuhakikisha wanagombea na wanaume na kushindana kwa hoja badala ya kusubiri kuhonga kamati za chama / vyama ili vikupitishe kupitia vitandani na hongo nyingine nyingi za kila aina hasa za aibu.

Nne, tukiacha mambo ya mustakabali wa nchi yetu kisiasa, pia kifamilia tayari tujiulize mambo kadhaa: mojawapo ni hili la wanawake kujikomboa katika mtizamo wa kujilinganisha na wanaume ukiachilia mbali tofauti za kimaumbile (anatomy) na hata kimajukumu (roles). Katika hili kundi (radical feminists) naliona kama hatari sana katika Tanzania ya leo. Hawa ni wale wanawake wasomi kabisa na kwa mantiki hiyo ubinafsi umewajaa kwa kiwango kikubwa (highest ego) na matokeo yake hawawezi kudumu katika ndoa ama hata kama wanadumu wanaishi katika ndoa zilizofeli (failed marriages). Hawa ndio walioshindwa kuwa mifano bora kwa jamii; na wengi wana nafasi kubwa katika jamii wakibadilisha wanaume – vigogo kama njugu ili kuhakikisha wanaishi raha mustarehe. Wengi wao wanaishi wakiwa wamechanganyikiwa (frustrated).

Nimalizie kwa kumbushia nasaha za wanafalsafa wawili: mmoja ni Jeremy Benthamy, ambaye alikataa kata kata kuwa hatambui nafasi yeyote ya mwanamke katika jamii. Alisema: “Wife should submit to husband”, yaani mke shuruti awe chini ya utawala wa mume. Wako wanawake wengi ambao bado wana hisia za bwana huyu na ndio maana wamewafanya wanaume ni miradi yao. Mwanafalsafa wa pili ni John Stuart Mills, yeye anajulikana kama “Male feminist” yaani mwanaume – mke. Alipinga mwanamke kunyanyaswa kabisa. Alishawishi sana kwa wanawake kuruhusiwa kupiga kura nchini Uingereza wakati wa maisha yake. Tunaweza kurejea pale alipoandika juu ya mke wake – Harriet Taylor.

Basi siku hii ya leo itufanye hasa kwa wale wanawake kufuata mawazo ya wanafalsafa hawa wawili kwa kuchagua mmoja. Kazi kwenu sijui mtachagua yupi kwani tukikosea tuataendelea kuishi maisha yaliyojaa hisia na imani potofu za kijinsia (stereotypes). Tufike pahali wanawake waamue kikwelikweli na si kimzaha mzaha kushiriki katika nyanja mbalimbali za maisha nchini Tanzania na kuachana na kuishi kwa unafiki ilimradi wanapata upendeleo kuwawezesha kupata mkate wa kila siku. Nashangazwa sana hadi leo bado wanawake wengi sana nchini mwetu na Afrika kwa ujumla wako tayari kujidhalilisha ilimradi wapate vyeo, upendeleo, na raha za kila aina kutoka kwa wanaume.

Ni katika mtizamo huu; bado wanawake wa Tanzania bado wako kizani hasa kama wanafikiri wameshajikomboa. Manake hata wengi wa wanaharakati si mfano bora kimaadili linapokuja swali la mahusiano bora ya kijinsia. Tujiulize je siku ya wanawake imetusaidia kubadili mwelekeo wetu? Au ni usanii kama kawaida?

Wednesday, February 27, 2008

ZIARA YA BUSH—NA UFISADI WA FIKRA ZETU

Mwezi wa februari utabakia wa kukumbukwa kwangu binafsi kwa matukio kadhaa ya kukumbukwa. Kwanza, tarehe ya pili tu nilimpoteza bibi yangu, Emilia aliyefariki akiwa na umri wa miaka tisini na sita (96). Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi. Tarehe saba wakati nikiwa nimesimama pembeni ya jeneza la bibi siku ya mazishi, ndugu yangu mmoja ananiuma sikio kuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa amejiuzulu.

