My Blog List

Wednesday, August 15, 2007

VITA YA MAFUTA CONGO DRC--UGANDA?

Unajua vita ya mafuta inakaribia kuanza kati ya Uganda na Kongo-DRC?Je Uganda itaweza kupigana vita nyingine na huku pia ikipimwa kama ni dola iliyofeli?(failed state)
Kama ni kweli mafuta ni chanzo cha ugomvi na Kongo, je ni nini nafasi ya Uganda katika biashara ya mafuta barani Afrika.
Ni lazima watu tutambue kuwa Ituri ni eneo lenye utajiri wenye balaa sana kwani ni chanzo cha mgogoro wa sasa kati ya nchi hizi mbili.

Saturday, August 11, 2007

SHIRIKISHO LA AFRICA MASHARIKI-- SI HATUA MUAFAKA

Leo nigusie tena juu ya hii jumuiya yetu ya Africa Mashariki (EAC) ambayo watanzania wengi wameikataa kwa kutoa maoni yao kwa tume ya Profesa Wangwe. Nianze kwa kuwafananisha wote wenye ndoto ya kuundwa ama kuharakisha (Fast Tracking) uundaji wa Shirikisho la Africa Mashariki (EAF) hawana tofauti na wapigania haki wa uhuru watanguliziwa bara la Afrika ambao ndoto yao ya Shirikisho la Afrika mpaka leo ni kiinimacho.

Baadhi ya wanaofuatilia mtizamo wangu ni wazi nimekuwa napinga Shirikisho la Afrika Mashariki ila nikiunganga mkono hatua ya Jumuiya tu kwani naamini Shirikisho la Afrika Mashariki itakuwa ni hatua ya kisiasa isiyokuwa na manufaa yeyote kwa mwanachi wa kawaida.

Mmoja wa watu wanaotaka Shirikisho la Afrika Mashariki liharakishwe ni Yoweri Kaguta Museveni--Rais wa Uganda. Aliweza hata kubadili katiba ya Uganda kwa kuwahonga wabunge Shilingi Millioni Tano za Uganda (chini ya shilingi milioni tano za Tanzania) kila mmoja ili tu wapitishe mabadiliko ya kuondoa "ukomo" wa vipindi viwili vya miaka mitano mitano cha mtu kuwa rais wa nchi. Lengo inasemekana na wachunguzi wengi wa siasa za Uganda likiwa ni ili aendelee kuwa madarakani hadi pale mchakato mzima wa Shirikisho utakapowadia ambapo ataweza kuwa Rais wa kwanza wa Shirikisho la Afrika Mashariki ifikapo 2013.

Museveni anaamini Shirikisho ndio njia pekee iliyobakia kutuletea umoja Afrika Mashariki; anafikiri ni rahisi namna hiyo; mwenyewa kwa miaka ishirini na ushehe sasa ameshindwa kuinganisha Uganda sijui Afrika Mashariki itawezekanaje. Hapa pananipa utata sana manake viongozi (wanasiasa) wetu kuna nyakati wanafanya mambo kikondoo sana. Hebu nivute hisia nikumbushe historia ya bara letu la Afrika, ambapo ndoto za waanzilishi wake za kuunda Shirikisho la Kisiasa mpaka leo zimebakia katika vitabu vya historia tu kwa visababu ambavyo hapa kwetu Afrika Mashariki navyo vipo pia.

Moja, mwaka 1958, Osagyefo Kwame Nkrumah alifanya juhudi sana kuinganisha Afrika kwa kuanzia na Ghana na Guinea, ikafuatiwa na Ghana-Guinea-Mali ambazo zote hazikudumu. Pili, kukaja Shirikisho la Senegambia kati ya mwaka 1981 na 1989. Zote hizi hazikudumu sana wala kuweza kusimama; kwa ujumla mashirikisho ya kisiasa yaliyojaribiwa katika karne iliyopita hayakufanikiwa pia si tu Afrika bali hata sehemu nyingine za ulimwengu na mifano ipo mingi: kwa mfano, Shirikisho la India Magharibi (West Indies Federation) kati ya mwaka 1952 hadi 1962.