Ukiacha hayo mawili, lingine ambalo kwangu naliona la kukumbuka ni ziara ya Rais George Bush nchini Tanzania. Imenishangaza sana huyu bwana kapata mapokezi makubwa sana barani Afrika kitu ambacho ni tofauti katika mabara mengine ambapo anachukiwa sana. Kwangu nadhani ina mafunzo mengi sana kwetu kama wananchi na hasa kwa viongozi wetu. Labda niseme pia siungi mkono hata kidogo kelele na pingamizi nyingi ambazo zilioneshwa na baadhi ya watanzania—waislamu wachache na jumuiya ya wasomi wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam. Nasema hivi kwani siamini kabisa kuwa rais Bush anazo sera zake binafsi ila kila kinachofanywa na serikali ya Bush ni matokeo ya sera ya nje ya serikali ya Marekani ikihanikizwa na imani za kihafidhina za Chama cha Republican.

Tatu, sijui kama Magaidi wasingeivamia Marekani September kumi na moja kama kweli leo majeshi ya Marekani yangekuwa Iraq na Afghanistan. Lakini pia sijui kama kweli kuna njia gani ya mazungumzo ingetumika kuleta mabadiliko ya kiutawala ya kidhalimu chini ya Matalebani ama Saddam Hussein. Si kura hata kidogo ingeumaliza udikteta wa Saddam ila kujitoa mhanga wa maisha ya watu—yaani damu kumwagika ili kuleta mabadiliko kutoka mfumo dhalimu. Kama hatutaki kuamini hivyo, basi tuangalie Kenya kama itatulia iwapo Kibaki atakuwa rais kwa miaka mitano ijayo. Kuna nyakati vita haiepukiki ili kuleta mabadiliko kwani hata nchi yetu ilibidi ipigane vita kumng’oa Iddi Amin ili kuung’oa udikteta wa Amin Uganda.

Kwa kuzingatia mwelekeo wa uchumi wa kileo duniani, na hata kihistoria, Taifa kubwa limejiimarisha kwa njia nyingi mojawapo ikiwa ni vita. Hivyo basi, Bush si wa kwanza kuendesha vita. Hata Nyerere aliendesha vita kwa maslahi ya nchi yake (Tanzania) kitu ambacho anafanya Bush. Hivyo basi, kumkataa Bush asitembelee nchi yetu si hoja yenye mashiko sana kiuhalisia leo hii; kwani kama asingekuja na hata alivyokuja, hakuna kitu amepoteza. Nguvu ya kujieneza ya Taifa kubwa kama Marekani haizuiliki; hivyo basi kimtizamo kelele za pale Mlimani zilikuwa zimejaa mantiki ya kitaaluma ambayo kwangu sina hoja kupinga uhalali wake kimaadili na katika suala zima la uadilifu unaotakikana kwa mwanadamu.

Lakini katika hali halisi ya dunia si hoja muafaka manake inaonekana maisha ya mwanadamu na mtanzania wa leo yamejaa matendo mengi ambayo si ya kimaadili lakini ndiyo yamefanywa haswa kama utamaduni. Hata Raisi Kikwete alimwambia Bush kuwa kwetu watanzania hatuana shida nae japo zipo serikali nyingine ambazo zina mitizamo tofauti na sera zake.

Kwa maana nyingine mtanzania anaongozwa na mbinu nyingi za kifisadi kufikia malengo yake; na ndio maana ziara ya Bush ilikuwa ya mapokezi mazuri sana sidhani kama amewahi kufanyiwa hivyo ugenini hata siku moja. Tanzania ni Taifa linalojiendesha kifisadi fisadi sana na ndio maana ni wananchi wachache sana waliokuwa na muda wa kutafakari hoja za wasomi wetu kule Mlimani. Watanzania na serikali yao hawajali jambo fulani linapatikana kwa njia gani ilimradi tu lina tija katika kutatua matatizo yao. Ni nchi ambayo kama kweli una elimu yako nzuri na ya juu kama vile Dr. Msabaha alivyofanya kwenye skandali ya Richmond, lazima uachane na kile unachokiamini ndio sahihi na ufuate matakwa ya utawala. Labda nieleze ni kwanini watanzania na serikali yao hawakuona haja ya kusikiliza busara za kisomi:

Moja, ziara hii imetoa msaada mkubwa kwa nchi yetu katika sekta ya afya na miundombinu. Japo nina mashaka na mafisadi hawataziacha salama, ila ni kielelezo kuwa Bush ana nia njema na nchi yetu. Na katika kutia shime vita dhidi ya ufisadi, Bush alisema baada ya kusaini mkataba kuwa fedha za Marekani si kwa mafisadi. Na kusisitiza kuwa moja ya masharti ya Mfuko wa Millenia ni serikali yetu kuzingatia “Utawala Bora”, vita dhidi ya ufisadi na kwa ujumla serikali inayojali watu wake.

Pili, ziara hii imeonesha ni jinsi gani Raisi Bush na mkewe walivyo watu wa kujitolea (compassionate)hata huruma ya kujali watu wa kawaida. Kwa viongozi wetu wamejifunza ni jinsi gani wanapaswa kuishi na kujichanganya na watu hohehahe kama walivyo watanzania wengi. Viongozi wetu wengi wa Afrika, kwa mfano, si rahisi mtu atembelee hospitali na umwone akikumbatiana na kukaa karibu kabisa kwa kujichanganya na wagonjwa. Hili Bush katoa funzo; nilitegemea kule hospitali ya Mount Meru nione makachero wakiwa karibu na Raisi wakimwongoza wapi apite na ashikane na nani mkono au hata kuwazuia watu wasimkaribie bwana mkubwa. Hili sikuliona ila niliona Raisi Bush akijiweka sawa na binadamu wengine na kukaa hata karibu nao kabisa, wala si kwenye kiti maalum bali viti vya kawaida wanavyokalia wagonjwa kwenye foleni. Wakubwa wetu watataka sofa maalum tofauti na walalahoi.

Kimavazi pia imekuwa ni funzo kwa viongozi na vigogo wetu. Unakwenda kuwatembelea watu masikini ni lazima angalau ufanane nao. Kwa Bush hili alilizingatia hasa na wala sikuona akiwa ndani ya suti, siku ile yenye joto ambalo lingemfanya achemke kwa joto na aogope kujichanganya. Nadhani ndio maana kulikuwa hamna haja ya wanausalama kumzuia kuwa karibu na watu kwani vigogo wetu inabidi makachero kuzuia watu ili bwana mkubwa apate hewa kwani mara nyingi unakuta watu wamevaa misuti. Hapa katukumbusha mavazi rahisi (simplistic). Hili nalo ni funzo gumu kwa vigogo wa kiafrika kulimeza.

Wakati akiitembelea shule ya sekondari maalum kwa wasichana wa kimasai kutoka mazingira magumu alinigusa hasa. Labda niseme mwaka jana Raisi Jakaya Kikwete alifungua shule moja ya sekondari kule Moshi. Ilikuwa ni ziara ya saa moja kufungua shule rasmi; na mara alipowasili pale shuleni si walimu wala wanafunzi waliopata muda wa kumfariji na kumpokea rais wao. Kilichotokea nilishangaa kuona makada kibao wa CCM pamoja na vigogo wa serikali kutoka mkoani na wilaya za jirani wakihangaika kugombania kujipanga mstari ili tu kushikana mkono na bwana mkubwa. Walimu waliokuwa wamejipanga sehemu maalum walifunikwa na wala hawakuweza kupata nafasi hiyo. Wala raisi hakuwa na muda wa kusalimiana ama kuzungumza sana na wanafunzi zaidi ya kupiga kejeli za kisiasa katika hotuba yake. Nadhani angeteta na wanafunzi kadhaa na kusikia hisia zao ingependeza zaidi.