Nyingine ikawa ni Shirikisho la Kijamaa la Mataifa ya Kiarabu (Federation of Socialist Arab States) kati ya mwaka 1972 hadi 1977 ambapo msisitizo ulikuwa wa kizalendo yaani Pan Arabinism; alafu likawepo lile shirikisho la Yugoslavia kati ya mwaka 1945 hadi 1992; na mfano wa mwisho kabisa ni lile shirikisho kubwa kubwa kabisa la kisiasa wakati wa vita baridi la Urusi ( Union of Socialist States of Russia) la mwaka 1922 hadi 1991.

Unaweza kuona mashirikisho niliyoyataja hapo juu yalianza na kufa kwa sababu mbalimbali ambazo pia zipo hapa Afrika Mashariki. Lakini pia mtu anaweza kujiuliza mbona yapo mashirikisho ya kisiasa ambayo bado wamo na yanaendelea? kwa mfano, Shirikisho la Nigeria lenye watu takriban millioni mia moja na kumi (110) au lile la Ethiopia lenye wakazi takriban milioni sabini na nane (78). Kama kweli Mashirikisho haya mawili ya kiafrika yana tija hasa kwa wananchi wa kawaida ni kwanini basi nchi zote hizi mbili bado ziko katika kundi la nchi zinazoendelea na si nchi zilizoendelea?

Hii ni sababu inayonifanya mimi kutokuunga mkono wazo la Shirikisho la Kisiasa la Afrika Mashariki. Nikihakikishiwa ni dawa ya kutuondoa kutoka katika nchi zinazoendelea, au zile masikini sana ulimwenguni (LDCs) basi nitaunga mkono; ila kwa hali ya sasa nafikiri shirikisho halina maslahi makini ukiacha matakwa binafsi ya wachache.

Nimejaribu kutizama pia lile shirikisho ambalo nadhani ni mfano wa mafanikio ulimwenguni, nalo ni ule Muungano wa Mataifa ya Amerika ( United States of America) ambalo kisiasa ni mfano wa kuigwa kimafanikio. Je hiki ni kielelezo cha Shirikisho la Afrika Mashariki kufikiwa? Mimi sioni kama ni kweli kabisa: nikumbushe kihistoria ilihitajika takriban miaka mia moja (100)--1776 hadi 1865 pamoja na vita kali na kubwa ya kiraia ya mwaka 1861 hadi 1865 ndipo Marekani ikakomaa na kuweza hata kustawi kama taifa lenye nguvu kabisa ulimwenguni.

Ni wazi kuundwa kwa Shirikisho sio mchakato wa kuharakishwa kama akina Museveni, Kibaki na Kikwete wanavyotaka. Kuna mambo mengi ya kuzingatia hasa ukiangalia EAC ni jumuiya yenye nchi zenye historia ya kupiganapigana katika kila jambo la kisiasa.

Labda nisisitize kuwa si Marekani tu ambapo mambo hayakuwa rahisi kama vile maraisi wetu wanavyotaka tuharakishe kufikia Shirikisho. Niwapeleke katika jumuiya ya Ulaya--(European Union). Kuanzia juhudi za mwanzo kabisa pale uliposainiwa mkataba wa Roma- 1957, kuanzisha Jumuiya ambayo mpaka leo mchakato wa kuunda Shirikisho la Kisiasa umebaki kiini macho. Mwaka juzi tu wanachi wa Ufaransa na Uholanzi walikataa kuunga mkono Katiba mpya ya Jumuiya ya Ulaya kwenye kura ya maoni, ambapo lilikuwa ni pigo katika kukwamisha mchakato mzima wa kufikia Shirikisho la Kisiasa. Tunaweza kuona ni miaka zaidi ya hamsini sasa Ulaya inashindwa kuunda Shirikisho la Kisiasa.

Mambo yote haya niliyoyataja yananifanya niamini kuwa muungano ya kiuchumi ni hatua muafaka ambayo itatufaidisha kiuchumi baada ya kipindi fulani. Nionavyo, Shirikisho la Kisiasa halitaweza kwa jinsi yeyote kuleta faida yeyote kwa mwananchi wa kawaida zaidi ya kuwafaidisha wanasiasa wetu. Wanasiasa wetu waache mawazo eti ile kuwa tu na idadi kubwa ya watu basi utakuwa na soko kubwa ambayo ni kielelezo cha nguvu za kiuchumi. Kwa Jumuiya yetu kweli soko litakuwa kubwa ila ni dhaifu sana kiuchumi; ni soko la wateja wengi ila ni masikini sana na ndio hapa nadhani zifanyike juhudi kuendeleza wananchi kielimu na kiuchumi hasa kiujasiriamali (entreprenuership) ndipo tutegemee soko lenye tija. Kinyume chake, hii "uharakishaji" ni usanii mwingine wa watawala kama walivyowahi kujaribu hapo nyuma na kutofanikiwa.

Mwisho ni vyema tuangalie historia ya mashirikisho ya kisiasa katika sehemu kadhaa za dunia ili tuweze kung'amu tufanye nini katika juhudi zetu za kujumuika kimataifa; lisiwe suala la kuharakisha bila kujiuliza je ni kwa maslahi ya nani? Je watawala wanawaza juu ya mwananchi wa kawaida katika jumuiya? Mimi nashangazwa sana na hili zoezi la kukusanya maoni juu ya Shirikisho kufanyika wakati tayari wameshatia saini kuruhusu "kuharakisha mchakato" mzima wa kuunda Shirikisho. Zoezi zima la kukusanya maoni naamini ilikuwa ni ufujaji wa fedha kwani viongozi wetu walishaamua jambo walilotaka kutuuliza; sasa sijue kwanini wanakusanya maoni kwa kitu walichokwisha kitolea maamuzi. Ama kweli tusipokuwa makini tutaburuzwa bila kutafakari.

Namaliza nikisema: "Shirikisho si hatua muafaka"; ila Jumuiya inahitajika kwa sasa yaani mambo ya sarafu moja, umoja wa forodha ni mambo ya msingi yatakayotusaidia kuendeleza wananchi wetu kwa miongo kadhaa labda na ndipo tufikiri Shirikisho tutakapokomaa vya kutosha.

UMOJA WA AFRIKA--USA NI NDOTO NYINGINE ZA ALINACHA

Mwaka 1963, tarehe 25, mwezi Mei, Umoja wa Nchi Huru za Afrika (OAU) ulianzishwa rasmi chini ya hekima za muasisi mkuu Asagyefo Kwame Nkrumah. Lengo lake lilikuwa ni kulifanya bara la Afrika kama nchi moja kubwa ambayo aliamini itakuwa na nguvu ulimwenguni dhidi ya hujuma zozote za mabeberu. Julius Kambarage Nyerere, 'mchonga meno' alimpinga vilivyoo kwa hoja yake ya miungano ya kimkoa (regional blocks).

Leo hii, karibu miongo mitano, bado tuko palepale hatujaweza kuamua tufuate hoja ya Asgyefo au Julius. Mwaka 2002, October 15, ikiwa ni miaka 38 ya OAU, viongozi wetu walikutana Durban, Afrika Kusini na kuunda Umoja wa Afrika (AU) mbadala wa OAU. Ilikuwa ni hatua moja mbele kuongeza nguvu za kisiasa na kiuchumi kama hatua moja kuelekea muungano kamili. Mapema mwezi Julai, viongozi wetu wamekutana Accra-Ghana ili sasa waunde Shirikisho la Afrika. Raisi wa Libya akawa kinara na kuivalia njuga hoja ya Nkrumah kuunda Shirikisho la kisiasa (USA).

Mkutano wa maraisi wa Afrika kule Accra unezua tofauti na hali ya sintofahamu sana baina ya viongozi wetu. Kwa mfano, raisi Muammar Ghadafi alikazia sana kuwa shirikisho liharakishwe; yaani, kuanzishwa kwa wizara ya mambo ya nje na ulinzi ifikapo January 2008. Hali hii haikuwapendeza viongoz wengine wengi: Moja, raisi Umaru Yar'Adua alipinga hali ya kuharakisha na akaungana na Nyerere kwenye hoja ya "Mashirikiano ya Kimkoa"(regional blocks).

Mwishoni mwa mkutano ule, ni wazi ilijionesha wazi kuwa Umoja wa Afrika (AU) tulionao umefeli kabisa. Raisi wa kamisheni ya AU, Alpha Oumar Konare wa Mali alikiri kuwa ni chombo kisichokuwa na nguvu kabisa. Alisema lengo ni kufikia shirikisho ila 'mpango barabara' (road map) ya kufikia hapo ni kuwa tumechanganyikiwa na hatujui tufanye nini.