Lakini kwa Bush tumeoneshwa nini maana ya kuwa kiongozi na nini cha kujali wakati unapotembelea sehemu. Raisi Bush alisalimiana na watoto wote wa shule ile pale Arusha; pia alisalimiana na hata kucheza ngoma na wamasai waliokuwa wakiburudisha ikiwa ni pamoja na kuwakumbatia baadhi yao. Hapa kwetu na Afrika kwa ujumla sivyo inavyokuwa, wanausalama hawaruhusu hili kabisa. Hivi huwa najiuliza kila Rais wetu anapokuwa mahali utaona mlinzi wake/ msaidizi wake kasimama nyuma. Hivi hiyo ndio kumaanisha ulinzi wa rais ni imara? Mbona watu kama akina Bush si hivyo na ulinzi ni imara? Nadhani ziara hii iwe mwanzo wa kuiga jambo kwa wanausalama na kwa ujumla wale watu wa karibu wa bwana mkubwa.

Labda niungane na waziri Dr. Jumanne Maghembe aliponukuliwa na ITV katika ziara ya Bush kule Arusha: “Marekani ni Taifa kubwa na tajiri na lina fursa nyingi. Ni vizuri tukashirikiana nayo na kudumisha urafiki na udugu na Taifa hili”. Nikiwarudia wale walionesha kutokutaka ziara hii: Hasa wasomi wa Mlimani, wajameni hivi tunajua kuwa wahenga waliwahi kusema kwa kiingereza tafsiri isiyo rasmi: “Every black has its white”, kuwa kila cheusi kina weupe wake pia”. Hapa namaanisha pamoja na uovu na unyama unaoambatanishwa na haiba ya Raisi George Bush, huyu ni mwanadamu mwenye pande mbili. Na kwa kutilia mkazo kwenu mabaya yake naamini mlighafilika tu; na mashiko ya kihisia yalitawala zaidi ya busara, mbona hamkutizama upande wa pili wa Bush?. La sivyo wala msingefikia hatua hiyo ya kutaka kuandamana.

Ziara ya Bush imetuonesha upande wa pili Bush mwanadamu. Mpaka kaondoka sijasikia akiongelea habari za Africom kama wasomi wetu walivyokazia kuwa anatafuta mahali pa kujenga kambi za kijeshi. Pia nadhani kilio chenu kingine kuwa kumkaribisha Bush ni kuonesha serikali yetu imeamua kuacha marafiki wa zamani na kufuata mabepari kama hatua isiyo muafaka si sahihi. Tumefuata sera za marafiki zetu kama Cuba, China na wengine wengi kwa miongo minne kwa mafanikio sana ya kiuchumi. Dunia ya leo tusiogope sana juu ya hali ya baadaye ila tutumie fursa zinazojitokeza hasa kama zina mwelekeo wa kukuza uchumi wetu.

Tukiwa bado tuna marafiki zetu wa zamani hakuna ubaya kama tunaongeza mwingine bila kuwapoteza wa zamani. Hii ndio hisia ninayoipata kwa ugeni wa Bush. Ziara hii kupitia mkataba wa Millenium Challenge naamini ni fursa ambayo tusingepaswa tuiache kwani ina tija sana hasa kama “mafisadi” watadhibitiwa wasiweke pua zao hapa. Tukumbuke hata jirani yetu Yoweri Museveni alikuwa na uswahiba na Bush na hata enzi za Clinton na kwa sasa wamemtupa kiana na kwa kipindi chote Uganda haikuwahi kuathiriwa kijeshi na Marekani ingawa kwa sasa kuna makampuni kibao ya Marekani yakianza kuchimba mafuta nchini humo.

Funzo lingine la ziara ya Bush kwangu ni pale kung’amua kuwa kweli nchi yetu ni masikini sana. Yaani bado hatuna uwezo wa kujikinga na Malaria? Yaani Bush anatununulia chandarua watanzania? Yaani watanzania walio wengi hawana uwezo wa kununua chandarua? Kwa maana nyingine watanzania wengi tu wachafu hatuwezi kuishi kwenye mazingira safi yasiyoruhusu mbu kuzaliana. Hatujui wajibu wa kiafya kusafisha mazingira yetu ili kuondoa mazalia ya mbu. Ni aibu lakini tufanyeje? Mpaka aje Bush atununulie chandarua. Hili linanipa shida sana kwani nadhani fedha ya malaria ni nyingi na ingefaa itumike kwenye sekta kama ya elimu. Sidhani kama unamzuia mtu asiugue malaria lakini hapo hapo humpi elimu bora kama unamsaidia sana. Bado umasikini hautoki kwa njia hii.