Je tumuenzi Julius Nyerere au Kwame Nkrumah? Hadi sasa wazo la Nyerere linaungwa mkono na wengi wa viongozi waliokutana kule Ghana.

YAWEZEKANA RAISI KIKWETE NI MWOGA!


Kama sijakosea Raisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni mwoga katika kuwachukulia hatua watendaji kadhaa pale panapotokea tuhuma zenye kustahili mtu kuadhibiwa. Hii kusema bei ya mafuta kushindwa kudhibitiwa na serikali ni udhaifu wa Ewura kunanitia wasiwasi sana, kwani raisi anajaribu kutupa mpira. Ninahisi wauza mafuta ni kundi linaloendesha mambo kimafia mafia hivi na lina uswahiba na baadhi ya vigogo wenye nguvu (untouchables).

Serikali inaogopa kuwagusa na inarusha mpira kwa Ewura iwashughulikie situ ambacho nadhani Ewura hawataweza. Kuna uwezekano serikali yetu imeshanunuliwa na hawa mafia wa mafuta ndio maana wanaogopwa na wanajipangia bei watakavyo. Kama sivyo, basi serikali ijaribu kufanya yale iliyofanyiwa Shirika la ndege la Uingereza wiki hii kwa kupigwa faini dhidi ya kupanga bei ghali kuwanyanyasa wasafiri. Nitaeleza juu ya muono wangu huu wa labda raisi wetu ni mwoga mwishoni mwa waraka wangu wa leo; ila kwanza nigusie hisia zangu kadhaa pale nilipobahatika kumuuliza Raisi Kikwete maswali mawili wakati akihojiwa na shirika la utangazaji la VOA la Marekani hivi majuzi.

Kwa miaka sita sasa nimekuwa mfuatiliaji wa kipindi cha mahojiano cha redio na televisheni "Straight Talk Africa" kinachorushwa na shirika la utangazaji la Sauti ya America (VOA) na kuendeshwa na mtangazaji Shaka Sally. Hivi karibuni pia nimekuwa pia mshiriki na nimepata nafasi kutoa ama kuuliza maswali juu ya mada zilizokuwa zikijadiliwa. Wiki hii, yaani tarehe 1/8/2007, Raisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete alikuwa ndiye mgeni akihojiwa kutoka Dodoma. Washiriki tulitakiwa tutume maswali mapema kwa barua pepe. Nilifanya hivyo ili nipate nafasi ya kipekee kumuuliza Raisi swali juu ya mustakabali wa nchi yetu. Na kwa bahati nzuri kabisa, maswali mawili ya kwanza yalitoka kwangu; yalihusu wasiwasi wangu juu ya mchango wa sekta ya madini kwa uchumi wetu. Mheshimiwa Raisi alinijibu na nikaridhika hasa swali la kwanza ila sehemu ya pili kidogo kutokana na uhariri uliofanywa na Shaka Sally, sikuridhika na jibu la mheshimiwa Raisi.

Swali langu la kwanza nilitaka mheshimiwa Raisi lilikuwa ni kwa vipi ametimiza ahadi yake ya kuipitia upya mikataba ya madini iliyosainiwa na serikali iliyopita ili sasa ituletee tija? Raisi alijibu vyema kwa maoni yangu na napenda nimshukuru sana kwani alieleza makubaliano kati ya serikali na makampuni mawili: Barrick Gold na Resolute Mines, kuwa sasa yanalipa kwa takriban asilimia 33% ya kodi ikijumuisha pia na mrabaha.Na akasema kuwa kiwango cha dunia au kimataifa ndio hicho kinachotumika katika nchi nyingine. Raisi aliahidi kuwa kuanzia sasa mchango wa makampuni ya madini itakuwa asilimia 33% na si tena yale mambo ya 3%.

Swali langu la pili ambalo mheshimiwa Raisi Kikwete hakuniridhisha kwa majibu na ningependa kama inawezekana atoe ufafanuzi zaidi pindi akipata wasaa niliuliza: Je ni kweli Tanzania hatuna uwezo wa ndani wa kuweza kuzalisha madini hadi hatua ya mwisho na badala yake tunauza nje madini katika hatua ya malighafi?