Ukimwi pia ingawa ni janga ambalo binafsi limeniathiri sana; ila ni wakati tujiulize kuwa hivi kama tukiweza kujihadhari na maambukizi, hizi fedha zote za Bush si zingefanya mambo mengine? Napata mashaka sana kama tunaendelea kupata ufadhili hasa wa kurefusha maisha na kwa wakati huo huo hatuna utaratibu wa kuwalinda wale ambao hawajaambukizwa ambao kwa kujichanganya kwao na waathirika wengi ni hatari.Ni wazi waathirika Fulani wana hasira sana na lengo lao kubwa ni kuondoka na wengine. Sisemi hili kwa kunyanyapaa ila ni lazima tufike mahali tujiulize hii misaada mikubwa ya kulinda maisha ya waathirika ina matokeo mazuri? Ni kwa vipi tuifanye tuwe na mazingira mapya kiutaratibu wa maisha ili tupate tija. La sivyo Taifa zima litaangamia na mamilioni ya dola za Bush.

Mwisho, nimalizie kama nilivyoanza: wakati nikiwa pale pembeni ya jeneza la bibi yangu baada tu ya kunong’onezwa na ndugu yangu kuwa Waziri Mkuu kajiuzulu, mara moja nilichoropoka nikaingia ndani nikafungua kiredio changu kidogo, radio sauti ya Ujerumani na nikakutana na sauti yake ikisema: Nimefadhaishwa, nimesononeshwa, …..mengine nimeyasahau manake yalinishangaza kwanini sasa kaamua kujiuzulu. Taifa linapotekwa nyara na mafisadi mtu hushangai pale hata busara za wasomi kama wale wa pale Mlimani zinapoonekana ni kejeli.

Nilisikitika tu pale jeshi la polisi lilipokataa kiaina kutoa ulinzi kwa maandamano ya wasomi wa mlimani kupinga ziara ya Bush. Ingawa sikuwa naunga mkono hoja zao, nadhani walinyimwa haki yao ya msingi kuandamana kupinga ujio wa Bush. Kweli February sitaisahau kama wakati muafaka wa mapinduzi ambayo sina imani sana kama yatabadilisha mwelekeo wa Taifa letu dhidi ya ufisadi. Hii ni nchi inaathiriwa na tabia na hulka ya kubebana, kupendeleana na utapeli wa kila aina. Na ndio maana baada ya Raisi kukabidhiwa ripoti ya Ernst & Young iliyokwishagundua kila ufisadi ndani ya BoT bado anaunda kamati nyingine ya uchunguzi. Lengo ni kulindana tu. Nimeshangazwa pia na mtuhumiwa mmojawapo wa ufisadi karudi kwa wapiga kura wake na kupokewa kwa shangwe na hata kupewa baraka za Askofu wa kanisa lake. Kweli kwa Tanzania ya leo bila ufisadi labda maisha ya wengi yatasimama.

Wednesday, January 30, 2008

KIIZA BESIGYE NA MWAKA 2008

Kiiza Besyige anajulikana sana Uganda. Leo bado ni mwiba mkubwa kwa jeshi la uganda na anadai analijua wazi. Hivi tunajua ilimbidi amwache rafiki wake wa kike ili kujiunga na Museveni msituni na kuacha fani ya udaktari?
Kama unataka kujua madhara ya kupingana na Museveni, basi ona haya yaliyowakumba hawa waliojaribu.

MLIMA KILIMANJARO



Hii ndio Moshi, unauona mlima Kilimanjaro? Wanadai eti karibu theluji yake itakwisha. Ndivyo unavyoonekana leo hii.