Raisi alijibu kuwa hatuna nibu la ndani kwa hili na imetubidi tutegemee mitaji ya nje ya kimataifa kama hali halisi inavyodhihiri. Binafsi, nilitegemea ajibu hivyo kwani si mara ya kwanza kusikia viongozi wetu wakisema hivyo. Jibu hili linanisumbua sana na litaendelea kuniuma roho labda mpaka atakapotokea mtu anipe maelezo fulani ambayo sidhani kama huwa yanazingatiwa tunaposema eti nchi ya miaka arobaini na zaidi ya uhuru haina uwezo wa kuuza rasilimali zake katika thamani stahili kupata faida halisi. Je ni kwanini nasema hivi?

Ili nimtendee haki Raisi Kikwete, labda nioneshe swali langu ambalo Shaka Sally alilihariri lilikuwa hivi: Je ni kweli Tanzania hatuna uwezo wa teknolojia au kitaaluma kutengeneza madini ya nchi yetu hadi hatua ya mwisho? Kama ni kweli, ni nini maana ya kuwa na idara ya Geolojia kwa mfano pale Chuo Kikuu cha Dar es salaam? Ina maana kwa miaka yote ya uwepo wa idara hii imekua ikifanya nini kama imeshindwa kutupatia wataalam katika sekta ya madini?

Manake kwa hoja ya kutegemea mitaji kutoka nje, inamaanisha chuo chetu kimeweza tu kutuzalishia wataalamu wa kusaini mikataba bila kuzingatia maslahi ya nchi, hii ni hatari kwa elimu yetu kwani haikidhi haja ya kuzalisha wasomi wazalendo, kweli tumekwisha. Nimpongeze mheshimiwa Raisi alishang'amua hili alipokuwa ziarani kule nchi za Nordic.

Nikiacha maswali ambayo niliyazua binafsi, niseme tu mahojiano ya Raisi yalikuwa mazuri sana na ya uwazi wa dhati. Kwa mfano, Raisi Kikwete akijibu swali la Juma Iddi, juu ya "Kupaa kwa Uchumi Wetu", Raisi aliweka wazi kuwa kwa sasa tuko kwenye mchakato tu na kusema Uchumi unapaa ni mapema sana. Alitumia kauli: "We are yet to see the trickle down". Hapa Raisi Kikwete aliifunga ile hoja ya majibizano kati ya Ofisi ya Waziri Mkuu na waandishi kadhaa katika gazeti hili la Tanzania Daima.

Raisi aliulizwa na Shaka Sally juu ya Visheni yake kwa Taifa: Alisema lengo lake kuu ni kuona Tanzania inaondoka kutoka kundi la nchi masikini kabisa (Least Developed Countries) hadi kuwa kati ya nchi za pato la kati (Middle Income) mara moja ifikapo 2010. Hapa mkazo ataweka kwenye Kilimo na Miundo Mbinu. Na ndio hapa Raisi Kikwete alipoungana na akina Padri Kitambo, Mwanakijiji na Malera kuwa kusema 'uchumi unapaa si kweli kabisa'. Kwa visheni ya Raisi Kikwete, tutegemee ndege itaanza kuwasha injini zake ifikapo 2010; kwa sasa iko gereji ikishughulikiwa.

Shaka Sally alitaka kujua kuwa tangu Raisi Kikwete awe raisi ni jambo gani au uamuzi gani mkubwa na muhimu anaweza kujivunia kati ya mengi aliyokwishafanya? Alisema ni upanuzi wa elimu ya sekondari ambapo asilimia 96% ya wanafunzi wameandikishwa shuleni. Ila alikiri kiwango cha elimu kinachotolewa hakina viwango madhubuti. Na alikiri ni changamoto iliyobakia kuboresha ubora (quality) akitumia neno 'tall order'. Hapa raisi Kikwete alinikuna kwa kuwa mkweli kwani ni kweli kabisa kunahitajika kazi ya ziada; yaani walimu bora na zana bora.

Jambo lingine Raisi Kikwete aliulizwa: je ni nini kinaichoisumbua sana roho yake tangu awe Raisi katika majukumu yake? Jibu la Raisi lilinipa hisia mchanganyiko; kwani raisi alisema kuwa pale anapomuondoa mtu kutoka kwenye madaraka yake amegundua imekuwa ikiambatana na habari za uzushi zaidi na si ukweli. Kwa maana nyingine majungu ni mengi sana anayofikishiwa Raisi wetu. Na ndio maana amesisitiza katika kikao cha NEC kilichomalizika hivi karibuni kuwa tuhuma zozote dhidi ya watendaji ziambatane na ushahidi.

Hapa napata hisia raisi wetu labda hajui kwa nafasi aliyopo majungu lazima yawepo mengi sana; ila kwa kiongozi ni lazima mtu ujifunze kuamini hisia zako pale unapopata jambo na kulitafakari. Kwenye mambo ya utawala kuna kitu kinaitwa "INTUITION" yaani hali ya kung'amua jambo lisilohitaji kufikiri sana na kiongozi unachukua hatua stahili.

Raisi amenishtua kidogo labda hana karama za kiuongozi za kutosha. Kwani kama ni kweli anaumia roho kwa kugundua baadhi ya mabadiliko ya viongozi aliyofanya hayakustahili kwa ajili ya majungu; basi inamaana kuwa hii kuongezeka kashfa kila kukicha na Raisi anakaa kimya labda pia anaumia roho?

Nitoe mifano michache ambapo kashfa zisizohitaji hata mtu kufikiri na kuchukua hatua dhidi ya wahusika: hivi waliosaini Richmond, Kashfa ya Minara ya BOT au hii ya hivi majuzi mtu kwenda kusaini mkataba na kampuni ya madini huko ughaibuni kinyume na taratibu tulizojiwekea ni mambo ya majungu kweli? Raisi Kikwete acha woga, usiumwe roho; chukua hatua, bila maamuzi magumu hasa kutoka kwako nchi hii haitajengwa wala kwenda mbele.

Visheni yako haitafikiwa hata kidogo ukiumia roho kwa kupima majungu, wajibisha watu kwa ujasiri. Angalia hisia za wananchi juu ya kashfa mbalimbali alafu chukua maamuzi kuwaadhibu waliokuzunguka ambao wanakosa kila kukicha wakijua hawafanywi kitu. Woga wako utalifikisha Taifa hili katika siasa za kiushirika vikundi (patronage au cronyism) kama utajaribu kupima uzito wa majungu yanayoambatana na kashfa kadhaa. Si ulishasema huna ubia na mtu; sasa ukiumia roho dhidi ya maamuzi yako hii itapalilia "ubia".

Mwisho, nitoe hongera kwa mheshimiwa Raisi kwa mahojiano yale na VOA; Mungu Ibariki Tanzania iwe na viongozi majasiri wasio waoga na wenye kutenda badala ya kutoa sababu kwa kila jambo lililo ndani ya uwezo wao.

DRC-UGANDA VITANI?

Kuna mgogoro wa mpaka kati ya Uganda na Congo-DRC.Kiini ni kisiwa kimoja ndani ya ziwa Albert ambapo pia kinahusishwa na uwepo wa mafuta. Mgogoro huu unakuwa na kuna mgogoro wa kidiplomasia kati ya nchi mbili hizi.
Kuna habari za wanajeshi wa Kongo kuwavamia wa Uganda mpakani.

Saturday, August 04, 2007

LIGI YA UINGEREZA YAANZA

Msimu mpya wa ligi ya Uingereza unaanza na kwa wale wapenda soka, mambo mtindo mmoja. Kesho mechi ya kufungua pazia itapigwa kati ya Chelsea na Man United. Utabiri unaonesha huu ni mwaka wa Chelsea au Liverpool kwa nionavyo japo Arsenal nina shaka wataonesha maajabu. Huko Uganda, chama cha soka kinafanya mabo kibiashara ambapo ligi ya Uganda itaoneshwa runingani.
Sasa ligi inaanza na utabiri unaonesha ni mwaka wa timu zilezile za msimu uliopita.
Huko Hispania kuna uvumi kuwa Barcelona kumwongeza Henry haitafua dafu kiushambuliaji kabisa.

Ukiacha soka kuna mambo ya personality yamenikuna kidogo. Alafu kuna hii hali ya Zimbabwe inakuwa mbaya kila kukicha na inaonekana Robert Mugabe kaamua kukomalia urais.